Tuesday, 24 March 2020

Makonda apongeza TAA kwa kujidhatiti kwa corona

·       Ataka wananchi kufuata masharti yaliyotolewa
·       Asema kuanzia kesho mitaa kupuliziwa dawa
 
Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Paul Makonda akipimwa joto alipotembelea Kiwanja cha Ndege cha Kimataifa cha Dar es Salaam (JNIA). 
Na Bahati Mollel,TAA
MKUU wa Mkoa wa Dar es Salaam, Paul Makonda ameipongeza Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Tanzania (TAA), kwa kujipanga vyema kwa kushirikiana na wahudumu wa afya kwa kuweka maji yenye dawa maalum ya kunawa mikono na kupima joto la mwili kwa watu wote wanaoingia na kutoka maeneo ya viwanja vya ndege, ili kuzuia kuingia zaidi kwa watu walioambukizwa ugonjwa wa homa kali ya Mapafu inayosambazwa na virusi vya corona (COVID19).

RC Makonda ametoa pongezi hizo leo alipofanya ziara kwenye Kiwanja cha Ndege cha Kimataifa cha Julius Nyerere, ambapo alianzia jengo la Tatu la abiria ambalo linahusisha zaidi ndege zinazotoka nje ya nchi, na baadaye kwenda Jengo la Pili la abiria lenye ndege zenye safari za ndani ya nchi na pia nje ya nchi.

Amesema ameridhishwa na hatua zilizochukuliwa na TAA kwa kuhakikisha hakuna ongezeko la watu walioambukizwa wanaoweza kuingia nchini kupitia Kiwanja hiki.

“Nimejionea mwenyewe kila kona kumewekwa sanitizers, na pale nje lipo tanki kubwa lenye maji yenye dawa lazima kila mtu anawe, na hata huku ndani abiria wanaowasili na wanaoondoka wanapimwa joto la mwili kwa mashine ya mkono na ile ya scanner, hivyo ninaimani kwa udhibiti huu hakuna maambukizi zaidi yanayoweza kutokea,” amesema Mhe. Makonda.

Hatahivyo, amesema pia kuanzia tarehe 25 Machi, 2020 asilimia 98 ya ndege zenye safari za nje hazitaingia nchini baada ya zenyewe kufuta safari zao kutokana na kukosekana kwa abiria, hivyo itasaidia kwa asilimia 80 ya abiria kupungua kuingia kwa kuwa ni nchi nyingi zimeweka makatazo na kufunga mipaka yao.

“Sisi hatujafunga mipaka lakini hadi sasa idadi ya abiria wakigeni imeshuka kwa kiasi kikubwa mfano ndege yenye kubeba abiria 250 sasa inabeba abiria 20, hivyo asilimia 80 ya abiria aidha wenyewe kutokana na elimu waliyopata kutokana na huu ugonjwa wameona hakuna sababu ya kusafiri na wengine baada ya kuona masharti yaliyowekwa ya kwenda nchi moja ama nyingine wakaamua kukaa majumbani mwao, na hii inadhihirisha jinsi gani Mhe. Rais John Pombe Magufuli aliposema kuwa kama unaona safari haina ulazima basi usiende,” amesisitiza Mhe. Makonda.

Pia amesema mashirika ya ndege yamekuwa na ushirikiano na JNIA kwa kutoa taarifa kabla ya kutua endapo wanaabiria mwenye kuhisiwa anaugua ugonjwa huo, na ikifika taratibu za kumpeleka katika kituo kilichoteuliwa zinachukuliwa.

“Tunashukuru sana tena na tena hapa JNIA wamesema hata idadi ya wasindikizaji imepunguzwa ili kuondoa kabisa msongamano katika majengo ya abiria, maana wakiwa wengi itakuwa shida zaidi endapo yupo ambaye anamaambukizi,” amesema.

Pia amesema kwa sasa abiria wote wanaowasili kutoka kwenye nchi zilizokuwa na maambukizi wanapekelekwa kwenye hoteli na hosteli zilizoteuliwa na mkoa kwa ajili ya uchunguzi zaidi kwa siku 14 kwa gharama zao wenyewe. Katika hatua nyingine amesema leo abiria 200 wa nchi ya Comoro wamezuiwa kuondoka baada ya nchi yao kufunga mpaka kutokana na kuzuia maambukizi ya corona.

Pia amewataka watu wote wanaoingia na kutoka nchini kwa kutumia usafiri wa ndege, mabasi na meli kufuata utaratibu uliowekwa na Mamlaka za juu ili kuepukana na maambukizi, ambapo pia amesema katika usafiri wa umma (Daladala) watu wasipande likiwa limejaa kupita kiasi na amesisitiza kuwa ugonjwa huu hauna umri kuwa vijana hawafi,  hivyo wanajidanganya na wachukue tahadhari zilizowekwa.

Hali kadhalika amesema wananchi na watu wote kutokuwa na hofu kuanzia kesho Jumatano tarehe 25 Machi, 2020, Ofisi yake kwa kushirikiana na Maafisa Afya watapulizia dawa kwenye mitaa ili kuua wadudu mbalimbali; na ofisi yake itaendelea kutoa elimu ya kujikinga na maradhi ya corona.

Naye Mkurugenzi wa JNIA, Paul Rwegasha amesema wameendelea kutoa elimu kwa watu wote wanaoingia na kutoka kwenye kiwanja hicho kwa kuweka mabango yanayoelekeza namna ya kujikinga, na pia wameweka sabuni maalum za kunawa mikono wanapoingia na kutoka maeneo hayo.
  

