Saturday 1 September 2018

TAA Yachangia Vyoo Salama kwa Mtoto wa Kike


1.   Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Tanzania (TAA), Bw. Richard Mayongela (kulia) akiwaongoza Wafanyakazi wa Mamlaka hiyo, Mkurugenzi wa Kiwanja cha Ndege cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNIA), Bw. Paul Rwegasha (katikati) na Ofisa Uhusiano, Bi. Bahati Mollel (wapili kulia) kukabidhi mfano wa hundi yenye thamani ya Sh Mil 5 Spika Mstaafu wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Anne Makinda (wapili kushoto) na Mwenyekiti wa Kamati ya maandalizi ya hafla hiyo, Mbunge wa Muleba Kusini, Prof. Anna Tibaijuka. Hafla hiyo ilifanyika jana usiku kwenye ukumbi wa Mlimani City jijini Dar es Salaam.



Na Mwandishi Wetu

MAMLAKA ya Viwanja vya Ndege Tanzania (TAA), imeunga mkono juhudi za Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kupitia Umoja wa Wabunge Wanawake wa Bunge hilo (TWPG) kukusanya fedha kwa ajili ya kujenga vyoo salama vya shule nchi nzima kwa ajili ya mtoto wa Kike kwa kutoa mchango wa kiasi cha Sh Mili 5.

Hafla hiyo imefanyika katika ukumbi wa Mlimani City Jijini Dar es Salaam.

Mkurugenzi Mkuu wa TAA, Bw. Richard Mayongela, alikabidhi msaada huo wa fedha kwa mgeni rasmi, Spika Mstaafu wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Anne Makinda.

Akizungumza kwenye hafla hiyo iliyoudhuriwa na viongozi mbalimbali, wakiwemo Wabunge, Wakuu wa Taasisi za Umma na Binafsi, Spika wa Bunge Mhe. Job Ndugai, aliwapongeza Wabunge hao kwa hatua hiyo ya kuhakikisha kunakuwepo kwa mazingira bora shuleni ili kutoa haki sawa ya kupata elimu kwa wanafunzi wa jinsia zote.

“Wazo hili litasaidia sana serikali katika kuhakikisha mazingira ya shule yanaboreshwa ili kutoa nafasi sawa kwa wanafunzi wote wa kike na kiume,” alibainisha Spika Ndugai.

Alisema Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. John Pombe Magufuli, amefurahishwa na kitendo hicho na kwamba ameshindwa kuhudhuria hafla hiyo kwa vile bado yupo kwenye msiba wa dada yake huko Chato mkoani Geita.

Kwa upande wake, mgeni rasmi Mhe. Anne Makinda aliwapongeza Wabunge hao wanawake kwa hatua hiyo ya kuunga mkono juhudi za serikali na kuwataka Wabunge wanaume kuwaunga mkono wenzao katika kufanikisha kampeni hiyo inayolenga kukusanya kiasi cha shilingi bilioni 3.5 zitakazowezesha kujenga vyoo salama vya shule kwenye majimbo yote 264 nchi nzima.
Taasisi Mbalimbali zilichangia kwenye harambee hiyo, ambapo pia vitu mbalimbali vilinadiwa na fedha zitakazopatikana zitakwenda kufanya kazi ya ujenzi huo.

No comments:

Post a Comment