Friday 22 November 2019

TAA Kujenga Madarasa Sekondari Wilaya Kibaha

Mwenyekiti wa Halmashauri ya Mji Kibaha, Leonard Mlowe (kushoto) leo akisalimiana na Kaimu Mkurugenzi wa Fedha na Biashara wa Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Tanzania (TAA), Josephine Kolola, ambaye alimwakilisha Mkurugenzi Mkuu, Mhandisi Julius Ndyamukama kutoa msaada wa mifuko 300 ya saruji kwa ajili ya ujenzi wa madarasa ya shule za sekondari. Kulia ni Mkurugenzi wa Mji Kibaha, Jenifer Omolo na kushoto ni Afisa Habari wa Mji Kibaha, Innocent Byarugaba.

Na Mwandishi Wetu, Kibaha
MAMLAKA ya Viwanja vya Ndege Tanzania (TAA), leo imetoa mifuko 300 ya saruji kwa ajili ya ujenzi wa madarasa ya shule za sekondari za Wilaya ya Kibaha, inayokabiliwa na upungufu wa madarasa 65.

Kaimu Mkurugenzi wa Fedha na Biashara wa TAA, Josephine Kolola aliyemwakilisha Mkurugenzi Mkuu, Mhandisi Julius Ndyamukama amesema Mamlaka hiyo inaunga mkono jitihada za serikali ya Awamu ya Tano, inayoongozwa na Mhe. Rais Dkt. John Pombe Magufuli za kutoa elimu bure kuanzia shule za msingi hadi sekondari, ambapo sasa kuongezeka kwa madarasa hayo kutachangia watoto wengi kupata elimu.

   Mkuu wa Wilaya ya Kibaha, Assumpter Mshama leo akizungumzia masuala mbalimbali ya wilaya hiyo, wakati wa hafla ya kuchangia mifuko 300 ya saruji, iliyotolewa na Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Tanzania (TAA), ambapo kulia ni Kaimu Mkurugenzi wa  Fedha na Biashara wa TAA,  Josephine Kolola, aliyemwakilisha Mkurugenzi Mkuu, Mhandisi Julius Ndyamukama.

“Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Tanzania, ipo bega kwa bega na jamii katika kuziunga mkono jitihada mbalimbali za maendeleo zinazofanywa na Serikali ya Awamu ya Tano, iliyopo chini ya Mhe. Dkt John Pombe Magufuli, ambapo inahakikisha vijana wengi wanapata elimu ya msingi na sekondari bure katika mazingira bora. Elimu wanayopata vijana wetu itawasaidia kukabiliana na changamoto za maisha kwa ajili ya ustawi wao na Taifa kwa ujumla,” amesema Kolola

Amesema katika kufanikisha jitihada hizo kwa vitendo na pia ni sera ya Mamlaka kurudisha kwa jamii kiasi cha mapato wanayozalisha ili waweze kutatua changamoto zinazowakabili, hivyo wametoa mifuko hiyo wakiwa na imani itasaidia kujenga madarasa hayo.

Amesema TAA ni taasisi ya serikali iliyoanzishwa kwa mujibu wa Sheria ya Wakala wa Serikali Na.30 ya mwaka 1997 na kupewa dhamana na Serikali ya kusimamia na kuendesha jumla ya viwanja 58 vilivyopo Tanzania Bara, ambapo Serikali inafanya jitihada kubwa katika kuboresha miundombinu mbalimbali Viwanjani ili viweze kuendana na mahitaji ya soko na ushindani wa kibiashara.

 Kaimu Mkurugenzi wa  Fedha na Biashara wa Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Tanzania (TAA),  Josephine Kolola, leo akizungumza na waandishi wa habari na watendaji wa Halmashauri ya Mji Kibaha (hawapo pichani), wakati alipomuwakilisha Mkurugenzi Mkuu wa TAA, Mhandisi Julius Ndyamukama na kukabidhi mifuko 300 ya saruji kwa ajili ya kujenga madarasa ya shule za sekondari za wilaya hiyo.


“Hivyo kupitia juhudi hizi za serikali zimezalisha fursa mbalimbali viwanjani zikiwemo fursa za kibiashara, ajira rasmi na zisizo rasmi”, amesema.

Naye Mkuu wa Wilaya ya Kibaha, Assumpter Mshama pamoja na kuishukuru TAA kwa msaada huo mkubwa, amesema katika Kampeni yao ya “Elimisha Kibaha”, wamekusudia kujenga madarasa 65, na kununua viti 3250 na meza 3250 ili kuweka mazingira bora ya kusoma kwa wanafunzi.

“Tunaupungufu mkubwa wa madarasa ambapo wanafunzi 700 wa kidato cha Kwanza mwaka huu (2019) wamekumbwa na kadhia hii, nasi tukaamua waingie darasani kwa awamu mbili asubuhi na mchana, lakini bado ikawa shida kutokana na kuwa na watoto wengi, ndio maana tukaanzisha kampeni hii kwa lengo la kupunguza na ikiwezekana kuondoa kabisa tatizo na watoto wasome katika mazingira bora,” amesema Mkuu huyo.

