Saturday, 25 May 2019

NEMC Yawaondoa Hofu Wadau Viwanja vya Ndege


Mwanasheria wa Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC), Manchare Heche (aliyenyanyua mikono) akisisitiza jambo wakati akiongea na wadau wanaotoa huduma mbalimbali kwenye Kiwanja cha Ndege cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNIA), juu ya katazo la mifuko ya plastiki iliyopigwa marufuku kuendelea kutumika nchini ifikapo Juni Mosi mwaka huu. Wapili kulia ni Mkurugezi wa JNIA, Paul Rwegasha na wa kwanza kushoto ni mkuu wa kitengo cha Mazingira cha TAA, Maxmilian Mahangila.

Na Mwandishi Wetu
BARAZA la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC), leo limewaondolea hofu wadau wanaoendesha huduma mbalimbali kwenye Viwanja vya ndege, katika mkutano ulioitishwa na Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Tanzania (TAA), uliofanyika kwenye Ukumbi wa Watu Mashuhuri (VIP), kuhususiana na katazo la matumizi ya mifuko ya plastiki ambalo litaanza rasmi Juni Mosi, 2019.

Mwanasheria wa NEMC, Manchare Heche amesema kwa upande wa viwanja vya ndege ipo mifuko, ambayo itaendelea kutumika kwa mujibu wa Kanuni namba tisa (9) ya sheria ya kuzuia matumizi ya mifuko ya plastiki ya mwaka 2019, lakini baada ya kutumika inatakiwa ihifadhiwe sehemu maalum na kupekekwa mahali itakapoteketezwa.
Kaimu Meneja wa Mamlaka ya Hali ya Hewa kwenye Kiwanja cha Ndege cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNIA), Joachim Philipo akitoa ushauri kwenye mkutano wa wadau wanaotoa huduma mbalimbali JNIA ulioitishwa na Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Tanzania (TAA), na kuhusisha Wataalam kutoka Baraza ka Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC), ambao walitoa maelezo mbalimbali juu ya katazo la matumizi ya mifuko ya plastiki litakaloanza rasmi Juni Mosi, 2019 kwa mujibu wa sheria.
“Kweli katazo linahusu Watanzania wote na wageni na hapa Airport wapo wanaotumia nikiwa na maana ya wafanyakazi na wateja wakiwemo abiria, lakini katika sheria ukiangalia kanuni ya tisa 9 ipo mifuko ya vifungashio ambayo haijazuiwa ni kama ile ya kuhifadhi vyakula, dawa, kilimo na inayohifadhia takataka, mfano korosho au keki wanazopewa abiria kwenye ndege mfuko wake upo katika kipengele cha chakula, hivyo itaendelea kutumika lakini baada ya matumizi tu itahuifadhiwa sehemu iliyoelekezwa tayari kwa kwenda kuteketezwa,” alisisitiza Heche.

Alisema kwa upande wa plastiki zinazofungia mizigo ya abiria wanaosafiri kutoka ndani na nje ya nchi kwa usafiri wa ndege itatakiwa kuondolewa abiria anapofika nchini, na zitakusanywa na kuhifadhiwa maeneo maalum kabla ya kupelekwa eneo lililotengwa kwa ajili ya kuziteketeza.
Kaimu Meneja wa Mamlaka ya Hali ya Hewa kwenye Kiwanja cha Ndege cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNIA), Joachim Philipo akitoa ushauri kwenye mkutano wa wadau wanaotoa huduma mbalimbali JNIA ulioitishwa na Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Tanzania (TAA), na kuhusisha Wataalam kutoka Baraza ka Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC), ambao walitoa maelezo mbalimbali juu ya katazo la matumizi ya mifuko ya plastiki litakaloanza rasmi Juni Mosi, 2019 kwa mujibu wa sheria.
Hatahivyo, kutokana na matumizi makubwa ya mifuko ya plastiki nchini imesababisha uharibifu mkubwa wa mazingira ikiwemo ya kuziba kwenye mifereji ya maji, kuua wanyama, na kuharibu ardhi, Heche amesema kufuatia katazo hilo serikali imefuta leseni za viwanda vinavyotengeneza mifuko ya plastiki na pia haijawapa tena leseni wale wote leseni zao zilizomaliza muda, ili kuhakikisha sheria na kanuni ya kuzuia matumizi ya mifuko ya plastiki namba 394 ya mwaka 2019.   

Heche ametoa angalizo kwa wale wote wanaohusika na ukamataji wa watumiaji wa mifuko hiyo, kutotumia nguvu ili kuepusha mikwaruzano na kutoelewana.

      Mrakibu Msaidizi wa Uhamiaji, Anna Mushi wa Kiwanja cha Ndege cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNIA), leo akizungumza katika mkutano wa wadau wanaotoa huduma mbalimbali JNIA katika mkutano ulioitishwa na Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Tanzania (TAA), na kuwahusisha Wataalam kutoka Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC) kutokana na katazo la matumizi ya mifuko ya plastiki ifikapo Juni Mosi, 2019.

