Tuesday, 19 March 2019

MultiChoice Yatangaza Fursa kwa Wadau wa Filam Nchini, Afrika


Na Mwandishi Wetu
KAMPUNI ya MultiChoice-Tanzania imetangaza  fursa ya kipekee kwa wadau wa tasnia ya filamu Tanzania na barani Afrika kwa ujumla ijulikanayo kama MultiChoice Talent Factory Portal iliyodhamiria kuleta mapiduzi ya hali ya juu katika uaandaaji wa filamu zenye viwango vya kimataifa kutoka barani Afrika.

Akizungumza wakati wa uzinduzi wa programu hiyo, Mkuu wa kitengo cha Uhusiano kutoka MultiChoice Tanzania Johnson Mshana alieleza kuwa programu hiyo ni muendelezo wa programu maalum ya iliyodhamiria kuleta mabadiliko katika tasnia ya filamu barani Afrika.

 “MultiChoice Talent Factory ambayo ni progamu mama  ilizinduliwa rasmi mapema  Mei mwaka jana na imedhamiria kuleta mabadiliko chanya kwenye tasnia ya filamu hapa nyumbani Tanzania na Afrika kwa ujumla.

Tulianza kwa kupeleka vijana wanne katika kambi maalum ya mafunzo ya uandaaji filamu katika akademia maalum kule Nairobi nchini Kenya, kisha mafunzo maalum kwa magwiji wa sauti yaliyofanyika Januari mwaka huu na hatimaye leo hii tumekuja tena na platform maalum yenye dhamira ile ile ya kuleta mapinduzi katika tasnia ya filamu barani Afrika”, alisema Mshana.

Kwa upande wake Katibu Mtendaji wa Bodi ya Filamu Tanzania, Joyce Fisoo alisema kuwa, anaishukuru sana Kampuni ya MultiChoice kwani imekuwa mstari wa mbele katika kuleta mapinduzi kwenye tasnia ya filamu hapa Tanzania.

 “Binafsi nilishuhudia uzinduzi wa programu ya MultiChoice Talent Factory mapema mwaka jana kule mjini Dodoma na leo hii tunazindua tena sehemu nyingine ya programu hiyo hiyo. Hakika ni fursa ya kipekee na ninapenda kuchukua nafasi hii kuwahamasisha wadau wote waliopo katika tasnia yetu kuitumia nafasi hii ipasavyo ili kuweza kujifunza, kubadilishana ujuzi na hatimaye kupata kazi zenye maudhui ya hali ya juu kutoka hapa hapa Afrika”,  alisema Fisoo.

Naye Ofisa Uhusiano wa MultiChoice Tanzania Grace Mgaya alimalizia kwa kueleza kuwa ukurasa huu ni wa wazi kwa watu wote hususani wadau wa filamu waliopo hapa nyumbani na Afrika kwa ujumla.

 “Tunaamini kwa kupitia program hii tutaweza kuwafikia wadau wengi zaidi na tunatarajia kazi zenye ubora wa hali ya juu kutoka barani Afrika kwa siku zijazo kutokana na matokeo chanya yatakyoletwa na program hii ya MultiChoice Talent Factory”, alisema Grace.


Wednesday, 6 March 2019

Tanzania Kinara Tena Tuzo za ‘DStv Eutelsat Star Awards’


Mkuu wa Uhusiano wa MultiChoice Tanzania, Johnson Mshana akimkabidhi mshindi wa tuzo za Kimataifa za DStv Eutelsat Star Awards, Pricilla Marealle cheti cha ushindi wakati wa mahafali ya kidato cha sita katika shule ya St Mary Goretti hivi karibuni. Kulia ni Ofisa Uhusiano  wa MultiChoice Tanzania. Grace Mgaya. 

Na Mwandishi Wetu

KWA mara nyingine tena Tanzania imeibuka kinara  katika tuzo za kimataifa za wanafunzi zijulikanazo kama DStv Eutelsat Star Awards ambapo mwanafunzi Priscilla Marealle kutoka shule ya sekondari ya St. Mary Goreti mkoani Kilimanjaro ameweza kuipeperusha bendera ya Tanzania kwa kunyakua nafasi ya kwanza katika kipengele cha uchoraji bango  ikiwa ni baada ya mchuano mkali baina ya mamia ya wanafunzi kutoka nchi zaidi ya 10 kote barani Afrika.

Kwa upande wa uandishi wa insha kijana Tanaka Chonyera kutoka  nchini Botswana aliweza kujinyakulia ushindi wa kwanza.

