Saturday 7 May 2016

GGM, Tacaids wamteua Mrisho Mpoto `Mjomba' kuwa Balozi wa kampeni ya Kili Challenge


Mrisho Mpoto akisaini mkataba wa kuwa Balozi wa Kili Challenge.

Na Mwandishi Wetu
MGODI wa Dhahabu wa Geita (GGM) kwa Kushirikiana na Tume ya Kupambana na Ukimwi nchini (Tacaids) imemteua msanii maarufu wa mashairi Mrisho Mpoto kuwa balozi wa kampeni ya Kili Challenge.

Hafla hiyo ilifanyika katika ofisi za GGM jijini Dar es Salaam, ambapo Mpoto alisaini mkataba wa mwaka mmoja kuwa balozi wa Kili Challenge.

Kili Challenge ni kampeni inayolenga kukusanya fedha kwa ajili ya kutunisha mfuko wa mapambano dhidi  ya VVU na Ukimwi. Kampeni hiyo ilianza miaka 15 iliyopita na hufanyika kila mwaka kwa wadau mbalimbali kupanda mlima Kilimanjaro, ambapo kwa mwaka jana walipanda watu 39 na kuchangisha takribani bilioni 1.2, sehemu ya fedha itagaiwa kwa asasi mbalimbali za kiserikali na za kijamii wakati wa sherehe za uzinduzi rasmi za sherehe ya mwaka huu zitakazofanyika Mei 20 katika hoteli ya Hyatt Kilimanjaro, ambapo mgeni rasmi atakuwa Makamu wa Rais Mh. Samia Suluhu Hassan.

Mpoto ameteuliwa kuwakilisha na kuitangaza kampeni hii ili kusaidiana na serikali pamoja na wadau mbalimbali ndani na nje ya Tanzania, kupambana na janga hili la Taifa. Pia kwa kuwa ni msanii na kupitia kazi zake za sanaa na ushawishi wake ndani ya jamii ataweza kuihamasisha jamii ipasavyo kuona umuhimu wa kumaliza tatizo hili hasa katika masuala ya unyanyapa.
 
Kwa mujibu wa Mkurugenzi Mtendaji wa TACAIDS, Dk. Fatma Mrisho, “Inakadiriwa kuwa watu milioni 1.6 nchini wanaishi na VVU na Ukimwi. Ugonjwa wengi umewaathiri zaidi vijana na watoto yatima zaidi ya milioni 1.3. Tunahitaji kubadilisha hali hii. TACAIDS kwa kushirikiana na mgodi wa Dhahabu wa Geita (GGM) na wadau wengine kwa kupitia mpango huu wa Kilimanjaro Challenge tunapenda kutoa mchango na ushirikiano wetu kwa Taifa ili kutunisha mfuko utakaowezesha kuendeleza mapambano dhidi ya ugonjwa huo,”

“Napenda kuupongeza mgoni wa Dhahabu wa Geita kwa kushirikiana na wadau wengine kwa kuamua kwa dhati kwa kipindi cha miaka 15 kuwekeza katika mradi huu kwa kuuwezesha kuwa mradi wa kitaifa na si wa GGM, hivyo pamoja na balozi wetu hivi sasa Mpoto tuungane nao ili kuongeza chachu kwa wadau wengine kujitokeza kuongeza nguvu katika mapambana dhidi ya janga hili,” alisema Dk. Mrisho.

Mrisho Mpoto 'Mjomba' akiwa na Mkurugenzi Mtendaji wa Tacaids nchiniDk.  Fatma Mrisho.
Aliongeza … “Kwa kushirikiana na Mpoto tunamatumaini ya kujenga timu imara yenye hamasa ya kutuma ujumbe popote Tanzania na duniani ili kupambana na janga hili. Tunatoa wito kwa makampuni na wadau mbalimbali wa ndani na nje ya nchi wajitokeze ili kushirikiane kutunisha mfuko wa Kilimanjaro Challenge na mwishowe kufikia ndoto au malengo ya nchi yetu ya kuhakikisha tunakuwa na kizazi kisicho na maambukizi ya VVU na Ukimwi,” Bw. Saimon Shayo, Makamu Rais wa miradi endelevu wa Anglogold Ashanti (GGM).