Wednesday, 18 March 2020

Corona Yazidi Kutikisa Soka la Ulaya


ZURICH, Uswisi

 SHIRIKISHO la Soka la Ulaya (Uefa) limeahirisha mashindano ya Mataifa ya Ulaya, Euro 2020 hadi Juni na Julai mwaka 2021, kutokana na kusambaa kwa virusi vya corona.

Hatua hiyo ya kusogeza mbele mashindano hayo makubwa barani Ulaya kwa timu za taifa, ilifikiwa jana Jumanne katika kikao cha dharura kilichofanyika kwa njia ya video.

Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa mapema jana na Chama cha Soka cha Norway, mpango huo mpya umepanga mashindano hayo kufanyika kwa mwezi mmoja kuanzia Juni 11 hadi Julai 11.

Uamuzi huo wa Uefa umetoa nafasi kwa ligi Ulaya kote kupata nafasi ya kumaliza misimu yao pamoja na mashindano ya Ligi ya Mabingwa wa Ulaya na Ligi ya Ulaya, baada ya kuodolewa kwa vikwazo ambavyo sasa wanaruhusiwa kufanyika kwa mashindano hayo.

Hadi sasa hakuna utaratibu uliowekwa wa jinsi ya kufanyika kwa mashindano hayo ambayo yamepangwa kufayika katika miji 12 ya Ulaya: Amsterdam, Baku, Bilbao, Budapest, Bucharest, Copenhagen, Dublin, Glasgow, London, Munich, Romena Saint Petersburg.

Nusu fainali za Ero zimepangwa kufanyika jijini London.

Tuesday, 17 March 2020

BMT yapongeza Kilimanjaro Premium Lager kwa Udhamini


Mshindi wa mbio za Kilometa 42 za Kilimanjaro Marathon 2020, Kiplagat akimaliza mbio hizo Moshi hivi karibuni.
BARAZA la Michezo la Taifa (BMT), limesema Kilimanjaro Premium Lager ni mfano pekee wa kuigwa katika udhamini wa mchezo wa riadha hapa nchini.

Kampuni ya Bia Tanzania (TBL), kupitia bia yake ya Kilimanjaro, imekuwa mdhamini mkuu wa mbio maarufu za Kilimanjaro Marathon mfululizo toka zilipoanzishwa hadi sasa zinatimiza miaka 18.

Kauli hii inakuja siku chache baada ya kumalizika mbio maarufu za Kilimanjaro Premium Lager Marathon 2020 mjini Moshi ambazo zilihusisha washiriki zaidi ya 11,000 na idadi kama hiyo ya watazamaji.

Kaimu Katibu Mkuu wa BMT, Neema Msitha, ambaye alishuhudia msimu wa 18 Kili Marathon Machi Mosi mwaka huu, aliwapongeza wadhamini hao huku akitoa wito kwa wadau wengine kujitokeza kudhamini mashindano mbalimbali katika kukuza mchezo wa Riadha Tanzania.

Msitha, alisema kwa miaka yote hiyo 18 kumekuwa na mabadiliko makubwa Kilimanjaro Marathon na leo limekuwa tukio kubwa ndani na nje ya nchi, hivyo Kilimanjaro Premium Lager wanapaswa kupongezwa na kuigwa na wengine pia.
Waziri wa Maliasili na Utalii Dk Hamisi Kigwangalla akikabidhi hundi kwa mshindi wa mbio za Km 42 upande wa wanawake, Lydia Wafula (kulia) huku Mkurugenzi wa Masoko wa TBL Group, Doreen Tumubeebire akishuhudia. Kilimanjaro Premium Lager imekuwa mdhamini wa mbio hizi kwa miaka 18 sasa.
Aliongeza kuwa, mashindano kama hayo husaidia pia kuleta umoja kwa jamii.

“Tunatoa wito kwa wadau mbalimbali wanaohitaji kutoa udhamini katika matukio kama haya, kujitokeza kwani husaidia katika kuleta umoja wa kipekee kwa jamii,” alisema.

Hivi karibuni, BMT ililiagiza Shirikisho la Riadha Tanzania (RT), kupunguza tozo kwa waandaaji wa mbio za barabarani kutoka Sh. Milioni 3 hadi Sh. Milioni 1.5 ili kuwasaidia waandaaji katika kuandaa matukio yenye uhakika.

Naye Meneja wa Bia ya Kilimanjaro Premium Lager, Irene Mutiganzi amewashukuru watanzania na washiriki wote kwa kujitokeza kwa wingi katika mbio za mwaka huu ambapo namba za mbio za km 42 na 21 ziliisha mapema kabla ya muda wa mwisho uliotangazwa.

“Hii ni dhahiri kuwa mbio hizi zimekuwa maarufu sio nchini tu ila hata nje ya nchi ndio maana sisi kama wadhamini tumekuwepo kwa miaka 18 sasa tangu mbio ghizi zianzishwe,” alisema.

Wadhamini wengine waliofanikisha mbio za mwaka huu ni TPC Limited, Simba Cement, Unilever, Absa Bank Tanzania Limited na watoa huduma rasmi ni Kibo Palace Hotel, Keys Hotel, GardaWorld Security, Precision Air na CMC Automobiles.
  