Hatahivyo, amewataka wadau hao kuhakikisha wanadai vitambulisho kwa wale wote watakaofika kwenye maeneo yao ya kazi kudai wanakagua endapo wanaendelea kuuza au kutumia mifuko ya plastiki.

Kwa upande wa Mkurugenzi wa Kiwanja cha Ndege cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNIA), Paul Rwegasha amesema tayari kupitia Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Tanzania (TAA), wameshatoa taarifa inayokwenda kwenye vituo vyote vya Kimataifa, ambapo kuna shirika la ndege linaloleta abiria Tanzania, ikitaarifu juu ya katazo la mifuko ya plastiki.
Mwanasheria wa Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC), Manchare Heche akiwaonesha wadau wanaotoa huduma mbalimbali kwenye Kiwanja cha Ncdege cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNIA) moja ya mifuko ya plastiki iliyopigwa marufuku kuendelea kutumika nchini ifikapo Juni Mosi, 2019 katika mkutano uliofanyika leo kwenye ukumbi wa Watu Mashuhuri (VIP).  Kulia ni   Mkurugenzi wa Kiwanja cha Ndege cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNIA), Paul Rwegasha.
“Hii taarifa inajulikana kitaalam kama ‘timatic pre-information’ ambayo inatumwa kwenye centre zote duniani, ambapo kuna shirika la ndege ambalo linaleta abiria Tanzania itakuwa rahisi wao kupata taarifa ya katazo hilo na kuwafanya wasibebe mifuko hiyo,” amesema Rwegasha.

Pia amewataka wadau wote wanaofanya shughuli mbalimbali kwenye viwanja vya ndege kutoa ushirikiano mkubwa kuwaeleza abiria juu ya katazo hilo, na kuwaelekeza watumie mifuko mbadala, ambayo itakuwa ikipatikana kwenye maduka yaliyopo kwenye majengo ya Kwanza na Pili ya JNIA.

Kwa mujibu wa NEMC imesema watumiaji wa kawaida endapo watakamatwa na mifuko hiyo watatozwa faini ya Tshs. 30,000, kifungo cha siku saba, au vyote kwa pamoja;  wakati kwa muuzaji anapigwa faini ya Tshs 100,000 haizidi Tshs 500,000, kifungo cha miezi mitatu; na watengenezaji watapigwa faini ya kuanzia Tshs milioni 20 na haitazidi bilioni moja na kifungo cha miaka miwili.

Arsenal watangulia Baku kucheza dhidi ya Chelsea

Mchezaji wa Arsenal, Lucas Torreira akiwa mwe ari kubwa akipanda ndege kwenda Baku.

LONDON, England

KLABU ya Arsenal leo imekwea pipa na kwenda Baku tayari kwa nchezo wao wa fainali ya Ligi ya Ulaya utakaopigwa Jumatano, imeelezwa.

The Gunners walipigwa picha wakipanda pipa kutoka Kiwanja cha Ndege cha Luton leo Jumamosi.

Mesut Ozil alionekana akiwa mtulivu kabisa wakati wakianza safari yao hiyo ya saa sita hadi saba kutoka London hadi Baku.

Arsenal wanatakiwa kuifunga Chelsea katika mchezo huo wa wiki ijayo ili kutwaa taji hilo na kupata nafasi ya kucheza Ligi ya Mabingwa wa Ulaya msimu ujao.

Arsenal imesafiri mapema kwenda Baku, siku tano kabla mchezo huo watakaocheza dhidi ya wapinzani wao wa jiji la London, Chelsea.

Kikosi hicho cha kocha Unai Emery kitakabiliana na Chelsea nchini Azerbaijan kwenye Uwanja wa Olimpiki wa Baku, ambapo wanahitaji ushindi ili kufuzu kwa michuano ya Ligi ya Mabingwa wa Ulaya msimu ujao.

Na leo Jumamosi asubuhi, the Gunners walionekana katika picha wakipanda ndege tayari kwa mchezo huo wa fainali utakaofanyika Jumatano ijayo.
Danny Welbeck akionekana yuko fiti tayari kwa mchezo wa fainali ya Ligi ya Ulaya Jumatano wiki ijayo.
Nahodha wa Arsenal Laurent Koscielny, Mesut Ozil, Lucas Torreira na wachezaji wengine walionekana wakiwa katika ari kubwa wakati wakianza safari hiyo ya saa sita kwenda Baku wakitokea jijini hapa.

Danny Welbeck ameshinda mbio zake za kuwa fiti kwa ajili ya mchezo huo wa fainali ya Ulaya wakati mshambuliaji huyo wa Uingereza naye pia alipigwa picha akisafiri na wachezaji wenzake wa Arsenal akisafiri na timu hiyo ya Arsenal mwishoni mwa wiki.

Mshmabuliaji huyo hajacheza tangu alipoumia kifundo cha mguu Novemba mwaka jana na sasa anatarajiwa kutajwa katika benchi la Emery dhidi ya Chelsea.
Ozil akicheeeka ndami ya ndege kabla ya kupaa kwenda Baku leo.
Huo utakuwa mchezo wa mwisho wa Welbeck katika timu hiyo yenye maskani yake kaskazini ya London, huku mchezaji hyo mwenye umri wa miaka 28 ambaye ni mchezaji wazamani wa Manchester United ataondoka mwishoni mwa msimu wakati mtataba wake utakapomalizika.

