Friday 26 August 2016

DSTV YAWAANDALIA TAFRIJA NZITO NA ZAWADI NONO WACHEZAJI WA TANZANIA WALIOSHIRIKI OLIMPIKI RIO 2016




 Mshindi wa tano wa mbio za Marathon za Olimpiki Rio 2016, Alphonce Felix (katikati) pamoja na washiriki wenzake wa mbio hizo, Fabian Joseph na Said Makula mara baada ya kuwasili kwenye Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere (JNIA) Alhamisi wakitokea Brazil.

Na Mwandishi Wetu
WACHEZAJI wa Tanzania walioshiriki Michezo ya 31 ya Olimpiki iliyofanyika Rio de Janeiro, Brazil wamerejea nchini na Jumapili watafanyiwa tafrija nzito na kupewa zawadi na Kampuni ya Multchoive-Tanzania kupitia DSTV.


Katibu Mkuu wa Kamati ya Olimpiki Tanzania (TOC) akiteta jambo na katibu wa Kamati ya Ufundi ya Riadha Tanzania (RT), Rehema Killo kabla ya kuwasili kwa wanariadha wa Tanzania walioshiriki Michezo ya Olimpiki.
Kwa mujibu wa Katibu Mkuu wa Kamati ya Olimpiki Tanzania (TOC), Filbert Bayi, tafrija hiyo itafanyikia kwenye hoteli ya Serena jijini Dar es Salaam.

Mbali na tafrija hiyo ambako pia watazawadiwa zawadi nono kwa mujibu wa taarifa kutoka DSTV, wanariadha Alhamisi walikabidhiwa zawadi za fedha taslimu kuanzia sh.500,000 hadi 200,000.
 
SABABU YA ALPHONCE
Shamrashamra hizo zote tangu kuwapokea uwanja wa kimataifa wa ndege wa Julius Nyerere (JNIA), ambako wanamichezo wengi walijitokeza kuwalaki na baadae kukabidhiwa mashada ya maua na mabusu manono kutoka kwa wake zao, zilitokana na nafasi ya tano iliyoshikwa na Alphonce Felix katika mbio za marathoni.


Wake wa wanariadha, Alphonce Felix, Rehema (kushoto) na yule wa Said Makula, Fatuma wakati wakisubiri kuwasili kwa waume zao kwenye Uwanja wa Kimataifa wa Ndege wa Julius Nyerere (Jnia) Alhamisi.
Felix alimaliza mbio hizo katika nafasi hiyo kwa kutumia saa 2:11:15 na kuhitimisha umwamba wa Juma Ikangaa wa kushika nafasi ya juu kwa wanariadha wa Tanzania katika Michezo ya Olimpiki.

Ikangaa alimaliza wa sita katika Michezo ya Olimpiki iliyofanyika Los Angeles, Marekani 1984 kwa kutumia saa 2:11:10 na hivyo kubaki bado akishikilia rekodi ya kuwa mwanariadha wa Tanzania mwenye kasi zaidi katika Michezo ya Olimpiki pamoja na Felix kumaliza katika nafasi ya juu kuliko Ikangaa.


Kaimu Katibu Mkuu wa Baraza la Michezo la Taifa (BMT) Mohamed Kiganja (kulia) akimkabidhi zawadi ya fedha taslimu mwanariadha Alphonce Felix wakati wa tafrija fupi kwenye Uwanja wa Taifa Dar es Salaam.
ZAWADI ZA FEDHA TASLIMU
Felix kwenye Uwanja wa Taifa alizawadi kitita cha sh 500,000 huku wenzake Said Makula aliyemaliza katika nafasi ya 43 na Fabian Joseph aliyeshika nafasi ya 112 pamoja na Sara Ramadhani ambaye hakuwepo siku hiyo na kocha Francis John,  kila mmoja aliondoka na sh 200,000.

Kwa mujibu wa taarifa kutoka DSTV, kamapuni hiyo ya king’amuzi cha michezo yote imeahidi kutoa zawadi nono siku hiyo mbali na kuwaandalia chakula cha jioni wachezaji hao pamoja na viongozi wao.
 
Taarifa hiyo ilisema kuwa wachezaji hao wote saba, wanne wa riadha, mmoja wa judo (Andrew Mlugu) na wawili wa kuogelea (Hilal Hilal na Magdalena Moshi), wote watakabidhiwa zawadi hizo nono ambazo zimeahidiwa na DSTV.