Corona Yasimamisha Michezo Yote



Na Mwandishi Wetu
SERIKALI imetangaza kusimamisha kwa mwezi mmoja michezo yote inayokusanya watu wengi, ikiwa ni tahadhari ya kujikinga na virusi vya ugonjwa wa corona, ambao tayari umeshaingia nchini.

Waziri Mkuu Kassim Majaliwa (pichani) alitangaza hayo wakati akilihutubia taifa kwa njia ya radio na televisheni, kuhusu hatua zinazochukuliwa na serikali dhidi ya janga hilo la corona.

Kwa tamko hilo, kuanzia mechi za mchangani hadi zile za Ligi Kuu Tanzaia Bara na ile ya Zanzibar, zitakuwa zimesimamishwa kwa mwezi mmoja, kwani ligi hizo zinahusisha mkusanyiko wa watu wengi.

 “Tunatangaza kusimamishia rasmi michezo yote inayokusanya idadi kubwa ya watu, makundi ya watu kama Ligi Kuu, Ligi Daraja la Kwanza, Daraja la pili na Umishumta, Umisseta na mashindano ya mashirika ya umma na michezo mingine kwa kipindi cha mwezi mmoja,” alisema Majaliwa.

Alisema baada ya tamko hilo wizara yenye dhamana na michezo ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo watasambaza barua kwa mashirikisho yote nchini wakitakiwa kufanya hivyo.

Kabla ya kutolewa tamko hilo la jana, tayari Ofisi ya Rais, Tawala za  Mikoa na Serikali za Mitaa kupitia  waziri wake, Selemani Jafo ilifuta Mashindano ya Shule za Msingi na Sekondari kuanzia hatua ya mashule, ambayo yalitarajia kuanza hivi karibuni.

Nchi kadha zikiwemo zile zenye ligi tano kubwa kama England, Hispania, Italia, Ujerumani na Ufaransa zimesimamisha ligi zao hadi mwanzoni mwa mwezi ujao ili kuamgalia mwenendo wa jango hilo la corona, ambalo tayari limewakumba baadhi ya wachezaji wa ligi hizo.

Mbali na kusimamishwa kwa ligi kubwa Ulaya, Shirikisho la Soka la Ulaya (Uefa) limesogeza mbele fainali za Mataifa ya Ulaya, Euro 2020 hadi mwakani kuanzia Juni 11 hadi Julai 11, 2021.

Pia Shirikisho la Soka Afrika (Caf), Ijumaa lilitangaza kusimamisha mechi zote za kufuzu kwa fainali za Mataifa ya Afrika (Afcon 2021) na jana ilitangaza kusimamisha fainali za Mashindano ya Mataifa ya Afrika kwa wachezaji wa ndani (Chan 2020), ambazo zingefanyika Cameroon mwezi ujao.

Wakati huo huo, Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) jana lilitangaza kikao cha dharura ambacho kitafanyika leo jijini Dar es Salaam kuzungumza hatma ya Ligi Kuu Tanzania Bara kuhusu janga la corona.

Kikao hicho pia kitajadili kambi ya timu ya taifa, Taifa Stars inayoendelea kujiandaa na fainali za Kombe la Chan nchini Cameroon pamoja na mechi za majaribio za timu hiyo.

Rais wa TFF, Wallace Karia aliagiza Kamati ya Uongozi ya Bodi ya Ligi Kuu Tanzania Bara kuitisha kikao cha dharula leo kujadili mustakabali wa michuano hiyo wakati huu wa mlipuko wa virusi vya corona.

Karia alisema kikao hicho kitakachoanza saa 3:00 asubuhi kitafanyika katika ukumbi wa mikutano wa Hoteli ya Golden Tulip, Dar es Salaam.

“Ajenda kubwa katika kikao hicho ni kuangalia mustakabali wa ligi kutokana na mlipuko wa virusi vya ugonjwa wa corona ambao umeingia nchini,”alisema Karia.

Friday, 6 March 2020

MAB Yaridhishwa Ukaguzi Corona JNIA TB-3


Mwenyekiti wa Bodi ya Ushauri (MAB) ya Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Tanzania (TAA), Dkt Masatu Chiguma akipimwa joto la mwili na Afisa Afya, Yusta Malisa wakati bodi hiyo ilipotembelea Jengo la Tatu la Abiria la Kiwanja cha Ndege cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNIA-TB3), kwa ziara ya kikazi.

Na Bahati Mollel, TAA

BODI ya Ushauri (MAB) ya Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Tanzania (TAA), imeridhishwa na ukaguzi wa abiria wanaotoka nje ya nchi wanaotumia Jengo la Tatu la Abiria la Kiwanja cha Ndege cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNIA-TB3).

Mwenyekiti wa MAB, Dk Masatu Chiguma amesema leo mara baada ya kumalizika kwa ziara yao ya kwanza ya kikazi tangu kuteuliwa kwao hivi karibuni ya wametembelea jengo hilo kuwa maafisa afya waliopo kwenye Jengo hilo wanafanya ukaguzi kulingana na taratibu zilizowekwa, ili kuzuia maambukizi ya Homa Kali ya mapafu inayoambukizwa na virusi aina ya Corona, isiingie nchini.

Dkt Chiguma amesema tahadhari ya kuzuia ugonjwa huo ulioanzia nchini China na kusambaa kwenye nchi mbalimbali Duniani, imefanyika ipasavyo kwenye Jengo hilo, baada ya kulitembelea na kuona, vifaa na utendaji wa watumishi hao wa afya.
 
