Thursday 22 December 2016

Multichoice-Tanzania yatoa msaada msimu wa Krismasi kwenye Kituo cha kulelea watoto yatima cha Al-Madima Tandale




Mkurugenzi Mtendaji wa Multichoice-Tanzania, Maharage Chande akizungumza kabla ya kukabidhi msaada kwa Kituo cha Kulelea Watoto Yatima cha Al-Madina. Kushoto ni Mlezi wa kituo hicho, Kuruthum Yussuf leo.

Na Mwandishi Wetu
KAMPUNI ya Multchoice-Tanzania mapema leo imekabidhi msaada wa vitu mbalimbali vyenye thamani ya sh. Milioni 5 kwa Kituo cha Watoto Yatima cha Al-Madina kilichopo Tandale kwa Tumbo jijini Dar es Salaam kwa ajili ya Siku Kuu ya Krismasi na Mwaka Mpya.

Msaada huo uliohusisha sare za shule, unga wa ngano, unga wa mahindi, biskuti, juice za aina mbalimbali, soda, mafuta ya kupikia, mchele na nguo zingine ulitolewa na Mkurugenzi Mtendaji wa Multchoice-Tanzania, Maharage Chande kwa niaba ya wafanyakazi wenzake, ambao baadhi yao aliambatana nao hadi Uswazi.

Vingine walivyokabidhi leo ni pamoja na vyombo vipya kabisa vya kulia chakula, fedha taslimu za kusaidia kulipia gharama zao za pango wanapoishi watoto hao na vitu vingine.

Akizungumza kabla ya kumkabidhi msaada huo, Chande alisema kuwa kampuni yao kwa miaka mingi imekuwa na mahusiano mazuri na kituo hicho cha Watoto Yatima cha Al-Madina, ambapo wamekuwa wakisaidia mara kwa mara.
Mbali na msaada huo wa vyakula, vinywaji na sare za shule na nguo, Multchoice-Tanzania pia imelipa pango la miezi sita la Kituo hicho, ikiwa ni moja ya changamoto inayokisumbua sana kituo hicho chenye watoto 60.

Chande alisema kuwa wataendelea kukisaidia kituo hicho pamoja na vingine ikiwa ni sehemu ya kusaidia jamii kupitia fedha wanazopata kwa kuuza ving’amuzi bora kabisa vya DStv, ambavyo vimekuwa vikinunuliwa kwa wingi.

Alisisitiza kuwa Multchoice-Tanzania itaendelea kushirikiana na kituo hicho ili kuhakikisha watoto wanasonga mbele kwani ndio taifa la kesho, ambapo kila mmoja wetu ana wajibu wa kujitolea kwa namna moja au nyingine.

Hii sio mara ya kwanza kwa Multchoice-Tanzania kukisaidia kituo hicho,  kwani miezi kadhaa iliyopita wakati wa Mfungo wa Mwezi Mtukufu wa Ramadhani walikabidhi cherehanui kadhaa, ambazo zinatumiwa kuendeleza kipato chao kwa kushona nguo na kuziuza.

Akitoa shukrani Mkuu wa Kituo hicho, Bi. Kuruthum Yussuf alimshukuru Chande na Multchoice-Tanzania kwa ujumla kwa misaada wanaokipatia kituo hicho kwa miaka mingi sasa.

Hatahivyo, Bi. Kuruthum alisema kituo chao kinakabiliana na baadhi ya changamoto kama ukosefu wa eneo kwani kituo kipo katika eneo dogo lililobanwa sana, ambalo linawafanya watoto washindwe kucheza na kufanya shughuli zingine.
Aliwataka watu na taasisi mbalimbali kujitokeza kusaidia kama wanavyofanya Multchoice, ambao wamekuwa wamkikisaidia kituo hicho bila ya kuchoka.
 
Baada ya kumalizika kwa hafla ya kukabidhi msaada huo, Chande alitembezwa katika kituo cha ushonaji, ambacho kiko meta chache kutoka kilipo kituo hicho cha watoto yatima.




 
 


 


No comments:

Post a Comment