Mkuu wa Wilaya ya Kibaha, Assumpter Mshama (kushoto) akipokea mifuko 300 ya saruji kutoka kwa Kaimu Mkurugenzi wa Fedha na Biashara wa Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Tanzania (TAA), Josephine Kolola (kulia), katika hafla iliyofanyika leo nje ya jengo la Halmashauri ya Mji Kibaha. Kushoto ni Mkurugenzi wa Halmashauri hiyo, Jenifer Omolo.
Amesema hadi sasa tayari wamekusanya vifaa vya kutosheleza ujenzi wa madarasa 26, lakini bado hawajaanza ujenzi kutokana na fedha zilizowasilishwa Hazina kushindwa kutolewa hadi sasa kutokana na kuwa na utaratibu mrefu, ambapo amekuwa na hofu huenda hadi kufika Januari mwaka 2020 wakakumbwa na kadhia ya wanafunzi kushindwa kuendelea na kidato cha Kwanza kutokana na kukosekana na madarasa ya kutosha.

“Tunaomba huko tulipopeleka hizi fedha cash basi wazitoe ili ujenzi uanze mlolongo ni mrefu sana hatujui tatizo lipo wapi, na watui ndio kama hivi wanachangia vifaa tunashindwa kuanza ujenzi,” amesisitiza Mhe. Mkuu wa Wilaya.  

 Kamati ya Ulinzi na Usalama ya Wilaya ya Kibaha (kulia), ikiwa katika picha ya pamoja na Mkuu wa Wilaya hiyo, Assumpter Mshama (wapili kushoto), Mkurugenzi wa Halmashauri ya Mji Kibaha, Jenifer Omolo (kushoto), Katibu Tawala wa Mji Kibaha, Sosi Ngate (mwenye kilemba) wakiwa pamoja na Kaimu Mkurugenzi wa Fedha na Biashara wa Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Tanzania (TAA), Josephine Kolola aliyemwakilisha Mkurugenzi Mkuu, Mhandisi Julius Ndyamukama.


Hatahivyo, amemshukuru. Rais Dk John Pombe Magufuli kwa jitihada zake za kutoa elimu bure ambayo imesababisha mwamko mkubwa kwa wazazi wengi kuwapeleka watoto wao shule. Hali kadhalika kawashukuru wananchi, walimu na wadau wote waliojitokeza kuchangia kwa kutoa fedha taslimu, vifaa na ahadi, ambapo tayari wameshakusanya Shilingi milioni 950
.

Wednesday 20 November 2019

Wataalam Usafiri wa Anga Jumuiya ya Afrika Mashariki Wakutana Dar es Salaam


 Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Usafiri wa Anga Tanzania (TCAA), Hamza Johari (mbele), leo  kwenye ukumbi wa Watu Mashuhuri wa Kiwanja cha Ndege cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNIA-TBII), akifungua mkutano wa siku tatu wa Wataalam wa Usafiri wa Anga WA Jumuiya ya Afrika Mashariki, ambao wanajadili namna ya kuboresha huduma na miundombinu ya usafiri huo kwa nchi wanachama. Mkutano huo unashirikisha wajumbe zaidi ya 90.

Mkurugenzi wa Kiwanja cha Ndege cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNIA), Paul Rwegasha (aliyesimama kushoto)  akiwasilisha maelezo yanayohusu majengo matatu ya abiria ya Kiwanja hicho kwa Wataalam wa Usafiri wa Anga wa Jumuiya ya Afrika Mashariki, leo wameanza mkutano wa siku tatu wa kujadili namna ya kuboresha huduma na miundombinu ya usafiri huo kwa nchi wanachama.
Meneja wa Jengo la Tatu la Abiria la Kiwanja cha Ndege cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNIA-TBIII), Mhandisi Burton Komba (mwenye koti la bluu kushoto), leo akiwaelezea mifumo mbalimbali ya jengo hilo Wataalam wa Usafiri wa Anga wa Jumuiya ya Afrika Mashariki, ambao wanashiriki mkutano wa siku tatu wa kujadili namna bora ya kuboresha huduma na miundombinu ya usafiri huo kwa nchi wanachama.


Wataalam wa Usafiri wa Anga wa Jumuiya ya Afrika Mashariki, ambao wapo nchini kushiriki mkutano wa siku tatu wa kujadili namna bora ya kuboresha huduma na miundombinu ya usafiri huo, ambapo leo wametembelea majengo ya mizigo yaliyopo kwenye Kiwanja cha Ndege cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNIA).

Friday 15 November 2019

Mchezo Mpya wa Teq Ball Wazinduliwa Rasmi Nchini

Makamu wa Rais na Katibu Mkuu wa Kamati ya Olimpiki Tanzania (TOC), Henry Tandau (kushoto) na Filbert Bayi (kulia) wakiwa na Mkuu wa Uhusiano wa Kimataifa FITEQ, Marius Vizer Jr kabla ya uzinduzi wa mchezo huo Kibaha jana.

Na Mwandishi Wetu, Kibaha
MCHEZO mpya ujulikanao kama Teq Ball umetambulishwa rasmi Tanzania, ikiwa ni nchi ya kwanza katika Kanda ya Tano ya Afrika, imeelezwa.