 Tuzo hizi ambazo huhusisha uandishi wa insha maalum au kuandaa bango yenye ujumbe kuhusiana na elimu ya anga hususan Setelait ni za wazi kwa wanafunzi wote wa shule za sekondari wenye umri kati ya miaka 14 – 19 kote barani Afrika ambapo kampuni ya MultiChoice inaendesha shughuli zake.
Mkuu wa shule ya  St Mary Goretti Sr. Lucrecia Njau akifurahi baada ya kupokea cheti kutoka kwa Mkuu wa Uhusiano wa MultiChoice Tanzania Johnson Mshana mara baada ya shule hiyo kufanikiwa kutoa mshindi wa jumla wa wa tuzo za kimataifa za DStv Eutelsat Star Awards Pricilla Marealle. 
  Katika msimu huu wa nane, washindani walitakiwa kuandika insha au kubuni bango litakaloelezea licha ya Satelait kutumika katika shughuli mbalimbali, ni namna gani zitaweza kutumika zaidi ili kuleta maendeleo chanya ulimwenguni.

 Priscilla ambaye ni mwanafunzi wa kidato cha sita wa mchepuo wa Sayansi katika shule ya Mtakatifu Maria Goreti alitangazwa rasmi kuwa mshindi mjini Accra nchini Ghana ambapo ndipo jopo la watahini liliongozwa na Paolo Nespoli, mwanaanga nguli kutoka European Space Agency (ESA) lilikaa kupitia kazi kutoka kwa wanafunzi walioshinda katika nchi mbalimbali.
Mshindi wa Jumla wa tuzo za kimataifa za DStv Eutelsat Star Awards Pricilla Marealle akikabidhiwa kikombe cha ushindi na Mkuu wa shule ya St Mary Goretti Sr. Lucrecia Njau baada ya kutangazwa kuwa mshindi wa jumla wa wa tuzo za kimataifa za DStv Eutelsat Star Awards. Kulia ni Mkuu wa Uhusiano wa MultiChoice Tanzania Johnson Mshana.
 Akiongea baada ya kukabidhiwa cheti cha uthibitisho wa ushindi wakati wa mahafali ya kidato cha sita ya shule ya Mtakatifu Mary Goreti iliyopo Moshi Kilimanjaro, Priscilla amesema amefurahi sana kwa ushindi huo mkubwa ambao umemletea yeye, shule yake na taifa zima kwa ujumla sifa kubwa. “Nimefurahi sana kupokea taarifa hizi nzuri. Naamini ushindi wangu utakuwa ni chachu kubwa kwa wanafunzi wenzangu kote nchini kujitokeza kwa wingi na kushiriki katika tuzo kama hizi na mashindano mengine ya kitaaluma ya ndani na nje ya nchi, na kusisitiza  kuwa Ndoto huanza kufanya kazi pale unapojiamini” alisema Priscilla.
 
Kwa upande wake mkuu wa shule hiyo ya Mtakatifu Maria Goreti Sister Lucresia Njau alisema kuwa anaishukuru sana kampuni ya MultiChoice Tanzania kwa kuwapatia nafasi ya kushiriki katika Mashindano hayo na hatimaye kuweza kunyakua tuzo hiyo kupitia mwanafunzi wao Priscilla.

 “Huyu kijana ana jitahidi sana katika chochote kile anachokifanya, iwe ni darasani au hata katika majukumu mengine nje ya darasani. Ni msikivu mtiifu lakini zaidi ya yote ni mbunifu sana. Naamini haya ndiyo yaliyomfanya aweze kushinda tuzo hizi” alisema Sr. Lucrecia Njau.
  
Naye, Mkuu wa Uhusiano MultiChoice Tanzania Johnson Mshana alisema,” Huu ni msimu wa tatu mfululizo kwa Tanzania kuendelea kung’ara katika tuzo hizi za DStv Star Awards. Tulianza kupeperusha bendera yetu na kijana Davids Bwana msimu wa sita baada ya kushika nafasi ya pili Afrika katika kipengele cha uandishi wa insha, kisha tukaibuka kidedea baada ya kupokea taarifa za ushindi wa kwanza wa kijana Taheer Rashid katika msimu wa saba mwaka jana na leo hii tunayofuraha kubwa kuona kuwa tumeendeleza wimbi la ushindi.”

Saturday, 2 February 2019

Denis Suarez Kuichezea Arsenal Ikiikabili Man City


LONDON, England
KOCHA Mkuu wa Arsenal Unai Emery kumpanga mchezaji mpya aliyesajiliwa juzi Denis Suarez  (pichani) na kuichezea kwa mara ya kwanza katika Ligi Kuu ya England dhidi ya Mabingwa wa ligi hiyo Manchester City katika mchezo utakaofanyika kesho.

The Gunners wanasafiri hadi kwenye Uwanja wa Etihad kwa ajili ya mchezo huo unaotarajia kuwa mkali na wa kusisimua baada ya kukamilika kwa dirisha la usajili, ambapo klabu hiyo ilikamilisha usajili wa Suarez kwa mkopo akitokea Barcelona hadi mwishoni mwa msimu.

