Saturday 15 July 2017

Hotuba ya mgeni rasmi Injinia Ndigilo wakati akifunga mafunzo ya makocha wa riadha

 
Wakufunzi wa Kimataifa, Tagara Tendai na Charles Mukiibi (waliofunikwa vitenge) katika picha ya pamoja baada ya kukabidhiwa zawadi na washiriki wa mafunzo ya ufundishaji riadha kwa watoto wenye umri chini ya miaka 16 yaliyofanyika katika Kituo cha Michezo cha Filbert Bayi Kibaha mkoani Pwani.
Rais, Kamati ya Olimpiki Tanzania,Ndugu Gulam Rashid,

Makamu wa Rais, Kamati ya Olimpiki Tanzania, Ndugu Henry Tandau

Katibu Mkuu, Kamati ya Olimpiki Tanzania, Ndugu Filbert Bayi,

Katibu Mkuu, Riadha Tanzania, Ndugu Wilhelm Gidabuday

Mwakilishi, Chama cha Riadha Zanzibar

Wakufunzi wa Kimataifa, Ndugu Tagara Tendai na Charles Mukiibi

Waratibu wa Mafunzo, Ndugu Irene Mwasanga (TOC) na Robert Kalyahe (RT)

Washiriki wa Mafunzo,

Wageni waalikwa,

Mabibi na Mabwana.

Mkuu wa Mkoa wa Pwani, Injinia Evarist Ndigilo (kushoto) akipokea zawadi kutoka kwa Makamu wa Rais wa Kamati ya Olimpiki Tanzania (TOC), Henry Tandau.
Napenda kuchukua nafasi hii kuishukuru ofisi ya TOC kwa kunipa heshima hii ya kuwa mgeni rasmi katika kufunga mafunzo haya ya walimu wa mchezo wa Riadha daraja la 1.

Nimefahamishwa kwamba mafunzo haya yalifunguliwa siku 11 zilizopita na Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo Mhe. Harrison George Mwakyembe. Ni matumaini yangu kuwa mmepata dozi nzuri ya taaluma na mbinu mbalimbali ya kufundisha mchezo huu. TOC inauthamini sana  mchezo wa Riadha, kwani ni kati ya michezo ambayo imeiletea heshima Taifa Taifa letu katika Michezo ya Kimataifa kama Jumuiya ya Madola, Afrika.

Siwezi kuzungumzia Olimpiki kwani  nimefahamishwa tangu tuanze kushiriki Olimpiki mwaka 1964 mjini Tokyo, Tanzania imewahi kupata medali mbili za fedha kupitia Filbert  Bayi (        Mita 3000 kuruka Magongo) na Suleiman Nyambui (Mita 5000).
 
Mgeni Rasmi Mkuu wa Mkoa wa Pwani Everist Ndigilo (kushoto) akimkabidhi cheti mmoja wa washiriki wa mafunzo hayo ya takribani wiki mbili, Suleiman Ame ambaye ni Katibu Mkuu wa Chama cha Riadha Zanzibar (ZAAA) wakati wa hafla hiyo.
Sote tunakumbuka mwaka 2016 wakati wa Michezo ya Olimpiki ya Rio, Mtanzania Alphonce Felix Simbu pamoja na kuwa mshindi wa 5 katika mbio za Marathon aliweza kuitoa Tanzania kimasomaso kwa nafasi ambayo kwa mara ya mwisho ilikuwa mwaka 1992 mjini Barcelona wakati mkimbiaji wa Tanzania Kanali Mstaafu Juma Ikangaa alipokuwa wa sita (6) katika mbio za Marathon.

Kama nilivyofahamishwa haya  ni mafunzo ya nne kufanyika kwa walimu wetu hapa Tanzania. Mafunzo ya awali yalifanyika mjini Dar Es Salaam mwaka 1991, mjini Dodoma mwaka 2004 na mwaka 2010 mjini Dar Es Salaam na mwaka huu 2017 hapa Mkuza, Kibaha. Mafunzo yote yakifadhiliwa na Olimpiki Solidariti (OS) kupitia Kamati ya Olimpiki Tanzania (TOC).

Pia naamini mmefaidika na elimu mliopata kutoka kwa wataalamu wa Kimataifa ambao wamekuwa wakiwaandalia masomo yote ya nadharia na vitendo kwa muda wote wa siku 11. Ni mategemeo yangu elimu mliyopata itawasaidia kuandaa timu zenu na kutambua vipaji vipya katika maeneo mnayotoka. Ni ukweli usiopingika kwamba mmejiongezea elimu ya kufundisha mchezo huu wa riadha kwa kiwango cha hali ya juu, mkilinganisha uwezo na elimu mliyokuwa nayo awali.

