Saturday 27 January 2018

TAA Yarudishiwa Kiwanja cha Ndege cha Kahama

 Naibu Waziri Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano (Sekta ya Ujenzi), Mhe. Elias Kwandikwa (wanne kulia), Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga, Bi. Zainab Telack (Mwenye ushungi) na Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Tanzania (TAA), Bw. Richard Mayongela (watatu kulia), jana wakikagua miundombinu ya Kiwanja cha Ndege cha Kahama kabla ya makabidhiano ya kurudishwa serikalini na Kampuni ya Madini ya ACACIA.
Na Mwandishi Wetu, Kahama
KAMPUNI ya madini ya ACACIA yenye kumiliki migodi ya dhahabu ya Buzwagi na Bulyahulu imekirudisha serikalini Kiwanja cha Ndege cha Kahama kwa ajili ya kuchochea maendeleo kwa ujumla.

Awali mwaka 2005 kiwanja hicho kilikabidhiwa kwa makabidhiano maalum kati ya serikali na iliyokuwa kampuni ya madini ya Barrick walioomba ili kurahisisha shughuli zao za migodini ikiwemo ya kutumia ndege kusafirisha wafanyakazi wao na vifaa.
 Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga, Bi. Zainabu Telack akihutubia wananchi waliofika kushughudia makabidhiano ya Kiwanja cha Ndege cha Kahama yaliyofanyika jana baina ya Kampuni ya Madini ya ACACIA na Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Tanzania (TAA).
Katika makabidhiano hayo yaliyofanyika jana mbele ya Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga, Bi. Zainab Telack na Naibu Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano (Sekta ya Ujenzi), Mhe. Elias Kwandikwa, Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Tanzania (TAA), Bw. Richard Mayongela aliiomba serikali kusaidia kurefusha barabara ya kutua na kuruka kwa ndege kutoka Km. 1.5 hadi kufikia Km 2, ili kufanikisha utuaji wa ndege kubwa ikiwemo ya Shirika la ndege la Tanzania (ATCL) aina ya Bombardier Q400.
Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Tanzania (TAA), Bw. Richard Mayongela (watatu kulia), akisaini nyaraka za makubaliano ya kurudishwa Kiwanja cha Ndege cha Kahama kwa serikali kutoka kwa Kampuni ya Madini  ya ACACIA, ambapo wa pili kulia ni Meneja wa migodi ya dhahabu ya Buzwagi na Bulyahulu, Bw. Benedict Busuzu na wakwanza kulia ni Mwanasheria wa ACACIA, Bi Diana Wamuza, huku Naibu Waziri Sekta ya Ujenzi, Mhe. Elias Kwandikwa (mwenye miwani) na Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga, Bi. Zainab Telack wakishughudia.
“Tunashukuru wenzetu wa ACACIA kwa kurudisha tena serikalini kiwanja hiki, lakini bado tunaimani tutaendeleza ushirikiano baina yetu, lakini ombi langu kwa serikali ni kuongeza urefu wa barabara ya kutua na kuruka kwa ndege ili ndege kubwa zaidi ziweze kutua ninaimani zitachochea shughuli za kilimo, biashara na madini na uchumi wananchi utaimarika zaidi,” alisema Bw. Mayongela.
 Mwanasheria wa ACACIA, Bi. Diana Wamuza (wa kwanza kulia) akishughudiana makabidhiano ya nyaraka za kurudishwa kwa Kiwanja cha ndege cha Kahama uliofanywa jana na Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Tanzania (TAA) na Meneja wa migodi ya dhahabu ya Buzwagi na Bulyahulu, Bw. Benedict Busuzu.
Naye Naibu Waziri, Mhe. Kwandikwa alisema serikali itahakikisha inasaidiana na wadau mbalimbali ili waweze kurefusha barabara ya kutua na kuruka kwa ndege, ili kufanikisha utuaji wa ndege kubwa za abiria na mizigo, ambazo zitachochea maendeleo ya Wilaya ya Kahama na Mkoa wa Shinyanga kwa ujumla.

Hatahivyo, Mhe. Kwandikwa aliwataka ACACIA kuweka katika mipango yao ya kusaidia ujenzi wa upanuzi na urefushaji wa Kiwanja cha ndege cha Kahama, ili kiweze kutumika kwa lengo la kutua kwa ndege kubwa, ambapo itachochea sera ya kukuza viwanda.
Naibu Waziri Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano (Sekta ya Ujenzi), Mhe. Elias Kwandikwa akizungumza mara baada ya makabidhiano ya kurudishwa serikalini Kiwanja cha Ndege cha Kahama kutoka kwa Kampuni ya Migodi ya ACACIA, uliofanyika jana mkoani Shinyanga.  Mwenye ushungi ni Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga, Bi. Zainab Telack na wa kwanza kulia ni Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Tanzania (TAA), Bw. Richard Mayongela.
“Tunamaeneo mengi sana hapa Shinyanga, tunawaita wawekezaji waje kuwekeza kwa wingi katika ujenzi wa viwanda, kilimo, madini na biashara nyingine, sasa usafiri wa uhakika upo ukizingatia tunaviwanja viwili vya ndege kikiwemo hiki cha Kahama na kile cha Shinyanga, na malighafi, umeme na maji vipo vya kutosha hivyo waje tu kuwekeza,” alisisitiza Mhe. Kwandikwa.

Kwa upande wake Mkuu wa Mkoa, Bi. Telack alisema sasa mkoa wake utainuka kwa kuwa umepata fursa ya kuongezewa kiwanja cha pili cha ndege cha Kahama, ambapo sasa wananchi wataweza kusafirisha mazao ya kilimo na kufanya biashara na mikoa mingine kutokana na usafiri wa ndege ni wa haraka na uhakika.

“Ninakuomba Naibu Waziri najua hili lipo kwenye wizara yako, utusaidie kuharakisha kumalizika kwa kiwanja cha ndege cha Shinyanga, maana hiki hapa tayari kipo ili na sisi tuweze kupata wawekezaji katika viwanda mfano Wachina wasiende kuwekeza mkoani Pwani pekee bali waje na huku, tunaimani tutachochea maendeleo sio ya mkoa wetu tu ila kwa Taifa kwa ujumla,” alisema Bi. Telack.

Kwa upande wa Meneja wa migodi ya dhahabu ya Buzwagi na Bulyahulu, Bw. Benedict Busuzu alisema wanajivunia tukio la kurudisha kiwanja cha ndege cha Kahama kwa serikali, ili sasa kiweze kutumika na Watanzania wote katika kuchochea ukuaji wa viwanda.


Hata hivyo, Bw. Busuzu ameahidi wataendelea kutoa huduma mbalimbali kwenye kiwanja hicho kama ilivyokuwa awali, na wataendeleza ushirikiano mzuri ulipo kati yao na TAA.

No comments:

Post a Comment