Mchezaji huyo mwenye umri wa miaka 25, ambaye ameichezea mara mbili timu ya wakubwa ya Man City katika kipindi chake cha mwanzo cha kuichezea klabu hiyo, ndio mchezaji pekee aliyetua Arsenal, ambaye alishindikana kupata mkataba wa kudumu kutokana na ufinyu wa fungu.

Mkataba huo wa mkopo ni pamoja na kuwemo kipengele cha kuweza kuongeza mkataba wa muda mrefu kwa Suarez katika kipindi cha majira ya joto wakati mchezaji huyo wa kimataifa wa Hispania akihusishwa na kiujiunga tena na Emery, wakati akicheza chini ya Mhispania mwenzake katika klabu ya Sevilla.

"Nitafanya uamuzi kesho (leo) lakini endapo ataanza katika mchezo huo nina imani naye, “alisema Emery alipouilizwa ikiwa Suarez ataenda moja kwa moja katika timu ya Arsenal katika mchezo huo wa Jumapili.

"Namjua mchezaji huyo na alianza kujifua binafsi juzi. Leo alikuwa na wenzake. Ni jambo zuri, anaonekana kuelewa haraka.

"Ni mchezaji mwenye kiwango na nafikiri anaweza kutusaidia sisi kutokana na kiwango chake…, “alisema.

Ushindi kwa Manchester City utashuhudia timu hiyo ikiwakaribia vinara wa ligi hiyo Liverpool kwa pointi mbili, ambao watacheza dhidi ya West Ham siku moja baadae.

Kikosi cha Pep Guardiola alikuwa mpinzani wa kwanza wa Emery katika soka la Uingereza, ambako waliibuka na ushindi wa mabao 2-0 dhidi ya Arsenal Agosti.

Emery anatarajia kukutana na kikwazo kingine lakini alisema wachezaji wake wako tayari kuonesha uwezo wao dhidi ya wapinzani wazuri.

"Itakuwa mechi ngumu, tunacheza dhidi ya timu bora, “alisema.

"Sasa, Liverpool, wamefanya kazi kubwa sana wakati wa Ligi Kuu msimu huu. Labda wamepoteza baadhi ya mechi., lakini hiyo ni kama ajali tu.

Qatar Mabingwa Wapya Kombe la Asia

Qatar baada ya kutwaa ubingwa wa Kombe la Asia kwa mara ya kwanza, abada ya kuifunga Japan kwa mabao 3-1 juzi. (Picha na Mtandao).

TOKYO, Japan
WENYEJI wa Kombe la Dunia 2022 Qatar wametwaa kwa mara ya kwanza kabisa taji la Asia baada ya kuibuka na ushindi wa mabao 3-1 dhidi ya mabingwa mara nne wa taji hilo Japan.

Mshambuliaji Almoez Ali alivunja rekodi ya mchezaji kupachika mabao mengi katika mashindano hayo ya Kombe la Asia pale alipofunga bao lake la tisa kwa kichwa katika mchezo huo wa fainali.

Abdulaziz Hatem aliiweka timu yake kuwa mbele kwa mabao 2-0 baada ya kufunga kwa shuti la umbali wa kama meta 20 kabla Japan haijafunga bao lao la kufutia machozi kupitia kwa  Takumi Minamino akiwa ndani ya boksi.

Mabao yalikuwa 3-1 baada ya Akram Afif (mtoto wa kiungo wazanmani wa Simba, Hassan Afif) kufunga kwa penalti baada ya mchezaji anayeichezea klabu ya Southampton, Maya Yoshida kuunawa mpira katika eneo la hatari.

Teknolojia ya VAR ilithibitisha kuwa beki huyo wa Southampton, ambayo inajukana kama Watakatifu aliishika kwa makusudi mpira huo, ingawa picha marudio za TV zilionesha kama aliushika kwa bahati mbaya.

Penalti hiyo ya Afif ilikuwa na maana kuwa mchezaji huyo alifunga bao moja na kusaidia mara 10, ikiwemo mara mbili katika mchezo huo wa fainali, wakati wa mechi saba za Qatar katika mashindano hayo huko Umoja wa Falme za Kiarabu.

Kikosi cha kocha waQatar, Felix Sanchez kimecheza saa 10 na dakika nane bila ya kuruhusu bao hata moja katika mashindano ya mwaka huu ya Asia kabla ya kufungwa na Minamino.

Kijazi Aagiza Makatibu Wakuu Kuhimiza Michezo

Katibu Mkuu Ofisi ya Waziri Mkuu (Bunge), Bi Maimuna Tarishi (mwenye miwani) akisalimiana na Katibu Mkuu Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano (Sekta ya Uchukuzi), Mhandisi Dr. Leonard Chamuriho kabla ya kuanza kwa mbio za pole (jogging) za bonanza la Michezo ya Shirikisho la Michezo ya Wizara, Idara, Taasisi, Wakala wa Serikali na Ofisi za Wakuu wa Mikoa (Shimiwi), iliyoanzia kwenye Uwanja wa Jamhuri hadi Ofisi za Bunge na baadaye kurudi Jamhuri


Mwandishi Wetu, Dodoma
KATIBU Mkuu Kiongozi, ambaye pia ni Mkuu wa Utumishi wa Umma, Balozi Mhandisi John Kijazi amewaagiza Makatibu Wakuu kuhimiza michezo mahala pa kazi kwa vitendo ili kuwa na watumishi wa Umma wenye afya njema.

