Friday 7 June 2019

Michezo Yote 52 ya Afcon 2019 Mubashara DStv



1.        Mwenyekiti wa Bodi ya kampuni ya MultiChoice Tanzania Balozi Ami Mpungwe {Kulia} sambamba na Mkurugenzi Mtendaji wa kampuni ya Jacqueline Woiso , akizungumza wakati wa hafla ya uzinduzi wa kampeni hiyo maalum ya Afcon 2019 ijulikanayo kama “DStv Tupogo”.


Na Mwandishi Wetu
HUKU zikiwa zimebaki siku chache kabla ya kuanza kwa fainali za Kombe la Mataifa ya Afrika, Afcon 2019, Misri, Kampuni ya MultiChoice Tanzania (DStv) imetangaza rasmi kampeni maalumu kwa Watanzania itakayowawezesha kushuhudia michezo yote 52 ya mashindano ya Kombe hilo mubashara kupitia chaneli za Supersport zilizo katika mfumo wa HD.

Akizungumza katika hafla ya kuzindua kampeni hiyo ya DStv ijulikanayo kama ‘DStv Tupogo’ hivi karibuni, Mkurugenzi Mtendaji wa MultiChoice Tanzania Jacqueline Woiso amesema wana furaha kubwa kupata fursa hiyo.

“Tuna furaha kubwa kwa nchi yetu kupata fursa ya kushiriki katika michuano hii ya kimataifa baada ya takribani miaka 39 toka iliposhiriki kwa mara ya mwisho mnamo mwaka 1980. Na kama ilivyo ada, ni jukumu letu na la kila Mtanzania kuhakikisha kuwa tunawatia moyo vijana wetu na kuifanya nchi yetu ifanye vizuri katika michuano hii ya kimataifa.
 
1.        Baadhi ya wachambuzi wa Kiswahili wa Supersport  wakiwa katika picha ya pamoja wakati wa utambulisho wa mchambuzi mpya mwadada Salama Jabir.


Kwa kuzingatia hilo DStv imehakikisha kuwa mechi zote 52 za michauano hii ya kimataifa ya Afcon 2019 itarushwa mubashara DStv kupitia chaneli za Supersport na kwa lugha adhimu ya Kiswahili  na katika mfumo wa HD. 

Zaidi ya hayo, DStv imehakikisha kuwa mechi hizo zinaonekana katika vifurushi vyote kuanzia kile cha  DStv Bomba cha Sh. 19,000 tu. “Tumehakikisha kuwa mechi hizi zinakuwepo hadi kwenye kifurushi cha chini kabisa ili kuwawezesha watanzania wengi kushuhudia mtanange huo na kuwa sehemu ya historia ya nchi yetu kwani tunashiriki baada ya zaidi ya miaka 30”, alisema Jacqueline.

Sambamba na uzinduzi huo pia ulifanyika utambulisho wa wachambuzi wa Kiswahili wa Supersport, ambapo kwa mara ya kwanza mwanadada Salama Jabir ataungana na timu hiyo katika kuongeza ladha na vionjo na hivyo kuongeza burudani na msisimko wa watazamaji. Wenginde ni wachambuzi mahairi akiwemo Aboubakar Liongo, Ibrahim Maestro, Edo Kumwembe, Maulid Kitenge pamoja na Oscar Oscar.

1.        Mkurugenzi wa Maendeleo ya Michezo Dk Yussuf Singo akizungumza wakati wa hafla ya uzinduzi wa kampeni maalum ya Afcon 2019 ya “DStv Tupogo”.

 Akielezea zaidi jinsi Watanzania watakavyopata uhundo huo,  Mkuu wa Masoko wa MultiChoice Tanzania, Ronald Baraka Shelukindo amesema, “Wateja wa DStv pia wateweza kupokea matangazo ya moja kwa moja kwa kupitia application ya “DStv Now” kupitia katika vifaa mbalimbali ikiwamo  simu ya mkononi, lap top au tablet na televisheni ya kawaida”. Amesema kwa kutumia DStv Now, mteja anaweza kuunganisha vifaa hadi vine kwa wakati mmoja bila grarama yoyote ya ziada katika kifurushi chake.

 Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Maendeleo ya Michezo Dk Yussuf Singo amesema kuwa kitendo cha DStv kuonesha mubashara michuano hiyo ni cha kupongezwa kwani ni sifa kubwa kwa nchi yetu. Pia amesema mchango mkubwa unaotolewa na MultiChoice Tanzania katika sekta ya michezo umechangia sana katika kukuza michezo na kuliletea taifa sifa kubwa.

1.        Baadhi ya wachezaji wa zamani timu ya Taifa walioshiriki katika mashindano ya Afcon 1980, wakiwa katika picha ya pamoja na Mkurugenzi na Maendeleo ya Michezo wizara  Dk Omar Singo sambamba na Mwenyekiti wa Bodi ya Kampuni ya Multihoice Tanzania,  Balozi Ami Mpungwe na Mkurugenzi Mtendaji wa kampuni hiyo, Jacqueline Woiso.

 “Serikali inathamini sana michango ya aina mbalimbali inayotolewa na wadau kama DStv katika kukuza michezo hapa nchini. Tunaamini kuwa kwa ushirikiano huu mafanikia haya ambayo tumeanza kuyapata yataendelea na tutafikia azma yetu ya kuwa taifa kubwa kimichezo duniani,” alisema Dk Singo.

Akiongea katika uzinduzi wa kampeni hiyo ya Tupogo Hussein Ngulungu moja kati ya wachezaji nguli waliowahi kushiriki katika michuano ya Afcon 1980, alisema kuwa, “Kwa mara ya kwanza baada ya takribani miongo minne, Tanzania imepata tena heshima kubwa ya kushiriki katika mashindano haya makubwa hivyo ni wajibu wetu sisi watanzania kuonyesha uzalendo na kuwatia moyo vijana wetu ili kuhakikisha wanafanya vyema katika michuano hii ili kuipatia sifa nchi yetu“ alisema Hussein.

Mbali na michuano ya Kombe la Afcon 2019 itakayoanza hivi karibuni, wateja wa DStv pia wataendelea kufurahia maudhui mbalimbali zikiwemo sinema na tamthilia mbalimbali kutoka nje na hapa nyumbani kama vile msimu mpya wa vichekesho vya Kitimtim, tamthilia ya HUBA, Rebeca kipindi maarufu cha Shilawadu Xtra na bila kusahau cha Maisha Yangu kinachoelezea maisha na mapito ya watu mashuhuri kutoka hapa nyumbani Tanzania vyote vikiwa vinapatikana kupitia chaneli ya Maisha Magic Bongo iliyopo katika kifurushi cha Bomba.

No comments:

Post a Comment