Arsenal inaingia katika mchezo huo wa Jumatano usiku ikiwa na presha kubwa zaidi ya Chelsea ili kupata taji hilo la Ulaya kwa ajili ya mashabiki wao.


Chelsea iliipita Arsenal katika mbio za kusaka nne bora katika Ligi Kuu ya England ili kujihakikishia nafasi ya kufuzu kwa hatua ya nne bora na kucheza Ligi ya Mabingwa wa Ulaya msimu ujao.

The Gunners nafasi yake pekee iliyobaki ya kucheza Ligi ya Mabingwa wa Ulaya ni kutwaa taji la Ligi ya Ulaya katika mchezo ho nan i taji la kwanza tangu ili;otwaa taji hilo la Ulaya mwaka 1994.

Monday, 20 May 2019

Guardiola Sasa Ataka Taji Ligi ya Mabingwa Ulaya


LONDON, England
MAFANIKIO ya Manchester City yatakuwa na thamani endapo tu timu hiyo itafanya vizuri katika Ligi ya Mabingwa wa Ulaya licha ya kuweka historia ya kutwaa mataji matatu msimu huu, anasema kocha Pep Guardiola.

Kocha huyo wa Man City, anajua kuwa atakosolewa endapo atashindwa kuiwezesha timu hiyo kufanya vizuri katika mashindano ya Ulaya.

Ushindi wa 6-0 dhidi ya Watford Jumamosi katika fainali ya Kombe la FA likifuatiwa na taji la Ligi Kuu ya England pamoja na lile la Ligi msimu huu.

"Nilisema tangu awali kuwa najua tutahukumiwa mwishoni kama tumeshinda Ligi ya Mabingwa, “alisema Guardiola.

"Bila ya kutwaa taji la Ligi ya Ulaya, basi tutakuwa hatujafanya jambo la kutosha.

"Hilo nililijua mapema, kwani nilipowasili Barcelona, tulikuwa na bahati tulishinda taji hilo la Ulaya mara mbili ndani ya kipindi cha miaka minne na watu walitarajia  kitu maalum kutoka kwangu, ambacho kingetuwezesha kushinda taji la Ligi ya Mabingwa wa Ulaya hapa City, na hilo litaendelea kuwa sahihi.

"Katika klabu hii, rekodi ya klabu katika mashindano ya nyumbani ni nzuri, lakini Ligi ya Mabingwa wa Ulaya hatujawahi kushinda, hivyo sasa tunajukumu la kushinda taji hilo kwa kuwa tuna wachezaji wazuri sana, “alisema.

Man City imeshinda mara nne taji la Ligi Kuu ya England, mawili ya Kombe la FA na manne ya Ligi, tangu klabu hiyo ilipoanza kumilikiwa na Sheikh Mansour mwaka 2008, lakini pamoja na mafanikio hayo haijawahi kutwaa taji la Ligi ya Mabingwa wa Ulaya.

Beki Vincent Kompany amekuwa katika timu hiyo kwa wakati wote huo, ikiwemo miaka nane akiwa nahodha wa Man City, lakini alitangaza Jumapili kuwa ataondoka katika klabu hiyo na kwenda kucheza soka Ubelgiji.

Kompany, 33, atajiunga na klabu ya Ubelgiji ya Anderlecht kama kocha mchezaji kwa mkataba wa miaka mitatu.

Mkandarasi Terminal 3 JNIA Kukabidhi Jengo Mapema


Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Mhandisi Isack Kamwelwe (Mwenye suti ya bluu) akisalimiana na Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Tanzania (TAA) Mhandisi Julius Ndyamukama  mara baada ya kuwasili kwa ajili ya ziara ya ukaguzi wa maendeleo ya ujenzi katika jengo la tatu la abiria (TB III) katika Kiwanja cha Ndege cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNIA) jioni ya leo.

Na Mwandishi Wetu
JENGO la Tatu la Kiwanja cha Ndege cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNIA),  Terminal 3, litakabidhiwa mapema kwa wamiliki, imeelezwa.

Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, Isack Kamwelwe amesema kuwa jengo hilo, ambalo litakuwa na uwezo wa kuchukua abiria milioni 6 kwa mwaka, litakabidhiwa Mei 29, ikiwa ni siku moja kabla tarehe ile ya awali iliyoahidiwa na mkandarasi kulikabidhi.

Awali, mkandarasi aliahidi kukabidhi jeingo hilo, Mei 30 kwa wamiliki, ambao ni Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Tanzania (TAA) kwa ajili ya maandalizi ya mwisho kabla ya kuzinduliwa rasmi na Rais John Pombe Magufuli baadae mwaka huu.

JENGO TAYARI
Tayari ujenzi wa jengo hilo umekamilika kwa asilimia 99.5  na sasa vitu vikubwa vinavyofanyika ni kufunga vifaa mbalimbali, vikiwemo vile vya usalama, milango, vitu na vile vya Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TRA).

