Monday, 20 May 2019

Mkandarasi Terminal 3 JNIA Kukabidhi Jengo Mapema


Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Mhandisi Isack Kamwelwe (Mwenye suti ya bluu) akisalimiana na Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Tanzania (TAA) Mhandisi Julius Ndyamukama  mara baada ya kuwasili kwa ajili ya ziara ya ukaguzi wa maendeleo ya ujenzi katika jengo la tatu la abiria (TB III) katika Kiwanja cha Ndege cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNIA) jioni ya leo.

Na Mwandishi Wetu
JENGO la Tatu la Kiwanja cha Ndege cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNIA),  Terminal 3, litakabidhiwa mapema kwa wamiliki, imeelezwa.

Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, Isack Kamwelwe amesema kuwa jengo hilo, ambalo litakuwa na uwezo wa kuchukua abiria milioni 6 kwa mwaka, litakabidhiwa Mei 29, ikiwa ni siku moja kabla tarehe ile ya awali iliyoahidiwa na mkandarasi kulikabidhi.

Awali, mkandarasi aliahidi kukabidhi jeingo hilo, Mei 30 kwa wamiliki, ambao ni Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Tanzania (TAA) kwa ajili ya maandalizi ya mwisho kabla ya kuzinduliwa rasmi na Rais John Pombe Magufuli baadae mwaka huu.

JENGO TAYARI
Tayari ujenzi wa jengo hilo umekamilika kwa asilimia 99.5  na sasa vitu vikubwa vinavyofanyika ni kufunga vifaa mbalimbali, vikiwemo vile vya usalama, milango, vitu na vile vya Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TRA).

Alisema kuwa tayari ujenzi umeshakamilika na watu wa TRA, TTCL, Fire na wengine wanaweka mifumo yao ya huduma ili kukamilisha ujenzi huo.


 Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Mhandisi Isack Kamwelwe katikati akiwa anaelekea katika jengo la tatu la Abiria (TB III) kuona maendeleo ya mradi wa ujenzi, kulia kwake ni Mhandisi Msimamizi wa Ujenzi wa jengo hilo Barton Komba na kushoto kwake ni Msimamizi wa miradi ya Viwanja vyote vya Ndege Tanzania Mhandisi Godson Ngomuo.

“Mtendaji Mkuu kwa sasa anahangaika na watoa huduma na wanaotakiwa ni wale wenye uwezo mkubsa na ambao hawafanyakazi kwa mazoea na ni bora wakapata vijana wa kitanzania wenye uwezo mkubwa wa kutoa huduma katika jengo hilo bora kabisa na la kisasa, “ alisema Kamwele baada ya kukagua jengo hilo.

MAJARIBIO
Alisema baada ya Mei 29  wataanza kufanya majaribio ya matumizi mbalimbali katika jengo hilo, ambalo halina tofauti kabisa na majengo ya viwanja vya Ulaya nan chi nyingine zilizoendelea.

Aidha, Kamwele alisema baada ya kukamilika kwa Jengo l Terminal 3, ujenzi utahamia katika terminai 2, ambalo lenyewe litatumika kwa ajili ya abiria wa hapa nchini ambao wanatoka na kuwasili kutoka mau kwenda mikoani.

Terminal 3 ina madaraja 12, ambayo yana uwezo wa kuegesha ndege kubwa za idadi hiyo kwa wakati mmoja pia kutakuwa na mageti 16 ya kuingilia na kutokea katika ndege.
Alisema kuwa katika kudhihirisha kuwa ujenzi wa Terminal 3 tayari wafanyakazi wamebaki 1,000 kutoka 2,900 ambao walikuwa wakifanya shuhghuli mbalimbali za ujenzi.

Tayari baadhi ya majengo yaliokuwa ofisi za muda zilizojengwa na mkandarasi katika eneo hilo la Terminal 3 kwa ajili ya kutoa huduma mbalimbali za ujenzi, zimeshavunjwa.
Waziri alisema ameridhishwa kabisa na maendeleo ya ujenzi wa jingo hilo na baada ya Mei 29, TAA itakuwa ikiendesha mafunzo mbalimbali kwa ajili ya watoa huduma uwanjani hapo.

  Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Mhandisi Isack Kamwelwe akisikiliza maelezo kutoka kwa Mhandisi Msimamizi wa Ujenzi Barton Komba kutoka Wakala wa barabara (TANROADS) alienyoosha mkono juu kuhusu eneo la maegesho ya magari katika Jengo la tatu  la Abiria (TB III) wakati wa ziara yake Kiwanja cha Ndege cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNIA) jioni ya leo.

Alisema Mtendaji Mkuu tenda anayohangaika nayo ni watoa huduma kwani wanataka wale wenye uwezo mkubwa, ambao wataendana na ubora wa jingo hilo, hivyo hawataki wale wanaotoa huduma kwa mazoea.

Waziri alipotembelea jengo hilo alishuhudia watu wa TRA, Uhamiaji na wengine wakifunga vifaa vyao, tayari kutoa huduma wakati wowote kiwanja hicho kitapoanza kutumika.

Juni mosi wataanza kutoa huduma kwa majaribio uwanjani hapo, hasa ,ujaribu mifumo mbalimbali kabla ya kutoa taarifa kwa Rais Magufuli kuuzindua jengo hilo la tatu la abiria.

Awali, akisoma taarifa ya utekelezaji wa mradi wa ujenzi wa TB III, Kaimu Mkurugenzi Mkuu TANROADS Mhandisi Crispin Akoo alisema kutokana maendeleo mazuri ya ujenzi Mkandarasi anatarajia kukabidhi jengo mapema.

