Sunday 29 March 2015

Shule za Filbert Bayi zang'ara tena mbio za nyika Zanzibar


Wachezaji wa timu ya Shule ya Filbert Bayi wakipiga dua kabla ya kuanza kwa mbio za nyika za Zanzibar Jumamosi. Timu hiyo iling'ara katika mbio ilizoshiriki za kilometa nne na sita kwa wasichana wa shule za msingi na sekondari.

Na Cosmas Mlekani, Zanzibar
TIMU ya shule ya Filbert Bayi jana ilitamba katika mbio za nyika za shule za msingi na sekondari za Zanzibar baada ya kushika nafasi ya kwanza hadi ya tatu katika umbali wa kilometa nne na sita.

Mbio hizo za kila mwaka, mwaka huu zilishirikisha shule zaidi ya 30 za Unguja na shule ya Filbert Bayi ambayo ni pekee kutoka Tanzania bara iliyoshiriki.

Mwaka jana pia shule za Filbert Bayi za msingi na sekndari ndizo zilishinda katika mbio hizo ambazi husimamiwa na Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Amali kwa kushirikiana na Idara ya Michezo na Utamaduni.

Katika mbio za kilometa kwa wasichana wa shule za msingi, Teresia Joseph, Evodia Martin na Tumaini wote wa shule ya Filbert Bayi walishika nafasi ya kwanza hadi ya tatu kwa kutumia dakika 17:41:45, 17:1:40 na 17:55:10.

Wanariadha wakijiandaa kwa ajili ya mbio za nyika Zanzibar Jumamosi.
Mshindi wa nne wa mbio hizo alikuwa Nasra Khamis wa shule ya msingi Ndijani ya Zanzibar aliyetumia dakika 18:10:96.

Katika mbio za kilometa sita kwa wasichana; Dorcus Boniface wa shule ya Filbert Bayi aliibuka wa kwanza kwa kutumia dakika 27:17:12 huku Regina Deogras na Betrima Matiku nao wa Filbert Bayi walishika nafasi ya pili na tatu.

Katika mbio za kilometa sita wanaume; Hussein Said Hassa wa shule ya Ndijani alimaliza wa kwanza kwa kutumia dakika 24:03:94 huku Othman Yussuf Abdallah naye wa Ndijani alimaliza wa pili kwa kutumia dakika 24:40:18 na Aboubakar Ame Jecha alimaliza watatu kwa kutumia dakika 24:44:60.

Wasichana wa shule za msingi waianza mbio za nyika za kilometa nne Zanzibar Jumamosi.
Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Amali Ali Juma Shamhuna aliyekuwa mgeni rasmi katika mbio hizo aliisifu shule ya Filbert Bayi kwa ushindi ilioupata na kuzitaka shule zingine kuiga mfano wake.

Alisema, Bayi ambaye aliwahi kuvunja rekodi ya dunia ya mbio za mita 1500 ni mfano wa kuigwa kwa wanafunzi wake kuwa mahiri katika mchezo huo wa riadha hapa nchini.

Naye Waziri wa Habari, Utalii, Utamaduni na Michezo Said Ali Mbarouk alisema kuwa, michezo hiyo lazima iendelezwe ili kuinua vipaji vya wanafunzi wa shule za msingi na sekondari.

Mashindano hayo pia ni muendelezo wa jitihada na mapendekezo kutoka kwa Rais wa Zanzibar Dr. Ali Mohammed Shein akiwa ni miongoni mwa wakimbiaji wazuri wa mbio kama hizo akiwa mwanafunzi miaka ya nyuma.

No comments:

Post a Comment