Alisema kuwa tayari ujenzi umeshakamilika na watu wa TRA, TTCL, Fire na wengine wanaweka mifumo yao ya huduma ili kukamilisha ujenzi huo.


 Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Mhandisi Isack Kamwelwe katikati akiwa anaelekea katika jengo la tatu la Abiria (TB III) kuona maendeleo ya mradi wa ujenzi, kulia kwake ni Mhandisi Msimamizi wa Ujenzi wa jengo hilo Barton Komba na kushoto kwake ni Msimamizi wa miradi ya Viwanja vyote vya Ndege Tanzania Mhandisi Godson Ngomuo.

“Mtendaji Mkuu kwa sasa anahangaika na watoa huduma na wanaotakiwa ni wale wenye uwezo mkubsa na ambao hawafanyakazi kwa mazoea na ni bora wakapata vijana wa kitanzania wenye uwezo mkubwa wa kutoa huduma katika jengo hilo bora kabisa na la kisasa, “ alisema Kamwele baada ya kukagua jengo hilo.

MAJARIBIO
Alisema baada ya Mei 29  wataanza kufanya majaribio ya matumizi mbalimbali katika jengo hilo, ambalo halina tofauti kabisa na majengo ya viwanja vya Ulaya nan chi nyingine zilizoendelea.

Aidha, Kamwele alisema baada ya kukamilika kwa Jengo l Terminal 3, ujenzi utahamia katika terminai 2, ambalo lenyewe litatumika kwa ajili ya abiria wa hapa nchini ambao wanatoka na kuwasili kutoka mau kwenda mikoani.

Terminal 3 ina madaraja 12, ambayo yana uwezo wa kuegesha ndege kubwa za idadi hiyo kwa wakati mmoja pia kutakuwa na mageti 16 ya kuingilia na kutokea katika ndege.
Alisema kuwa katika kudhihirisha kuwa ujenzi wa Terminal 3 tayari wafanyakazi wamebaki 1,000 kutoka 2,900 ambao walikuwa wakifanya shuhghuli mbalimbali za ujenzi.

Tayari baadhi ya majengo yaliokuwa ofisi za muda zilizojengwa na mkandarasi katika eneo hilo la Terminal 3 kwa ajili ya kutoa huduma mbalimbali za ujenzi, zimeshavunjwa.
Waziri alisema ameridhishwa kabisa na maendeleo ya ujenzi wa jingo hilo na baada ya Mei 29, TAA itakuwa ikiendesha mafunzo mbalimbali kwa ajili ya watoa huduma uwanjani hapo.

  Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Mhandisi Isack Kamwelwe akisikiliza maelezo kutoka kwa Mhandisi Msimamizi wa Ujenzi Barton Komba kutoka Wakala wa barabara (TANROADS) alienyoosha mkono juu kuhusu eneo la maegesho ya magari katika Jengo la tatu  la Abiria (TB III) wakati wa ziara yake Kiwanja cha Ndege cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNIA) jioni ya leo.

Alisema Mtendaji Mkuu tenda anayohangaika nayo ni watoa huduma kwani wanataka wale wenye uwezo mkubwa, ambao wataendana na ubora wa jingo hilo, hivyo hawataki wale wanaotoa huduma kwa mazoea.

Waziri alipotembelea jengo hilo alishuhudia watu wa TRA, Uhamiaji na wengine wakifunga vifaa vyao, tayari kutoa huduma wakati wowote kiwanja hicho kitapoanza kutumika.

Juni mosi wataanza kutoa huduma kwa majaribio uwanjani hapo, hasa ,ujaribu mifumo mbalimbali kabla ya kutoa taarifa kwa Rais Magufuli kuuzindua jengo hilo la tatu la abiria.

Awali, akisoma taarifa ya utekelezaji wa mradi wa ujenzi wa TB III, Kaimu Mkurugenzi Mkuu TANROADS Mhandisi Crispin Akoo alisema kutokana maendeleo mazuri ya ujenzi Mkandarasi anatarajia kukabidhi jengo mapema.

 “Hadi kufikia terehe 31 Julai 2018 maendeleo yalikua ni asilimia 78.33, lakini hadi kufikia tarehe 18 Mei 2019 ujenzi wote ulikua umefikia asilimia 99.5, ” alisema.

Kuhusu maandalizi ya uendeshaji Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Tanzania (TAA) Mhandisi Julius Ndyamukama alimweleza Waziri kwamba majaribio na maandalizi ya uendeshaji yalianza tangu mwezi machi mwaka 2018 na yapo katika hatua za mwisho.

“Majaribio ya kwanza ya kwanza ya mifumo na vifaa vinavyotumia umeme yalianza mwezi Julai 2018 kwa sasa yamefikia asilimia 96 na muda sio mrefu yatakamilika.”

Aidha Mhandisi Ndyamukama aliongeza kwamba majaribio hayo yanatarajiwa kufanyika ndani ya miezi mitatu kuanzia mwezi Mei na ifikapo mwezi Agosti yatakua yamekamilika.