Kauli hiyo ilitolewa leo na Katibu Mkuu Ofisi ya Waziri Mkuu (Bunge), Maimuna Tarishi kwa niaba ya Balozi Kijazi katika Bonanza la Michezo lililoandaliwa na Shirikisho la Michezo ya Wizara, Idara, Wakala wa Serikali na Ofisi za Wakuu wa Mikoa (SHIMIWI), na kufanyika kwenye Uwanja wa Jamhuri Dodoma.

Tarishi ameweka msisitizo kwa kuwa michezo ni kazi na kazi ni michezo, ambapo sasa Makatibu Wakuu waweke mazingira yatakayowezesha watumishi wa umma kupitia taasisi zao waweze kushiriki kwenye michezo mbalimbali, ambayo inajenga umoja na ushirikiano baina ya watumishi.


“Haya ni maagizo ya Katibu mkuu kiongozi amenituma nije niseme kwa kuwa yupo katika kazi nyingine, wito ni kwa Makatibu Wakuu wote na wakuu wa taasisi kuhakikisha wanaweka mazingira wezeshi yatakayowezesha watumishi kufanya mazoezi mara kwa mara na hata katika michezo kama hii ya Shimiwi,” amesema Bi. Tarishi.

Amesema sasa uwekwe utaratibu kwa Watumishi wa Umma kushiriki michezo ambayo haitatumia gharama kama wanavyodhania wengine.

“Kwa waajiri hatuna budi kuweka mazingira wezeshi ya kuwawezesha Watumishi kuwa na utaratibu wa kushiriki kwenye michezo yeyote na hii inafanyika bila gharama yeyote kabisa kwani wakati mwingine tunakimbilia hatuna fedha au hajatenga kifungu katika bajeti wakati hata hapa ukiangalia hakuna gharama kubwa iliyotumika,” amesisitiza Bi. Tarishi.
Amewataka watumishi wa umma kufanya mazoezi ya kila wakati ili kujiweka katika afya kwa wakati wote, ambayo itawasaidia kufanya kazi kwa weledi.

Bi. Tarishi ametoa pia maagizo kwa viongozi wa Shimiwi, kwa kuwa sasa wameanza kufufua michezo hii baada ya kusimama kwa muda mrefu, na sasa waendelee mbele kwani yanawakutanisha Watumishi wa maeneo mbalimbali ya kazi ya serikali na husaidia kubadilishana uzoefu.

“Hii ni rai yangu kwenu kwa kuwa sasa mmeanza tena michezo yenu hii tunapenda tuone inasonga mbele kwani hushirikisha watumishi kutoka Wizara na Taasisi mbalimbali, na yanajenga umoja kama watumishi wa umma, na tuwekee maanani na kutekeleza haya,” amesema Bi. Tarishi.

Hatahivyo, amesema michezo ni nidhamu hivyo kuwe na nidhamu kwenye michezo kwani kutasaidia watumishi kufanya kazi kwa bidii na kuwa na ubinifu wa hali ya juu.

Naye Mwenyekiti wa Shimiwi, Daniel Mwalusamba amesema wachezaji wanahimizwa kufanya mazoezi kwa ajili ya kujenga, kulinda na kuimarisha afya zao.

“Michezo ni kazi hivyo wanapaswa kuzingatia taratibu na miongozo inayokuwa imetolewa kila wakati na serikali, na kama agenda ya kitaifa ilivyo ya kujenga Tanzania ya Viwanda, na ili tufanikiwe tunahitaji kuwa na Watumishi wenye afya bora wanaoweza kufanya majukumu yao kwa wakati na kushiriki michezo mbalimbali, ambapo sasa wanaweza kuandaa mabonanza sehemu za kazi kwa siku ya za mwishoni mwa wiki,” amesema Bw. Mwalusamba.

