Sunday 9 September 2018

Pakacha Group Yapongezwa Kutoa Elimu ya Maji kwa Wananchi wa Kwembe, Kibamba, Msigani



Na Mwandishi Wetu
ASASI ya Pakacha Group imepongezwa kwa kutoa elimu kwa wananchi juu ya ufuatiliaji wa miradi ya maji na utekelezaji wake ili kuondokana na shida ya maji katika maeneo yao.

Wakizungumza katika mkutano wa siku moja uliondaliwa hivi karibu na Pakacha Group kwa ufadhili wa The Foundation For Civil Society, wananchi wamesema ongezeko la idadi ya watu na ujenzi holela wa makazi ni miongoni mwa changamoto zinazopelekea  ukosefu wa upatikanaji wa huduma za maji kwa wananchi.
 
Washiriki wa mkutano huo walikuwa wananchi wa Kata tatu za Kwembe, Kibamba na Msigani, viongozi wa serikali za mtaa, watendaji, madiwani na wakuu wa idara ya maji kutoka Halmashauri ya Manispaa ya Ubungo.

Adam Kingu, mjumbe wa serikali ya mtaa wa Malamba Mawili amesema Pakacha inafanya kazi nzuri, huku akiwaomba viongozi wa serikali za mitaa watoe elimu ili kuzuia ujenzi holela ambao umepelekea uharibifu wa miundombinu ya maji.

“Watu wamejenga bila kufuata utaratibu hivyo ni rahisi miundombinu ya maji kuharibiwa”, amesema  Kingu.

Everyline Francis, mjumbe wa kamati ya maji ya Kata ya Kwembe amesema jamii ipewe elimu ya kutunza vyanzo vya maji na kuzuia uharibifu wa mazingira. 
 
Upatikanaji wa maji umekuwa na changamoto katika kata za Kwembe, Msigani na KIbamba, hivyo asasi ya Pakacha, kwa ufadhili wa The Foundation For Civil Society kulazimika kutoa elimu kwa wananchi juu ya ufuatiliaji na utunzaji wa vyanzo vya maji.

Diwani wa Kata ya Kwembe wilayani Ubungo, Dweza Kolimba amesema asasi za kiraia kama Pakacha zina nafasi kubwa ya kuleta maendeleo katika jamii kwa kushirikiana na wananchi na watendaji wa serikali.

Akizungumza katika semina hiyo kwa ajili ya kujadili utatuzi wa changamoto ya maji, kuanzia ufuatiliaji wa rasilimali fedha na utekelezaji wake, Kolimba amesema upatikanaji wa maji katika kata yake umekuwa wa shida huku akisema kuwa wananchi wengi watapata maji baada ya mradi mkubwa wa Luguruni kukamilika.
 
“Tayari mabomba yamesambazwa, hivyo tunaomba mradi huu uishe mapema ili watu wapate maji,” amesema Kolimba.

Akizungumza kwa niaba ya Mhandisi wa maji wa Manispaa ya Ubungo, Hamad Sendekwa amesema ameomba wananchi washirikiane na watendaji ili kutatua kero za maji na jitihada zinaendelea kuhakikisha huduma hiyo muhimu inapatikana wakati wote. Alisema ushirikiano huo utasaidia kuibua changamoto zinazokwamishwa na rasilimali fedha au kutowajibika kwa baadhi ya watendaji.

Alisema asasi zinaweza kuleta mabadiliko kwa kufuatilia miradi ya maji, ambayo inakwamishwa kwa sababu mbalimbali na kuwaelimisha wananchi jinsi ya kulinda miundo mbinu ya maji na ufuatiliaji wake.

Katibu wa Pakacha, Haroun Jongo amesema lengo la mkutano huo ni kutoa msukumo kwa utelekezaji wa miradi kwa kuibua hoja kwa wananchi, kwa lengo moja tu, kuleta maendeleo.

Amesema lengo lingine la mkutano huo lilikuwa kuleta jukwaa la majadiliano kati ya viongozi, wananchi na watendaji wa serikali za mitaa ili kutatua kero za maji kwa wananchi kupitia mfumo wa Pets.

Pets ni mfumo unaowezesha ufuatiliaji matumizi ya rasilimali za umma zinazotoka Serikali Kuu au halmashauri kwa maendeleo ya wananchi kuanzia ngazi za mitaa hadi kata na kuendelea.

No comments:

Post a Comment