Mkurugenzi wa Kiwanja cha Ndege cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNIA), Paul Rwegasha (wa kwanza kulia), akiwasilisha taarifa fupi ya Jengo la Tatu la Abiria la Kiwanja cha Ndege cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNIA-TB3), kwa Bodi ya Ushauri (MAB) ya Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Tanzania (TAA), ilipotembelea jengo hilo leo. 

“Matayarisho ya kujihadhari na huu ugonjwa wa Corona yamefanyika kwa hali ya juu na wajumbe wa Bodi tumeridhika baada ya kuona vifaa vinavyohitajika kuvaliwa na watendaji wa kitengo cha afya na pia watumishi wa TAA waliopo maeneo ya kuwasili na maeneo mengine,” amesema.

Akizungumzia jengo hilo, Dkt Chiguma amesema anaipongeza serikali kwa ujenzi wa jengo hili la kisasa lenye vifaa vya kimataifa, ambapo uendeshaji wake ni wa hali ya juu.

“Tumepita kuanzia mwanzo wa jengo hadi mwisho wa jengo na tumejionea namna lilivyo bora na zuri, hata vifaa vyake ni vya kitaalam sana, ukiangalia eneo la mizigo ni mashine tu zinafanyakazi  pamoja na kuwa na Watumishi wachache lakini kila kitu kinaongozwa na mashine za kisasa,” amesema.

Kaimu Meneja wa Jengo la Tatu la Abiria la Kiwanja cha Ndege cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNIA-TB3), Mhandisi Barton Komba (kulia), akitoa maelezo mbalimbali kwa Bodi ya Ushauri (MAB) iliyotembelea jengo hilo leo. Aliyevaa tai ni Mwenyekiti wa Bodi hiyo Dkt. Masatu Chiguma.
Hatahivyo, amesema Bodi imebaini bado katika jengo hili kuna upungufu mkubwa wa watumishi, ambapo sasa waliopo wengi ni wanaofanya kazi kwa mikataba mifupi na wale wanaendelea kujifunza (Internship), ambapo ni hatari kwa kuwa sio wakutegemewa zaidi kutokana kuweza kuondoka wakati wowote watakapopata ajira ya kudumu.

Pia ameitaka menejimenti ya TAA kuhakikisha inaboresha maslahi ya watumishi ili waendelee kulitunza jengo hilo kwa kufanya kazi kwa bidii.

Halikadhalika amesema ulinzi na usalama wa abiria na mizigo yao kwenye Jengo hilo ni wa hali ya juu na uliopangiliwa vyema, kwa kuanzia abiria anapoingia wakati akisafiri hadi kufika kwenye ndege, hata mizigo inavyokaguliwa kwa kupitia hatua tano napo panaridhisha.

Wajumbe wa Bodi ya Ushauri (MAB) ya Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Tanzania (TAA), wakiangalia ramani ya jengo hilo wakati wakilitembelea katika ziara ya kikazi iliyofanyika leo.
Katika hatua nyingine, Dkt Chiguma amewaita Watanzania kujitokeza kwa wingi kuwekeza kwenye jengo hilo, pale TAA itakapotangaza zabuni mbalimbali, maana bado yapo maeneo mengi ya uwekezaji.

Awali akiwasilisha ripoti ya ujenzi wa jengo hilo, Mkurugenzi wa JNIA, Paul Rwegasha amesema wanakabiliwa na changamoto ya gharama kubwa za uendeshaji, ambapo jengo zima kwa asilimia 100 linatumia umeme wa Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO), na ukikatika hutumika jenereta ambazo zinatumia mafuta mengi.

Ofisa Afya, Yusta Malisa (mwenye koti jeupe), akiwapa maelezo ya Wajumbe wa Bodi ya Ushauri (MAB) ya Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Tanzania (TAA), namna anavyowakagua abiria wanaowasili kutoka nchi mbalimbali, kuzuia virusi vya Corona vinavyosambaza homa kali ya mapafu visiingie nchini, walipotembelea jengo hilo leo.
Pia amesema wanakabiliwa na upungufu wa watumishi, ambapo wanalazimika kutumia zamu fupifupi na wengine waliotoka asubuhi kurudi jioni kuongeza nguvu (supporting).
Wajumbe wa Bodi ya Ushauri (MAB) ya Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Tanzania (TAA), wakiangalia moja ya begi likipita kwenye mkanda ikiwa ni hatua ya tatu kwa ukaguzi kabla halijafika hatua ya mwisho tayari kupelekwa kwenye ndege, walipotembelea jengo hilo leo katika ziatra ya kikazi.

Sunday, 16 February 2020

TAKUKURU Kubaini Mamluki Michezo Mei Mosi 2020


Wajumbe wa Kamati ya Michezo ya mashindano ya Mei Mosi wakiwa kwenye kikao cha Kwanza cha maandalizi ya michezo hiyo kilichofanyika mwishoni mwa wiki kwenye ukumbi wa mikutano wa Chuo cha Kikuu cha Sokoine cha Kilimo (SUA) mkoani Morogoro

 Na Bahati Mollel, Morogoro
TAASISI ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa Tanzania (Takukuru) mkoa wa Mwanza itashirikishwa kwenye Michezo ya Mei Mosi inayotarajiwa kuanza Aprili 16-29, 2020 kwenye Uwanja wa CCM Kirumba jijini humo, endapo kutakuwa na timu za Wizara, Taasisi za Umma  na Binafsi zitawatumia wachezaji wasiokuwa watumishi wao halali.