Hatahivyo, amesema katika kikao cha juzi kilichofanyika kwenye ukumbi wa Hazina na kuwahusisha Wenyeviti na Makatibu wa klabu za michezo mahala pa kazi, ambapo wamekumbushwa kusimamia michezo kwa kuwa ni sehemu ya kazi na wanapaswa kusimamia na kutekeleza majukumu yote yanayotolewa na serikali.
Meneja wa Kiwanja cha Ndege cha Dodoma, Bi. Bertha Bankwa (wa kwanza kulia mstari wa nyuma) leo akijumuika kufanya mazoezi na watumishi wa Umma katika bonanza la Shirikisho la Michezo Wizara, Idara, Taasisi, Wakala wa Serikali na Ofisi za Wakuu wa Mikoa (SHIMIWI), lililofunguliwa na Katibu Mkuu Ofisi ya Waziri Mkuu (Bunge), Bi. Maimuna Tarishi (Hayupo pichani). (PICHA NA BAHATI MOLLEL WA MAMLAKA YA VIWANJA VYA NDEGE TANZANIA- TAA).
Katika michezo iliyochezwa jana kwa upande wa kuvuta Kamba wanaume timu ya Waziri Mkuu wametoa jasho na Mambo ya Ndani na kutoka sare ya mvuto 1-1; wakati katika netiboli timu ya Utumishi imechapwa na Tamisemi magoli 24-17; huku Afya wakiwashinda GST magoli 9-6.

Katika mchezo wa soka Utumishi wamewachapa Afya magoli 2-0; huku Ardhi wamewashinda Mwanasheria Mkuu kwa magoli 4-0.

Friday, 1 February 2019

Shimiwi wahimiza mabonanza kuimarisha afya

Mwenyekiti wa Shirikisho la Michezo la Wizara, Idara, wakala wa Serikali na Ofisi za Wakuu wa Mikoa (Shimiwi, Daniel Mwalusamba (katikati) akiendesha kikao cha viongozi wa klabu mbalimbali kilichofanyika leo, kwenye ukumbi wa mikutano wa Hazina, jijini Dodoma. Wengine kushoto ni Makamu Mwenyekiti Ally Katembo na kulia ni Katibu Mkuu Moshi Makuka.

Na Mwandishi Wetu, Dodoma
SHIRIKISHO la Michezo ya Wizara, Idara, Wakala wa Serikali, na Ofisi za Wakuu wa Mikoa (Shimiwi), imehimiza ushiriki wa mabonanza ya michezo mbalimbali kwa Watumishi wa Umma ili kuboresha afya zao.

Mwenyekiti wa Shimiwi, Daniel Mwalusamba amesema leo jijini Dodoma, katika mkutano wa wenyeviti na makatibu uliofanyika kwenye ukumbi wa Naibu Waziri wa Fedha katika jengo la Hazina.

Mwalusamba amesema kwa sasa serikali inahimiza ujenzi wa viwanda, ili tufikie uchumi wa kati, ambapo Watumishi wa Umma wanatakiwa kuunga mkono hatua hiyo iliyotangazwa na Mhe. Rais John Pombe Magufuli.

“Tuondokane na zana ya Shimiwi kuwa imekufa kwani hili ni Shirikisho la michezo ambalo lipo kihalali na linaendeshwa kwa utaratibu, na mapendekezo yote yapo kisheria,” amesema Mwalusamba.

Hatahivyo, Mwalusamba amesema Shimiwi inakumbwa na changamoto za klabu kwa kushindwa kwenda na katibka kwa kufanya chaguzi zake kwa wakati, ikiwa ni kufuata katiba iliyopo.

“Hairihusiwi kikatiba kwenye mkutano mkuu kuingia na viongozi ambao hawajachaguliwa kihalali na kukaa kwa muda mrefu, kwani ni kinyume na katiba yetu ya Shimiwi na pia Katiba Mama ya Serikali, ambayo imeweka wazi juu ya muda wa ukomo wa uongozi,”

Amesema ni kinyume na katiba na viongozi wa shimiwi wanaweza kwenda kwa Katibu Mkuu wa wizara husika, na sasa Shimiwi itafanya ukaguzi na kugundua klabu iliyo na uongozi uliomaliza muda, hali kadhalika katiba za klabu zinapitishwa na baraza, na sio kikundi kinachojiendesha chenyewe bila kufuata katiba.

Ameagiza klabu sugu zikafanye chaguzi zao ili kuepusha mgogoro, kwani  Shimiwi  imekuwa mfano wa kuigwa kwa kufuata taratibu tofauti na mashirikisho mengine.

Kijazi kubariki Bonanza la Shimiwi Dodoma kesho

Katibu Mkuu Kiongozi, Balozi John Kijazi

Na Mwandishi Wetu, Dodoma
WATUMISHI zaidi ya 1,000 kutoka Wizara na Idara za Serikali leo watashiriki kwenye Bonanza la Michezo litakaloongozwa na Katibu Mkuu Kiongozi na Mkuu wa Utumishi wa Umma ambaye pia ni Mlezi wa Shirikisho la Michezo la Wizara na Idara za Serikali (SHIMIWI), litakalofanyika Jijini Dodoma.

Mwenyekiti wa SHIMIWI, Daniel Mwalusamba amesema bonanza hilo litatanguliwa na mbio fupi fupi (jogging) zitakazoanzia kwenye uwanja wa Jamhuri hadi maeneo ya Bunge na kurudi kiwanja cha Jamhuri, ambapo mbali na Katibu Mkuu Kiongozi, pia watashiriki Watendaji Wakuu wa kutoka taasisi mbalimbali za Umma.