Mchezo huo ulitambulishwa rasmi juzi katika Kituo cha Michezo cha Filbert kilichopo Mkuza Kibaha mkoani Pwani na wawakilishi wa Shirikisho la Kimataifa la Teq Ball (FITEQ), viongozi wa Kamati ya Olimpiki Tanzania (TOC), na viongozi wa kituo hicho pamoja na wanafunzi.

FITEQ imetoa meza tatu na mipira 12, ambapo mbili zitakuwa katika Kituo cha Olimpafrica, ambacho kinatumia vifaa vilivyopo katika Kituo cha Michezo cha Filbert Bayi mjini hapa.
Kwa Tanzania, meza mbili, moja ya TOC zitakuwa katika Kituo cha muda cha Olimpafrica kilichoko FBS Mkuza, nyingine Dole Zanzibar. Meza ya Zanzibar ilitarajia kukabidhiwa jana kisiwani humo.

Akizungumza katika uzinduzi huo, Mkuu wa Uhusiano wa Kimataifa FITEQ, Marius Vizer Jr, alisema shirikisho hilo makao yake makuu yako Hungary na sasa wako kwenye mikakati ya kuusambaza zaidi Duniani, baada ya kupata usajili wa kimataifa mwaka 2017.
Mwenyekiti wa Bodi ya Shule za Filbert Bayi, Fibert Bayi akizungumza wakati wa uzinduzi wa mchezo wa Teq Ball uliofanyika Mkuza, Kibaha jana.
Vizer Jr, alisema katika mikakati hiyo, mwaka huu wameingia mkataba na Kamati za Kitaifa za Olimpiki Afrika (ANOCAs), kuusambaza mchezo huo katika mashirikisho 40.
Hadi sasa nchi 14 tayari zimefikiwa na mchezo huo.

Alisema FITEQ itatoa Euro 6,000 (sawa na Sh 15,276,600) kwa mwaka kwa shirikisho la nchi husika kwa ajili ya uendeshaji, sambamba na kuendesha mafunzo kwa makocha na waamuzi.
Makamu Mwenyekiti wa Kamati ya Olimpiki Tanzania, TOC, Henry Tandau akipeana mkono na Mkuu wa Uhusiano wa Kimataifa FITEQ, Marius Vizer Jr wakati wa makabidhiano ya meza za mchezo huo Kibaha, Pwani jana. Kushoto ni Katibu Mkuu wa TOC, Filbert Bayi.
Naye Makamu wa Rais Kamati ya Olimpiki Tanzania (TOC), Henry Tandau, aliishukuru FITEQ na kusema kuwa historia imeandikwa kwa kuutambulisha mchezo huo.

Tandau, alisema wataitumia fursa hiyo kuhamasisha mchezo huo kwa kuundwa chama cha kitaifa, kuusambaza mikoani, kisha mashindano ya ngazi mbalimbali ili baadae uweze kuwa mchezo mkubwa nchini.
Alisema watajitahidi Tanzania ipate kuwa mwenyeji wa kwanza wa Fainali za Afrika za mchezo huo.

Naye Mwenyekiti wa Bodi ya Shule za Filbert Bayi (FBS), Filbert Bayi, mbali na kushukuru alisema watautendea haki msaada huo kwa kuhakikisha unachezwa na kuundwa timu mbalimbali.

Mchezo huo ni mchanganyiko wa Mpira wa Meza na Mpira wa Miguu, ambapo huhesabiwa kwa pointi zifikapo 20 kwa utofauti wa pointi mbili.
Huchezwa kwa mchezaji moja moja au wawili wawili, ukitumia meza iliyopinda, mpira kama wa miguu na viungo vya mwili miguu, kifua, mabega na kichwa, isipoluwa mikono hairuhisiwi.

Mchezaji hatakiwi kutumia kiungo kimoja mara mbili, pia kuugusa mpira zaidi ya mara tatu.
Mkurugenzi wa Shule za Filbert Bayi, Anna Bayi (kulia) akipiga mpira kwa kichwa wakati akicheza mchezo wa Teq Ball Kibaha mkoani Pwani jana. Kulia ni Makamu wa Rais na Katibu Mkuu wa Kamati ya Olimpiki Tanzania (TOC), Henry Tandau (kulia mbele) na Filbert Bayi. 
Na kabla ya uzinduzi wakufunzi wa mchezo huo kutoka hungary, Gondos Zoltan na Vasas Lea walionesha umahiri mkubwa wa kuucheza mchezo huo kwa kumiliki mpira na kuupiga kwa kutumia kichwa, mabega, miguu, magoti na viungo vingine isipokuwa mikono.
Mchezo huu uliasisiwa mwaka 2013 na umewahi kuchezwa na wanasoka maarufu Duniani kama akina Luis Figo na Ronaldihno Gaucho ambaye pia ndiye Balozi wa mchezo huo.

Usipime Usajili Kilimanjaro Marathon 2020


Na Mwandishi Wetu, Moshi
MAANDALIZI ya 18 ya Kilimanjaro Marathon 2020 yameanza kwa kasi huku ikiwa ni juu ya asilimia 30 ikilinganishwa na wakati kama huu mwaka jana, ikiwa ni ongezeko la asilimia 10 ndani ya wiki moja.