Mbali na zawadi zingine huenda DSTV wakampatia kila mchezaji king’amuzi kilicholipiwa kwa ajili ya kufaidi uhondo wa kungalia michezo yote duniani.

Kupokewa kwa Shangwe
Wengi wanajiuliza sababu za Felix kupokewa kwa shangwe wakati hakupata medali yoyote katika michezo hiyo ya Olimpiki.

  Kaimu Katibu Mkuu wa Riadha Tanzania (RT), Ombeni Zavalla `Avintishi’, Kaimu Katibu Mkuu wa Baraza la Michezo la Taifa (BMT), Mohamed Kiganja na Katibu wa Kamati ya Ufundi ya RT, Rehema Killo.
 Uongozi wa Riadha Tanzania (RT) pamoja na wadau mbalimbali wa michezo wanasema kuwa mwanariadha huyo amefanya kile ambacho kwa muda mrefu hakijafanywa na wanariadha wa Tanzania katika michezo hiyo mikubwa kabisa duniani inayoshirikisha zaidi ya mchezo mmoja.

Katibu Mkuu wa Riadha Tanzania  (RT), Ombeni Zavalla alisema kuwa Felix ameliondolea aibu taifa kwa kumaliza watano kwani kwa miaka mingi wanariadha wa Tanzania hawajawahi kumaliza katika nafasi 10 za kwanza.
 
Ikangaa anasemaje?
Ikangaa akizungumza katika mapokezi ya akina Simbu alisema kuwa kuwa amefarijika sana kuona mwanariadha huyo chipukizi akimaliza katika nafasi nzuri na hata kuipiku nafasi yake ya sita aliyoiweka mwaka 1984.

Anasema kuwa huu ni mwanzo mzuri baada ya miaka mingi ya kushindwa kufanya vizuri katika michezo mikubwa kama hiyo.

Anasema kuwa siri ya mafanikio ni maandalizi ya muda mrefu na kujali pia mchango wa wanariadha wakonge kama yeye ili kutoa uzoefu wao katika mbio hizo na zingine.

Anakiri kuwa mbio za marathoni ni ngumu sana hasa katika kipindi hiki cha sayansi na teknolojia kwani watu wamekuwa wajanja na mbinu nyingi.


Kocha wa timu ya riadha ya Tanzania iliyoshiriki Michezo ya 31 ya Olimpiki ya Rio 2016, Francis John (kulia) akiwa na Kaimu Katibu Mkuu wa BMT, Mohamed Kiganja kwenye Uwanja wa ndege.
Kocha wao anasemaje?
Kocha wa timu hiyo ya Tanzania, Francis John anasema kuwa tangu awali wakati wa mazoezi aliahidi kurudi na medali kutoka katika michezo hiyo, lakini ilibaki kido tu wamenusurika kupata medali.

Anasema kuwa kutokana na maandalizi na muda wa Felix alijua mwanariadha wake huyo anaweza kufanya vizuri licha ya uchanga wake na kushiriki mashindano machache ya kimataifa.

Anasema yeye ndio alimuhamisha Felix kutoka katika mbio za meta 10,000 za uwanjani na kumuhamishia katika marathon baada ya kuona kuwa mwanariadha huyo alishindwa kuboresha muda wake katika mbio hizo.

“Mimi ndio nilimuhamisha mbio Felix kutoka zile za meta 10,000 za uwanjani na kumuhamishia marathon baada ya kuona alishindwa kuboresha muda wake, “anasema Francis katika mahojiano hayo maalum baada ya kurejea kutoka Brazil walikoshiriki Michezo ya Olimpiki ya Rio 2016.


Kiongozi wa Msafara wa timu ya Tanzania iliyoshiriki Michezo ya Olimpiki ya Rio 2016, Suleiman Jabir mara baada ya kutua kwenye Uwanja wa Kimataifa wa Ndege wa Julius Nyerere akiwa na mkewe.



Naye kiongozi wa msafara wa timu hiyo Suleiman Jabir anasema kuwa mashindano yalikuwa mazuri na Wabrazil walijiandaa vizuri ukilinganisha na uchumi wa nchi yao.

Jabir ameendelea kusisitiza kuwa wachezaji wetu waanze maandalizi mapema kwa ajili ya Michezo ya Olimpiki ya Tokyo 2020 ili tuweze kurudi na medali.

























Wadau nao walifika kwenye Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Dar es Salaam siku hiyo.


No comments:

Post a Comment