Tuesday 3 December 2019

Uchukuzi Sports Club Yakabidhi Mataji ya Mei Mosi 2019


Kaimu Katibu Mkuu wa wizara hiyo Sekta ya Uchukuzi, Gabriel Migile (wa pili kushoto) akipokea moja ya vikombe vya Michuano ya Mei Mosi 2019 kutoka kwa Makamu Mwenyekiti wa Uchukuzi Sports Club (USC), Hassan Hemed. Wa pili kushoto ni Katibu wa USC, Mbura Tena na Mkurugenzi Msaidizi Utawala Hamidu Mbegu.

Na Mwandishi Wetu
TAASISI zilizopo katika Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano zimetakiwa kupanga bajeti ya michezo  katika bajeti zao za mwaka ili kuhakikisha wanashiriki vizuri katika michezo,  imeelezwa.
Hayo yalisemwa jana na Kaimu Katibu Mkuu wa wizara hiyo Sekta ya Uchukuzi, Gabriel Migile baada ya kukabidhiwa vikombe vya ushindi wa Mashindano ya Mei Mosi 2019 kutoka kwa Makamu Mwenyekiti wa Uchukuzi Sports Klabu (UCS), Hassan Hemed.

Akijibu changamoto zilizotolewa na Katibu Mkuu wa Uchukuzi Sports Club, Mbura Tenga, ambaye katika risala yake ya utangulizi alieleza moja ya changamoto zinazowakabili ni kwa baadhi ya taasisi kushindwa kutenga fedha kwa ajili ya michezo.

Tenga alisema kuwa hilo la kushindwa kutenga fedha linatokana na taasisi hizo kutokuwa na bajeti kabisa ya michezo na wengi wa maofisa rasilimali watu wake kutojua kabisa umuhimu wa michezo kazini na kuona kama ni kupoteza muda na fedha tu.

Migire alisema kuwa taasisi nazo zinatakiwa kuiweka michezo katika bajeti za idara zao za kila mwaka ili kuhakikisha wachezaji wao wanashiriki kutoa wachezaji katika Uchukuzi Sports Club.

Migile pia aliipongeza Uchukuzi Sport Klabu kwa kutwaa ubingwa wa jumla kwa mara ya pili mfululizo katika Mashindano ya Mei Mosi, baada ya mwaka huu kutwaa jumla ya vikombe tisa, vinne vikiwa katika nafasi ya kwanza, ambavyo ni Kuvuta Kamba kwa Wanaume na Wanawake na Baiskeli kwa Wanauame na Wanawake.

Uchukuzi Sports Klabu katika Mashindano ya Mei Mosi mwaka huu yaliyofanyika Mbeya, walitwaa vikombe tisa kati ya 14, ambavyo hushindaniwa kila mwaka.

Uchukuzi pia ndio klabu pekee katika mashindano hayo kupeleka timu za michezo yote 14 ya mashindano hayo, tofauti na wizara zingine, ambazo wakati mwingine hupeleka timu au mchezaji mmoja.

Akijibu kuhusu timu ya Uchukuzi mara mbili kualikwa Zanzibar (Unguja na Pemba) na Mamlaka ya Viwanja vya Ndege ya Zanzibar (ZAA) na kufanya utalii wa ndani,  alisema hilo ni suala ni muhimu sana, hasa ukizingatia linahusu Muungano, ambapo liwataka kupanga utaratibu kuona USC wanafanyaje ili kuwaalika Bara Wazanzibari.

Pia alisema changamoto ya kutokuwa na ofisi inayoikabili USC llinaweza kushughulikiwa, hasa ukizingatia kuwa Katiba ya UCS inaeleza kuwa Mwenyekiti wa klabu hiyo, lazim atoke wizarani, hivyo itakuwa rahisi kuwepo kwa ofisi wizarani kwa ajili ya klabu yao.

Akielezea kuhusu ushindi huo wa jumla, alisema kuwa ni mkubwa sana, hivyo hauwezi kupita kimya kimya, kwani lazima na wakubwa nao wajue nini kimeletwa na USC, hivyo hafla hiyo itaandaliwa tena kwa ukubwa wake.

Aidha, Tenga alisema wanatarajia Februari 7, 2020 kufanya Mkutano mkuu kwa ajili ya mabadiliko ya Katiba pamoja na kuchagua viongozi wapya, ambapo kila taasisi ina kuwa na mwakilishi katika klabu hiyo, tofauti na sasa ambapo taasisi moja inaweza kuwa na zaidi ya mjumbe mmoja na nyingine isiwe nayo kabisa.

No comments:

Post a Comment