 “Hadi kufikia terehe 31 Julai 2018 maendeleo yalikua ni asilimia 78.33, lakini hadi kufikia tarehe 18 Mei 2019 ujenzi wote ulikua umefikia asilimia 99.5, ” alisema.

Kuhusu maandalizi ya uendeshaji Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Tanzania (TAA) Mhandisi Julius Ndyamukama alimweleza Waziri kwamba majaribio na maandalizi ya uendeshaji yalianza tangu mwezi machi mwaka 2018 na yapo katika hatua za mwisho.

“Majaribio ya kwanza ya kwanza ya mifumo na vifaa vinavyotumia umeme yalianza mwezi Julai 2018 kwa sasa yamefikia asilimia 96 na muda sio mrefu yatakamilika.”

Aidha Mhandisi Ndyamukama aliongeza kwamba majaribio hayo yanatarajiwa kufanyika ndani ya miezi mitatu kuanzia mwezi Mei na ifikapo mwezi Agosti yatakua yamekamilika.

Naye Mhandisi Barton Komba alimwambia mwandishi wetu kuwa, kwa wakati mmoja jingo hilo linaweza kuhudumia hadi abiria 2800 bila tatizo, huku kukiwa na checking counter 42, 37 zikitoa huduma kwa abiria wa madaraja ya kawaida na wale wa business huku tano zikitoa huduma kwa Commecial Important People (CIP).

Saturday, 13 April 2019

Klabu 10 Zawania Ubingwa Taifa wa Kuogelea


Na Mwandishi Wetu
JUMLA ya klabu 10 zimethibitisha kushiriki katika mashindano ya Klabu Bingwa ya taifa ya mchezo wa kuogelea yatakayofanyika kwenye bwawa la kuogelea la Shule ya Kimataifa ya Tanganyika (IST), Upanga jijini Dar es Salaam kuanzia leo.

Klabu ambazo zitashiriki katika mashindano hayo ni Bluefins, Champion Rise, Mis Piranhas, klabu ya kuogelea ya Mwanza (MSC), FK Blue na Wahoo ya Zanzibar.

Nyingine zitakazochuana katika mpambano hou ni pamoja na ISM-Moshi, ISM-Arusha, FK Blue Marlins, Talis-IST na mabingwa watetezi, Dar es Salaam Swim Club (DSC).
Mashindano hayo ambayo yatamalizika kesho Jumapili, yamedhaminiwa na IST, Azam, Pepsi, Asas, Samsung, DTB Bank, Kaka’s, Food Lovers na Snow Cream.

Wadhamini wengine ni Kastipharn Ltd, Ruru Logistics, Knight Support, Oppotune Travel ltd, Pyramid Consumers, Print Galore, ITV Media, Clouds FM, Subway, NMB Bank and Umoja Grand Belt na  Road Restaurant.

Mwenyekiti wa Kamati ya Maandalizi ya mashindano hayo, Hadija Shebe alisema kuwa waogeleaji wa Tanzania wanaoishi nje ya nchi wamewasili tayari kwa mashindano hayo.
Waogeleaji  hao ni Sonia Tumiotto, Maia Tumiotto , Collins Saliboko, Dennis Mhini, Chichi Zengeni, Natalia Sanford, Smriti Gorkarn  na Delvin Barick ambao wote wanasoma Uingereza.

Wengine ni  Christian Shirima anayetokea nchini Ukraine,  Isam Sepetu (Afrika Kusini), Hilal Hemed Hilal na Kangeta wanaotokea klabu ya Hamilton Aquatic ya Dubai.

Alisema kuwa mashindano hayo yamepangwa kuanza saa 2.00 leo na waogeleaji watashindana katika staili tano, ambazo ni Freestyle, Breaststroke, Butterfly, Backstroke na Individual Medley.

Kwa mujibu wa Hadija, waogeleaji hao pia watashindana katika relay katika mashindano ambayo yamepitishwa na Shirikisho la Mchezo wa kuogelea Duniani (Fina) kuwa ya kutafuta alama za kufuzu mashindano ya Dunia yaliyopangwa kufanyika nchini Korea  Julai.

Kwa mujibu wa Hadija, kutakuwa na jumla ya vipengele  vya mashindano 108 na kila klabu imetakiwa kuwakilishwa na waogeleaji wawili katika kila kipengele cha mashindano ambavyo pia vimepangwa kutokana na umri.

Stars Yapangwa na Vigogo Senegal, Algeria Afcon 2019

Timu ya Taifa ya Tanzania, Taifa Stars, ikiwa mazoezi kwenye Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam hivi karibuni.

CAIRO, Misri
TIMU ya Taifa ya Tanzania, Taifa Stars, imepangwa pamoja na majirani zao wa Kenya, Senegal pamoja na Algeria katika Kundi C la fainali za Mataifa ya Afrika, Afcon 2019, zitakazofanyika Misri kuanzia Juni 21 hadi Julai 19 nchini Misri.

Taifa Stars ambayo kwa mara ya kwanza inashiriki hatua ya fainali hiyo baada ya miaka 39, ilijikuta katika kundi hilo baada ya Shirikisho la Soka la Afrika (Caf) kupanga ratiba hiyo jana usiku.

Sasa Stars itakuwa na kibarua kigumu kuhakikisha inatinga hatua ya mtoano kwa kupitia nafasi mbili za moja kwa moja,ambazo hutolewa kwa timu mbili za kwanza au kupitia `best looser’ endapo itafanya vizuri lakini itashindwa kupata nafasi mbili za kwanza.

