Friday 23 December 2016

DSTV yawakabidhi Ving'amuzi vya bure na vifurushi vya mwezi mzima washindi 24 wa Kapu la Sikukuu



Na Mwandishi Wetu
KAMPUNI ya Multichoice Tanzania kupitia king’amuzi chake cha DStv leo imekabidhi ving’amuzi 24 vya kisasa  pamoja na vifurushi vya mwezi mzima kwa washindi wa shindano la ‘Kapu la Sikukuu’ lililoendeshwa kwa ushirikiano na Kituo cha Radio cha EFM.

Washindi hao sasa wataweza kusheherekea kwa mbwembwe Siku Kuu ya Krismas na Mwaka Mpya huku wakiangalia chaneli zaidi ya 70 kupitia king’amuzi hicho cha DStv ikiwemo michezo mbalimbali pamoja na Ligi Kuu ya Hispania ya La Liga, Ligi Kuu ya England,

Pia katika kifurushi hicho walichopata kama zawadi kina chaneli ya Maisha Magic Bongo yenye sinema na tamthilia za Kitanzania ikiwemo ile maarufu kama ya Huba, ambapo wakongwe wa filamu nchini kama akina Muhogo Mchungu, Rihami Ali, Mboto, na Hashim Kambi wanaonekana katika tamthilia hiyo iliyopata umaarufu mkubwa.

Katika hafla hiyo msanii maarufu, Mboto na Irene Paul ndio waliokabidhi zawadi kwa washindi katika hafla hiyo iliyofanyika leo nje ya Kituo cha Radio cha EFM Kawe jijini Dar es Salaam.

Akizungumza kabla ya kukabidhi zawadi hizo kwa washindi Mkuu wa Wilaya ya Ilala, Sophia Mjema aliwapongeza EFM kwa jitihada zao na kuhakikisha wanapata wasikilizaji wengi.

Aidha, Mjema aliwasifu Dstv kwa kutoa zawadi hizo kwa washindi kwani ni kitu muhimu ambacho pia kitawasaidia kuongeza wateja kwa kuwashindanisha na washindi kuwapa zawadi katika bahati nasibu iliyoendeshwa na Kituo cha EFM.

Naye Meneja Masoko wa Multchoice-Tanzania, Alpha Mria alisema kuwa kampuni yao imeamua kuwatunuku washindi hao ving’amuzi na vifurushi vya mwezi mzima vya DStv ili kuwawezesha wao na familia zao kusherehekea vizuri Krismas na Mwaka Mpya majumbani kwao huku wakiangalia DStv.

Mria alisema kuwa Multichoice haijawatunuku washindi pekee yao, bali na Watanzania wengine ambao wanatumia king’amuzi chao kwani hivi karibuni walipunguza bei ya vifurushi zao kwa wastani wa asilimia 16, huku kile kifurushi maarufu zaidi cha DStv Bomba chenye chaneli zaidi ya 70 kikipunguzwa bei hadi kufikia sh. 19,975 tu kwa mwezi.

Baadhi ya washindi waliokabidhiwa zawadi leo ni pamoja na Kelvin Mhenzi, Asha Said, Dasatan Kaligo, Said Ponela, Grace Kimani, Leila Ramadhani, Ashura Bakary, Tamirway Kamote, Baraka Mbogoni, Ratipha Bakari, Gilbert Genese, Luicia John, Ezra Raphael, Nathan William, Caroline Peter, Seleman Dovya, Alice Sangwani, Mbwana Kuwangaya, Peter Doto, Fadhil Doto, Fadhil Yusuph, Hadija Hamisi na Mlani Mohamed.


 
 

No comments:

Post a Comment