Wakati wote TOC imekuwa mstari wa mbele katika kuendeleza taaluma ya ufundishaji na mbinu za kisasa za kuboresha uwezo wa walimu wetu, ili wachezaji wetu waweze kufikia viwango vinavyotakiwa na timu zetu zinaposhindana katika mashindano mbalimbali ya Kimataifa.

Hivi karibuni tumesikia wanariadha wetu wakifanya vizuri katika mashindano ya Kimataifa baada ya Alphonce Felix Simbu kufungua milango ya ufanisi kwa kuwa wa tano (5) kwenye mbio za masafa marefu (Marathon) wakati wa Olimpiki ya Rio 2016.

Baada ya mafanikio hayo ya Simbu, kumekuwa na misafara ya wanariadha wetu kushindana nchi mbalimbali duniani aidha kuongeza mapato au kufikia viwango vya kushiriki mashindano makubwa ya Dunia yanayofanyika Augusti, 2017.

Mkuu wa Mkoa wa Pwani, Ndigilo akimkabidhi cheti, Meta Petro wa Karatu wakati wa hafla hiyo ya kukabidhi vyeti kwa washiriki hao Kibaha.
Mara kwa mara tumesikia katika mafunzo yaliyopita walimu wengi wanapohitimu wanakimbilia kufundisha tu michezo ya kukimbia  hususan mbio za masafa marefu (Marathon) na ndefu (5000/10000) na kusahau michezo mingine, riadha siyo kukimbia tu, kuna mbio fupi (sprints) kati, (middle distance) kuruka (kuruka chini, miruko mitatu, kuruka juu na upondo) na kurusha (mkuki, kisahani, tufe na nyundo).

Ningependa kusisitizia sana kwenu walimu mnaomaliza mafunzo haya, kwamba  mhakikishe mchezo huu wa riadha  unapiga hatua katika maeneo yote na kufikia viwango vya miaka ya 70.

Tanzania haina tofauti na jirani zetu Kenya ambao wamekuwa tishio katika mchezo wa riadha duniani.

Ningependa kuwasihi walimu mnaomaliza mafunzo haya leo kuupeleka mchezo huu mashuleni walipo vijana wengi wenye vipaji vingi ambao wanafundishika na rahisi kuelewa. Inahitajika mipango mahususi ya mazoezi na mashindano ambayo nina imani Chama cha Riadha Taifa inayo.

Nyie wachache mliohudhuria hapa muwe mabalozi wa kupeleka elimu hii kwa wale ambao nao wangependa kuwa hapa, lakini kutokana na nafasi ndogo ya washiriki kwa maagizo ya Shirikisho la Kimataifa la Riadha (IAAF) hawakuweza kushiriki.

Kumekwepo na mapungufu ya walimu wa michezo mbalimbali hasa riadha wakati wa maandalizi ya Umisseta na Umitashumta. Ninaowaomba kwa kuwa mmetoka karibu kila Mkoa wa nchi yetu (Tanzania Bara/Zanzibar) muwasaidie walimu hao kabla na mara maandalizi yanapoanza.

Napenda nichukue nafasi hii kuwapongeza na kuwashukuru Wataalamu wa Kimatafa kwa jitihada zao za kutoa mafunzo haya kwa ufanisi mkubwa, waratibu wa RT/ZAAA, TOC na Walimu washiriki kwani bila wao kuwepo hapa mafunzo haya yasingefanyika.

Nitakuwa mchoyo wa fadhila kama sitawashukuru Olimpiki Solidariti kwa kufadhili mafunzo haya, Shirikisho la Kimataifa la Riadha (IAAF) kuwateua Wakufunzi wa kuendesha mafunzo, TOC na RT/ZAAA kwa maandalizi mazuri, mwisho wenyeji wenu katika Kituo hiki kwa mazingira mazuri na tulivu kwa mafunzo kama haya.

Mwisho kabisa nawashukuru wale wote waliohusika katika kufanikisha mafunzo haya kwa namna moja au nyingine.

Kwa haya machache sasa natamka kwamba mafunzo yenu ya ualimu wa mchezo wa Riadha ninayafunga rasmi na niko tayari kutoa vyeti mbalimbali.


Ahsanteni kwa kunisikiliza.



No comments:

Post a Comment