Monday 13 August 2018

Uchukuzi Sports Yakabidhi Vikombe vya Mei Mosi


Mkurugenzi wa Utawala na Rasilimali Watu wa Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano (Sekta ya Mawasiliano), Grayson Mwaigombe (watano kushoto) baada ya kupokea vikombe vya ushindi vya Mashindano ya Mei Mosi  2018 kutoka kwa Makamu Mwenyekiti wa Klabu ya Michezo ya Uchukuzi (USC), Hassan Hemed  (wanne kulia) Jijini Dar es Salaam jana, Watatu kulia ni Katibu wa klabu hiyo, Mbura Tenga. (Na Mpigapicha Wetu).

Na Mwandishi Wetu
KLABU ya Michezo ya Uchukuzi imekabidhi rasmi vikombe vya ushindi wa michezo mbalimbali vya mashindano ya Mei Mosi 2018 yaliyofanyika mwaka huu mkoani Iringa, ambako pia ilitwaa ubingwa wa jumla.

Makamu Mwenyekiti wa Uchukuzi Sports Club (USC), Hassan  Hemed ndiye aliyekabidhi vikombe hivyo kwa Mkurugenzi na Utawala na Rasilimali Watu, Grayson Mwaigombe aliyepokea kwa niaba ya Katibu Mkuu Wizara ya Uchukuzi,Ujenzi na Mawasiliano (Sekta ya Uchukuzi), Dk Leonard Chamuriho.
Katika hafla hiyo fupi iliyofanyi katika wizara hiyo jijini Dar es Salaam, USC ilikabidhi jumla ya vikombe 13 ilivyovitwaa katika Mashindano hayo ya Mei Mosi 2018, ambapo katika michezo iliyotwaa nafasi ya kwanza iibeba jumla ya vikombe saba.

Katika nafasi ya pili, USC ilitwaa vikombe viwili vya michezo ya netiboli na Kamba kwa wanawake, huku vikombe vya nafasi ya tatu vilikuwa viwili, ambavyo ni vya Karata kwa wanawake na wanaume.
Makamu Mwenyekiti wa Uchukuzi Sports Club (UCS), Hassan Hemed (kulia) akimkabidhi jezi Mwenyekiti wa TUGHE Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, Joseph Matiku katika hafla iliyofanyika jijini Dar es Salaam leo.
Kwa mujibu wa Katibu Mkuu wa USC Mbura Tenga, vikombe ambavyo klabu yao ilipata kwa kutwaa nafasi ya kwanza ni pamoja na Mbio za baskeli, bao, drafti na kuvuta kamba vyote kwa wanaume wakati kwa wanawake ushindi wa kwanza ulikwenda katika michezo ya mbio za baiskeli, draft na bao.

Chamuriho aliipongeza klabu hiyo kwa kutwaa ubingwa huo na kuwapa muda wa kuijenga zaidi klabu yao hiyo ili iweze kufanya vizuri katika mashindano mengine.
Makamu Mwenyekiti wa USC, Hassan Hemed (kulia) akiwa na wajumbe wengine wa klabu hiyo wakimsikiliza mgeni rasmi.
Klabu ya Uchukuzi mbali na mashindano hayo ya Mei Mosi,  pia hushiriki ile ya Shirikisho la Michezo ya Wizara na Idara za Serikali (Shimiwi), ambayo nayo hufanyika kila mwaka.

Timu ya Uchukuzi mwaka huu imefanya vizuri zaidi tofauti na miaka ya nyuma na pia ilitunikiwa cheti cha ushiriki cha Mei Mosi 2018 kama mshindi wa jumla, huku Ofisa Habari Bi Bahati Mollel wa Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Tanzania (TAA) alitunikiwa cheti maalum cha ushiriki kwa kutambua usambazaji wa taarifa kwa vyombo vya habari.

Mkurugenzi wa Utawala na Rasilimali Watu wa Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano (Sekta ya Mawasiliano), Grayson Mwaigombe akizungumza wakati  wa kupokea makombe ya Mashindano ya Mei Mosi kutoka kwa Klabu ya  Michezo ya Uchukuzi.

No comments:

Post a Comment