Wednesday 13 April 2016

Somalia, Djibout zathibitisha kushiriki mashindano ya riadha ya U-20 yatakayofanyika jijini Dar es Salaam Aprili 29-30

Na Mwandishi Wetu
NCHI za Somalia na Djibout zimethibitisha kushiriki mashindano ya riadha ya Afrika Mashariki na Kati kwa vijana wenye umri chini ya miaka 20 yatakayofanyika nchini Aprili 29 na 30, imeelezwa.

Kaimu Katibu Mkuu wa Riadha Tanzania, Ombeni Zavalla (pichani kushoto) alisema kuwa tayari nchi hizo zimethibitisha kushiriki kwa  kuleta majina ya wachezaji na viongozi wao watakaokuja nchini.

Mashindano hayo yatakayofanyika kwenye Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam, mbali na Djibout na Somalia, pia nchi zingine zinazotarajia kushiriki ni Kenya, Uganda, Ethiopia, Zanzibar, Sudan, Rwanda na Burundi.

Alisema kuwa mashindano hayo kabla ya kufanyika yatatanguliwa na mkutano wa viongozi wan chi shiriki, ambao utajadili maendeleo ya mchezo huo.

Aidha, timu ya taifa ya Tanzania Bara inaingia kambini kesho katika shule za Filbert Bayi kujiandaa na mashindano hayo.

Awali, timu hiyo mara mbili ilishindwa kuanza kambi kutokana na ukata na kusababisha makocha wake kuwa na hofu ya kutofanya vizuri.

Kocha Mkuu wa timu hiyo Robert Kalyahe alisema kuwa anahofu timu yao kutofanya vizuri katika mashindano hayo baada ya kuchelewa kuanza mazoezi wakati nchi zingine zilianza maandalizi mapema.

No comments:

Post a Comment