Wednesday 12 June 2019

Kwandika Awataka TAA Kufanya Kazi Kwa Ufanisi


Na Mwandishi Wetu, Dodoma
NAIBU Waziri wa Ujenzi Uchukuzi na Mawasiliano, Elias Kwandikwa  amewakumbusha  na kuwashauri Wafanyakazi  wa Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Tanzania (TAA) kuhusu ufanisi wa kazi na hatua zinazopaswa kuchukuliwa  ili Mamlaka hiyo  iweze kuongeza ufanisi wa kazi zaidi.

Akizungumza katika uzinduzi wa Mkutano Mkuu wa 23 wa  Baraza la Wafanyakazi leo Jijini  Dodoma Kwandikwa alisema  Baraza lina nafasi kubwa  ya kuishauri Mamlaka juu ya maslahi bora kwa Wafanyakazi.

“Naomba  mjadili changamoto mnazokutana nazo mahala pa kazi na katika utekelezaji wa mipango ili kuhakikisha mnatoa huduma bora kwa wananchi, pia mjadili kuhusu makisio ya mapato na matumizi ya Mamlaka”alisema.

Pia alitaka  Baraza hilo lisaidie katika kuleta maelewano kazini kwani Rasilimali  watu ni muhimu katika kusimamia Rasilimali zingine na mipango katika Taasisi.

“Lazima tufanye kazi kwa umoja ili tuweze kupiga hatua, kwahiyo uwepo wenu ni muhimu  katika kujadiliana namna ya kuendeleza Taasisi kwa kushirikiana”alisema.
 
Pia Kwandikwa alisema Baraza liweke mazingira ya kuongeza tija kwa Watumishi wanaotimiza majukumu yao ambapo lengo ni kutambua mchango wao na kuuthamini.

“Watumishi pia watimize majukumu yao kwa weledi kwa kuzingatia sheria kanuni na taratibu za Utumishi wa umma”alisema.

Katika hatua nyingine Kwandikwa amewataka wafanyakazi wa Mamlaka  wafanye  maandalizi juu ya ufunguzi wa Jengo la tatu la abiria.

“Endeleeni kufanya uchunguzi juu ya vihatarishi vinavyoweza kujitokeza baada ya kuanza matumizi ya jengo hilo,na  mshirikishane na kudhibiti mapema vihatarishi hivyo”alisema.

Pia aliwataka Watumishi sekta ya Anga kufanya kazi kwa weledi ili kuboresha huduma za usafiri wa Anga ili kuongeza ushindani wa Kitaifa na Kimataifa.

Pia alisisitiza kuwa ni  muhimu  Watumishi wa Mamlaka kujitambua kuwa  wanamchango katika kukuza pato la Taifa kutokana na huduma wanazotoa ambazo  zina  mchango Mkubwa katika ujenzi wa Taifa.

Awali, Mkurugenzi Mkuu Mamlaka ya Viwanja vya Ndege (TAA) Mhandisi Julius Ndyamukama kabla ya kumkaribisha mgeni rasmi aliainisha baadhi ya changamoto zinazoitatiza Taasisi kuwa ni maslahi duni kwa Wafanyakazi, uchache wa Wafanyakazi pamoja na nyenzo za ufanyaji kazi kama magari ya Zimamoto.

Ambapo Kwandikwa alisema “Serikali itafanyia kazi changamoto hizo ili kuhakikisha inaboresha sekta ya Usafiri wa Anga huku akitoa wa wito kufanya kazi kwa bidii na  weledi mkubwa huku akisisitiza Maazimio ya Baraza hilo yale ambayo yamekuwa changamoto yawe fursa ili yaweze kufanyiwa kazi.

Mkutano huo wa 23 wa Baraza kuu la Wafanyakazi unafanyika kwa kwa siku mbili katika ukumbi wa Takwimu Jijini hapa.

No comments:

Post a Comment