Monday 14 March 2016

Mabingwa TP Mazembe waanza kwa sare na Saint George ya Ethiopia



CAIRO, Misri
MABINGWA wa Afrika wameanza kwa sare ya mabao 2-2 kutetea taji la Ligi ya Mabingwa ugenini dhidi ya Saint George ya Ethiopia katika mchezo wa kwanza wa hatua ya 32 bora.

Wakiwa chini ya kocha wao mpya Mfaransa Hubert Velud (pichani), Mazembe jana walijikuta katika wakati mgumu dhidi ya wapinzani wao hao wa Ethiopia.

Hatahivyo, mabingwa hao watetezi wameondoka Ethiopia wakiwa na faida ya mabao mawili ya ugenini kabla ya mchezo wa marudiano utakaofanyika wikiendi ijayo jijini Lubumbashi, Kongo.

Saint George walipata bao la kuongoza katika dakika ya 11 wakati Assefa Behaile alipowafanya wenyeji kuwa mbele kwa bao 1-0.

Mghana Daniel Nii Adjei aliisawazishia Mazembe, huku bao la kujifunga la Isaac Isiende yaliwapatia mabingwa hao watetezi uongozi wa mabao 2-1 hadi kipindi cha pili.

Saint George waliongeza presha kwa wapinzani wao na kufanikiwa kusawazisha kwa bao lililofungwa na Girma Adane na kufanya matokeo kuwa mabao 2-2.

Kwingineko katika mechi zilizofanyika Jumapili, kocha mpya wa Zamalek Alex McLeish alifurahia ushindi wa timu yake wa bao 1-0 dhidi ya Union Douala nchini Cameroon katika mchezo wake wa kwanza wa Ligi ya Mabingwa wa Afrika.

Kocha huyo wazamani wa Scotland, McLeish amekuwa kocha wan ne wa Zamalek msimu huu baada ya kocha Mreno, Mbrazil na Mmisri kutimuliwa katika timu hiyo.

Baada ya miaka kadhaa ya kupigania kutoshuka daraja England akiwa na timu ya Birmingham City na majirani zao wa Aston Villa, McLeish yuko mbioni kutwaa taji akiwa na Zamalek, ambayo imewahi kushinda taji la Afrika katika vipindi vitano.

Zamalek ilianza vizuri jijini Douala huku beki wa Burkina Faso Mohamed Koffi akifunga bao la ushindi katika dakika ya 59.

Jumamosi, Al Ahly, ambao ni majirani wa Zamalek walijikuta wakitoka suluhu dhidi ya Recreativo Libolo nchini Angola. Kwa sasa Ahly inafundishwa na Mholanzi Martin Jol kocha mwingine wa timu ya Ligi Kuu ya Uingereza.

Kwingineko, timu ya Nigeria ya Enyimba ilitawala mchezo wao wa nyumba dhidi ya Vital'O ya Burundi, baada ya kuibuka na ushindi wa mabao 5-1 katika mchezo uliopigwa Port Harcourt.

No comments:

Post a Comment