Mbali na mbio za kilometa 42, ambzo hudhaminiwa na wadhamini wakuu, Bia ya Kilimanjaro Lager, mbio zingine ni zile za kilometa 21 za Tigo na zile za Grand Malt za kilometa tano.

Kwa mujibu wa taarifa ya waandaaji, mwendendo ni mzuri na wamewataka washiriki kuchangamkia punguzo la bei litakalodumu hadi mwezi Januari mwakani. Washiriki wanajisajili kwa kupitia www.kilimanjaromarathon.com na kwa Tigopesa kwa kubonyeza *149*20#.

Mkurugenzi wa Mbio hizo nchini, John Bayo alisema kwa kupitia taarifa hiyo kuwa kuna idadi maalumu ya washiriki inayotakiwa kwa mbio zote tatu (Kilimanjaro Premium Lager Km 42, Tigo km 21 na Grand Malt Km 5) ili kuhakikisha kuwa mbio hizo zinaendana na viwango vya Shirikisho la Kimataifa la Riadha (IAAF) ili kuhakikisha usalama unazingatiwa.

Kwa mujibu wa Bayo, hii pia itahakikisha washiriki wanafurahia mbio hizo bila ya msongamano na pia kutoa nafasi kwa waandaaji waweze kutoa huduma zinazotakiwa katika njia ya mashindano na sehemu ya kumalizia pia.

Kuhusu punguzo la bei, waandaaji hao pia walitoa wito kwa washiriki wachangamkie utaratibu huo ambao ulianza Oktoba Mosi 2019 hadi Januari 14 , 2020.

Kwa raia wa Tanzania na wale kutoka nchi za Afrika Mashariki watalipa Sh 15,000 kwa mbio za kilometa 42 na 21 na Sh 5,000 kwa kilometa tano lakini kuanzia Januari 15, 2020 hadi Februari 16, 2020 washiriki watakaojisajili watalipa Sh 20,000 kwa kilometa 42 na 21 na Sh 5,000 kwa kilometa tano.

Kwa wageni wakazi au wenye vibali vya kuishi na kufanya kazi na wale wa nchi za SADC watalipa dola za Marekani 35 kwa kilometa 42 na 21 na dola tano kwa kilometa tano kuanzia Oktoba 1, 2019 hadi Januari 14, 2020, lakini kuanzia Januari 15, 2020 hadi Februari 16, 2020 wanaojisajili watalipa dola 45 kwa kilometa 42 na 21 na dola tano kwa kilometa tano.

Washiriki wa kimataifa watalipa dola 70 kwa kilometa 42 na 21 na dola tano kwa kilometa tano kuanzia Oktoba 1, 2019 hadi Januari 14, 2020 na kuanzia Januari 15 hadi Februari 16, 2020 watalipa dola 85 kwa marathon na nusu marathon na dola tano kwa kilometa tano.

Kwa mujibu wa waandaaji hao, usajili utafungwa rasmi saa sita usiku Februari 16, 2020 au pale ambapo idadi inayotakiwa itatimia.

Uzinduzi huo pia ulihudhuriwa na wawakilishi kutoka Chama Cha Riadha Tanzania, Baraza la Michezo Tanzania, Bodi ya Utalii Tanzania na wadau wengine wa riadha.

Washiriki pia walikumbushwa kuhusu vituo vya kuchukulia namba zao za ushiriki ambapo kwa Dar es Sallaam ni Mlimani City kuanzia Februari 22-23, 2020, Arusha ni Hoteli ya Kibo Palace kuanzia Februari 25-26 na Moshi ni Hoteli ya Keys kuanzia Februari 27-28.

 “Washiriki watatakiwa kujitambulisha na kuthibitisha kuwa wameshalipia kabla ya kukabidhiwa namba zao,” ilisema taarifa hiyo ya waandaaji.

Wadhamini wa mbio za Kilimanjaro Marathon 2020 ni Kilimanjaro Premium lager, Tigo, Grand Malt Kilimanjaro Water, TPC Limited, Simba Cement, Barclays Bank na watoa huduma rasmi ni Kibo Palace Hotel, Keys Hotel, GardaWorld Security, Precision Air na CMC Automobiles.

Mashindano ya Kilimanjaro Marathon yanayoandaliwa na Wild Frontiers na kuratibiwa kitaifa na Kampuni ya Executive Solutions,  yanatarajiwa kufanyika Machi 1, 2020 katika Chuo Kikuu cha Ushirika Moshi.

Uzinduzi wa Kilimanjaro Marathon 2020 ulifanyika hivi karibuni jijini Dar es Salaam na kuzinduliwa na Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Mjichezo, Dk Harrison Mwakyembe.


Wednesday 13 November 2019

Viwanja vya Ndege Nchini Kutumika Majira Yote

Ofisa Uhusiano wa Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Tanzania (TAA), Bahati Mollel akiwakaribisha waandishi wa Habari kutoka vyombo mbalimbali (hawapo pichani) kusikiliza Mafanikio yaliyofikiwa na TAA kwa kipindi cha Miaka Minne ya Serikali ya Awamu ya Tano, inayoongozwa na Rais Dk John Pombe Magufuli katika Kituo cha Mikutano cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNICC).