Shayo alisisitiza kwa kusema “GGM iko tayari kushirikiana na wadau wengine nia ya dhati, kuungana pamoja kupitia mfumo wa Kili Challenge katika kuhakikisha maambukizi haya hayaendelei kuleta athari kwa jamii yetu kwa sababu serikali yenyewe haitaweza kutokomeza tatizo hili,”
 
Naye Balozi mpya wa Kili Challenge, Mpoto alisema “Nashukuru sana kwa kupata fursa hii ya kuweza kutoa mchango wangu katika kuisadia jamii kuepukana na janga hili. Changamoto kubwa inayotokana na janga hili la VVU na Ukimwi ni ongezeko la maambukizi ya VVU kwa vijana ambao, ndio nguvu kazi ya Taifa letui pasipo kila mmoja wetu kujitoa kwa dhati hatutalimaliza janga hili.”

Pamoja na hatua kubwa zilizopigwa na serikali ikishirikiana na wadau, kumekuwepo na ongezeko la maelfu ya watoto yatima wanaohitaji misaada baada ya wazazi wao kufariki, wajane wasiokuwa na kipato, pamoja na wazee wanaolazimika kuwalea wajukuu walioachwa na watoto wao, ambao walifariki kutokana na ugonjwa huo ulisisitiza Mkurugenzi Mtendaji wa TACAIDS.

Kilimanjaro Challenge ni mradi unaolenga kutoa elimu kwa jamii kuhusu ugonjwa wa ukimwi na virusi vya ukimwi (VVU). Pia inalenga kuchangisha fedha ili kujenga timu itakayoendeleza mapambano dhidi ya ugonjwa huo.

Ili kuweza kuwa sehemu yawatakaopanda Mlima Kilimanjaro, kwa kupitia Kili Challenge mwaka huu, uwe mtu binafsi au kupitia shirika kulipia wafanyakazi wake kupanda mlima mchango ni $5,000 tu, ambazo zitalipia gharama za upandaji na kuchangia mfuko wa Kili Challenge.

Kilimanjaro Challenge imebakia kuwa chombo muhimu kinachoshirikiana na taasisi za nje na ndani ya nchi katika mapambano dhidi ya VVU na Ukimwi kwa jamii ya Kitanzania na dunia kwa ujumla ili kuwapa matumaini ya kuhakikisha jamii inabaki bila kuathiriwa na ugonjwa huo katika miaka ijayo. 

Mpango huo pia unalenga kusaidia serikali kukabiliana na VVU na Ukimwi sambamba na kutoa nafasi kwa watalii wa ndani kuupanda mlima Kilimanjaro.

KUHUSU Kili Challenge:
  Kwa maelezo zaidi tembelea tovuti ya www.anglogoldashanti.com na www.geitakilichallenge.com.
Mrisho Mpoto 'Mjomba' akiteta jambo na Mkurugenzi Mtendaji wa Tacaids nchini, Dk. Fatma Mrisho.
 

Mrisho Mpoto (katikati) pamoja na Makamu wa Rais GGM, Simon Shayo na Mkurugenzi wa Mtendaji wa Tacaids, Fatma Mrisho wakiwa wameshika mkataba wa kumfanya Mpoto kuwa Balozi wa Kili Challenge.

Mrisho Mpoto akizungumza na wanahabari wakati wa kusaini mkataba wa kuwa Balozi wa Kili Challenge. Kushoto ni Mkurugenzi Mtendaji wa Tacaids, Dk. Fatma Mrisho.


No comments:

Post a Comment