Aidha, wenyeji Misri, Pharaohs, wamepangwa pamoja na Zimbabwe au Chui,  Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo (DR) pamoja na Uganda, ambao walikuwa kundi moja na Tanzania katika hatua ya kufuzu.

Katika Kundi B, timu ya taifa ya Nigeria ya Super Eagles itakabiliana na timu mbili ambazo zimefuzu kwa mara ya kwanza katika Afcon, ambazo ni Burundi na Madagascar pamoja na Guinea.

Mmoja kati ya wachezaji wachezaji kivutio katika mashindano ya mwaka huu, Sadio Mané mwenyewe atakuwepo na timu yake ya Senegal katika Kundi C, ambalo iko Taifa Stars.

Katika Kundi D, Hervé Renard atakutana tena na Ivory Coast. Simba hao wa Milima ya Atlas itawabidi kuwa makini na Afrika Kusini pamoja na nchi ndogo ya Namibia.
Katika Kundi E, Tunisia watakabiliana na Mali pamoja na Mauritania,  ambayo inashiriki kwa bmara ya kwanza fainali hizo, pamoja na Angola.

Mabingwa watetezi Cameroon wenyewe watakabiliana na Black Stars ya Ghana, Benin na Guinea Bissau.

Kufanyika kwa mara ya kwanza kwa fainali hizo katika kipindi cha Juni kutawawezesha wachezaji wote wa Afrika wanaocheza soka Ulaya kuwemo katika timu zao za taifa, kwani wakati huo ligi zote za Ulaya zinakuwa zimemalizika.

Pia hizo zitakuwa fainali kubwa kabisa za Afcon, ambazo zitashirikisha timu 24 kwa mara ya kwanza baada ya huko nyuma kushirikisha timu 16 tu na zilikuwa zikianza Januari hadi Februari.

Kocha wa Morocco Herve Renard atakuwa akiangali kushinda mara ya tatu taji hilo la Afrika, akiwa na timu ya tatu. Simba hao wa Atlas wako katika Kundi D, pamoja na timu ya Ivory Coast aliyowahi kushindwa nayo taji hilo. Zingine ni Afrika Kusini pamoja na majirani zao Namibia.

Mchezo wa kwanza wa mashindano hayo utawakutanisha wenyeji Misri ambao watacheza na Chui wa Zimbabwe, huku Misri wakitarajia kuwa na nyota wa Liverpool Mohamed Salah katika kikosi chao katika mchezo utakaofanyika Juni 21 kwenye Uwanja wa Cairo.

Timu mbili kati ya tatu ambazo zinashiriki kwa mara ya kwanza fainali hizo, Madagascar na Burundi – ziko katika Kundi B pamoja na Nigeria na Guinea.

Ratiba kamili ya Makundi:

Kundi A: Misri, DR Congo, Uganda, Zimbabwe

Kundi B: Nigeria, Guinea, Madagascar, Burundi

Kundi C: Senegal, Algeria, Kenya, Tanzania

Kundi D: Morocco, Ivory Coast, Afrika Kusini, Namibia

Kundi E: Tunisia, Mali, Mauritania, Angola

Kundi F: Cameroon, Ghana, Benin, Guinea-Bissau

Friday, 12 April 2019

DStv Yazindua Kampeni Kuishangilia Serengeti Boys


Mkurugenzi wa Maendeleo ya Michezo nchini, Dk Yussuf Singo (kulia) akimkabidhi mpira msanii, Amisa Mobeto wakati wa hafla ya kuzindua kampeni ya kuishangilia timu ya taifa ya vijana wenye umri chini ya miaka 17, Serengeti Boys, iliyoandaliwa na DStv kwenye hoteli ya Double Tree Masaki jijini Dar es Salaam.


Na Mwandishi Wetu
WATANZANIA wametakiwa kujitokeza kwa wingi kuishangilia timu ya taifa ya vijana ya wachezaji wenye umri chini ya miaka 17 itakayoshiriki fainali za Mataifa ya Afrika ya Afcon 2019 itakayoanza jijini Dar es Salaam Jumapili.

Serengeti Boys itafungua dimba kwenye Uwanja wa Taifa kwa kucheza dhidi ya mabingwa mara mbili wa Afrika na mabingwa mara tano wa dunia Nigeria.

Mkurugenzi wa Maendeleo ya Michezo nchini, Dk Singo aliyasema jijini Dar e Salaam jana wakati wa hafla ya DStv ya kuhamasisha watu kujitokeza kwa wingi kuishangilia timu hiyo iliyopo katika Kundi A pamoja na Nigeria, Angola na Uganda.

Mkurugenzi wa Maendeleo ya Michezo nchini, Dk Yussuf Singo (wa pili kulia), Mkuu wa Masoko wa MultiChoice Tanzania, Ronald Shelukindo (watatu kulia), mchezaji wazamani wa timu ya taifa ya Tanzania, Amri Kiemba (kushoto) na Salum Salum wa DStv kulia kabisa.

Hafla hiyo iliwahusisha wachezaji wazamani, wasanii na wadau wengine wa michezo kuhakikisha wanatumia nafasi au tasnia zao kuwahamasisha watu kujitokeza kwa wingi kuujaza uwanja huo wa Taifa.

Singo alisema kuwa DStv ambayo imekuwa mstari wa mbele kusaidia maendeleo ya michezo mbalimbali hapa nchini, imebuni kitu cha maana kuhakikisha watoto wetu hao wanaungwa mkono kwa watazamaji kuingia kwa wingi uwanjani na kuwashangilia.
Shumbana.
Naye Mkuu wa Masoko wa MultiChoice Tanzania , Ronald Shelukindo alisema wakati akimkaribisha Singo kuwa ni jukumu la kila Mtanzania kujitokeza kuishangilia Serengeti na wale ambao hawatakuwa na nafasi ya kwenda uwanjani, basi wataziona mechi hizo kupitia DStv.

