Tuesday 11 December 2018

TAA Waendelea Kutoa Kwa Jamii,Yasaidia Tamasha la Ngoma


Mratibu wa Tamasha la Ngoma za Utamaduni na Maonesho ya Biashara la Chato, Amon Mkoga (katikati) akizungumza na waandishi wa habari wakati wa uzinduzi wa tamasha hilo katika Kijiji cha Makumusho Jiini Dar es Salaam leo. Tamasha hilo la tatu litafanyika Chato mkoani Geita Desemba 22, 2018. Kulia ni Meneja  Rasilimali Watu wa Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Tanzania (TAA). 

MAMLAKA ya Viwanja vya Ndege Tanzania (TAA) imeendelea kuwa mstari wa mbele katika kufanikisha shughuli mbali mbali za jamii, kwa kutoa misaada yenye tija.


Hilo limekuwa bayana leo tarehe 12 Disemba, 2018 kwenye Kijiji cha Makumbosho Jijini Dar es Salaam, ambapo TAA imetoa msaada wa fulana 100 kwa ajili ya kufanikisha Tamasha la Utamaduni la Chato linalotarajiwa kufanyika tarehe 22 Disemba, 2018 katika Uwanja wa Mazaina Chato.

Akizungumza katika Mkutano wa waandishi wa habari Kaimu Mkurugenzi Rasilimali Watu na Utawala wa TAA, Bw. Abdi Mkwizu amesema Mamlaka ina wajibu mkubwa wa kuunga mkono shughuli za kijamii, kwa kutoa misaada ya mbalimbali.

   Kaimu Mkurugenzi wa Rasimali Watu na Utawala wa Viwanja vya NdegeTanzania (TAA), Abdi Mkwizu akizungumza wakati wa uzinduzi wa Tamasha la za Utamaduni la Chato katika Kijiji cha Makumbusho ya Taifa Jijini Dar es Salaam leo. 
“Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Tanzania ina wajibu wa Kusimamia, kuendesha, kuboresha na kuendeleza Viwanja vya Ndege Tanzania lakini pia mbali na kutoa huduma hizo tuna wajibu wa kushiriki katika shughuli za kijamii, kwa wadau ambao wanatufanya sisi tuwepo,” amesema Bw. Mkwizu.

Pia Bw. Mkwizu amebainisha kwamba TAA inahudumia Viwanja 58 vilivyopo Tanzania Bara chini ya serikali, hivyo ni wajibu wao kushiriki katika shughuli za kusaidia jamii sehemu yeyote ile kulingana na uhitaji na bajeti iliyopo.



 Mwenyekiti wa Bodi ya Baraza la Sanaa Taifa (BASATA) Bw. Habbi Gunze (kushoto) akizungumza wakati wa uzinduzi wa Tamasha la Tatu la  za Utamaduni katika Kijiji cha Makumbusho. Kulia ni Meneja Rasilimali Watu wa Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Tanzania (TAA),Abdi Mkwizu na mwingine ni mratibu wa tamasha hilo, Amon Mkoga. Tamasha hilo litafanyika Chato mkoani Geita.


“Ikumbukwe siku za hivi karibuni TAA tumeshirika katika kufanikisha Tamasha la Urithi Wetu lililofanyika kuanzia Oktoba Mosi mpaka Oktoba 7, 2018 katika Kijiji cha Makumbusho, tumetoa pia msaada wa Mafuta Kinga jua ya Ngozi kwa watoto wenye ulemavu wa Ngozi katika baadhi ya shule hapa Dar es Salaam, lakini pia tarehe 24 Novemba mwaka huu tumekabidhi Shule ya Msingi ya Kisasa huko Bukoba inaitwa Tumaini,  na tunaamini itaongeza ufaulu kwa wanafunzi huko Bukoba na hayo ni macheche kati ya mengi ambayo Mamlaka inafanya kwa Jamii” amebainisha Bw. Mkwizu.
Kaimu Mkurugenzi Rasilimali Watu na Utawala wa Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Tanzania (TAA), Bw. Abdi Mkwizu (kulia) akikabidhi moja ya fulana,zilizotolewa na TAA kwa ajili ya Tamasha la Ngoma za Utamaduni la Chato, linalotarajia kufanyika Desemba 22, 2018.
Akizungumza kwa niaba ya Waziri Mkuu na niaba ya Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Mwenyekiti wa Bodi ya Baraza la Sanaa Taifa (BASATA) Bw. Habbi Gunze ameishukuru Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Tanzania kwa mchango wake kufanikisha Tamasha la Utamaduni la Chato.

“Niwashukuru sana Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Tanzania kwa mchango wao nap engine bila wao hili la leo lisingeweza kufanikiwa. Utamaduni ndio uhai wa Taifa, kwa hiyo nchi isipokua na Utamaduni nchi inakua sio hai, hivyo kwa Mchango huu wa kusaidia hili nawapongeza sana TAA” amesema Bw. Gunze.
Mcheza ngoma za asili, Bw,. Ally Mango akicheza na nyoka mbele ya waandishi wa Habari katika kikiji cha Makumbusho jijini Dar es Salaam, wakati wa utoaji wa fulana 100 kwa tamasha la Utamaduni la Chato zilizotolewa leo na Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Tanzania (TAA).  (PICHA ZOTE KWA HISANI YA MAMLAKA YA VIWANJA VYA NDEGE TANZANIA)
Naye Mkurugenzi wa Chief Promotions ambaye ndie mratibu wa Tamasha hilo Bw. Amon Mkoga amesema kwamba Tamasha litakuwa na mambo yote ya kiutamaduni ili kuenzi asili ya Kitanzania.

“Kauli mbiu ya Tamasha la Utamaduni la Chato inasema “Maendeleo ya Viwanda yasiache Utamaduni nyuma” ambapo Tamasha hili ni maalum kwa ajili ya kuuenzi utamaduni wa Mtanzania. Katika Tamasha hili kutakua na Vikundi mbalimbali vya Utamanduni. Vikundi vya ngoma vitakuwepo kutoka Simiyu, Shinyanga, Geita, Mwanza, Tabora na Chato wenyewe, hivyo tunawaomba wananchi mtusaidie kufikisha taarifa hizi kwa watanzania” ameeleza Bw. Mkoga.
Mkurugenzi wa Chief Promotions Bw. Amoni Mkoga (katikati), Mwenyekiti Bodi ya Baraza la Salaa la Taifa (BASATA), Bw. Habbi Gunze (kushoto) na Kaimu Mkurugenzi Rasilimali Watu na Utawala kutoka Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Tanzania (TAA), Bw. Abdi Mkwizu, wakionesha vipeperushi vya Tamasha la Ngoma za Utamaduni la Chato.
Tamasha la Utamaduni la Chato ni tamasha kubwa la ngoma ambalo hufanyika kila mwaka na hii itakua ni mara ya tatu mfululizo likifanyika Chato mkoani Geita.





No comments:

Post a Comment