Mwalusamba amesema baada ya mbio hizo wachezaji wote walioshiriki ;watafanya mazoezi ya viungo na baadaye kushiriki kwenye michezo ya netiboli, soka na kuvuta Kamba.
Wajumbe wa klabu mbalimbali za Shirikisho la Michezo ya Wizara, Idara, Wakala wa Serikali na Ofisi za Wakuu wa Mikoa wakimsikiliza Mwenyekiti, Daniel Mwalusamba alipoendesha kikao leo kwenye ukumbi wa mikutano Hazina Dodoma.
“Hili bonanza ni moja ya njia ya kuwaweka watumishi wa umma katika afya njema na kuepuka magonjwa nyemelezi, ambapo mtumishi ataweza kufanya kazi kwa weledi na bidi kwa kuwa wanakuwa na afya nzuri,” amesema Mwalusamba.

Pia amesema bonanza hilo litaendelea kesho (Jumapili) kwa michezo mbalimbali.
Akizungumzia uwepo wa mashindano ya michezo ya SHIMIWI, ambayo imekuwa ikiahirishwa mara kwa mara kutokana na sababu mbalimbali, Mwalusamba amesema mashindano hayo yapo na hayajafutwa na yatafanyika kulingana na taratibu.

“Hii michezo haijafutwa lakini kumekuwa na mabadiliko ya kiutaratibu, ambapo sasa serikali yetu ipo katika harakati za ujenzi wa viwanda na sisi ni watu muhimu wa kuimiza hilo, hivyo michezo itaendelea kama ilivyopangwa,” amesema Mwalusamba.
Hatahivyo, amehimiza Watumishi wa Umma kuhakikisha wanatekeleza agizo la Makamu wa Rais, Mhe. Samia Suluhu Hassan la watumishi wafanye mazoezi kila Jumamosi ya Pili ya kila mwezi, ili waweze kujiweka vyema katika afya.

Klabu mbalimbali zimekuwa zikiendesha michezo mbalimbali kwa kushirikisha klabu kwa kushirikiana.

Tuesday, 15 January 2019

DStv kuonesha Mubashara Michuano ya SportPesa 2019


Mkurugenzi Mtendaji wa MultiChoice-Tanzania, Jacqueline Woiso akizungumza na waandishi wa habari wa wakati wa kutangazwa rasmi kwa ushirika kati ya SportPesa na SuperSport ambapo SuperSport kupitia DStv itarusha mubashara michuano hiyo itakayoanza wiki ijayo hapa jijini Dar es Salaam. Kushoto ni Mkurugenzi wa Uendeshaji na Udhibiti wa SportPesa Tanzania Tarimba Abas.

Na Mwandishi Wetu
KING’AMUZI cha DStv ndicho pekee kitaonesha mubashara mashindano ya tatu ya SportPesa yatakayofanyika jijini Dar es Salaam kuanzia Januari 22 hadi 27 na kushindanisha timu za Tanzania na Kenya ili kumpata mshindi atakayecheza na Everton, imeelezwa.

Mkurugenzi Mtendaji wa Multchoice-Tanzania, Jacqueline Woiso alisema jijini Dar es Salaam jana kuwa mashindano ya kombe hilo yataoneshwa na DStv kupitia Super Sports, ambayo ndio iliyopata udhini ya kuonesha mashindano hayo kama mshirika rasmi.

Mkurugenzi wa Uendeshaji na Udhibiti wa SportsPesa Tarimba Abas (Katikati) akizungumza wakati wa kutangazwa rasmi kwa ushirika kati ya SportPesa na SuperSport ambapo SuperSport kupitia DStv itarusha mubashara michuano hiyo itakayoanza wiki ijayo hapa jijini Dar es Salaam. Kulia ni Mkurugenzi Mtendaji wa MultiChoice TanzaniaJacqueline Woiso na Mkuu wa Uendeshaji Baraka Shelukindo (kushoto)

Mbali na vigogo vya soka Tanzania vya Simba na Yanga, timu zingine zitakazoshiriki katika mashindano hayo ni pamoja na Mbao FC pamoja na Singida United za Tanzania wakati zile za Kenya ni Gor Mahia, AFC Leopard, Bandari na Kariobangi.

Gor Mahia ndio washindi wa kihistoria baada ya kulitwaa taji hilo mara mbili na kufanikiwa kucheza mara mbili dhidi ya Everton inayoshiriki Ligi Kuu ya England.

Michuano hiyo itakuwa na mvuto wa aina yake kwani mbali na ukubwa, umaarufu na utani wa timu shiriki, pia kila timu itataka kutwaa kombe hili na hatimaye kupata fursa ya kucheza na moja ya timu maarufu ya soka nchini Uingereza – Everton FC.

