Thursday 8 December 2016

Serikali yataka mashirikisho, vyama vya michezo kushuka vitongojini kwenda kusaka vipaji vipyaaa



Na Mwandishi Wetu Dodoma
SERIKALI imevitaka vyama na mashirikisho ya michezo nchini kwenda ngazi za vitongoji kusaka vipaji na kuviendeleza ili kuendeleza michezo nchini,.

Hayo yalisemwa leo na Mkuu wa Wilaya ya Dodoma mjini, Christina Mndeme wakati akifungua Mkutano Mkuu wa Uchaguzi wa Kamisheni ya Wachezaji Tanzania (Kawata) katika hoteli ya Dodoma jana.


Wanariadha wazamani, Mwinga Mwanjala (kushoto), Gidamis Shahana na Peter Mwita wakifuatilia mkutano wa Kawata mjini Dodoma leo.
Alisema wachezaji wenye vipaji wako ngazi ya vitongoji, vijiji na hata mitaa, hivyo alivitaka vyama na mashirikisho ya michezo kupiga hodi huko ili kusaka vipaji na kuviendeleza.

Akitolea mfano hilo alisema hata akina Filbert Bayi na Gidamisi Shahanga vipaji vyao viligundulika huko vitongojini na kuendelezwa hadi kuliletea sifa taifa kwa kutwaa ubingwa wa dunia kwa nyakati tofauti.


Katibu Mkuu wa Kamati ya Olimpiki Tanzania (TOC), Filbert Bayi akizungumza wakati wa ufunguzi wa Mkutano Mkuu wa Kawata leo.
Bayi alikuwa bingwa wa dunia katika mbio za meta 1,500 wakati Shahanga alikuwa bingwa wa dunia katika mbio za meta 10,000 na marathoni baada ya wote kutwaa medali za dhahabu katika Michezo ya Jumuiya ya Madola kwa miaka tofauti tofauti.

Aidha, Mndeme alisema kuwa Serikali imeitaka amati ya Olimpiki Tanzania (TOC) kuhamia Dodoma na iko tayari kuwapatia eneo kwa ajili ya kujenga ofisi.

Rais wa Kamati ya Olimiki Tanzania (TOC), Gulam Rashid akimkabidhi zawadi Mkuu wa Wilaya ya Dodoma Mjini, Christina Mndeme maara baada ya mkuu huyo kufungua Mkutano Mkuu wa Uchaguzi wa Kamisheni ya Wachezaji (Kawata) Dodoma Hoteli leo.
Mndeme alisema kuwa Makao Makuu yamehamia Dodoma na tayari Waziri Mkuu yuko Dodoma, hivyo aliwataka TOC kuwasilisha maombi ya kiwanja Mamlaka ya Ustawishaji Makao Makuu (CDA), na nakala ya barua hiyo kumpatia yeye ili wapatiwe eneo la kujenga ofisi.

“TOC kama bado hamjawasilisha maombi ya eneo CDA basi fanyeni hivyo haraka na nakala ya hiyo barua mnipatie mimi ili mpatiwe kiwanja hicho na nyinyi mhamie Dodoma, “alisema Mndeme.


Aidha, mkuu huyo wa wilaya pia aliwaasa wanamichezo kutopeleka mambo ya michezo mahakamani, kwani kufanya hivyo kunarudisha nyuma maendeleo ya michezo, ambapo viongozi wa michezo hutumia muda mwingi kutatua migogoro badala ya kuleta maendeleo ya mchezo husika.

Akizungumzia kuhusu matumizi ya dawa za kuongeza nguvu michezoni ambalo ni janga la dunia kwa sasa, Mndeme alisema kuwa lazima yapigwe vita kwani yanaharibu wanamichezo na hayatakiwi kutumiwa hata kidogo.

Alisema matumizi ya dawa za kuongeza nguvu michezoni ni hatari na yanatakiwa yapigwe vita kwa nguvu zote.

Pia mkuu huyo wa wilaya alivitaka vyama na mashirikisho ya michezo kuwashirikisha wachezaji katika kamati zao za utendaji ili wachezaji wawe na uwakilishi wao badala ya kusemewa kila kitu.
Awali akizunumza kabla ya mgeni rasmi, Katibu Mkuu wa TOC, Bayi alisema michezo kwa sasa ni ajira, ndiyo maana IOC imehamasisha Kamati za Olimpiki kuunda Kamisheni za Wanamichezo ili watambuliwe kuwa sekta muhimu ya maendeleo ya michezo katika Taifa letu.

“TOC inazidi kuviagiza na kushauri vyama/mashirikisho ya michezo ambayo bado hayajaunda Kamisheni zao kufanya hivyo ili kuwapa wanamichezo sauti ya kuchangia katika maendeleo ya michezo hasa kutetea haki zao panapohitajika, “alisema Bayi.

Bayi aliongeza kuwa, TOC inaamini kwamba kukiwa na uwakilishi wa wanamichezo katika vyama vya michezo na asasi za umma nchi yetu itakuwa imepiga hatua katika kupiga vita matumizi ya madawa ya kuongeza nguvu katika michezo.

Kamisheni itaweza kuendeleza hoja ya kuwasaidia wachezaji waliostaafu kucheza ili waweze kuishi maisha bora baada ya kustaafu kucheza.

No comments:

Post a Comment