Saturday 30 January 2016

CONGO DR YAWAFUNGISHA VIRAGO WENYEJI RWANDA KWA KUIFUNGA 2-1 KATIKA MUDA WA NYONGEZA



KIGALI, Rwanda
JAMHURI ya Kidemokrasia ya Congo (DRC), ilihitaji muda wa ziada kuwaondosha wenyeji Rwanda katika mashindan ya Mataifa ya Afrika kwa wachezaji wanaocheza ligi za nyumbani (Chan), baada ya kuibuka na ushindi wa mabao 2-1 katika mchezo wa robo fainali jijini hapa.

Doxa Gikanji aliipatia Congo bao la kuongoza dakika 10 tangu kuanza kwa mchezo huo uliofanyika kwenye Uwanja wa Amohoro.

Hatahivyo, wenyeji walisawazisha dakika 12 baada ya mapumziko kwa bao lililowekwa kimiani na Ernest Sugira.

Padou Bompunga aliifungia Congo bao la ushindi katika muda wa nyongez na hiyo ikiwa na maana kuwa washindi hao sasa watakutana ama na Zambia au Guinea katika nusu fainali itakayopigwa Jumatano.

Congo, ambayo iliwahi kutwaa taji hilo mwaka 2009, ilipata uongozi wa mchezo wakati Rwanda iliposhindwa kuokoa vizuri mpira na mpira huo kuangukia kwa Gikanji aliyekuwa nje ya eneo la hatari na kupiga shuti kali na kumuacha kipa wa Rwanda Eric Ndayishimiye akishindwa kuokoa shuti hilo.

Dakika tisa baadae, huku Chui hai wa Congo wakiwa wametawala, Jonathan Bolingi alipiga shuti lililogonga mwamba.

Bao la kusawazisha la Rwanda la kipindi cha pili lilipatikana kutoka kwa Sugira likiwa ni bao lake la tatu.

Mchezaji huyo alifunga bao hilo baada ya kufanikiwa kuwa nyuma ya mabeki wa Congo, na kupiga shuti lililompita kipa Ley Matampi.

Muda mfupi baadae mchezaji huyo nusura afunge baada ya kuitoka beki ya Congo na Matampi akiwa yeye na kipa, alipiga juu ya wavu wa goli.

Timu zote zilishambuliana kwa zamu kabla ya filimbi ya mwisho, lakini hadi dakika 90 za kawaida za mchezo zinamalizika, timu hizo zilikuwa sare ya bao 1-1.

Wakati muda ukiendelea kuyoyoma watu wakitarajia timu hizo zitapigiana penalty kumpata mshindi, Bompunga alipiga mpira wa kichwa cha nyuma na mpira kumpita Ndayishimiye.

No comments:

Post a Comment