Na Bahati Mollel,TAA
VIWANJA vya Ndege Tanzania sasa vinaweza kutumika majira yote ya mwaka ya masika na kiangazi kutokana vingi barabara zake za kutua na kuruka ndege kujengwa kwa kiwango cha lami, imeelezwa.

Mkurugenzi wa Idara ya Uhandisi na Huduma za Ufundi, Mhandisi Mbila Mdemu ametoa maelezo hayo leo kwenye Kituo cha Mikutano cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNICC), alipozungumza na Waandishi wa Habari kutoka vyombo mbalimbali vya habari nchini, wakati alipozungumzia mafanikio ya Mamlaka hiyo kwa kipindi cha miaka minne ya Serikali ya Awamu ya Tano, inayoongozwa na Mhe. Rais Dkt. John Pombe Magufuli.
Kaimu Mwanasheria wa Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Tanzania (TAA), Pamela Mugarula akizungumzia muundo na kazi za TAA mbele ya waandishi wa Habari kutoka vyombo mbalimbali vya habari (hawapo pichani) leo wakati Mamlaka hiyo ilipozungumzia Mafanikio iliyofikia kwa kipindi cha Miaka Minne ya Serikali ya Awamu ya Tano, inayoongozwa na Rais Dkt John Pombe Magufuli katika Kituo cha Mikutano cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNICC).



 Mhandisi Mdemu amesema Mamlaka inajivunia mafanikio ya kuwa na viwanja 16 vyenye barabara za kutua na kuruka ndege za kiwango cha lami, ambazo zinaruhusu kutumika kwa kipindi chote cha mwaka bila matatizo ya aina yeyote.

Viwanja hivyo ni Arusha, Tabora, Mwanza, Bukoba, Mafia, Iringa, Songwe, Tanga, Moshi, Songwe, Kigoma, Dodoma, Mtwara, Mpanda pamoja Viwanja vya Ndege vya Kimataifa vya Julius Nyerere (JNIA) na Kilimanjaro (KIA). 

“Tangu kuanzishwa Mamlaka vilikuwepo viwanja nane pekee vyenye viwango vya lami, lakini sasa mpaka Novemba mwaka 2015 tumeweza kuongeza na kufikisha 16 ambavyo vinapitika kwa uhakika zaidi katika majira yote ya mwaka ya kiangazi na masika,” amesema Mhandisi Mdemu.

Mbali na barabara za kutua na kuruka ndege, pia Mamlaka hiyo imefanikiwa kufanya ukarabati na upanuzi wa majengo ya abiria na kufanikisha kuweza kuhudumia abiria wengi zaidi ya wa awali, ambapo ni pamoja na jengo la tatu la abiria la JNIA, Bukoba, Dodoma, Iringa, Mpanda, Mtwara na Mwanza.
Mkurugenzi wa Idara ya Uhandisi na Huduma za Ufundi wa Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Tanzania (TAA),  Mhandisi Mbila Mdemu akizungumzia mafanikio ya TAA kwa kipindi cha Miaka minne ya Serikali ya Awamu ya Tano inayoongozwa na Rais Dkt John Pombe Magufuli, katika mkutano na waandishi wa Habari wa vyombo mbalimbali vya habari (hawapo pichani) uliofanyika kwenye Kituo cha Mikutano cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNICC).


Pia Mhandisi Mdemu amesema mafanikio mengine ni kuboresha ulinzi wa kutosha wa abiria na mizigo, kwa kufungwa kamera za kufuatilia matukio, kuwepo kwa mashine za kukagua abiria na mizigo na kujengwa kwa uzio kwenye baadhi ya viwanja,; pia kumefungwa mifumo ya kisasa ya kiyoyozi; na  kuanza kusimikwa kwa taa za kuongoza ndege ili ziweze kutua usiku.

Naye Meneja Mipango na Takwimu wa TAA, Asteria Mushi amesema kuwa Mamlaka imeweza kupata mafanikio kwa kuongeza mapato kutoka Tshs. Bil. 63 kwa mwaka 2015 na kufikia Bil. 105 kwa mwaka 2018, ambazo ni ongezeko la asilimia 66, ambapo lengo la Mamlaka ni kuongeza mapato na kufikia Tshs. Bil. 130 ifikapo mwaka 2020; pia wameweza kuongeza biashara za maduka na sasa serikali wanashirikiana na taasisi binafsi kujenga hoteli ya nyota nne yenye ghorofa nane (8) itakayojengwa karibu na jengo la pili la abiria (JNIA-TBII).

Hali kadhalika Mushi, amesema Mamlaka imeongeza idadi ya ndege za abiria ambazo awali zilikuwa zikifanya safari nchini, lakini baadaye zikasitisha na zimeanza tena safari hizo, ambazo ni Air Uganda na Zimbabwe. Ndege hizo zinafanya idadi ya ndege za nje kufikia 21.
Meneja wa Mipango na Takwimu wa Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Tanzania (TAA), Asteria Mushi (kulia) leo akizungumzia ongezeko la mapato kwenye Viwanja vya ndege mbele ya waandishi wa habari wakati Mamlaka hiyo ilipoelezea mafanikio yake kwa kipindi cha miaka minne ya Serikali ya Awamu ya Tano inayoongozwa na Rais Dkt. John Pombe Magufuli katika Kituo cha Mikutano cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNICC) jijini Dar es Salaam.