Naye Mhandisi Barton Komba alimwambia mwandishi wetu kuwa, kwa wakati mmoja jingo hilo linaweza kuhudumia hadi abiria 2800 bila tatizo, huku kukiwa na checking counter 42, 37 zikitoa huduma kwa abiria wa madaraja ya kawaida na wale wa business huku tano zikitoa huduma kwa Commecial Important People (CIP).

Saturday, 13 April 2019

Klabu 10 Zawania Ubingwa Taifa wa Kuogelea


Na Mwandishi Wetu
JUMLA ya klabu 10 zimethibitisha kushiriki katika mashindano ya Klabu Bingwa ya taifa ya mchezo wa kuogelea yatakayofanyika kwenye bwawa la kuogelea la Shule ya Kimataifa ya Tanganyika (IST), Upanga jijini Dar es Salaam kuanzia leo.

Klabu ambazo zitashiriki katika mashindano hayo ni Bluefins, Champion Rise, Mis Piranhas, klabu ya kuogelea ya Mwanza (MSC), FK Blue na Wahoo ya Zanzibar.

Nyingine zitakazochuana katika mpambano hou ni pamoja na ISM-Moshi, ISM-Arusha, FK Blue Marlins, Talis-IST na mabingwa watetezi, Dar es Salaam Swim Club (DSC).
Mashindano hayo ambayo yatamalizika kesho Jumapili, yamedhaminiwa na IST, Azam, Pepsi, Asas, Samsung, DTB Bank, Kaka’s, Food Lovers na Snow Cream.

Wadhamini wengine ni Kastipharn Ltd, Ruru Logistics, Knight Support, Oppotune Travel ltd, Pyramid Consumers, Print Galore, ITV Media, Clouds FM, Subway, NMB Bank and Umoja Grand Belt na  Road Restaurant.

Mwenyekiti wa Kamati ya Maandalizi ya mashindano hayo, Hadija Shebe alisema kuwa waogeleaji wa Tanzania wanaoishi nje ya nchi wamewasili tayari kwa mashindano hayo.
Waogeleaji  hao ni Sonia Tumiotto, Maia Tumiotto , Collins Saliboko, Dennis Mhini, Chichi Zengeni, Natalia Sanford, Smriti Gorkarn  na Delvin Barick ambao wote wanasoma Uingereza.

Wengine ni  Christian Shirima anayetokea nchini Ukraine,  Isam Sepetu (Afrika Kusini), Hilal Hemed Hilal na Kangeta wanaotokea klabu ya Hamilton Aquatic ya Dubai.

Alisema kuwa mashindano hayo yamepangwa kuanza saa 2.00 leo na waogeleaji watashindana katika staili tano, ambazo ni Freestyle, Breaststroke, Butterfly, Backstroke na Individual Medley.

Kwa mujibu wa Hadija, waogeleaji hao pia watashindana katika relay katika mashindano ambayo yamepitishwa na Shirikisho la Mchezo wa kuogelea Duniani (Fina) kuwa ya kutafuta alama za kufuzu mashindano ya Dunia yaliyopangwa kufanyika nchini Korea  Julai.

Kwa mujibu wa Hadija, kutakuwa na jumla ya vipengele  vya mashindano 108 na kila klabu imetakiwa kuwakilishwa na waogeleaji wawili katika kila kipengele cha mashindano ambavyo pia vimepangwa kutokana na umri.

Stars Yapangwa na Vigogo Senegal, Algeria Afcon 2019

Timu ya Taifa ya Tanzania, Taifa Stars, ikiwa mazoezi kwenye Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam hivi karibuni.

CAIRO, Misri
TIMU ya Taifa ya Tanzania, Taifa Stars, imepangwa pamoja na majirani zao wa Kenya, Senegal pamoja na Algeria katika Kundi C la fainali za Mataifa ya Afrika, Afcon 2019, zitakazofanyika Misri kuanzia Juni 21 hadi Julai 19 nchini Misri.

Taifa Stars ambayo kwa mara ya kwanza inashiriki hatua ya fainali hiyo baada ya miaka 39, ilijikuta katika kundi hilo baada ya Shirikisho la Soka la Afrika (Caf) kupanga ratiba hiyo jana usiku.

Sasa Stars itakuwa na kibarua kigumu kuhakikisha inatinga hatua ya mtoano kwa kupitia nafasi mbili za moja kwa moja,ambazo hutolewa kwa timu mbili za kwanza au kupitia `best looser’ endapo itafanya vizuri lakini itashindwa kupata nafasi mbili za kwanza.

Aidha, wenyeji Misri, Pharaohs, wamepangwa pamoja na Zimbabwe au Chui,  Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo (DR) pamoja na Uganda, ambao walikuwa kundi moja na Tanzania katika hatua ya kufuzu.

Katika Kundi B, timu ya taifa ya Nigeria ya Super Eagles itakabiliana na timu mbili ambazo zimefuzu kwa mara ya kwanza katika Afcon, ambazo ni Burundi na Madagascar pamoja na Guinea.

