Thursday 29 March 2018

Timu ya Madola Yaondoka na Matumaini Kibao


Wachezaji na viongozi wa timu ya Tanzania itakayoshiriki Michezo ya Jumuiya ya Madola wakiwa katika picha ya pamoja kwenye Kiwanja cha Ndege cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNIA) Dara es Salaam leo , kabla ya kuondoka kwenda Gold Coast, Australia.
Na Mwandishi Wetu
KUNDI la wachezaji 15 na viongozi kadhaa la timu ya Tanzania itakayoshiriki Michezo ya 21 ya Jumuiya ya Madola, limeondoka leo kwenda Gold Coast, Australia tayari kwa michezo hiyo itakayoanza Aprili 4 hadi 15.

Tanzania katika michezo hiyo inawakilishwa na timu za riadha, ngumi, mpira wa meza na kuogelea.

Timu hiyo ikiongozwa na meneja wao, Nasra Juma iliondoka kwa ndege ya Emirates huku nahodha wake, Masoud Mtalaso akitamba kuwa wako tayari kwa kuiletea nchi medali.
Makamu wa rais wa Kamati ya Olimpiki Tanzania (TOC), Henry Tandau akizungumza na wachezaji wa Tanzania watakaoshiriki Michezo ya Jumuiya ya Madola, kwenye Kiwanja cha Ndege cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNIA) Dar es Salaam.
Kwa mara ya mwisho Tanzania ilipata medali kutoka katika Michezo ya Jumuiya ya Madola mwaka 2006 Melbourne, Australia, ambako Samson Ramadhani na Fabian Joseph walirudi na medali ya dhahabu na shaba katika mbioza marathon na meta 10,000.

Rais na Katibu Mkuu wa Kamati ya Olimpiki Tanzania (TOC), Gulam Rashid na Filbert Bayi wenyewe waliondoka Jumatano mara baada ya timu hiyo kuagwa na Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo Dk Harrison Mwakyembe huku kiongozi wa msafara, ambaye ni Mkurugenzi wa Michezo Dk Yussuf Singo aliondoka tangu Jumapili.


“Tumekuwa tukifanya mazoezi ya nguvu kwa muda mrefu na ni matarajio yetu kuwa tutafanya vizuri katika michezo hiyo, “alisema Kidunda.

Naye Mtalaso alisema kuwa timu ya mpira wa meza imejiandaa vizuri hasa ukizingatia kuwa walipiga kambi nchini China kwa takribani miezi mitatu wakijifua kwa ajili ya michezo hiyo kabla ya kurejea nchini na kupiga kambi kwa mwezi mmoja Mkuza, Kibaha mkoani Pwani.


Australia imekuwa sehemu ya bahati kwa timu ya Tanzania, ambapo ilifanya vizuri mwaka 1982 wakati ilipotwaa medali sita: Moja ya ngumi, tatu za riadha na mbili zilitoka katika mbio za uwanjani.
Gidamis Shahanga alitwaa medali ya dhahabu katika mbio za meta 10,000, wakati Zakaria Barie, ambaye amesafiri na timu hiyo kama kocha, alishinda medali ya fedha katika mbio kama hizo. Juma Ikangaa alirudi na medali ya fedha katika marathon, huku ile ya shaba ikiletwa na bondia wa uzito wa juu, Willy Isangura na mtupa mkuki Zakayo Marekwa naye alileta medali ya shaba.

Mwanariadha wazamani wa Tanzania, Bayi ikiwa ni miaka 44 sasa anaendelea kushikilia rekodi ya Jumuiya ya Madola aliyoiweka mwaka 1974 ya meta 1500 michezo hiyo ilipofanyikia Christchurch, New Zealand. Bayi pia aliweka rekodi ya dunia, ambayo ilikuja kuvunjwa miaka mitano baadae na Sebastian Coe, ambaye sasa ni Rais wa Shirikisho la Kimataifa la Vyama vya Riadha (IAAF).
Ikiwa ni miaka 12 sasa tangu kufanyika kwa Michezo ya Melbourne, timu ya Tanzania yenye wachezaji 16 inarejea tena Australia, ikiwa pia na micezo ambayo haikuwepo walipofanya vizuri nchini humo kama mpira wa meza na kuogelea.

Timu ya riadha inaundwa na wanariadha wa marathon, Stephano Huche, Said Makula na Sarah Rama­dhani.

Wakati Failuna Abdul atashindana katika mbio za meta 10,000, huku Ali Khamisi Gulam, atafanya vitu vyake katika mbio za meta 100 na 200, akiwa ni mwanariadha pekee wa mbio fupi katika timu ya riadha.

Anthony Mwanga ambaye anasoma Afrika Kusini, yeye atachuana katika michezo ya uwanjani ya miruko na mitupo katika timu hiyo ambayo iko chini ya Barie na Lwiza John.

Kikosi cha timu ya ngumi kinaundwa na Ezra Paulo (bantam), Kassim Mbutike (welter), Seleman Kidunda (middle) na Haruna Swanga (heavy). Timu hiyo iko chini ya kocha Mkenya, Benja­min Oyombi.

Awali kulikuwa na waogeleaji wawili, Hilal Hilal na Sonia Franco, chini ya kocha Kha­lid Yahya Rushaka. Wacheza mpira wa meza wako wanne, ambao ni Amon Tumaini, Masoud Mtalaso, Neema Mwaisyula na Fathiya Paz, ambao wako chini ya kocha Ramadhani Othman Suleiman.

Naibu Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Juliana Shonza, anatarajia kujiunga na timu hiyo baadae.

No comments:

Post a Comment