Alisema  kuwa DStv imeanzisha kampeni hiyo ya uhamasishaji inayojulikana kama ‘DStv Inogile’ na imehakikisha kuwa michuano mbalimbali ya kimataifa inarushwa mubashara tena katika kifurushi cha chini kabisa cha DStv Bomba cha Sh. 19,000 tu.
Baadhi ya wachezaji wazamani walioudhuria hafla hiyo Double Tree Masaka, Dar es Salaam.
Kwa upande wa michuano ya Afcon ya U-17, Shelukindo alisema DStv itakuwa ikifanya kampeni kwa njia mbalimbali ikiwemo kwa njia ya mitandao na matangazo mbalimbali kuhamasisha na kuitia nguvu timu ya taifa ili iweze kufanya vizuri katika mashindano hayo.

Baadhi ya wachezaji wazamani waliodhuria hafla hiyo ni pamoja na Sekilojo Chambua, Edibily Lunyamila, Magoso, Kiemba, Madata Lubigisa na wengineo, wakati wasanii ni Mobeto, Nancy Sumari, John Makini na wengine.







Tuesday, 19 March 2019

MultiChoice Yatangaza Fursa kwa Wadau wa Filam Nchini, Afrika


Na Mwandishi Wetu
KAMPUNI ya MultiChoice-Tanzania imetangaza  fursa ya kipekee kwa wadau wa tasnia ya filamu Tanzania na barani Afrika kwa ujumla ijulikanayo kama MultiChoice Talent Factory Portal iliyodhamiria kuleta mapiduzi ya hali ya juu katika uaandaaji wa filamu zenye viwango vya kimataifa kutoka barani Afrika.

Akizungumza wakati wa uzinduzi wa programu hiyo, Mkuu wa kitengo cha Uhusiano kutoka MultiChoice Tanzania Johnson Mshana alieleza kuwa programu hiyo ni muendelezo wa programu maalum ya iliyodhamiria kuleta mabadiliko katika tasnia ya filamu barani Afrika.

 “MultiChoice Talent Factory ambayo ni progamu mama  ilizinduliwa rasmi mapema  Mei mwaka jana na imedhamiria kuleta mabadiliko chanya kwenye tasnia ya filamu hapa nyumbani Tanzania na Afrika kwa ujumla.

Tulianza kwa kupeleka vijana wanne katika kambi maalum ya mafunzo ya uandaaji filamu katika akademia maalum kule Nairobi nchini Kenya, kisha mafunzo maalum kwa magwiji wa sauti yaliyofanyika Januari mwaka huu na hatimaye leo hii tumekuja tena na platform maalum yenye dhamira ile ile ya kuleta mapinduzi katika tasnia ya filamu barani Afrika”, alisema Mshana.

Kwa upande wake Katibu Mtendaji wa Bodi ya Filamu Tanzania, Joyce Fisoo alisema kuwa, anaishukuru sana Kampuni ya MultiChoice kwani imekuwa mstari wa mbele katika kuleta mapinduzi kwenye tasnia ya filamu hapa Tanzania.

 “Binafsi nilishuhudia uzinduzi wa programu ya MultiChoice Talent Factory mapema mwaka jana kule mjini Dodoma na leo hii tunazindua tena sehemu nyingine ya programu hiyo hiyo. Hakika ni fursa ya kipekee na ninapenda kuchukua nafasi hii kuwahamasisha wadau wote waliopo katika tasnia yetu kuitumia nafasi hii ipasavyo ili kuweza kujifunza, kubadilishana ujuzi na hatimaye kupata kazi zenye maudhui ya hali ya juu kutoka hapa hapa Afrika”,  alisema Fisoo.

Naye Ofisa Uhusiano wa MultiChoice Tanzania Grace Mgaya alimalizia kwa kueleza kuwa ukurasa huu ni wa wazi kwa watu wote hususani wadau wa filamu waliopo hapa nyumbani na Afrika kwa ujumla.

 “Tunaamini kwa kupitia program hii tutaweza kuwafikia wadau wengi zaidi na tunatarajia kazi zenye ubora wa hali ya juu kutoka barani Afrika kwa siku zijazo kutokana na matokeo chanya yatakyoletwa na program hii ya MultiChoice Talent Factory”, alisema Grace.


Wednesday, 6 March 2019

Tanzania Kinara Tena Tuzo za ‘DStv Eutelsat Star Awards’


Mkuu wa Uhusiano wa MultiChoice Tanzania, Johnson Mshana akimkabidhi mshindi wa tuzo za Kimataifa za DStv Eutelsat Star Awards, Pricilla Marealle cheti cha ushindi wakati wa mahafali ya kidato cha sita katika shule ya St Mary Goretti hivi karibuni. Kulia ni Ofisa Uhusiano  wa MultiChoice Tanzania. Grace Mgaya. 

Na Mwandishi Wetu

KWA mara nyingine tena Tanzania imeibuka kinara  katika tuzo za kimataifa za wanafunzi zijulikanazo kama DStv Eutelsat Star Awards ambapo mwanafunzi Priscilla Marealle kutoka shule ya sekondari ya St. Mary Goreti mkoani Kilimanjaro ameweza kuipeperusha bendera ya Tanzania kwa kunyakua nafasi ya kwanza katika kipengele cha uchoraji bango  ikiwa ni baada ya mchuano mkali baina ya mamia ya wanafunzi kutoka nchi zaidi ya 10 kote barani Afrika.

