Tuesday 29 March 2016

Guinea ya Ikweta ya kwanza kutupwa nje mbio za Mataifa ya Afrika Gabon 2017


Mchezaji wa Libya, Sadik (kushoto) akigombea mpira na mchezaji wa São Tomé na Príncipe, Sousa Pontes wakati wa mchezo wa kufuzu kwa fainali za Kombe la Mataifa ya Afrika zitakazofanyika Gabon 2017 katika mchezo uliochezwa Cairo, Misri jana.

CAIRO, Misri
GUINEA ya Ikweta ambao mwaka jana walikuwa wenyeji wa fainali za Mataifa ya Afrika (Afcon), wamekuwa wa kwanza kutupwa nje ya mbio za kufuzu kwa fainali zile za Gabon 2017.

Timu hiyo imetupwa nje baada ya kupokea kichapo cha bao 1-0 kutoka kwa Mali.

Mustapha Yatabare ndiye aliyekuwa shujaa wa Mali baada ya kupachika bao katika dakika ya 89 katika mchezo uliofanyika Malabo na kuifanya timu yake kushika uongozi wa Kundi C, ikiwa pointi mbili juu ya Benin.

Guinea ya Ikweta, ambayo ilitinga nusu fainali ilipoandaa masindano hayo mwaka 2015, sasa wanashika mkia katika kundi lake hilo ikiwa na pointi moja huku zikiwa zimebaki mechi mbili kabla ya kumalizika mbio hizo za makundi.

Sudan Kusini ni ya tatu, wakiwa na pointi tatu, na wamebaki na nafasi finyu ya kufuzu kama moja ya timu bora zilizoshika nafasi ya pili.

Kwingineko, Zimbabwe iliisambaratisha Swaziland kwa mabao 4-0 katika mchezo wa kufuzu kwa fainali hizo kutoka katika Kundi L.

Wenyeji, walioambulia sare ya bao 1-1 na Swaziland katika mchezo wa Ijumaa, walitawala mchezo huo wa marudiano uliofanyika jijini Harare, Zimbabwe na kushika uongozi wa kundi wakiwa pointi tatu zaidi ya timu iliyopo katika nafasi ya pili.

Knowledge Musona ndiye aliyekuwa wa kwanza kufunga bao katika dakika ya 53 kwa penalti huku Costa Nhamoinesu akiifanya timu hiyo kuwa mbele kwa mabao 2-0 dakika sita baadae.

Evans Rusike aliongeza ushindi huo wa Zimbabwe huku Khama Billiat akikamilisha ushindi huo baada ya kufunga bao la nne.

Musona aliiambia BBC Sport: "Najisikia furaha sana. Timu yangu imekusanya pointi zote tatu nyumbani, sasa tunaongoza kundi letu na sasa tuna nafasi kubwa ya kufuzu.
Ni muhimu kuondoka na pointi zote tatu kutoka katika mchezo wetu uhao nyumbani (dhidi ya Malawi utakaofanyika Juni 3). 
Swaziland wanabaki wakiwa na pointi zao tano, tatu juu ya Malawi na Guinea ambao walitarajia kucheza jana.
Kila mshindi wa kundi na timu mbili zilizoshika nafasi bora za pili zitafuzu kwa fainali zijazo za Mataifa ya Afrika zitakazopigwa Gabon.

Katika Kundi B Jamhuri ya Afrika ya Kati ikiwa nyuma kwa bao moja, iliibuka na kuifunga Madagascar kwa mabao 2-1.
Faneva Andriatsima alikuwa wa kwanza kuwafungia wageni bao katika dakika ya 35 na kwenda mapumziko wakiwa mbele kwa bao 1-0.

Lakini mabao mawili yaliyofungwa ndani ya dakika 12, ambayo yalifungwa na Salif Keita katika dakika ya 53 na baadae Limane Moussa alipachika la ushindi.

Matokeo hayo yanaiweka Afrika ya Kati kileleni mwa msimamo wa kundi lao wakiwazidi Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo kwa pointi moja.

Libya walipata pointi za kwanza katika Kundi F baada ya kushinda mabao 4-0 dhidi ya Sao Tome e Principe.
Katika mchezo uliopigwa Misri kutokana na sabbau za kiusalama, Mohamed Zubya wa Libya alifunga hat-trick katika kipindi cha pili.

No comments:

Post a Comment