Katibu wa Kamati ya michezo hiyo, Moshi Makuka, alisema hayo mwishoni mwa wiki kwenye kikao cha kwanza cha maandalizi ya michezo hiyo kilichofanyika katika ukumbi wa mikutano wa Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo (SUA) Morogoro, ambapo suala hilo limewekwa kwenye kanuni namba 13 kati ya 15 zilizopitishwa na wajumbe wote walioshiriki kwenye kikao hicho.

Makuka alisema mbali na Takukuru kushirikishwa kubaini uhalali wa mchezaji aliyesajiliwa na timu iliyomchezesha, pia viongozi wote walioshiriki kumsajili mchezaji huyo wataripotiwa kwenye taasisi hiyo, ili sheria za nchi zichukue mkondo wake.

       Katibu Mkuu wa Kamati ya Michezo ya mashindano ya Mei Mosi, Moshi Makuka  (aliyenyoosha mikono) akisisitiza jambo kwenye kikao cha Kwanza cha maandalizi ya michezo hiyo kilichofanyika mwishoni mwa wiki kwenye ukumbi wa mikutano wa Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo (SUA) Mkoani Morogoro


“Haya mashindano yanajumuisha watumishi halali wa taasisi na wizara hivyo hairuhusiwi kuwachezesha wachezaji ambao sio watumishi halali, kwa lengo la kujipatia ushindi, hili ni katazo na kanuni yetu ipo wazi kabisa, hivyo timu zisithubutu kuja na wachezaji hao kabisa,” alisisitiza Makuka.

Alizitaja adhabu ambazo timu itakayobainika kumtumia mamluki ni pamoja na viongozi wake watafungiwa kushiriki michezo hiyo kwa muda wa miaka miwili na nakala ya barua itawasilishwa kwa Mwajiri wake; timu itatozwa faini  ya Tshs. 500,000; timu husika itapokonywa ushindi endapo itakuwa imeshinda; timu itaondolewa kwenye mashindano.

Kamati imesema mamluki wanadhibitiwa kwa wanamichezo kuwa na vitambulisho halisi vya kazi, Kadi ya Bima ya Afya, Kadi ya Mfuko wa Jamii na hati ya Malipo ya mshahara za miezi miwili ‘salary slip’.

Hatahivyo, Makuka alisema timu zote shiriki zinatakiwa kuwahi mkoani Mwanza tarehe 14 Aprili, 2020 ambapo ndipo sherehe za Sikukuu za wafanyakazi zitafanyika Kitaifa kama ilivyotangazwa awali, ambapo timu itakayochelewa hadi tarehe 20 Aprili, 2020 itakuwa imejiondoa kwenye michezo hiyo.

“Timu ikichelewa inawapa shida na kuwaumiza wachezaji kwa kuwa watacheza mfululizo ili kwenda na ratiba, hadi kufikia michezo yao iliyosalia, hivyo hii hatutaki kwani michezo itakuwa haina ushindani kwa kuwa wachezaji wa timu moja watakuwa wamechoka kwa kucheza mfululizo wa mechi mbili au tatu kwa siku, hivi huu ni mwezi wa pili muanze kufuatilia ruhusa za wachezaji wenu,” alisema Makuka.

Kamati inategemea ushiriki wa timu zaidi ya 25, kwa kuwa zinaongezeka kila mwaka ambapo mwaka jana zilishiriki timu 23. Michezo itakayoshindaniwa ni pamoja na soka, netiboli, kuvuta kamba, baiskeli, riadha, karata, bao na draft.

Pia Makuka amesisitiza timu shiriki kulipa ada ya ushiriki kwa wakati, ili fedha hizo zitumike katika ulipaji wa gharama mbalimbali za uendeshaji wa mashindano hayo.

Ada ya ushiriki ni Tshs. 1,000,000 ambapo kila timu inatakiwa kulipa mapema kabla ya tarehe 6 Aprili, 2020, ili timu ziweze kupewa kadi za ushiriki zitakazofanikisha usajili wao.

Halikadhalika Makuka amesema timu zote zilizotwaa vikombe kwa kuwa washindi wa Kwanza hadi wa tatu wanatakiwa kurejesha vikombe walivyoshinda kabla yatarehe 29 Machi, 2020 na timu itakayochelewa utatozwa faini ya Tshs. 200,000.

Wakati huo huo, Makuka amesema timu zinaruhusiwa kushiriki kwenye michezo ya mashirikisho mbalimbali yakiwemo ya Shimiwi, Shimmuta na Mei Mosi, na sio kusubiri michezo ya shirikisho moja, ambayo kwa wakati huo inakuwa haijafanyika kwa sababu mbalimbali.

TAA WATAKIWA KUTUMIA VIZURI MFUMO WA TANEPs


Kaimu Mkurugenzi wa Utawala na Rasilimali Watu wa Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Tanzania (TAA), akimkabidhi cheti cha kufuzu mafunzo ya mfumo wa Manunuzi kwa njia ya Mtandao (TANEPs),  Mkuu wa Kitengo cha Ukaguzi wa Ndani wa Bi. Irene Sikumbili (wa pili kushoto). Mafunzo hayo yaliendeshwa na Mwezeshaji Kenneth Nnembuka kutoka Mamlaka ya Udhibiti wa Manunuzi ya Umma (PPRA) (kulia)

Na Bahati Mollel
KAIMU Mkurugenzi wa Utawala na Rasilimali Watu wa Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Tanzania (TAA), Bw. Abdi Mkwizu amewataka wahitimu wa mafunzo ya mfumo wa Manunuzi kwa njia ya mtandao (TANEPs), kuutumia vyema mfumo huo ili kuongeza ufanisi katika taratibu za ununuzi wa Umma kwa maslahi ya taasisi na Taifa kwa ujumla.

