Saturday 20 August 2016

BASATA, WASANII WAMLILIA MKONGWE WA TAARAB BI SHAKILA SAID



Na Mwandishi Wetu
BARAZA la Sanaa la Taifa (BASATA) limepokea kwa masikitiko na majonzi kifo cha msanii wa muziki wa taarab, Bi Shakila Said (pichani) kilichotokea ghafla nyumbani kwao Mbagala jijini Dar es Salaam usiku wa kuamkia leo.

Katika taarifa ambayo imetumwa kwa vyombo vya habari na kusainiwa na Katibu Mkuu BASATA, Geofrey Mwingereza, Shakila ni msanii na mdau wa muda mrefu wa sekta ya Sanaa nchini na alikuwa na mchango mkubwa katika kukuza muziki wa taarab nchini.

Pia taarifa hiyo ilisema Shakila alibuni kazi za sanaa za muziki mbalimbali ambazo zilikuja kupata umaarufu mkubwa ambazo ni 'Macho Yanacheka' na 'Kifo cha Mahaba'.

Mwingereza alisema mchango wake katika muziki wa taarab hasa katika kubuni na kutunga nyimbo zenye ubora, ujumbe na maadili kwa jamii hautasahaulika kamwe kwani ameacha misingi na alijitolea kwa kuufikisha muziki wa taarab mahali ulipo leo.

"Baraza, wasanii na wadau wote wa sanaa hatuna budi kuendelea kuenzi mema aliyotuachia marehemu Shakila na baraza linatoa pole kwa ndugu wa marehemu, shirikisho la muziki, wasanii na wadau wote wa sanaa katika kipindi hiki kigumu cha kuondokewa na mpendwa wetu," alisema Mwingereza.


Bi Shakila Mwasisi wa taarab aliyesimama jukwaani kwa zaidi ya miaka 40, alipitia katika makundi mbalimbali ya taarab yakiwemo ya Lucky Star, JKT na mengineyo.

Alijaliwa kupata watoto 13 na wajukuu zaidi ya 20.

Alistaafu muziki akiwa na  JKT Taarab mwaka 2009, lakini amekuwa akiliimbia kundi hilo pale wanapomuhitaji na kumlipa posho.


Innalillah wainnah ilayh raajiuun



No comments:

Post a Comment