Mkurugenzi wa Uendeshaji na Udhibiti wa SportsPesa Tarimba Abas (kulia) akiteta jambo na Mkuu wa Uendeshaji wa MultiChoice Tanzania Baraka Shelukindo wakati wa hafla ya kutangazwa rasmi kwa ushirika kati ya SportPesa na SuperSport ambapo SuperSport kupitia DStv itarusha mubashara michuano hiyo itakayoanza wiki ijayo hapa jijini Dar es Salaam.

Woiso alisema  jana kuwa SuperSport kupitia DStv itarusha mubashara mashindano hayo yatakayoanza wiki ijayo jijini Dar es Salaam.

 “Tunafurahi kuujulisha umma wa watanzania kuwa hamu yao ya kushuhudia michuano hii mubashara kupitia DStv sasa imepatiwa jibu, sasa watashuhudia burudani hii ya aina yake tena kuanzia kifurushi cha chini kabisa cha Bomba,” alisema Jacqueline.

 “Michezo yote itaonekana kupitia DStv SuperSport 9, ambayo inapatikana katika vifurushi vyote. Tumeamua kufanya hivyo ili kuwapa watanzania fursa ya kushuhudia mashindano haya ambayo yanazidi kujipatia umaarufu kila uchao”.

Mkurugenzi Mtendaji wa MultiChoice Tanzania Jacqueline Woiso akimkabidhi mpira Mkurugenzi wa Uendeshaji na Udhibiti wa SportsPesa Tarimba Abas muda mfupi baada ya kutangaza rasmi ushirika kati ya SportPesa na SuperSport ambapo SuperSport kupitia DStv itarusha mubashara michuano hiyo itakayoanza wiki ijayo hapa jijini Dar es Salaam.

Naye Mkurugenzi wa Utawala na Udhibiti wa SportPesa Tanzania, Tarimba Abbas amesema “Tangu kuanzishwa kwa michuano hiyo miaka mitatu iliyopita, mashindano haya yamekua moja ya mashindano makubwa na yanayopendwa sana Afrika Mashariki yote.

Hili ni jambo kubwa sana kwani wachezaji wetu wataweza kuonesha vipaji na viwango vyao na hivyo kuwatangaza kote duniani. Natoa rai kwa timu zinazoshiriki kuhakikisha zinaonesha viwango vya juu  kabisa kwani huu ni ulingo muhimu wa kuonesha uwezo na ujuzi wao wa soka kwa timu husika lakini pia na kwa wachezaji,” alisema Tarimba.

 Mshindi wa Kombe la SportPesa 2019 atajishindia dola za Marekani 30,000 pamoja na kucheza dhidi ya Everton, moja ya timu maarufu kabisa za soka Uingereza wakati mshindi wa pili atapata dola za Marekani 10,000 wakati mshindi wa tatu atapata dola 7,500 na mshindi wa nne dola 5,000. Timu zote zitakazo tolewa robo fainali zitapata dola 2,500 kila moja.

Michuano ya Kombe la SportPesa ilianza rasmi mwaka 2017 katika michuano iliyofanyika hapa Tanzania, ambapo mshindi – Gor Mahia alicheza na Everton hapa hapa Tanzania. Msimu wa pili wa mashindano hayo yalifanyika huko Nakuru Kenya mwaka jana, mshindi kwa mara ya pili Gor Mahia alikwenda kucheza na Everton huko Liverpool Uingereza mwezi Novemba.

Thursday, 10 January 2019

JNIA Yajipanga Madhubuti Kiusalama

Mkurugenzi wa Kiwanja cha Kimataifa cha Ndege cha Julius Nyerere (JNIA), Paul Rwegasha akitoa ufafanuzi wa baadhi ya mambo. 

