Sunday 19 July 2015

Diamond Plutinumz ang'ara tuzo za MTV Mama Afrika Kusini




Na Mwandishi Wetu
MWANAMUZIKI wa muziki wa kizazi kipya, Nassib Abdul, Diamond Plutinumz ameng'ara kwenye shindano la MTV Mama Awards lililofanyika usiku wa kuamkia leo, Afrika Kusini na anatarajiwa kuwasili nchini Jumanne.

Katika tuzo hizo zilizofanyika jijini Kwazulu Natal katika Ukumbi wa Kimataifa wa Durban Diamond alishinda kwenye kipengele cha mburudishaji bora wa mwaka.

Katika kinyang'anyiro hicho wasanii kutoka Nigeria waling'ara zaidi katika vipengele mbalimbali huku Tanzania ikiwakilishwa na Diamond.

Akizungumza na gazeti hili kuhusianana ushindi huo Meneja wa msanii huyo, Babu Tale alisema kuwa ushindi huo ni mafanikio kwa Tanzania na sekta nzima ya muziki kwa kuwa umeliletea heshima taifa.

Alisema kuwa kwa ushindi huo umesaidia kumtangaza kimataifa zaidi na umeanza kufungua milango nje ya nchi kwa kuwa kwa sasa inakuwa kwake ni rahisi zaidi kumnadi msanii wake huyo.

Alisema " Hii ni zawadi kwa watanzania wote kwa ujumla na msanii wetu amewainua kimasomaso na huu ni mwanzo tu kwa kuwa kazi ndio kwanza inaanza na tuna uhakika wa kufika mbali zaidi na kuwakilisha vema sanaa ya Tanzania"
  
Katika shindano hilo wasanii mapacha wanaounda kundi la P square, Peter and Paul walichaguliwa kama wasanii bora wa mhongo huu

Kwa upande wa mwanamuziki bora wa kike nafasi ilichukuliwa na mwanamuziki Yemi Alade wa Nigeria huku mshindi wa kipengele cha mburudishaji bora wa kiume ikienda kwa Davido.

Kundi la P Square pia lilichaguliwa kama kundi bora la mwaka, Cassper Nyovest wa Nigeria aliibuka kama mwanamuziki bora wa Hip Hop na mwanamuziki AKA wa Afrika Kusini akiwa na mwenzake Burna Boy walishinda kwenye kipengele cha wimbo bora wa kushirikishwa.

Wimbo bora wa mwaka ulikuwa ni ule wa All Eyes On Me ulioimbwa na Da Les kwa ushirikiano na & JR huku ule wimbo wa  Dorobucci nao kutoka Nigeria ukishika nafasi ya kuwa wimbo bora wa jukwaani.


No comments:

Post a Comment