Friday 18 September 2015

Mamlaka ya Ngorongoro yaichangia Taswa sh. Milioni 10



Meneja Uhusiano wa Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro, Adam Akyoo, (kushoto) akimkabidhi mfano wa hundi Katibu Mkuu wa TASWA, Amir Mhando.  Katikati ni Katibu Msaidizi wa TASWA, Grace Hoka.
Na Mwandishi Wetu
MAMLAKA ya Hifadhi ya Ngorongoro ( NCAA),imetoa Sh. 10, 486,000 kwa ajili ya kudhamini tuzo za Wanamichezo Bora waliofanya vizuri zaidi katika kipindi cha miaka 10 ya uongozi wa Rais Jakaya Kikwete.

Tuzo hizo zinazoandaliwa na Chama cha Waandishi wa Habari za Michezo Tanzania (TASWA zinatarajiwa kufanyika Oktoba 8, mwaka huu ukumbi wa Mlimani City, Dar es Salaam, ambapo pia TASWA itatoa Tuzo ya Heshima kwa Rais Kikwete ikiwa ni kuthamini mchango wake kwa sekta ya michezo katika uongozi wake.

Akizungumza katika mkutano na waandishi wa habari Dar es Salaam jana, Meneja Uhusiano wa Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro, Adam Akyoo, alisema wameamua kusaidiana na TASWA kwa sababu Rais Kikwete ni mdau mkubwa wa michezo na pia wa masuala ya utalii.

"Dk. Kikwete ni mdau mkubwa  wa Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro kwani kwa kipindi chote ambacho amekuwa Waziri wa Mambo Nje na Ushirikiano wa Kimataifa na hatimaye Rais wa Jamhuri ya Mungano wa Tanzania ametembelea hifadhi hii  mara nyingi zaidi kuliko viongozi wengine wote wa Taifa letu waliomtangulia.

"Pia amekuwa mdau muhimu na wa mstari wa mbele wa Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro katika  kutangaza vyema vivutio vya watalii vya hifadhi ya Ngorongoro katika mataifa mbalimbali duniani alikokwenda kwa ziara za kikazi.

"Jambo hili limeleta watalii wengi nchini kutoka mataifa  mbalimbali dunini. Vile vile ziara zake za mapumziko hifadhini wakati wa sikukuu mbalimbali zimewahamasisha sana  Watanzania walio  wengi kutembelea  hifadhi hii kutoka kote nchini na hata nchi jirani," alisema Akyoo.

Pia alisema waandishi wa habari ni wadau wakubwa na muhimu katika harakati za utalii na ndiyo sababu wameamua kuisaidia TASWA ifanikishe shughuli yake.

Kwa upande wake, Katibu Mkuu wa TASWA, Amir Mhando aliishukuru mamlaka ya hifadhi hiyo na kusema kuwa msaada huo ni mkubwa na kuomba wadau wengine waungane nao kufanikisha jambo hilo.

"Kama tulivyosema bajeti yetu ni Sh milioni 130, juzi (Jumatano) tulipata watu wa GSM Foundation waliotupa Sh. Milioni 50, tunaomba na wengine tushirikiane nao katika hili," alisema Mhando.

Alisema TASWA imeamua kuandaa hafla ya wanamichezo kumuaga Rais na pia kumpa tuzo kwa vile wakati wa uongozi wake amefanya mambo makubwa katika sekta ya michezo.

Kwa mujibu wa Mhando, wanamichezo pia watatumia tuzo hizo zilizoandaliwa na TASWA kumuaga Rais Kikwete anayemaliza muda wake kikatiba baada ya Uchaguzi Mkuu wa Rais, Wabunge na Madiwani Oktoba 25, mwaka huu.

No comments:

Post a Comment