Monday 28 December 2015

Kibira aendelea na matibabu Hospitali ya Taifa ya Muhimbili




Mwenyekiti wa Chaneta, Annie Kibira (kulia) na mwenyekiti wa Baraza la Michezo la Taifa (BMT), Dioniz Malinzi wakati wa kukabidhi bendera ya taifa timu ya taifa ya netiboli iliyodhiriki mashindano ya Afrika nchini Namibia mwaka huu. Timu hiyo haikufanya vizuri.
Na Mwandishi Wetu
MWENYEKITI wa Chama cha Netiboli Tanzania (Chaneta), Annie Kibira anaendelea kupatiwa matibabu katika hospitali ya Taifa ya Muhimbili baada ya kupooza.

Kibira alianguka ghafla baada ya kupatwa na shinikizo la damu na kuanguka wakati akisimamia mashindano ya netiboli ya Muungano kisiwani Zanzibar na baadae kulazwa katika hospitali ya Mnazi Mmoja kisiwani humo kabla ya kuhamishiwa Muhimbili.

Mashindano ya Muungano ya netiboli yalimalizika wiki iliyopita kwenye Uwana wa Gymkhana huku mabingwa wa Tanzania Bara Uhamiaji wakiibuka mashujaa baada ya kulitwaa taji hilo kwa mara ya kwanza.

Mtoto wa Kibira, Kelvin amesema kuwa mama yake kesho Jumanne anatarajiwa kufanyiwa vipimo vya MR1 katika hospitali hiyo kwa ajili ya matibabu zaidi.

Alisema kuwa Kibira amelazwa Mwaisela word namba 7 chumba namba 311, ambako anaendelea na matibabu baada ya kupooza upande wa kulia kuanzia mguuni hadi usoni.

Alisema kuwa kutokana na kuongozana kwa Siku Kuu za Maulidi, Krismas na wikiendi, ndiko kulikosababisha mama yake kuchelewa kufanyiwa baadhi ya vipimo.

Alisema kuwa leo Jumatatu mama alitarajia kuanza kufanyiwa mazoezi ikiwa ni sehemu ya matibabu yake.
Akizungumzia hali ya mama yake, Kelvin alisema kuwa anaendelea vizuri tofauti na alivyokuwa awali.

Kibira kabla ya mashindano hayo ya netiboli ya Muungano alihudhuria Mkutano Mkuu wa kawaida wa mwaka wa Kamati ya Olimpiki Tanzania (TOC) mjini Zanzibar, kabla ya kufanyika mashindano hayo ya Muungano, huku akiwa mwenye afya tele.

No comments:

Post a Comment