Mmoja kati ya wachezaji wachezaji kivutio katika mashindano ya mwaka huu, Sadio Mané mwenyewe atakuwepo na timu yake ya Senegal katika Kundi C, ambalo iko Taifa Stars.

Katika Kundi D, Hervé Renard atakutana tena na Ivory Coast. Simba hao wa Milima ya Atlas itawabidi kuwa makini na Afrika Kusini pamoja na nchi ndogo ya Namibia.
Katika Kundi E, Tunisia watakabiliana na Mali pamoja na Mauritania,  ambayo inashiriki kwa bmara ya kwanza fainali hizo, pamoja na Angola.

Mabingwa watetezi Cameroon wenyewe watakabiliana na Black Stars ya Ghana, Benin na Guinea Bissau.

Kufanyika kwa mara ya kwanza kwa fainali hizo katika kipindi cha Juni kutawawezesha wachezaji wote wa Afrika wanaocheza soka Ulaya kuwemo katika timu zao za taifa, kwani wakati huo ligi zote za Ulaya zinakuwa zimemalizika.

Pia hizo zitakuwa fainali kubwa kabisa za Afcon, ambazo zitashirikisha timu 24 kwa mara ya kwanza baada ya huko nyuma kushirikisha timu 16 tu na zilikuwa zikianza Januari hadi Februari.

Kocha wa Morocco Herve Renard atakuwa akiangali kushinda mara ya tatu taji hilo la Afrika, akiwa na timu ya tatu. Simba hao wa Atlas wako katika Kundi D, pamoja na timu ya Ivory Coast aliyowahi kushindwa nayo taji hilo. Zingine ni Afrika Kusini pamoja na majirani zao Namibia.

Mchezo wa kwanza wa mashindano hayo utawakutanisha wenyeji Misri ambao watacheza na Chui wa Zimbabwe, huku Misri wakitarajia kuwa na nyota wa Liverpool Mohamed Salah katika kikosi chao katika mchezo utakaofanyika Juni 21 kwenye Uwanja wa Cairo.

Timu mbili kati ya tatu ambazo zinashiriki kwa mara ya kwanza fainali hizo, Madagascar na Burundi – ziko katika Kundi B pamoja na Nigeria na Guinea.

Ratiba kamili ya Makundi:

Kundi A: Misri, DR Congo, Uganda, Zimbabwe

Kundi B: Nigeria, Guinea, Madagascar, Burundi

Kundi C: Senegal, Algeria, Kenya, Tanzania

Kundi D: Morocco, Ivory Coast, Afrika Kusini, Namibia

Kundi E: Tunisia, Mali, Mauritania, Angola

Kundi F: Cameroon, Ghana, Benin, Guinea-Bissau

Friday, 12 April 2019

DStv Yazindua Kampeni Kuishangilia Serengeti Boys


Mkurugenzi wa Maendeleo ya Michezo nchini, Dk Yussuf Singo (kulia) akimkabidhi mpira msanii, Amisa Mobeto wakati wa hafla ya kuzindua kampeni ya kuishangilia timu ya taifa ya vijana wenye umri chini ya miaka 17, Serengeti Boys, iliyoandaliwa na DStv kwenye hoteli ya Double Tree Masaki jijini Dar es Salaam.


Na Mwandishi Wetu
WATANZANIA wametakiwa kujitokeza kwa wingi kuishangilia timu ya taifa ya vijana ya wachezaji wenye umri chini ya miaka 17 itakayoshiriki fainali za Mataifa ya Afrika ya Afcon 2019 itakayoanza jijini Dar es Salaam Jumapili.

Serengeti Boys itafungua dimba kwenye Uwanja wa Taifa kwa kucheza dhidi ya mabingwa mara mbili wa Afrika na mabingwa mara tano wa dunia Nigeria.

Mkurugenzi wa Maendeleo ya Michezo nchini, Dk Singo aliyasema jijini Dar e Salaam jana wakati wa hafla ya DStv ya kuhamasisha watu kujitokeza kwa wingi kuishangilia timu hiyo iliyopo katika Kundi A pamoja na Nigeria, Angola na Uganda.

Mkurugenzi wa Maendeleo ya Michezo nchini, Dk Yussuf Singo (wa pili kulia), Mkuu wa Masoko wa MultiChoice Tanzania, Ronald Shelukindo (watatu kulia), mchezaji wazamani wa timu ya taifa ya Tanzania, Amri Kiemba (kushoto) na Salum Salum wa DStv kulia kabisa.

Hafla hiyo iliwahusisha wachezaji wazamani, wasanii na wadau wengine wa michezo kuhakikisha wanatumia nafasi au tasnia zao kuwahamasisha watu kujitokeza kwa wingi kuujaza uwanja huo wa Taifa.

Singo alisema kuwa DStv ambayo imekuwa mstari wa mbele kusaidia maendeleo ya michezo mbalimbali hapa nchini, imebuni kitu cha maana kuhakikisha watoto wetu hao wanaungwa mkono kwa watazamaji kuingia kwa wingi uwanjani na kuwashangilia.
Shumbana.
Naye Mkuu wa Masoko wa MultiChoice Tanzania , Ronald Shelukindo alisema wakati akimkaribisha Singo kuwa ni jukumu la kila Mtanzania kujitokeza kuishangilia Serengeti na wale ambao hawatakuwa na nafasi ya kwenda uwanjani, basi wataziona mechi hizo kupitia DStv.