“Katika viwanja vya ndege tumetenga asilimia 30 kwenye majengo ya abiria tumetenga huduma za abiria na biashara, lakini tunaangalia na ongezeko la ndege za Air Tanzania ambapo sasa zinakwenda njia 10 za ndani ya nchi na njia tano za kimataifa,” amesema Mushi.

Friday 8 November 2019

Bombardier Nayo Kutua Kiwanja cha Arusha


Na Mwandishi Wetu
NDEGE aina ya Bombardier zitaweza kutua katika Kiwanja cha Ndege cha Arusha baada ya kukamilika mpango wa kuongezwa barabara ya kutua na kuruka ndege, imeelezwa.

Hayo yalisema bungeni mjini Dodoma juzi na Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, Mhe. Issac Kamwelwe wakati akijibu swali la Mhe Husna Malima, Mbunge wa Kigoma Kusini aliyetaka kujua Serikali ina mpango gani kuboresha Kiwanja cha Ndege cha Arusha ili ndege kubwa ziweze kutua.

Malima alisema kuwa kuongezwa kwa uwanja huo kutawawezesha wananchi wa mikoa ya Singida, Manyara, Simiyu, Mara na Dodoma kuamasika kutumia usafiri wa ndege, ambao unatosheleza kwa sasa?


Amesema mafaniko ya uwepo wa ndege nyingi za abiria nchini ni pamoja na ndege hizo kutumika kwa wananchi kuzipanda.

Kamwelwe amesema kurefushwa huko kutafanikisha ndege aina ya Bombardier ambayo inabeba abiria kuanzia 70 kutua na kuruka bila tatizo kwenye kiwanja hicho kilichopo Kisongo mkoani Arusha.


Amesema tayari bajeti imetengwa kwa ajili ya kazi hiyo, ambapo kiwanja hicho ni cha tatu nchini kwa kutua na kuruka ndege nyingi, ambapo hutua ndege zaidi ya 125 kwa siku.

“Tumeweka bajeti kuendeleza kiwanja cha ndege cha Arusha na tayari tenda imetangazwa, kiwanja hiki kinaongoza kwa kutua ndege nyingi zaidi kwa siku ni biashara kubwa na ndio maana tunataka ndege ya Bombardier itue hapo,” alisisitiza Mhe. Kamwelwe.

Amesema mikoa jirani na Arusha ya Manyara, Singida, Dodoma, Simiyu na Mara itafaidika na maboresho ya kiwanja hicho kwa kuwa wataweza kukitumia ipasavyo.

Naye Meneja wa Kiwanja hicho, Mhandisi Elipid Tesha amesema barabara ya kutua na kuruka ndege itaongezwa urefu kwa meta 200, ambapo sasa ina urefu wa meta 1600 na itakuwa 1800, na pia patajengwa eneo la kugeuza ndege.

Mhandisi Tesha amesema kwa sasa kazi inayoendelea ni ujenzi wa eneo la maegesho ya ndege (Apron), ambayo yakikamilika yatapunguza msongamano kwa asilimia 30; pia barabara ya kupita ndege kwenda katika maegesho (taxiway);  ujenzi wa maegesho ya magari yapatayo 350 kwa kiwango cha lami.

Pia ujenzi wa mfumo wa malipo ya maegesho hayo unaendelea sambamba na ule wa maegesho ya magari.

Pia amesema ujenzi huo wa maboresho ya kiwanja cha ndege cha Arusha utahusisha ujenzi wa eneo la kupumzika abiria, ofisi za waegesha ndege (mashellers), kibanda cha ulinzi na vyoo.

Monday 4 November 2019

Mwakyembe Azindua Kili Marathon 2020 Awataka Wanariadha wa Tanzania Kuchangamkia Zawadi


Na Mwandishi Wetu
WAZIRI wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Dk Harrison Mwakyembe amewataka watanzania kujitokeza kwa wingi kushiriki mbio za 18 za Kilimanjaro zitakazofanyika Machi mwakani,

Mwakyembe pia aliwataka wanariadha wa Tanzania kufanya maandalizi ya uhakika ili kuhakikisha wanafanya vizuri katika mbio hizo, ambazo ni kubwa zaidi hapa nchini na hushirikisha watu wengi kutoka ndani na nje ya nchi.

Akizungumza jijini Dar es Salaam mwishoni mwa wiki wakati wa uzinduzi wa mbio hizo, ambazo zitafanyika mjini Moshi Machi mosi, 2020, mwakyembe alisema ni aibu kwa zawadi zote kwenda nje ya nchi, hivyo aliwataka wanariadha wa Tanzania kujiandaa vizuri ili kuhakiisha zawadi hizo zinabaki nchini.

Mwakyembe aliwapongeza wadhamini wa mbio hizo wakiongozwa na Kilimanjaro Premium, ambao hudhamini mbio za kilometa 42, Tigo (kilometa 21), Grand Malt (kilometa 5), ambazo ni mbio za kujifurahisha na hushirikisha watu wengi.