Kwa upande wa uandishi wa insha kijana Tanaka Chonyera kutoka  nchini Botswana aliweza kujinyakulia ushindi wa kwanza.

 Tuzo hizi ambazo huhusisha uandishi wa insha maalum au kuandaa bango yenye ujumbe kuhusiana na elimu ya anga hususan Setelait ni za wazi kwa wanafunzi wote wa shule za sekondari wenye umri kati ya miaka 14 – 19 kote barani Afrika ambapo kampuni ya MultiChoice inaendesha shughuli zake.
Mkuu wa shule ya  St Mary Goretti Sr. Lucrecia Njau akifurahi baada ya kupokea cheti kutoka kwa Mkuu wa Uhusiano wa MultiChoice Tanzania Johnson Mshana mara baada ya shule hiyo kufanikiwa kutoa mshindi wa jumla wa wa tuzo za kimataifa za DStv Eutelsat Star Awards Pricilla Marealle. 
  Katika msimu huu wa nane, washindani walitakiwa kuandika insha au kubuni bango litakaloelezea licha ya Satelait kutumika katika shughuli mbalimbali, ni namna gani zitaweza kutumika zaidi ili kuleta maendeleo chanya ulimwenguni.

 Priscilla ambaye ni mwanafunzi wa kidato cha sita wa mchepuo wa Sayansi katika shule ya Mtakatifu Maria Goreti alitangazwa rasmi kuwa mshindi mjini Accra nchini Ghana ambapo ndipo jopo la watahini liliongozwa na Paolo Nespoli, mwanaanga nguli kutoka European Space Agency (ESA) lilikaa kupitia kazi kutoka kwa wanafunzi walioshinda katika nchi mbalimbali.
Mshindi wa Jumla wa tuzo za kimataifa za DStv Eutelsat Star Awards Pricilla Marealle akikabidhiwa kikombe cha ushindi na Mkuu wa shule ya St Mary Goretti Sr. Lucrecia Njau baada ya kutangazwa kuwa mshindi wa jumla wa wa tuzo za kimataifa za DStv Eutelsat Star Awards. Kulia ni Mkuu wa Uhusiano wa MultiChoice Tanzania Johnson Mshana.
 Akiongea baada ya kukabidhiwa cheti cha uthibitisho wa ushindi wakati wa mahafali ya kidato cha sita ya shule ya Mtakatifu Mary Goreti iliyopo Moshi Kilimanjaro, Priscilla amesema amefurahi sana kwa ushindi huo mkubwa ambao umemletea yeye, shule yake na taifa zima kwa ujumla sifa kubwa. “Nimefurahi sana kupokea taarifa hizi nzuri. Naamini ushindi wangu utakuwa ni chachu kubwa kwa wanafunzi wenzangu kote nchini kujitokeza kwa wingi na kushiriki katika tuzo kama hizi na mashindano mengine ya kitaaluma ya ndani na nje ya nchi, na kusisitiza  kuwa Ndoto huanza kufanya kazi pale unapojiamini” alisema Priscilla.
 
Kwa upande wake mkuu wa shule hiyo ya Mtakatifu Maria Goreti Sister Lucresia Njau alisema kuwa anaishukuru sana kampuni ya MultiChoice Tanzania kwa kuwapatia nafasi ya kushiriki katika Mashindano hayo na hatimaye kuweza kunyakua tuzo hiyo kupitia mwanafunzi wao Priscilla.

 “Huyu kijana ana jitahidi sana katika chochote kile anachokifanya, iwe ni darasani au hata katika majukumu mengine nje ya darasani. Ni msikivu mtiifu lakini zaidi ya yote ni mbunifu sana. Naamini haya ndiyo yaliyomfanya aweze kushinda tuzo hizi” alisema Sr. Lucrecia Njau.
  
Naye, Mkuu wa Uhusiano MultiChoice Tanzania Johnson Mshana alisema,” Huu ni msimu wa tatu mfululizo kwa Tanzania kuendelea kung’ara katika tuzo hizi za DStv Star Awards. Tulianza kupeperusha bendera yetu na kijana Davids Bwana msimu wa sita baada ya kushika nafasi ya pili Afrika katika kipengele cha uandishi wa insha, kisha tukaibuka kidedea baada ya kupokea taarifa za ushindi wa kwanza wa kijana Taheer Rashid katika msimu wa saba mwaka jana na leo hii tunayofuraha kubwa kuona kuwa tumeendeleza wimbi la ushindi.”

Saturday, 2 February 2019

Denis Suarez Kuichezea Arsenal Ikiikabili Man City


LONDON, England
KOCHA Mkuu wa Arsenal Unai Emery kumpanga mchezaji mpya aliyesajiliwa juzi Denis Suarez  (pichani) na kuichezea kwa mara ya kwanza katika Ligi Kuu ya England dhidi ya Mabingwa wa ligi hiyo Manchester City katika mchezo utakaofanyika kesho.

The Gunners wanasafiri hadi kwenye Uwanja wa Etihad kwa ajili ya mchezo huo unaotarajia kuwa mkali na wa kusisimua baada ya kukamilika kwa dirisha la usajili, ambapo klabu hiyo ilikamilisha usajili wa Suarez kwa mkopo akitokea Barcelona hadi mwishoni mwa msimu.

