Thursday 22 September 2016

Mkuu wa mkoa wa Mwanza aizawadia Sh. milioni 1 KILIMANJARO QUEENS



MKUU wa mkoa wa Mwanza John Mongela akiwapongeza wachezaji wa Kilimanjaro Queens walipowasili jijini Mwanza leo kabla ya kupanda ndege kwenda Dar es Salaam.

Na Mwandishi Wetu, Mwanza
MKUU wa mkoa wa Mwanza John Mongela ameipongeza timu ya taifa ya wanawake ya Tanzania Bara, The Kilmanjaro Queens baada ya kuchukua ubingwa wa michuano ya Afrika Mashariki na Kati (Cecafa) iliyomalizika Jinja, Uganda hivi karibuni.

Timu hiyo ilitwaa ubingwa wa mashindano hayo ya kwanza ya wanawake kuandaliwa na Cecafa baada ya kuifunga timu ya soka ya Kenya kwa mabao 2-1 katika mchezo wa fainali uliochezwa jijini Jinja, Uganda.

Katika mapokezi hayo ya timu timu hiyo mkoani hapa,Mongela alizawadia timu hiyo shilingi milioni 1 kama pongezi.

Mongela amepongeza pia Chama cha Soka cha Wanawake(Twfa) kwa juhudi zao mpaka timu hiyo imechukua ubingwa.

Mongela ameiomba timu hiyo ihakikishe inafanya juhudi kuhakikisha wanaendelea kuwa mabingwa. Mwenyekiti wa soka la wanawake nchini(TWFA) Amina Karuma ameomba makampuni yaendelee kujitokeza katika kudhamini soka la wanawake.

Karuma pia amepongeza kampuni ya Airtel na Azam kwa juhudi zao za kusaidia timu hiyo wakati ilipokuwa Uganda.

Karuma amesema ushindi huo umetokana na matunda ya michuano ya Airtel Rising Star, ambapo wameweza kupata wachezaji.

Kwa upande wake kocha mkuu wa timu hiyo Sebastian Mkomwa amesema michuano hiyo ilikuwa migumu sana kwa kuwa waliohofia timu za Kenya na Ethiopia kutokana zimecheza michuano ya Afcon kwa wanawake. 

"Mashindano yalikuwa magumu sana kutokana na tumefanya mazoezi ya zima moto tulijiandaa wiki moja kabla ya mashindano,kingine kilichotugharimu ni urefu wa safari kutoka Dar-es-salaam mpaka Jinja kwa bus".

Mkomwa ameomba wachezaji wawe wanaingia kambini mapema sana ili kujianda mapema katika mashindano yoyote yale.

Nahodha wa timu hiyo,Sophia Mwasikili ameiomba Serikali iwekeze zaidi katika soka la wanawake hiyo itasaidia soka la wanawake kufanya vizuri.

Mwasikili amesistiza wachezaji wawe wanajaliwa zaidi katika kupewa posho zao na mishahara kwa wakati italeta motisha kwa wao kufanya vyema.

Mfungaji kutokea timu hiyo,Mwanahamisi Omary'Gaucho' ambae amefunga magoli matatu amesema yeye aliweka malengo ni lazima ahakikishe kila mechi anafunga ili kusaidia timu yetu kufanya vyema. 

Wachezaji wa Kilimanjaro queens waliofunga magoli ni Asha Rashid magoli matatu,Donasia Donald mawili, Stumai Rajab magoli mawili.

Wachezaji walioshinda ubingwa huo ni  Fatuma Omary,Sophia Mwakisili,Anastazia Anthony,Fatuma Issa,Fadhila Hamad,Donisia Donald,Happy Hezron na Asha Rashid.

Wengine ni Wema Richard,Mwanahamisi Omari,Maimuna Hamis,Fatuma Hassan,Amina Ally,Sherida Boniface,Anna Hebron,Najat Abass na Fatuma Bashir.

No comments:

Post a Comment