“Inatia moyo sana kuona kuwa Kilimanjaro Marathon sasa ina washiriki zaidi ya  11,000 kutoka nchi zaidi ya 56 kote duniani. Hili ni jambo zuri sana kwa taifa, kwani tunapata fedha za kigeni kutokana na matumizi yanayofanywa na wageni hawa nchini, ikiwemo utalii, “alisema.

Rais wa Shirikisho la Riadha Tanzania (RT), Anthony Mtaka, alitoa wito kwa washiriki wazalendo kuchangamkia zawadi zinazotolewa na Kilimanjaro Marathon badala ya kukimbilia kushiriki mbio za nje, ambazo zawadi zake ni ndogo.

 “Ni vizuri kwenda kupata exposure lakini tusiache zawadi nzuri nyumbani na kufuata hela ndogo huko nje wakati tunaweza kuzipata hapa hapa nchini, “alisema Mtaka.

Meneja wa Bia ya Kilimanjaro Premium Lager, Pamela Kikuli, alisema tangu mashindano yaanze Kilimanjaro Premium Lager imewekeza hela nyingi sio tu kusukuma mauzo ambayo wamefanikiwa kwa kiasi kikubwa, lakini pia kutengeneza ajira na kuchangia uchumi kwa ujumla kupitia gharama za kuyatangaza, promosheni na masuala mengine ya kimasoko.

Naye Meneja Mawasiliano wa Tigo, Woinde Shisael alisema kampuni yake inajivunia kudhamini mbio za kilometa 21 kwa mwaka wa tano mfulululizo, ambayo ni sehemu ya mbio hizo. “Tunajivunia kuwa sehemu ya tukio hili kubwa ambalo linawaleta pamoja wanariadha wakubwa, “alisema.

Wadhamini wengine katika Kilimanjaro Marathon ni pamoja na Kilimanjaro Water, Barclays Bank, Simba Cement, TPC Sugar, Precision Air, Kibo Palace Hotel, Garda World Security, Keys Hotel na CMC Automobiles.

Kwa mujibu ya waandaaji wa Kilimanjaro Marathon-Wild Frontiers na Executive Solutions, usajili umeshaanza kwa mtandao kupitia www.kilimanjaromarathon.com.

Uzinduzi huo pia ulihudhuriwa na mwenyekiti na kaimu katibu mkuu wa Baraza la Michezo la Taifa, Leodegar Tenga na Neema Msitha, kaimu msaijili wa michezo nchini, Mwita, Bodi ya Utalii na wadau wengine swa mchezo wa riadha.

TAA Kufanikisha Mazingira Bora ya Kujisomea Wanafunzi 1560

Skauti wa shule ya Sekondari ya Ilala (kushoto) akimvisha skafu mgeni rasmi wa mahafali ya 13 ya shule hiyo, Bi. Harieth Nyalusi, Kaimu Meneja Biashara na Masoko wa Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Tanzania (TAA), aliyemwakilisha Mkurugenzi Mkuu Mhandisi Julius Ndyamukama. Mahafali hayo yamefanyika hivi karibuni.



Na Bahati Mollel,TAA
WANAFUNZI 1560 wa shule ya sekondari ya Ilala ya Jijini Dar es Salaam, watasoma kwa furaha baada ya Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Tanzania (TAA), kukubali kufanya ukarabati wa jengo la maktaba, ambalo ni chakavu.


Ahadi hiyo imetolewa hivi karibuni na Kaimu Meneja Masoko na Biashara wa TAA, Harieth Nyalusi ambaye alikuwa mgeni rasmi wa mahafali ya 11 ya shule hiyo, akimwakilisha Mkurugenzi Mkuu, Mhandisi Julius Ndyamukama.

Nyalusi alisema kuwa Mamlaka inaunga mkono jitihada kubwa zinazofanywa na Mhe. Rais wa Jamhuri wa Muungano wa Tanzania, Dkt. John Pombe Magufuli za kutoa elimu bure, ambapo sasa itaungana naye katika kukarabati chumba hicho cha maktaba, ili kuwezesha wanafunzi kusoma katika mazingira bora, yatakayochangia kufanya vyema katika masomo yao na katika  mitihani ya kidato cha pili na yake ya kuhitimu kidato cha nne.

     Mwanafunzi Diana Seth wa shule ya sekondari ya Ilala (kulia) akionesha moja ya majaribio katika maabara ya Biolojia, wakati wageni waalikwa pamoja na mgeni rasmi wa mahafali ya 13 ya shule hiyo, Bi. Harieth Nyalusi kutoka Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Tanzania  (wa pili kushoto), akimwakilisha Mkurugenzi Mkuu, Mhandisi Julius Ndyamukama walipotembelea maabara hiyo.


“Pamoja na kuunga juhudi za Mhe. Rais pia ni sera ya taasisi yetu kutoa kwa jamii katika kusaidia kutatua changamoto zinazozibabili jamii hizo, hivyo kama Mamlaka tutasaidia kufanya ukarabati wa ndani wa jengo hilo ambalo limekuwa chakavu, linalosababisha ari ya kusoma kushuka,” amesema.