Alisema  kuwa DStv imeanzisha kampeni hiyo ya uhamasishaji inayojulikana kama ‘DStv Inogile’ na imehakikisha kuwa michuano mbalimbali ya kimataifa inarushwa mubashara tena katika kifurushi cha chini kabisa cha DStv Bomba cha Sh. 19,000 tu.
Baadhi ya wachezaji wazamani walioudhuria hafla hiyo Double Tree Masaka, Dar es Salaam.
Kwa upande wa michuano ya Afcon ya U-17, Shelukindo alisema DStv itakuwa ikifanya kampeni kwa njia mbalimbali ikiwemo kwa njia ya mitandao na matangazo mbalimbali kuhamasisha na kuitia nguvu timu ya taifa ili iweze kufanya vizuri katika mashindano hayo.

Baadhi ya wachezaji wazamani waliodhuria hafla hiyo ni pamoja na Sekilojo Chambua, Edibily Lunyamila, Magoso, Kiemba, Madata Lubigisa na wengineo, wakati wasanii ni Mobeto, Nancy Sumari, John Makini na wengine.







Tuesday, 19 March 2019

MultiChoice Yatangaza Fursa kwa Wadau wa Filam Nchini, Afrika


Na Mwandishi Wetu
KAMPUNI ya MultiChoice-Tanzania imetangaza  fursa ya kipekee kwa wadau wa tasnia ya filamu Tanzania na barani Afrika kwa ujumla ijulikanayo kama MultiChoice Talent Factory Portal iliyodhamiria kuleta mapiduzi ya hali ya juu katika uaandaaji wa filamu zenye viwango vya kimataifa kutoka barani Afrika.

Akizungumza wakati wa uzinduzi wa programu hiyo, Mkuu wa kitengo cha Uhusiano kutoka MultiChoice Tanzania Johnson Mshana alieleza kuwa programu hiyo ni muendelezo wa programu maalum ya iliyodhamiria kuleta mabadiliko katika tasnia ya filamu barani Afrika.

 “MultiChoice Talent Factory ambayo ni progamu mama  ilizinduliwa rasmi mapema  Mei mwaka jana na imedhamiria kuleta mabadiliko chanya kwenye tasnia ya filamu hapa nyumbani Tanzania na Afrika kwa ujumla.

Tulianza kwa kupeleka vijana wanne katika kambi maalum ya mafunzo ya uandaaji filamu katika akademia maalum kule Nairobi nchini Kenya, kisha mafunzo maalum kwa magwiji wa sauti yaliyofanyika Januari mwaka huu na hatimaye leo hii tumekuja tena na platform maalum yenye dhamira ile ile ya kuleta mapinduzi katika tasnia ya filamu barani Afrika”, alisema Mshana.

Kwa upande wake Katibu Mtendaji wa Bodi ya Filamu Tanzania, Joyce Fisoo alisema kuwa, anaishukuru sana Kampuni ya MultiChoice kwani imekuwa mstari wa mbele katika kuleta mapinduzi kwenye tasnia ya filamu hapa Tanzania.

 “Binafsi nilishuhudia uzinduzi wa programu ya MultiChoice Talent Factory mapema mwaka jana kule mjini Dodoma na leo hii tunazindua tena sehemu nyingine ya programu hiyo hiyo. Hakika ni fursa ya kipekee na ninapenda kuchukua nafasi hii kuwahamasisha wadau wote waliopo katika tasnia yetu kuitumia nafasi hii ipasavyo ili kuweza kujifunza, kubadilishana ujuzi na hatimaye kupata kazi zenye maudhui ya hali ya juu kutoka hapa hapa Afrika”,  alisema Fisoo.

Naye Ofisa Uhusiano wa MultiChoice Tanzania Grace Mgaya alimalizia kwa kueleza kuwa ukurasa huu ni wa wazi kwa watu wote hususani wadau wa filamu waliopo hapa nyumbani na Afrika kwa ujumla.

 “Tunaamini kwa kupitia program hii tutaweza kuwafikia wadau wengi zaidi na tunatarajia kazi zenye ubora wa hali ya juu kutoka barani Afrika kwa siku zijazo kutokana na matokeo chanya yatakyoletwa na program hii ya MultiChoice Talent Factory”, alisema Grace.


Wednesday, 6 March 2019

Tanzania Kinara Tena Tuzo za ‘DStv Eutelsat Star Awards’


Mkuu wa Uhusiano wa MultiChoice Tanzania, Johnson Mshana akimkabidhi mshindi wa tuzo za Kimataifa za DStv Eutelsat Star Awards, Pricilla Marealle cheti cha ushindi wakati wa mahafali ya kidato cha sita katika shule ya St Mary Goretti hivi karibuni. Kulia ni Ofisa Uhusiano  wa MultiChoice Tanzania. Grace Mgaya. 

