Tuesday 17 March 2015

Wenger aiponda Monaco licha ya kutolewa Mabingwa Ulaya


Arsene Wenger (kulia) akishika kichwa baada ya timu yake kutolewa katika Ligi ya Mabingwa wa Ulaya licha ya kuifunga Monaco 2-0.

MONACO, Ufaransa
KOCHA wa Arsenal Arsene Wenger anasema kuwa Monaco hawakustahili kabisa kupata nafasi ya kuchezahatua ya robo fainali ya Ligi ya Mabingwa wa Ulaya baada ya kushindwa kupiga shuti lililolenga goli katika mchezo wa marudiano uliofanyika Jumanne usiku.

Timu hiyo inayoshiriki Ligi Kuu ya Ufaransa ya Ligue 1 ilisonga mbele kwa faida ya bao la ugenini baada ya kuichapa Arsenal bao 3-1 katika mchezo uliofanyika kwenye uwanja wa Emirates kabla ya kufungwa 2-0 jijini hapa.
Alipoulizwa kama Monaco ilistahili nafasi hiyo ya kucheza robo fainali, Wenger alisema: "Siamini kabisa hilo.

"Endapo utaangalia idadi ya mashuti yaliyolenga goli waliyopiga utashangaa. Pamoja na kufungwa huwa kuna uma lakini sisi hatujashindwa."
Hatahivyo, kauli hiyo ya kocha Wenger inapingana na ile iliyotolewa na nahodha wake Per Mertesacker.
Mchezaji huyo wa timu ya taifa ya Ujerumani iliyotwaa taji la dunia alisema: "Timu bora imesonga mbele. Monaco ilistahili hilo kwa sababu walicheza vizuri zaidi mchezo wa kwanza.
"Tulikuja hapa na kujaribu kufanya kila kitu. Tungeweza kufunga zaidi ya mabao mawili. Tunajutia mchezo wa kwanza."
Huu ni mwaka wa tano mfululizo Arsenal inatolewa katika hatua ya 16 bora na kushindwa kucheza robo fainali ya Ligi ya Mabingwa wa Ulaya.

Vipigo vilivyopita timu hiyo ilivipata kutoka kwa Bayern Munich (mara mbili), AC Milan na Barcelona, Wenger alisema hii imesikitisha zaidi.

Kutolewa huku naweza kukuchukulia tofauti kabisa na vile vya miaka mingine, " alisema. "Hali nzima ilikuwa ni ya kusikitisha lakini endapo utaangalia mchezo usiku huu ulikuwa mzuri. Mchezo huu unaonesha jinsi tunavyofanya wakati huu."

Ushindi wa Arsenal ni wa nane katika mechi tisa na umemaliza mechi 17 za Monaco bila kufungwa nyumbani.
Lakini Wenger, ambaye aliwahi kuifundisha Monaco, alilalamikia matokeo yote kwa ujumla na hasa yalitokana na kutofanya vizuri katika mchezo wa kwanza.
Benchi la Monaco likishangilia baada ya filimbi ya mwisho licha ya timu yao kufungwa 2-0 na Arsenal katika mchezo wa Ligi ya Mabingwa wa Ulaya. Monaco imefuzu kucheza robo fainali baada ya kushinda 3-1 mchezo wa kwanza. 
Mchezaji wa Arsenal akifunga bao la kuongoza dhidi ya Monacho. Arsenal ilishinda 2-0.

No comments:

Post a Comment