Pia alisema Mamlaka inatambua jitihada kubwa inayofanywa kwa kushirikiana kwa Walimu, wazazi na wanafunzi katika kuhakikisha shule inaboresha utoaji wa elimu bora na ufaulu wa wanafunzi wa mitihani yao ijayo kuongezeka.

Hatahivyo, ametoa wito kwa wahitimu wa kidato cha Nne 2019 kuhakikisha wanaweka nia thabiti ya kujiendeleza zaidi kwa wale watakaobahatika kuchaguliwa  kwenda kidato cha Tano na vyuo mbalimbali, na ambao hawatabahatika waangalie nyanja mbalimbali za elimu ili kujitengenezea wigo mpana wa uwezo wa utambuzi wa kubadilisha changamoto zinazoizunguka jamii kuwa fursa.

  Kaimu Meneja wa Biashara na Masoko  wa Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Tanzania (TAA), Bi. Harieth Nyalusi (aliyesimama), akiwakilisha salamu kutoka kwa Mkurugenzi Mkuu, Mhandisi Julius Ndyamukama wakati wa mahafali ya 13 ya shule ya sekondari ya Ilala ya Jijini Dar es Salaam, yaliyofanyika hivi karibuni.
“Ikumbukwe kuwa vijana ni hazina ya Taifa, hivyo napenda kuwasisitiza kuwa thamani yako kama kijana iko mikononi mwako, ishi kwa malengo, jitambue, jithamini, jilinde na ujitunze kwani wewe ni wathamani kuwa na Taifa linakutegemea,” amesema.

Akiizungumzia TAA, Nyalusi amesema imepewa jukumu la kusimamia na kuendeleza viwanja vya ndege 58 vilivyopo Tanzania Bara kati ya hivyo ni viwanja vya Kimataifa vya Julius Nyerere (JNIA) na Kilimanjaro (KIA), ambavyo ndivyo milango mikuu ya kuingia nchini kwa kutokea nje ya nchi.

Amesema katika viwanja vya ndege kuna fursa mbalimbali za kibiashara, ajira rasmi na zisizo rasmi, ambapo amewataka vijana wanaohitimu kuzichangamkia ajira na fursa hizo pindi zitakapotangazwa.

Wanafunzi skauti wa shule ya sekondari ya Ilala wakionesha ukakamavu kwa kupasuliwa tofali kichwani katika sherehe za mahafali ya 13 ya shule hiyo yaliyofanyika hivi karibu.


Kwa upande wa risala ya wahitimu, imeeleza kuwa shule hiyo iliyoanzishwa miaka 13 iliyopita pamoja na kufanya vyema kwenye mitihani yao ya taifa ya kumaliza kidato cha nne kila mwaka, imekuwa ikikabiliwa na changamoto mbalimbali ikiwemo ya upungufu wa vyoo vya wanafunzi, ambapo yapo matundu 18  kati ya 72 yanayohitajika; ukosefu wa maabara mbili za masomo ya Biolojia na Fizikia ambazo ujenzi wake haujakamilika.

Changamoto nyingine ni uchakavu wa majengo ya shule ikiwemo kuvuja kwa paa na ubovu wa sakafu madarasani; uchakavu wa rangi katika majengo yote ya shule; ukosefu wa chumba maalum cha watoto wa kike na wagonjwa pindi wapatapo matatizo wanapokuwa eneo la shule; ukosefu wa vifaa vya teknolojia na mawasiliano zikiwemo komputa, projeta, mashine za kurudufia na ‘printer’.

 Mmoja wa skauti wa shule ya sekondari ya Ilala ya Jijini Dar es Salaam akizuia pikipiki mbili kwa mikono na kichwa katika sherehe za mahafali ya 13 ya shule hiyo yaliyofanyika hivi karibuni.

Risala hiyo imeainisha pia changamoto za ukosefu wa jengo la ofisi za walimu, ambapo sasa wanatumia madarasa mawili kama ofisi jambo ambalo pia kumesababisha kuwe na upungufu wa madarasa; uchakavu wa maktaba na ukosefu wa vifaa muhimu ndani ya maktaba zikiwemo meza, viti, vitabu vya kiada na ziada, makabati; ukosefu wa kantini bora ya shule na ukosefu wa bwalo.
Mwanafunzi Salvatory Jeremia (kushoto), akipokea cheti cha kuhitimu kidato cha nne kutoka kwa mgeni rasmi Bi. Harieth Nyalusi, Kaimu Meneja Biashara na Masoko wa Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Tanzania (TAA), aliyemwakilisha Mkurugenzi Mkuu, Mhandisi Julius Ndyamukama.  (Picha zote na Bahati Mollel wa TAA).
Pamoja na changamoto hizo, wahitimu hao wameahidi kufanya vyema katika mitihani yao ya kuhitimu kidato cha nne, ambapo kila mwaka ufaulu umekuwa ukiongezeka ambapo sasa umefikia asilimia 70.

   
Wahitimu wa kidato cha Nne katika shule ya sekondari ya Ilala wakiimba wimbo wa kuwaaga wenzao pamoja na walimu katika mahafali yao yaliyofanyika hivi karibuni  jijini Dar es Salaam.