Akifunga mafunzo hayo ya siku tano jana yaliyokuwa yakifanyika kwenye ukumbi wa mikutano wa Watu Mashuhuri wa Kiwanja cha Ndege cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNIA), Bw. Mkwizu alisema tayari Mamlaka imeanza kutumia mfumo huo ulioagizwa na serikali kupitia Mamlaka ya udhibiti wa Ununuzi wa Umma (PPRA).

Ofisa Manunuzi na Ugavi wa Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Tanzania (TAA), Bw. Honest Mushi (mwenye fulana) akipokea cheti cha kufuzu mafunzo ya mfumo wa Manunuzi kwa njia ya Mtandao (TANEPs), kutoka kwa Kaimu Mkurugenzi wa Utawala na Rasilimali Watu, Bw. Abdul Mkwizu. Kulia ni Mwezeshaji wa Mafunzo hayo Bw. Kenneth Nnembuka kutoka Mamlaka ya Udhibiti wa Manunuzi ya Umma (PPRA)

Mkufunzi wa mafunzo hayo Bw. Kenneth Nnembuka kutoka PPRA, aliwataka wahitimu kuanza haraka kutumia maarifa waliyoyapata ili wasije wakasahau. Pia aliwasihi kutosita kuomba msaada mara wapatapo mkwamo kuhusu mfumo huo mpya.

Naye Kaimu Mkuu wa Kitengo cha Manunuzi na Ugavi cha TAA, Bw. Josephat Msafiri alishukuru uongozi wa juu wa TAA kukubali kufanyika kwa mafunzo hayo muhimu yenye lengo la kuongeza ufanisi wa utendaji wa ndani wa taasisi.

Aliahidi kuendelea kutumika bila kuharibu kada hiyo.


Kaimu Mkuu wa Kitengo cha Manunuzi cha Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Tanzania (TAA), Josephat Msafiri (wa pili kulia) akiandika mambo mbalimbali yanayofundishwa na Mwezeshaji Kenneth Nnembuka kutoka Mamlaka ya Udhibiti wa Manunuzi ya Umma (PPRA), katika mafunzo ya mfumo wa manunuzi kwa njia ya mtandao (TANePs), yanayoendelea kwenye ukumbi wa Mikutano wa Watu Mashuhuri wa Kiwanja cha Ndege cha Kimataifa cha Julius Nyerere (VIP -JNIA-TB2).
Kwa upande wake Mkuu wa Kitengo cha Ukaguzi wa ndani ya Taasisi, Bi Irene Sikumbili aliweka msisitizo kwenye matumizi sahihi ya mfumo kwa mujibu wa miongozo, taratibu, kanuni na sheria za serikali.

Mkurugenzi wa JNIA, Bw. Paul Rwegasha, alisisitiza mapendekezo ya TAA na wadau mbalimbali kuhusu changamoto za kimfumo yafanyiwe kazi ili kuepusha uwezekano wa ukwamishaji wa huduma viwanjani.
Naye mratibu wa mafunzo hayo, Bw. Soud Saad amesema mafunzo hayo yalishirikisha watendaji wakuu wa TAA; Wakaguzi wa ndani; wataalam wa TEHAMA na Wataalam wa Ununuzi na Ugavi kutoka Makao Makuu na JNIA.

Wednesday, 5 February 2020

Kamwelwe Ataka MAB Kuweka Uzalendo Mbele

Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Tanzania (TAA), Mhandisi Mshauri, Julius Ndyamukama (aliyesimama kulia) akitoa taarifa fupi kwa Waziri wa Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, Mhandisi Isaack Kamwelwe (mbele), wakati wa uzinduzi wa Bodi ya Ushauri ya TAA, (MAB) uliofanyika mwishoni mwa wiki kwenye Jengo la TPA (One Stop Centre) jijini Dar es Salaam. 

Na Bahati Mollel,TAA
WAZIRI wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, Mhandisi Isaack Kamwelwe ameiasa Bodi ya Ushauri ya Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Tanzania (MAB), kutanguliza Utaifa na Uzalendo mbele katika majukumu yao.

Kauli hiyo ameitoa mwishoni mwa wiki katika halfa ya uzinduzi wa Bodi hiyo, ambao umefanyika kwenye Jengo la Bandari nchini (TPA One Stop Centre) lililopo jijini Dar es Salaam.

“Napenda kutumia nafasi hii kuwaasa kwamba, nafasi hizi mlizopewa ni kwa ajili ya kulitumikia Taifa letu kwa weledi, uaminifu na uadilifu mkubwa huku mkitanguliza maslahi mapana ya taifa na uzalendo mbele”. Amesema Waziri Kamwelwe
Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, Mhandisi Isaack Kamwelwe (mbele) mwishoni mwa wiki akiongea na Walioteuliwa kuunda Bodi ya Ushauri ya Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Tanzania (MAB), pamoja na Menejimenti ya TAA wakati wa uzinduzi wa bodi hiyo katika Jengo la TPA (One Stop Centre) jijini Dar es Salaam.
Pia Waziri Kamwelwe ameitaka Bodi hiyo kuhakikisha inashirikiana bega kwa bega na menejimenti ya Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Tanzania (TAA), na taasisi za serikali hususan Wakala wa Barabara nchini (TANROADS) katika ujenzi wa viwanja vingi zaidi ya wanavyovisimamia 58 kwa lengo ya kuviongeza, ili ndege za Shirika la ndege Tanzania (ATCL) na mashirika mengine yaweze kupanua wigo wa safari.

