Thursday 1 November 2018

Baraza la Michezo Laipa Yanga Wiki Tatu


Na Mwandishi Wetu
BARAZA la Michezo la Taifa (BMT) limetoa wiki tatu kwa klabu ya Yanga kuhakikisha wanachama wake wanajisajili upya katika matawi yote nchini kwa ajili ya Uchaguzi Mkuu, huku ikilipa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) mwezi mmoja  kutangaza tarehe ya Uchaguzi Mkuu wa klabu hiyo.

Hivi karibuni Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Dr Harrison Mwakyembe alikutana na viongozi wa Yanga pamoja na wazee wa klabu hiyo kusikiliza kero zao.

Kaimu Katibu Mkuu wa wa BMT, Alex Mkeyenge alisema jana kuwa wamefanya hivyo baada ya wanachama wa Yanga kuwasilisha malalamiko yao  kwa Waziri, na baada ya kuwahoji wakafikia muafaka na ndipo suala hilo likarejeshwa kwa BMT.

Mkyenge alisema Yanga ni timu ya wananchi na inahitaji kutoa burudani kwa wanachana na wapenzi wake pamoja na kutoa ajira kwa wachezaji iliowasajili, hivyo migogoro haina nafasi kwa sababu inaua soka nchini.

Na ndio maana BMT imeamua kutoa agizo kwa viongozi wa Yanga pamoja na TFF ili litekelezwe kwa wakati huo.

"Tunaomba wale kwenye kadi za Benki ya Posta na CRDB wote watumie muda waliopewa kwenda kwenye matawi yao kwa ajili ya kujisajili," alisema kiongozi huyo wa BMT.
Kikosi cha Yanga.
Alisema lengo ni kuhakikisha uchaguzi huo unafanyika kwa amani na haraka ili Yanga wapete viongozi wao halali, ambao wataingia madarakani kwa kupigiwa kura.

Akizungumzia  tarehe ya uchaguzi alisema wameiagiza TFF kupitia kamati yake ndani ya mwezi mmoja watangaze tarehe ya kufanyika kwa Uchaguzi Mkuu wa Yanga.

Alisema anaamini TFF itafanya kazi kwa weledi ili kuhakikisha wananusuru migogoro midogo, ambayo inarudisha nyuma hadhi ya klabu hiyo, ikiwemo kushusha ari za wachezaji wake.

"Tunataka kuona Yanga kama ilivyokuwa mwanzo,sio malumbano tena wanachama wameshatoa.madukuduku yao wakitaka uchaguzi ufanyike, “alisema Mkeyenge.

Kwa upande wa Makamu wa Rais wa TFF Athuman Nyamlani alisema Kamati ya TFF iko kamili kwa ajili ya kusimamia uchaguzi huo, huku ikisisitiza ndani ya muda huo tarehe ya uchaguzi itatangazwa.

"Kila kitu safari hii kitakwenda sawa kwa sababu kila mtu Yanga anataka uchaguzi na hili sio suala la mtu mmoja, “alisema Nyamlani.

Alisema muda waliopewa inatosha sana kufanya walichoagizwa kwa sababu uchaguzi huo umeahirishwa mara nyingi kutokana na wanachama mwenyewe kutoelewana.

Alifafanua zaidi ya kuwa, Yanga inahitaji kuwaburudisha wanachama na mashabiki wake, hivyo anapoendekeza migogoro,wanashindwa hata kusajili nakuwatunza vizuri wachezaji.

No comments:

Post a Comment