Saturday 22 September 2018

Waziri Ummy Avipongeza Viwanja vya Ndege Kudhibiti Ebola

Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Ummy Mwalimu akiwa pamoja na Mwakilishi wa Shirika la Afya Duniani (WHO), Dk Adiele Onyeze wakati wa matembezi ya uelimishaji kuhusu gonjwa la Ebola leo jijini Dar es Salaam.

Na Mwandishi Wetu
WIZARA ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto imeipongeza Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Tanzania (TAA), kwa kuchukua hatua za haraka za kudhibiti ugonjwa wa Ebola usiingie nchini, imeelezwa.

Kauli hiyo imetolewa leo na Waziri wa Wizara hiyo, Mhe. Ummy Mwalimu katika hotuba yake kwa wananchi walioshiriki Matembezi ya Hiyari ya kuelimisha na kuhamasisha Jamii kuzuia ugonjwa huo usiingie nchini yaliyoanzia kwenye viwanja vya Mnazi Mmoja na kuishia Viwanja vya Karimjee jijini Dar es Salaam, ambapo imesharipotiwa ugonjwa huo umeingia nchi jirani ya Jamhuri ya Demokrasia ya Kongo.
Meneja Rasilimali Watu na Utawala  wa Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Tanzania, TAA, Abdi  Mkwizu (mwenye fulana ya bluu) wakati wa matembezi hayo leo. 
Mhe. Mwalimu amesema TAA inafanya jambo jema kwa kuhakikisha wasafiri wote wanaoingia nchini kupitia viwanja vya ndege wanafanyiwa ukaguzi na kutoa taarifa za afya zao kwa wale ambao watabainika kuwa na joto la mwili lisilokuwa la kawaida.

“Nawapongeza sana tena sana Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Tanzania kwa kuhakikisha nchi inakuwa salama bila kupata maambukizi ya ugonjwa huu wa Ebola, imeripotiwa sasa huu ugonjwa upo Kivu Kaskazini, ambapo ni karibu na nchini na Wavuvi wanakuwa na muingiliano kwa kutoka huko na kuja nchini,” amesema Mhe. Mwalimu.
Hatahivyo, amesema pamoja na ugonjwa huo kutoingia nchini, lakini kwa mujibu wa taarifa kutoka Shirika la Afya Duniani (WHO), tayari imeripotiwa wananchi 111 wa Kongo wamepata maambukizi na kati yao 75 sawa na asilimia 67 wamefariki, hivyo inakisiwa endapo Tanzania ikiwa na wagonjwa 100 anaweza kusababisha vifo vya watu 50.    

"Ebola bado haujaingia nchini Tanzania, lakini ni kweli kwamba tupo katika hatari kubwa zaidi kupata ugonjwa huu, hii inatokana na mlipuko wa ugonjwa huu kuwepo katika eneo la Kivu Kaskazini na imesharipotiwa kuua watu na sisi hatupo mbali na eneo la Kivu, hivyo tusikubali ugonjwa huu kuingia nchini na tutoe elimu juu ya ugonjwa huu,” amesisitiza Mhe. Waziri Ummy Mwalimu.
 
Aidha, Mhe. Mwalimu aliwaomba Viongozi wa Dini kutumia majukwaa yao katika mahubiri yao kutoa tahadhari kwa wananchi kuhusiana na ugonjwa huu wa Ebola, ambapo pia awaomba wasanii wa muziki na viongozi wa Siasa nchini kutumia majukwaa yao ili kufikisha taarifa kwa wananchi juu ya ugonjwa huu.

Naye Kaimu Mkurugenzi wa Rasilimali Watu na Utawala wa TAA, Bw. Lawrence Thobias aliyemwakilisha Mkurugenzi Mkuu, Bw. Richard Mayongela amesema viwanja vya ndege vimekuwa na mikakati ya muda mrefu kwa kushirikiana na Wataalamu wa Afya ya kudhibiti magonjwa ya kuambukiza ukiwemo Ebola.
Bw. Thobias amesema sasa viwanja vyote hususan vilivyopo katika mipaka ya nchi zimefungwa mashine maalum (thermos scanner) za kutambua joto la mwili wa binadamu, na ikibainika limezidi nyuzi joto 38, abiria huyo anapelekwa katika chumba maalum na kufanyiwa mahojiano ya kina juu ya afya yake na pia abiria wanaowasili na ndege zinazofanya safari nchi jirani na Kongo nao hunawa mikono kwa dawa maalum kabla ya kutoka nje ili kuendelea na safari zao.

“Kwa upande wetu tumeweka mikakati kamambe ili huu ugonjwa usiweze kuingia nchini, mbali na abiria kunawa kwa dawa maalum anapoingia tu ndani ya mlango wa wasafiri wanaotoka nje ya nchi, pia kuna mashine maalum (thermo scanners) ambazo zinaonesha joto la mwili wa kila abiria anapoingia kwenye lango hilo, na kimetekwa chumba maalum cha mahojiano kwa wale wanaobainika kuwa na joto la juu, na pia katika hospitali ya Temeke napo kipo chumba maalum endapo atabainika mgonjwa aliyepatikana kupitia viwanja vyetu anapelekwa huko,” amesema Bw. Thobias.
Mbali na kuweka mashine mbalimbali kwenye viwanja vya ndege nchini, pia TAA ikiwa ni mmoja wa wadhamini imechangia Tshs. Milioni 5 kwa ajili ya kampeni ya kutoa elimu juu ya ugonjwa wa Ebola kwa wananchi.

Ugonjwa wa Ebola unasambazwa na virusi vya Ebola na husababisha homa kali inayoweza kuambatana na kutokwa damu mdomoni, puani, masikioni, machoni na sehemu nyingine za wazi na unaenea kwa haraka, na namna ya kujikinga na ugonjwa huu ni pamoja na kuepuka kugusa damu, machozi, jasho, matapishi, kamasi, mkojo au kinyesi cha mtu mwenye dalili za ugonjwa; pia mtu hatakiwi kugusa, kuosha au kuzika maiti ya aliyekufa kwa Ebola; pia usiguse au kula wanyama kama popo, sokwe au swala wa msituni.
Mwakilishi wa Mkurugezi Mkuu wa Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Tanzania (TAA), Raulence Thobias akizungumza wakati wa hafla ya kuelimishana kuhusu ugonjwa wa Ebola iliyofanyika Karimjee Jijini Dar es Salaam leo.
Dalili za Ebola ni pamoja na homa kali, maumivu ya kichwa na misuli, mwili kulegea, kutapika, kuharisha, vipele na kutokwa damu maeneo mbalimbali ya mwili.






No comments:

Post a Comment