Wednesday 18 May 2016

Makamu wa Rais Samia Suluhu Hassan Ijumaa kuzindua mfuko wa uchangishaji fedha za kupambana na Ukimwi


Mkurugenzi Mtendaji wa Tume ya Kupambana na Ukimwi (Tacaids), Dk. Fatma Mrisho akizungumza na waandishi wa habari leo. Kulia ni makamu wa rais wa Geita Gold Mine (GGM), Simon Shayo na Balozi wa Kili Challenge, Mrisho Mpoto.

Na Mwandishi Wetu
MAKAMU wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan Ijumaa atakuwa mgeni rasmi katika uzinduzi wa kuchangisha fedha kwa ajili ya kupambana na Ukimwi utakaofanyika jijini Dar es Salaam, imeelezwa.

Hafla hiyo imeandaliwa na Mgodi wa  Dhahabu wa Geita (GGM) kwa kushirikiana na Tume ya Kupambana na Ukimwi Tanzania (Tacaids),ambapo mwaka huu wanatarajia kukusanya zaidi ya sh. bilioni 1.
Makamu wa Rais wa GGM, Simon Msuya akzungumza na waandishi wa habari mapema leo. Wengine pichani ni Mkurugenzi Mtendaji wa Tacaids, Dk. Fatma Mrisho na Balozi wa Kili Challenge Mrisho Mpoto.

Mkurugenzi Mtendaji wa Tacaids, Fatma Mrisho alisema jana kuwa GGM kwa kushirikiana na Tacaids kila mwaka imekuwa ikichangisha fedha kwa ajili ya kusaidia vituo na taasisi mbalimbali zinazopambana na Ukimwi.

Fedha hizo zitachangishwa kwa utaratibu wa kupanda Mlima Kilimanjaro, ambapo watu mbalimbali wanatarajia kuchangia, ambapo fedha hizo zitasaidia vituo mbalimbali vinavyosaidia waathirika wa Ukimwi.

Balozi wa Kili Challenge, Mrisho Mpoto au Mjomba (kushoto) akizungumza wakati wa mkutano na waandishi wa habari mapema leo jijini Dar es Salaam. Katikti ni Mkurugenzi Mtendaji wa Tacaids, Dk. Fatma Mrisho na makamu wa rais wa GGM, Simon Shayo.
Alisema vifo vitokanavyo na Ukimwi vimepungua kwa takribani asilimia 40 lakini vinatakiwa kufikia asimilia 100.

Aidha, makamu wa rais wa GGM Simon Shayo alisema kuwa kesho katika hafla hiyo pia wataitumia kuzipa fedha taasisi mbalimbali za umma na zila za binafsi zinazopambana na Ukimwi.

Alisema mwaka jana walikusanya kiasi cha Sh Bilioni 1 na mwaka huu wanatarajia kukusanya fedha zaidi kwa ajili ya kusaidia vikundi au taasisi zinazopambana na Ukimwi.

Alisema GGM itaendelea kushirikiana na serikali katika vita hiyo ya kupambana na ukimwi ili kuhakikisha unapungua na kumalizika kabisa ifikapo mwaka 2030.

Alisema kuwa katika hafla hiyo kesho watatoa fedha zilizokusanywa mwaka jana kwa taasisi mbalimbali.

Balozi wa Kili Challenge Mrisho Mpoto alisema kuwa jana kuwa  jamii bado ina unyanyapaa kwa watu wanaoishi na Virusi vya UKIMWI pamoja na UKIMWI, ambapo hali hiyo inasababisha kuchelewa kukabiliana na janga hilo.

Imeelezwa kuwa tatizo hilo limesababisha waathirika wa tatizo hilo kuwa na woga kwa kuhofia unyanyapaa miongoni mwa jamii, kitu ambacho kinaumiza sana.
 
Alisema kuwa, usiri huo na elimu ndogo ya kukabiliana na ugonjwa huo ikiwemo matumizi sahihi ya kinga na dawa za kupunguza makali yake vimezidi kufanya hali izidi kuwa mbaya.

Alisema atajitahidi kuhakikisha uteuzi wake unakuwa na matokeo chanya katika jamii, hasa vijana ambao ndio waathirika wakubwa wa ugonjwa huo hapa nchini.

Kwa kipindi kirefu sasa Tanzania imeendelea kuwa na watu wengi wanaoishi na Virusi vya Ukimwi pamoja na wagonjwa wa Ukimwi.

Kwa mujibu wa takwimu kutoka Tacaids, inakadiriwa kuwa watu milioni 1.6 nchini wanaishi na VVU na Ukimwi, na kuwaathiri zaidi ya vijana na watoto yatima milioni 1.3.

Bado ipo changamoto miongoni mwa jamii kuhusu elimu ya ugonjwa huo kwa kuwa kuna vituo vichache sana vya taarifa juu ya janga hilo.

No comments:

Post a Comment