Thursday 19 May 2016

Ndege ya EgyptAir ikitokea Paris kwenda Cairo yaanguka leo Alhamisi na kuua abiria 66


Ndege ya EgyptAir iliyoanguka leo asubuhi ikipaa katika moja ya viwanja vya ndege vya Misri hivi karibuni.

CAIRO, Misri
NDEGE ya Shirika la Ndege la EgyptAir kutoka jijini Paris kwenda Cairo ikiwa na abiria 66 na wafanyakazi kadhaa ndani yake, imeanguka katika bahari ya Mediterranean mapema leo asubuhi, taarifa ya Mamlaka ya Anga ya Misri imeeleza.

Waziri Mkuu wa Misri Sherif Ismail alisema ilikuwa ni mapema mno kusema kama ndege hiyo ilikuwa na matatizo ya kiufundi au ni shambulio la kigaidi lililosababisha kuanguka kwake.

"Kwa sasa hatuwezi kusema lolote, alisema Waziri Mkuu huyo wakati akizungumza na waandishi wa habari kwenye Uwanja wa Ndege wa Cairo.

Ndege ya EgyptAir yenye namba 804 ilipotea katika rada kuanzia saa 8:45 alfajiri kwa saa za Misri wakati ikiruka futi 37,000 kutoka usawa wa bahari, ilisema taarifa hiyo.

Ilielezwa kuwa ndege hiyo aina ya Airbus A320 ilipotea maili 10 (sawa na kilometa 16) baada ya kuingia katika anga ya Misri, karibu kilometa 280 (maili 175) nje ya pwani ya kaskazini ya bandari ya Mediterranean katika jiji la Alexandria.
Ndege hiyo iliyoanguka leo ikiwa katika Uwanja wa Cairo mwaka 2014, ilikuwa ikitokea Paris, Ufaransa.

Viongozi wa Mamlaka ya Anga walisema baadae kuwa ndege hiyo ilianguka na uchunguzi wa kuitafuta unaendelea.

Uwezekano wa ndege kuanguka imethibitishwa, baada ya kutokuwepo uwezekano wa kutua katika uwanja wowote wa ndege wa karibu, alisema mtu aliyepewa mamlaka ya kuzungumza na vyombo vya habari mapema leo.

Ndege za jeshi la Misri na meli zinashiriki katika operesheni hiyo katika pwani ya Mediterranean kuisaka ndege hiyo, ambayo ilibeba abiria 56 akiwemo mtoto na vichanga viwili, na mafanyakazi 10.

Rubani alikuwa na zaidi ya saa 6,000 za kurusha ndege.
Waziri wa Mambo ya Nje wa Ufaransa Jean-Marc Ayrault aliahidi nchi yake kupeleka ndege za jeshi na boti kuungana na Misri kusaidia utafutaji wa mabaki ya ndege hiyo.

Kwa mujibu EgyptAir, waliokuwemo katika ndege hiyo ni pamoja na rais 15 wa Ufaransa, Wamisri 30, Wa Iraq wawili, Muingereza mmoja, Mkuwait mmoja, Msaudia mmoja, Msudan mmoja, Mchadi mmoja, Mreno mmoja, Mbelgiji mmoja, Mualgeria mmoja na Mcanada.

No comments:

Post a Comment