Halikadhalika amesema ulinzi na usalama katika viwanja vya ndege ukaimarishwe, ingawa bado kunachangamoto ya kukosekana kwa uzio wa ndani na nje ya viwanja vya ndege, ambapo pia suala la ugonjwa wa homa ya virusi vya Corona ulioanzia nchini China lipewe kipaumbele kwa kuzingatiwa maslahi mapana ya Taifa yazingatiwe.

“Hili la ugonjwa wa Corona liangaliwe kwa ukaribu zaidi ili viwanja vya ndege visiwe ndio njia ya kuingiza ugonjwa huu, pia usalama wa watendajikazi uangaliwe pia,” amesema na kuongeza.
Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, Mhandisi Isaack Kamwelwe (wa nne kulia), akiwa katika picha ya pamoja na Mwenyekiti Dkt Masatu Chiguma (wa nne kushoto) na Wajumbe ya Bodi ya Ushauri ya Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Tanzania (MAB), baada ya kuizindua Bodi hiyo mwishoni mwa wiki kwenye Jengo la TPA.
“... Vilevile mkahakikishe kuwepo na usimamizi mzuri wa wa ardhi na miundombinu ya viwanja vyetu ikiwemo Jengo la Tatu la abiria –JNIA na utoaji wa huduma bora zaidi kwa wateja, ukiangalia kwa sasa ni viwanja vichache tu ndio vina hati na hili sio jambo jema, hakikisheni viwanja vyote vinapimwa na hati kupatikana, kwani itasaidia kuongeza uhalali na kuongeza mapato ya TAA kwa kutumia ardhi hiyo,” amesema Waziri Kamwelwe.

Pia ameitaka Bodi hiyo kuhakikisha TAA inapata “control number” ili malipo mbalimbali yatafanyika kupitia huko, ambapo pia ameitaka kubuni njia mbalimbali za kuendesha viwanja vya ndege kibiashara, wakati sasa suala la TAA kuwa Mamlaka zaidi badala ya sasa kuwa Wakala pamoja na kwamba lipo chini ya Wizara linahitaji msukumo wa Bodi hiyo.
   Menejimenti ya Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Tanzania (TAA), leo wakiwa kwenye picha ya pamoja na Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, Mhandisi Isaack Kamwelwe (wanne kutoka kushoto), na Mwenyekiti, Dkt Masatu Chiguma na Wajumbe wa Bodi ya Ushauri ya Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Tanzania (MAB), iliyozinduliwa mwishoni mwa wiki kwenye Jengo la TPA.
Hatahivyo, Waziri Kamwelwe amesema pamoja na TAA kuwa na mafanikio bado inakabiliwa na changamoto za kushindwa kuboresha miundombinu mbalimbali iliyopo viwanjani.

Bodi hiyo inaundwa na Mwenyekiti Dkt. Masatu Chiguma na wajumbe ni Mhandisi Ven Kayamba, Dkt. Paschal Mugabe, Mhandisi Daniel Kiunsi, Mhandisi Christopher Mukoma na Alex Haraba.

Awali Mkurugenzi Mkuu wa TAA,  Mhandisi Mshauri, Julius Ndyamukama amesema Mamlaka hiyo imekuwa ikikua tangu kuanzishwa kwake hadi sasa, na kutolea mfano wa mapato kuongezeka kutoka Shilingi Bilioni 6.3 hadi kufikia Bilioni 105.2 kwa mwaka, ambalo ni sawa na ongezeko la asilimia 1,570.

Pia amesema Mamlaka ilianza na ikiwa na miruko na mituo ya ndege 62,221 kwa mwaka na sasa imefikia 146,593 kwa mwaka ni sawa na ongezeko la asilimia 135.6.

Kwa upande wa abiria, amesema ilianza ikiwa na idadi ya abiria 846,906 kwa mwaka na sasa imefikia 3,473,658 kwa mwaka ikiwa ni sawa na ongezeko la asilimia 310.

Naye Mwenyekiti wa MAB, Dkt. Masatu Chiguma, alimuahidi Waziri kuwa atafanya kazi bega kwa bega na TAA, ili kufanikisha malengo yalilowekwa.

Wednesday, 11 December 2019

TAA Yasaidia Kutokomeza Mimba za Utotoni Tabora


Mbunge wa Viti Maalum wa Jimbo la Tabora, Mhe. Munde Tambwe (wenye gauni la kijani na njano) hivi karibuni akiwa na Kaimu Meneja Masoko wa Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Tanzania (TAA), Rose Comino (wa tatu kushoto) akimwakilisha, Mhandisi Julius Ndyamukama kukabidhi saruji tani 12.5 kwa ajili ya ujenzi wa mabweni ya wanafunzi wa kike wa Kata mbalimbali za Tabora.
Na Mwandishi Wetu
 MAMLAKA ya Viwanja vya Ndege Tanzania (TAA), imeungana na Mbunge wa Viti Maalum na Wakazi wa Mkoa wa Tabora kusaidia jitihada zao za kutokomeza mimba za utotoni kwa kutoa msaada wa tani 12.5 za saruji kwa ajili ya ujenzi wa mabweni ya wanafunzi wa kike wa shule za sekondari.

