Monday 20 May 2019

Guardiola Sasa Ataka Taji Ligi ya Mabingwa Ulaya


LONDON, England
MAFANIKIO ya Manchester City yatakuwa na thamani endapo tu timu hiyo itafanya vizuri katika Ligi ya Mabingwa wa Ulaya licha ya kuweka historia ya kutwaa mataji matatu msimu huu, anasema kocha Pep Guardiola.

Kocha huyo wa Man City, anajua kuwa atakosolewa endapo atashindwa kuiwezesha timu hiyo kufanya vizuri katika mashindano ya Ulaya.

Ushindi wa 6-0 dhidi ya Watford Jumamosi katika fainali ya Kombe la FA likifuatiwa na taji la Ligi Kuu ya England pamoja na lile la Ligi msimu huu.

"Nilisema tangu awali kuwa najua tutahukumiwa mwishoni kama tumeshinda Ligi ya Mabingwa, “alisema Guardiola.

"Bila ya kutwaa taji la Ligi ya Ulaya, basi tutakuwa hatujafanya jambo la kutosha.

"Hilo nililijua mapema, kwani nilipowasili Barcelona, tulikuwa na bahati tulishinda taji hilo la Ulaya mara mbili ndani ya kipindi cha miaka minne na watu walitarajia  kitu maalum kutoka kwangu, ambacho kingetuwezesha kushinda taji la Ligi ya Mabingwa wa Ulaya hapa City, na hilo litaendelea kuwa sahihi.

"Katika klabu hii, rekodi ya klabu katika mashindano ya nyumbani ni nzuri, lakini Ligi ya Mabingwa wa Ulaya hatujawahi kushinda, hivyo sasa tunajukumu la kushinda taji hilo kwa kuwa tuna wachezaji wazuri sana, “alisema.

Man City imeshinda mara nne taji la Ligi Kuu ya England, mawili ya Kombe la FA na manne ya Ligi, tangu klabu hiyo ilipoanza kumilikiwa na Sheikh Mansour mwaka 2008, lakini pamoja na mafanikio hayo haijawahi kutwaa taji la Ligi ya Mabingwa wa Ulaya.

Beki Vincent Kompany amekuwa katika timu hiyo kwa wakati wote huo, ikiwemo miaka nane akiwa nahodha wa Man City, lakini alitangaza Jumapili kuwa ataondoka katika klabu hiyo na kwenda kucheza soka Ubelgiji.

Kompany, 33, atajiunga na klabu ya Ubelgiji ya Anderlecht kama kocha mchezaji kwa mkataba wa miaka mitatu.

No comments:

Post a Comment