Saturday 15 June 2019

Amunike Atamba Kutinga Raundi ya Pili Afcon 2019


CAIRO, Misri
KOCHA wa timu ya taifa ya Tanzania, Taifa Stars, Mnigeria Emmanuel Amunike (pichani) amesema kuwa kikosi chake kitafanya kila kitu kuhakikisha kinacheza raundi ya pili ya mashindano ya Mataifa ya Kombe la Afrika (Afcon 2019).

Licha ya kucheza vizuri katika safu ya ulinzi, timu hiyo ya Tanzania ilipoteza mchezo wake wa kimataifa wa kirafiki kwa kufungwa 1-0 dhidi ya Misri uliofanyika Alhamisi jijini Alexandria ukiwa ni mchezo wao wa kwanza wa kujipima nguvu kabla ya kuanza kwa fainali hizo za Afcon 2019.

Fainali hizo za Mataifa ya Afrika zinafanyika nchini Misri kuanzia Juni 21 hadi Julai 19 na kwa mara ya kwanza zikishirikisha jumla ya timu 24 badala ya 16 za awali.

Tanzania inatarajia kucheza mchezo wake wa pili wa marudiano utakaofanyika leo Jumapili dhidi ya Zimbabwe, ikiwa ni wiki moja kabla ya kuanza kutimua vumbi kwa fainali hizo za Afcon 2019.

Taifa Stars imepangwa katika kundi gumu la C pamoja na vigogo wa Afrika, Senegal na Algeria pamoja na nchi jirani ya Kenya.

Amunike alithibitisha walipata kila walichotarajia katika mchezo wao dhidi ya Misri na aliahidi kuwa watafanya kila wawezavyo kucheza raundi ya pili ya mashindano hayo.

“Tulicheza vzuri dhidi ya Misri na kuwabana, tulifanikiwa. Lengo letu ni kuimarisha kikosi chetu kadiri tuwezavyo, “alisema gwiji huyo wa Zamalek na nyota wazamani wa Barcelona.

“Bila shaka tunacheza katika kundi ngumu, lakini tutafanya kila tuwezalo kufuzu kucheza raundi ya pili ya mashindano hayo.

“Sifikiri kama Senegal itakuwa timu dhaifu bila ya kuwa na Mane, ni mchezaji mkubwa lakini wana wachezaji wengine wakubwa katika kikosi chao, ambacho kinaweza kutwaa taji la Afcon, “alikamilisha maelezo yake.

Tanzania itaanza kampeni zake kwa kucheza mchezo wake wa kwanza katika fainali za mwaka huu za Afco baada ya kutocheza kwa miaka 39 Juni 23 kwa kucheza dhidi ya Senegal kwenye Uwanja wa Juni 30.

Wakati huohuo, nahodha wa Misri Ahmed Elmohamady alisema kuwa ushindi dhidi ya Taifa Stars ni muhimu inasaidia wachezaji, benchi la ufundi na hata mashabiki kujiamini kabla ya kuanza rasmi kwa faiali hizo za Afcon 2019.

Kocha alijaribu mifumo tofauti tofauti na kubaini baadhi ya kasoro ambazo atazifanyia kazi na kuhakikisha timu hiyo inafanya vizuri katika mashindano hayo yanayofanyika katika ardhi yao ya nyumbani.

Elmohamady ndiye aliyefunga bao pekee wakati Misri ikishinda 1-0 dhidi ya Tanzania kwa ajili ya maandalizi ya mashindano hayo.

Misri leo inacheza mchezo wa mwisho wa kirafiki dhidi ya timu ya Guinea ya Naby Keita.

No comments:

Post a Comment