Mchezaji huyo mwenye umri wa miaka 25, ambaye ameichezea mara mbili timu ya wakubwa ya Man City katika kipindi chake cha mwanzo cha kuichezea klabu hiyo, ndio mchezaji pekee aliyetua Arsenal, ambaye alishindikana kupata mkataba wa kudumu kutokana na ufinyu wa fungu.

Mkataba huo wa mkopo ni pamoja na kuwemo kipengele cha kuweza kuongeza mkataba wa muda mrefu kwa Suarez katika kipindi cha majira ya joto wakati mchezaji huyo wa kimataifa wa Hispania akihusishwa na kiujiunga tena na Emery, wakati akicheza chini ya Mhispania mwenzake katika klabu ya Sevilla.

"Nitafanya uamuzi kesho (leo) lakini endapo ataanza katika mchezo huo nina imani naye, “alisema Emery alipouilizwa ikiwa Suarez ataenda moja kwa moja katika timu ya Arsenal katika mchezo huo wa Jumapili.

"Namjua mchezaji huyo na alianza kujifua binafsi juzi. Leo alikuwa na wenzake. Ni jambo zuri, anaonekana kuelewa haraka.

"Ni mchezaji mwenye kiwango na nafikiri anaweza kutusaidia sisi kutokana na kiwango chake…, “alisema.

Ushindi kwa Manchester City utashuhudia timu hiyo ikiwakaribia vinara wa ligi hiyo Liverpool kwa pointi mbili, ambao watacheza dhidi ya West Ham siku moja baadae.

Kikosi cha Pep Guardiola alikuwa mpinzani wa kwanza wa Emery katika soka la Uingereza, ambako waliibuka na ushindi wa mabao 2-0 dhidi ya Arsenal Agosti.

Emery anatarajia kukutana na kikwazo kingine lakini alisema wachezaji wake wako tayari kuonesha uwezo wao dhidi ya wapinzani wazuri.

"Itakuwa mechi ngumu, tunacheza dhidi ya timu bora, “alisema.

"Sasa, Liverpool, wamefanya kazi kubwa sana wakati wa Ligi Kuu msimu huu. Labda wamepoteza baadhi ya mechi., lakini hiyo ni kama ajali tu.

Qatar Mabingwa Wapya Kombe la Asia

Qatar baada ya kutwaa ubingwa wa Kombe la Asia kwa mara ya kwanza, abada ya kuifunga Japan kwa mabao 3-1 juzi. (Picha na Mtandao).

TOKYO, Japan
WENYEJI wa Kombe la Dunia 2022 Qatar wametwaa kwa mara ya kwanza kabisa taji la Asia baada ya kuibuka na ushindi wa mabao 3-1 dhidi ya mabingwa mara nne wa taji hilo Japan.

Mshambuliaji Almoez Ali alivunja rekodi ya mchezaji kupachika mabao mengi katika mashindano hayo ya Kombe la Asia pale alipofunga bao lake la tisa kwa kichwa katika mchezo huo wa fainali.

Abdulaziz Hatem aliiweka timu yake kuwa mbele kwa mabao 2-0 baada ya kufunga kwa shuti la umbali wa kama meta 20 kabla Japan haijafunga bao lao la kufutia machozi kupitia kwa  Takumi Minamino akiwa ndani ya boksi.

Mabao yalikuwa 3-1 baada ya Akram Afif (mtoto wa kiungo wazanmani wa Simba, Hassan Afif) kufunga kwa penalti baada ya mchezaji anayeichezea klabu ya Southampton, Maya Yoshida kuunawa mpira katika eneo la hatari.

Teknolojia ya VAR ilithibitisha kuwa beki huyo wa Southampton, ambayo inajukana kama Watakatifu aliishika kwa makusudi mpira huo, ingawa picha marudio za TV zilionesha kama aliushika kwa bahati mbaya.

Penalti hiyo ya Afif ilikuwa na maana kuwa mchezaji huyo alifunga bao moja na kusaidia mara 10, ikiwemo mara mbili katika mchezo huo wa fainali, wakati wa mechi saba za Qatar katika mashindano hayo huko Umoja wa Falme za Kiarabu.

Kikosi cha kocha waQatar, Felix Sanchez kimecheza saa 10 na dakika nane bila ya kuruhusu bao hata moja katika mashindano ya mwaka huu ya Asia kabla ya kufungwa na Minamino.

Kijazi Aagiza Makatibu Wakuu Kuhimiza Michezo

Katibu Mkuu Ofisi ya Waziri Mkuu (Bunge), Bi Maimuna Tarishi (mwenye miwani) akisalimiana na Katibu Mkuu Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano (Sekta ya Uchukuzi), Mhandisi Dr. Leonard Chamuriho kabla ya kuanza kwa mbio za pole (jogging) za bonanza la Michezo ya Shirikisho la Michezo ya Wizara, Idara, Taasisi, Wakala wa Serikali na Ofisi za Wakuu wa Mikoa (Shimiwi), iliyoanzia kwenye Uwanja wa Jamhuri hadi Ofisi za Bunge na baadaye kurudi Jamhuri


Mwandishi Wetu, Dodoma
KATIBU Mkuu Kiongozi, ambaye pia ni Mkuu wa Utumishi wa Umma, Balozi Mhandisi John Kijazi amewaagiza Makatibu Wakuu kuhimiza michezo mahala pa kazi kwa vitendo ili kuwa na watumishi wa Umma wenye afya njema.

Kauli hiyo ilitolewa leo na Katibu Mkuu Ofisi ya Waziri Mkuu (Bunge), Maimuna Tarishi kwa niaba ya Balozi Kijazi katika Bonanza la Michezo lililoandaliwa na Shirikisho la Michezo ya Wizara, Idara, Wakala wa Serikali na Ofisi za Wakuu wa Mikoa (SHIMIWI), na kufanyika kwenye Uwanja wa Jamhuri Dodoma.

