Saturday 21 March 2015

Maumivu yamuondoa Serena Indian Wells



CALFONIA, Marekani
SERENA Williams (pichani), amejitoa katika mchezo wake wa nusu fainali ya mashindano ya BNP Paribas Open kwa sababu ya maumivu ya goti la mguu wa kulia, imeelezwa.

Mchezaji huyo anayeongoza katika viwango vya ubora kwa upande wa wachezaji wakike, alitakiwa kucheza na Simona Halep wa Romania anayeshikilia nafasi ya tatu kwa ubora, katika nusu fainali ya pili.

Williams alikuwa akicheza kwa mara ya kwanza mashindano hayo katika kipindi cha miaka 14 cha kugomea mashindano hayo baada ya kumaliza mgomo wa kucheza mashindano hayo baada ya kushinda mwaka 2001 na baadae kuzomewa.

Halep sasa atakabiliana na Jelena Jankovic katika fainali ya mashindano hayo baada ya mchezaji huyo wa Serbia kumchapa Sabine Lisicki 3-6 6-3 6-1.

Katika ukurasa wake rasmi wa Instagram, Williams aliandika: "Miezi minne iliyopita nilianza safari ya kucheza mashindano ya Indian Wells na ilikuwa bomba.

"Kamwe sikuwahi kuota hilo. Lakini sikuweza kufanya hivi bila mashabiki.

"Ingawa nimehitimisha mapema kutokana na kuwa majeruhi mwaka huu, Napenda kusema siwezi kusubiri kujaribu tena mwaka ujao."

No comments:

Post a Comment