Na Mwandishi Wetu

KWA mara nyingine tena Tanzania imeibuka kinara  katika tuzo za kimataifa za wanafunzi zijulikanazo kama DStv Eutelsat Star Awards ambapo mwanafunzi Priscilla Marealle kutoka shule ya sekondari ya St. Mary Goreti mkoani Kilimanjaro ameweza kuipeperusha bendera ya Tanzania kwa kunyakua nafasi ya kwanza katika kipengele cha uchoraji bango  ikiwa ni baada ya mchuano mkali baina ya mamia ya wanafunzi kutoka nchi zaidi ya 10 kote barani Afrika.

Kwa upande wa uandishi wa insha kijana Tanaka Chonyera kutoka  nchini Botswana aliweza kujinyakulia ushindi wa kwanza.

 Tuzo hizi ambazo huhusisha uandishi wa insha maalum au kuandaa bango yenye ujumbe kuhusiana na elimu ya anga hususan Setelait ni za wazi kwa wanafunzi wote wa shule za sekondari wenye umri kati ya miaka 14 – 19 kote barani Afrika ambapo kampuni ya MultiChoice inaendesha shughuli zake.
Mkuu wa shule ya  St Mary Goretti Sr. Lucrecia Njau akifurahi baada ya kupokea cheti kutoka kwa Mkuu wa Uhusiano wa MultiChoice Tanzania Johnson Mshana mara baada ya shule hiyo kufanikiwa kutoa mshindi wa jumla wa wa tuzo za kimataifa za DStv Eutelsat Star Awards Pricilla Marealle. 
  Katika msimu huu wa nane, washindani walitakiwa kuandika insha au kubuni bango litakaloelezea licha ya Satelait kutumika katika shughuli mbalimbali, ni namna gani zitaweza kutumika zaidi ili kuleta maendeleo chanya ulimwenguni.

 Priscilla ambaye ni mwanafunzi wa kidato cha sita wa mchepuo wa Sayansi katika shule ya Mtakatifu Maria Goreti alitangazwa rasmi kuwa mshindi mjini Accra nchini Ghana ambapo ndipo jopo la watahini liliongozwa na Paolo Nespoli, mwanaanga nguli kutoka European Space Agency (ESA) lilikaa kupitia kazi kutoka kwa wanafunzi walioshinda katika nchi mbalimbali.
Mshindi wa Jumla wa tuzo za kimataifa za DStv Eutelsat Star Awards Pricilla Marealle akikabidhiwa kikombe cha ushindi na Mkuu wa shule ya St Mary Goretti Sr. Lucrecia Njau baada ya kutangazwa kuwa mshindi wa jumla wa wa tuzo za kimataifa za DStv Eutelsat Star Awards. Kulia ni Mkuu wa Uhusiano wa MultiChoice Tanzania Johnson Mshana.
 Akiongea baada ya kukabidhiwa cheti cha uthibitisho wa ushindi wakati wa mahafali ya kidato cha sita ya shule ya Mtakatifu Mary Goreti iliyopo Moshi Kilimanjaro, Priscilla amesema amefurahi sana kwa ushindi huo mkubwa ambao umemletea yeye, shule yake na taifa zima kwa ujumla sifa kubwa. “Nimefurahi sana kupokea taarifa hizi nzuri. Naamini ushindi wangu utakuwa ni chachu kubwa kwa wanafunzi wenzangu kote nchini kujitokeza kwa wingi na kushiriki katika tuzo kama hizi na mashindano mengine ya kitaaluma ya ndani na nje ya nchi, na kusisitiza  kuwa Ndoto huanza kufanya kazi pale unapojiamini” alisema Priscilla.
 
Kwa upande wake mkuu wa shule hiyo ya Mtakatifu Maria Goreti Sister Lucresia Njau alisema kuwa anaishukuru sana kampuni ya MultiChoice Tanzania kwa kuwapatia nafasi ya kushiriki katika Mashindano hayo na hatimaye kuweza kunyakua tuzo hiyo kupitia mwanafunzi wao Priscilla.

 “Huyu kijana ana jitahidi sana katika chochote kile anachokifanya, iwe ni darasani au hata katika majukumu mengine nje ya darasani. Ni msikivu mtiifu lakini zaidi ya yote ni mbunifu sana. Naamini haya ndiyo yaliyomfanya aweze kushinda tuzo hizi” alisema Sr. Lucrecia Njau.
  
Naye, Mkuu wa Uhusiano MultiChoice Tanzania Johnson Mshana alisema,” Huu ni msimu wa tatu mfululizo kwa Tanzania kuendelea kung’ara katika tuzo hizi za DStv Star Awards. Tulianza kupeperusha bendera yetu na kijana Davids Bwana msimu wa sita baada ya kushika nafasi ya pili Afrika katika kipengele cha uandishi wa insha, kisha tukaibuka kidedea baada ya kupokea taarifa za ushindi wa kwanza wa kijana Taheer Rashid katika msimu wa saba mwaka jana na leo hii tunayofuraha kubwa kuona kuwa tumeendeleza wimbi la ushindi.”