Tarishi ameweka msisitizo kwa kuwa michezo ni kazi na kazi ni michezo, ambapo sasa Makatibu Wakuu waweke mazingira yatakayowezesha watumishi wa umma kupitia taasisi zao waweze kushiriki kwenye michezo mbalimbali, ambayo inajenga umoja na ushirikiano baina ya watumishi.


“Haya ni maagizo ya Katibu mkuu kiongozi amenituma nije niseme kwa kuwa yupo katika kazi nyingine, wito ni kwa Makatibu Wakuu wote na wakuu wa taasisi kuhakikisha wanaweka mazingira wezeshi yatakayowezesha watumishi kufanya mazoezi mara kwa mara na hata katika michezo kama hii ya Shimiwi,” amesema Bi. Tarishi.

Amesema sasa uwekwe utaratibu kwa Watumishi wa Umma kushiriki michezo ambayo haitatumia gharama kama wanavyodhania wengine.

“Kwa waajiri hatuna budi kuweka mazingira wezeshi ya kuwawezesha Watumishi kuwa na utaratibu wa kushiriki kwenye michezo yeyote na hii inafanyika bila gharama yeyote kabisa kwani wakati mwingine tunakimbilia hatuna fedha au hajatenga kifungu katika bajeti wakati hata hapa ukiangalia hakuna gharama kubwa iliyotumika,” amesisitiza Bi. Tarishi.
Amewataka watumishi wa umma kufanya mazoezi ya kila wakati ili kujiweka katika afya kwa wakati wote, ambayo itawasaidia kufanya kazi kwa weledi.

Bi. Tarishi ametoa pia maagizo kwa viongozi wa Shimiwi, kwa kuwa sasa wameanza kufufua michezo hii baada ya kusimama kwa muda mrefu, na sasa waendelee mbele kwani yanawakutanisha Watumishi wa maeneo mbalimbali ya kazi ya serikali na husaidia kubadilishana uzoefu.

“Hii ni rai yangu kwenu kwa kuwa sasa mmeanza tena michezo yenu hii tunapenda tuone inasonga mbele kwani hushirikisha watumishi kutoka Wizara na Taasisi mbalimbali, na yanajenga umoja kama watumishi wa umma, na tuwekee maanani na kutekeleza haya,” amesema Bi. Tarishi.

Hatahivyo, amesema michezo ni nidhamu hivyo kuwe na nidhamu kwenye michezo kwani kutasaidia watumishi kufanya kazi kwa bidii na kuwa na ubinifu wa hali ya juu.

Naye Mwenyekiti wa Shimiwi, Daniel Mwalusamba amesema wachezaji wanahimizwa kufanya mazoezi kwa ajili ya kujenga, kulinda na kuimarisha afya zao.

“Michezo ni kazi hivyo wanapaswa kuzingatia taratibu na miongozo inayokuwa imetolewa kila wakati na serikali, na kama agenda ya kitaifa ilivyo ya kujenga Tanzania ya Viwanda, na ili tufanikiwe tunahitaji kuwa na Watumishi wenye afya bora wanaoweza kufanya majukumu yao kwa wakati na kushiriki michezo mbalimbali, ambapo sasa wanaweza kuandaa mabonanza sehemu za kazi kwa siku ya za mwishoni mwa wiki,” amesema Bw. Mwalusamba.

Hatahivyo, amesema katika kikao cha juzi kilichofanyika kwenye ukumbi wa Hazina na kuwahusisha Wenyeviti na Makatibu wa klabu za michezo mahala pa kazi, ambapo wamekumbushwa kusimamia michezo kwa kuwa ni sehemu ya kazi na wanapaswa kusimamia na kutekeleza majukumu yote yanayotolewa na serikali.
Meneja wa Kiwanja cha Ndege cha Dodoma, Bi. Bertha Bankwa (wa kwanza kulia mstari wa nyuma) leo akijumuika kufanya mazoezi na watumishi wa Umma katika bonanza la Shirikisho la Michezo Wizara, Idara, Taasisi, Wakala wa Serikali na Ofisi za Wakuu wa Mikoa (SHIMIWI), lililofunguliwa na Katibu Mkuu Ofisi ya Waziri Mkuu (Bunge), Bi. Maimuna Tarishi (Hayupo pichani). (PICHA NA BAHATI MOLLEL WA MAMLAKA YA VIWANJA VYA NDEGE TANZANIA- TAA).
Katika michezo iliyochezwa jana kwa upande wa kuvuta Kamba wanaume timu ya Waziri Mkuu wametoa jasho na Mambo ya Ndani na kutoka sare ya mvuto 1-1; wakati katika netiboli timu ya Utumishi imechapwa na Tamisemi magoli 24-17; huku Afya wakiwashinda GST magoli 9-6.

Katika mchezo wa soka Utumishi wamewachapa Afya magoli 2-0; huku Ardhi wamewashinda Mwanasheria Mkuu kwa magoli 4-0.

Friday, 1 February 2019

Shimiwi wahimiza mabonanza kuimarisha afya

Mwenyekiti wa Shirikisho la Michezo la Wizara, Idara, wakala wa Serikali na Ofisi za Wakuu wa Mikoa (Shimiwi, Daniel Mwalusamba (katikati) akiendesha kikao cha viongozi wa klabu mbalimbali kilichofanyika leo, kwenye ukumbi wa mikutano wa Hazina, jijini Dodoma. Wengine kushoto ni Makamu Mwenyekiti Ally Katembo na kulia ni Katibu Mkuu Moshi Makuka.

