Saturday 11 February 2017

Mwandishi Arnold Swai aliyekufa kwa ajali ya gari azikwa kwao Hai, Kilimanjaro



Na Mwandishi Wetu
VILIO, majonzi na simanzi vilitawala jana katika kijiji cha Mbweera, Wilaya ya Hai mkoani Kilimanjaro wakati wa mazishi ya Mwandishi wa gazeti la Habarileo, Arnold Swai (28) anayetajwa kuwa ni "Nyota iliyong'aa na kuzimika ghafla".

Swai aliyekuwa pia Mwenyekiti wa Umoja wa Vijana CCM, (UVCCM) wilayani Hai alifikwa na mauti jumapili iliyopita katika ajali ya gari iliyotokea katika eneo la Mwika, Moshi vijijini na kusababisha vifo vya watu wanane.

Kwa mujibu wa gazeti la leo la Habarileo, Katibu Mkuu wa CCM, Abdulrahman Kinana, aliongoza umati wa waombolezaji waliofika kuuga mwili wa Swai katika kanisa la Kiinjili Kilutheri (KKKT) usharika wa Masama kati na kuzikwa kijijini kwao.

Kinana alisema, Swai alikuwa na maono makubwa na kama asingefariki angekuwa kijana ambaye angeshika nafasi mbalimbali za uongozi na angetoa mchango kwa taifa na kwa taaluma yake.

"Mungu ametuleta duniani na atatutoa kwa muda wake, lakini ameweka siri ya siku ya kutuondoa ndiyo maana tunahuzunika. Tuwe watu wema wenye huruma, tumkumbuke Mungu na kuwasaidia wengine, Arnold alitimiza hilo". Alisema

Akizungumza katika ibada, Mchungaji Andrew Munisi aliwataka vijana kuacha kujihusisha na dawa za kulevya na kunywa pombe badala yake wafanye kazi na kuiga mfano wa Swai ambaye alikuwa kijana mwenye maono na muwajibikaji.

Baadhi ya waandishi wa habari waliofanyakazi na Swai walisema, ingawa alikuwa mwanasiasa, lakini alitofautisha muda wake wa kufanya siasa na kazi zake kitaaluma.

Msiba huo ulihudhuriwa na viongozi mbalimbali wa serikali na wa CCM, akiwemo Waziri wa Maliasili na Utalii, Profesa Jumanne Maghembe, Mkuu wa Mkoa wa Kilimanjaro, Said Meck Sadiki, Kamanda wa Polisi Mkoa, Wilbroad Mutafungwa, Mwenyekiti wa CCM mkoa, Iddy Juma, viongozi mbalimbali wa UVCCM, wakuu wa wilaya na madiwani.

Swai alifikwa na mauti ajalini wakati akitoka kwenye maadhimisho ya miaka 40 ya kuzaliwa kwa CCM, ambayo kimkoa yalifanyika Rombo, katika tarafa tano kwa kufanya mikutano ya ndani.

No comments:

Post a Comment