Akikabidhi saruji hiyo hivi karibuni katika Kata ya Itonjanda, Manispaa ya Tabora, kwa niaba ya Mkurugenzi Mkuu wa TAA, Mhandisi  Julius Ndyamukama, ambayo ni sawa na mifuko 250 ya saruji, Kaimu Meneja wa Biashara wa Kiwanja cha Ndege cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNIA), Rose Comino, amesema TAA, ipo bega kwa bega katika suala zima la kusaidia jamii katika masuala mbalimbali likiwemo la Elimu, ambapo watoto wote ni sawa na wanastahili kupata elimu na sio kukatizwa masomo kutokana na vikwazo mbalimbali zikiwemo mimba za utotoni.
Kaimu Meneja Masoko wa Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Tanzania (TAA), Rose Comino (wa pili kushoto) hivi karibuni  akimwakilisha, Mhandisi Julius Ndyamukama akiwa kwenye picha ya pamoja na Mbunge Viti Maalum (CCM), Mhe. Munde Tambwe (wa tatu kushoto) mara baada ya kukabidhi msaada wa saruji tani 12.5, kwa ajili ya ujenzi wa mabweni ya watoto wa kike wa shule za sekondari. Wengine pichani ni Kaimu Mkurugenzi wa Manispaa ya Tabora, Joseph Kashushura (kushoto) na Kaimu Meneja wa Kiwanja cha Ndege cha Tabora (wapili kulia).
 Rose amesema Wananchi wa Tabora waungane kwa pamoja kuunga mkono jitihada za  Mbunge wa Viti Maalum Munde Tambwe la ujenzi wa mabweni kwa ajili ya watoto wa kike wa shule za sekondari, ambao wanatembea umbali mrefu kwenda shule, ambapo sasa wanatokomeza mimba za utotoni na kushirikiana kuwabaini wale wote wenye kutenda matendo hayo maovu.

“Kwa pamoja tuoneshe jitihada za dhati kwa kuhakikisha watoto wetu wanakuwa sehemu salama mabwenini, nina uhakika wa asilimia 100 kwa 100 tutapata watoto wengi wa kike watakaomaliza shule na kufanya vizuri katika masomo yao,” amesema Rose.

Amesema TAA ni miongoni mwa taasisi ya serikali iliyoanzishwa kwa mujibu wa Sheria ya Wakala wa Serikali Na.30 ya mwaka 1997 na kupewa dhamana na Serikali ya kuvisimamia na kuviendesha jumla ya viwanja 58,  imekuwa ikitekeleza sera yake ya kurudisha kwa Jamii katika masuala mbalimbali yakiwemo ya elimu.

Moja wa Shule ya sekondari ya Kata ya Itonjanda ya Manispaa ya Tabora, ambayo itajengwa bweni la watoto wa kike ili kuondoa mimba za utotoni. Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Tanzania (TAA) hivi karibuni  imetoa msaada wa saruji tani 12.5 kwa ajili ya ujenzi wa mabweni hayo.
Rose amesema viwanja vya ndege vinatoa fursa mbalimbali za kibiashara zikiwemo za kuendesha migahawa, hoteli, maduka ya bidhaa mbalimbali, usafirishaji wa mizigo ikiwemo mazao ya kilimo, mifugo na uvuvi.

Pia viwanja vya ndege vimekuwa miongoni mwa eneo linalozalisha ajira rasmi na zisizo rasmi, ambazo zinahusisha mashirika mbalimbali ya ndani na nje ya nchi yenye kutoa huduma katika maeneo ya viwanja vya ndege.

Naye Tambwe ameushukuru uongozi mzima wa TAA kwa kusaidia jitihada hizo, ambazo anauhakika kwa lengo alilojiwekea ataweza kusaidia ujenzi wa mabweni mengi katika kila kata ya Mkoa wa Tabora.

“Naomba ndugu zangu tuunge mkono jitihada hizi nilizoanzisha, na pia kuungana na  Rais John Pombe Magufuli za kutoa elimu bure, mimi nimezaliwa hapa Tabora na nimeona jinsi gani mabinti zetu wanavyotembea umbali mrefu kwenda na kurudi shule jambo ambalo linachangia kupata vishawishi njiani na kujikuta wanapata mimba za utotoni.” Amesema Tambwe.

Hatahivyo, amesema mifuko 100 kati ya hiyo 250 itapelekwa kwenye Kata ya Itonjanda, ili ujenzi uanze mara moja, na 150 iliyosalia itapelekwa kwenye shule nyingine.

Naye Mwenyekiti wa Chama cha Mapinduzi (CCM) Kata ya Itonjanda ameshukuru msaada huu uliotolewa na TAA kwani watoto wamekuwa wakitembea umbali wa Kilometa 10 kwenda shule, na wamekuwa wakiathirika kutokana na kupata mimba.

“Tumuunge mkono Rais wetu kwani Tanzania bila elimu haitaenda tuunge jitihada hizi kwani watoto wanakuwa wananawiri sana wanapoingia shule za sekondari, kwani wamekuwa wakipewa fedha ndogo ndogo ambazo zimekuwa zikiwaponza na kujikuta wanapata ujauzito, ” amesema.