Na Mwandishi Wetu, Dodoma
SHIRIKISHO la Michezo ya Wizara, Idara, Wakala wa Serikali, na Ofisi za Wakuu wa Mikoa (Shimiwi), imehimiza ushiriki wa mabonanza ya michezo mbalimbali kwa Watumishi wa Umma ili kuboresha afya zao.

Mwenyekiti wa Shimiwi, Daniel Mwalusamba amesema leo jijini Dodoma, katika mkutano wa wenyeviti na makatibu uliofanyika kwenye ukumbi wa Naibu Waziri wa Fedha katika jengo la Hazina.

Mwalusamba amesema kwa sasa serikali inahimiza ujenzi wa viwanda, ili tufikie uchumi wa kati, ambapo Watumishi wa Umma wanatakiwa kuunga mkono hatua hiyo iliyotangazwa na Mhe. Rais John Pombe Magufuli.

“Tuondokane na zana ya Shimiwi kuwa imekufa kwani hili ni Shirikisho la michezo ambalo lipo kihalali na linaendeshwa kwa utaratibu, na mapendekezo yote yapo kisheria,” amesema Mwalusamba.

Hatahivyo, Mwalusamba amesema Shimiwi inakumbwa na changamoto za klabu kwa kushindwa kwenda na katibka kwa kufanya chaguzi zake kwa wakati, ikiwa ni kufuata katiba iliyopo.

“Hairihusiwi kikatiba kwenye mkutano mkuu kuingia na viongozi ambao hawajachaguliwa kihalali na kukaa kwa muda mrefu, kwani ni kinyume na katiba yetu ya Shimiwi na pia Katiba Mama ya Serikali, ambayo imeweka wazi juu ya muda wa ukomo wa uongozi,”

Amesema ni kinyume na katiba na viongozi wa shimiwi wanaweza kwenda kwa Katibu Mkuu wa wizara husika, na sasa Shimiwi itafanya ukaguzi na kugundua klabu iliyo na uongozi uliomaliza muda, hali kadhalika katiba za klabu zinapitishwa na baraza, na sio kikundi kinachojiendesha chenyewe bila kufuata katiba.

Ameagiza klabu sugu zikafanye chaguzi zao ili kuepusha mgogoro, kwani  Shimiwi  imekuwa mfano wa kuigwa kwa kufuata taratibu tofauti na mashirikisho mengine.

Kijazi kubariki Bonanza la Shimiwi Dodoma kesho

Katibu Mkuu Kiongozi, Balozi John Kijazi

Na Mwandishi Wetu, Dodoma
WATUMISHI zaidi ya 1,000 kutoka Wizara na Idara za Serikali leo watashiriki kwenye Bonanza la Michezo litakaloongozwa na Katibu Mkuu Kiongozi na Mkuu wa Utumishi wa Umma ambaye pia ni Mlezi wa Shirikisho la Michezo la Wizara na Idara za Serikali (SHIMIWI), litakalofanyika Jijini Dodoma.

Mwenyekiti wa SHIMIWI, Daniel Mwalusamba amesema bonanza hilo litatanguliwa na mbio fupi fupi (jogging) zitakazoanzia kwenye uwanja wa Jamhuri hadi maeneo ya Bunge na kurudi kiwanja cha Jamhuri, ambapo mbali na Katibu Mkuu Kiongozi, pia watashiriki Watendaji Wakuu wa kutoka taasisi mbalimbali za Umma.

Mwalusamba amesema baada ya mbio hizo wachezaji wote walioshiriki ;watafanya mazoezi ya viungo na baadaye kushiriki kwenye michezo ya netiboli, soka na kuvuta Kamba.
Wajumbe wa klabu mbalimbali za Shirikisho la Michezo ya Wizara, Idara, Wakala wa Serikali na Ofisi za Wakuu wa Mikoa wakimsikiliza Mwenyekiti, Daniel Mwalusamba alipoendesha kikao leo kwenye ukumbi wa mikutano Hazina Dodoma.
“Hili bonanza ni moja ya njia ya kuwaweka watumishi wa umma katika afya njema na kuepuka magonjwa nyemelezi, ambapo mtumishi ataweza kufanya kazi kwa weledi na bidi kwa kuwa wanakuwa na afya nzuri,” amesema Mwalusamba.

Pia amesema bonanza hilo litaendelea kesho (Jumapili) kwa michezo mbalimbali.
Akizungumzia uwepo wa mashindano ya michezo ya SHIMIWI, ambayo imekuwa ikiahirishwa mara kwa mara kutokana na sababu mbalimbali, Mwalusamba amesema mashindano hayo yapo na hayajafutwa na yatafanyika kulingana na taratibu.

“Hii michezo haijafutwa lakini kumekuwa na mabadiliko ya kiutaratibu, ambapo sasa serikali yetu ipo katika harakati za ujenzi wa viwanda na sisi ni watu muhimu wa kuimiza hilo, hivyo michezo itaendelea kama ilivyopangwa,” amesema Mwalusamba.
Hatahivyo, amehimiza Watumishi wa Umma kuhakikisha wanatekeleza agizo la Makamu wa Rais, Mhe. Samia Suluhu Hassan la watumishi wafanye mazoezi kila Jumamosi ya Pili ya kila mwezi, ili waweze kujiweka vyema katika afya.

Klabu mbalimbali zimekuwa zikiendesha michezo mbalimbali kwa kushirikisha klabu kwa kushirikiana.