Na Mwandishi Wetu
UONGOZI wa Kiwanja cha Ndege cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNIA) jijini Dar es Salaam umesema kuwa umejipanga mathubuti kiusalama.
Hayo yameelezwa na Mkurugenzi wa JNIA, Paul Rwegasha wakati akitoa ufafanuzi kuhusu madai ya abiria kuchukua muda mrefu katika jengo la pili la abiria wakati wakiwasili kiwanjani hapo kabla ya kutoka nje ya jengo hilo.
Mbali na madai hayo, pia Rwegasha alitolea ufafanuzi madai ya msanii maarufu nchini Ray Kigosi kuwa aliibiwa raba na perfume kiwanjani hapo kutoka katika begi lake wakati akisafiri kwenda Dubai akitokea JNIA tarehe 3 Jan, 2019.
Alisema kuwa mtangazaji wa Radio Clouds, Ephahimu Kibonde alilalamika katika kipindi cha Jahazi kuwa, alitumia saa mbili kabla ya kutoka nje ya Kiwanja hicho baada ya kuwasili akitokea Afrika Kusini.
Kibonde alishangaa abiria raia wa Tanzania kuchukua muda mrefu Kiwanjani hapo wakati  alitakiwa kutumia muda mfupi kwa kuwa hana mambo mengi ya kukaguliwa,  tofauti na wale wanaotoka nje ya nchi.
Kamishna Msaidizi Mwandamizi wa Idara ya Uhamiaji JNIA, Kanankira Mbise (kuhoto) akizungumza huku Mkurugenzi wa kiwanja hicho, Paul Rwegasha akimsikiliza.
Rwegasha alisema kuwa JNIA imefungwa kamera za usalama za CCTV katika maeneo yote ili kuhakikisha usalama wa abiria na mali zao wakati wakiwasili au kuondoka nchini kupitia kiwanjani hapo.
 Alisema kuwa mbali na mifumo mathubuti ya ulinzi na usalama, pia uongozi wa kiwanja hicho unasera ya kutotoa msamaha kwa Mtumishi yeyote atakayefanya udokozi na uwizi wa mali za abiria, ambapo akibainika anapelekwa kwenye vyombo vya sheria na kufukuzwa kazi moja kwa moja.
“Kamwe hatutamvumilia mfanyakazi yeyote mwenye tabia za kidokozi, ambaye atabainika kuiba mzigo wa abiria, kwani tutamtimua mara moja, na hilo kila mfanyakazi analijua ipo katika sera yetu,, “alisema Rwegasha.
Damas Temba (kushoto), ambaye ni Meneja Msaidizi wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) kiwanjani hapo akizungumza sula la usalama.
Aliomba watu wanapopata matatizo au changamoto kiwanjani hapo, kwanza wawasiliane na uongozi wa kiwanja ili kupata ufafanuzi na utatuzi wa matatizo yao kwa haraka, ambapo mwenendo wake utaangaliwa kwenye kamera za usalama ambazo zipo tangu abiria akiingia kiwanjani hadi anapopanda ndege, badala ya kukimbilia kuandika kwenye mitandao ya kijamii, kwani kufanya hivyo sio tu kunadhalilisha kiwanja, bali na nchi nzima kwa ujumla.
Akizungumzia Jengo la tatu la abiria linalojengwa maeneo ya Kipawa, Rwegasha alisema kuwa wanatarajia kuanza kulitumia mara baada ya kukamilika kwani kwa sasa kuna maeneo yanaendelea na ujenzi, licha ya nje kuonekana kama jengo hilo limekamilka. Jengo hili linatarajiwa kukabidhiwa kwa serikali Mei 2019.
Naye Kanankira Mbise, ambaye ni Kamishna Msaidizi Mwandamizi wa Idara ya Uhamiaji kiwanjani hapo alisema kuwa, idara yake imekuwa ikihakikisha inafanya shughuli zake kwa haraka na kufuata taratibu ili kuondoa msongamano wa abiria wanaowasili kutoka nje ya nchi.
Kwa upande mwingine, naye Damas Temba, ambaye ni Meneja Msaidizi wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) kiwanjani hapo alisema wananchi wanatakiwa kupata elimu zaidi ya kodi, kwani kuna vitu vikiingizwa nchini lazima vilipiwe kodi, hata kama ni zawadi, ambazo zikiwa ni nyingi.
“Abiria wanaosafiri na usafiri wa ndege wasione eneo la Forodha kama ni adui watoe ushirikiano kwa kuwa wakweli wa vitu walivyobeba, kwani hata zawadi zinalipiwa ushuru, mfano mtu anaweza akawa na begi lililojaa nguo na kudai ni zawadi, au saa za mkononi zaidi ya tatu, zipo sheria kabisa zenye kuonesha na kuzungumzia hili,” amesisitiza Temba.
Pia alisema mizigo lazima ikaguliwe kwa ajili ya usalama na mambo mengine, lakini wanajitahidi kufanya mambo kwa haraka ili kuepusha msongamano wa watu katika eneo la Forodha.
Hatahivyo, katika kipindi cha jana Jumatano cha Jahazi katika Radio ya Clouds, Kibonde alionekana kushangazwa tena na maelezo ya Temba kuwa hata zawadi  zinatozwa kodi.

Tuesday, 8 January 2019

Bonanza la Shimiwi Kufanyika Dodoma Mwezi Ujao

Mchezo wa netiboli nao utakuwepo katika bonanza hilo la michezo la Shimiwi.

Na Mwandishi Wetu
BONANZA la Michezo la Shirikisho ya Michezo ya Wizara na Idara za Serikali (Shimiwi) litafanyika jijini Dodoma Februari 2 na 3 kwenye Uwanja wa Jamhuri, imeelezwa.

Tamasha hilo litatanguliwa na mkutano wa viongozi wa michezo, ambao ni wenyeviti na makatibu wa klabu za michezo za Wizara, Idara zinazojitegemea, Wakala wa Serikali na Ofisi za Wakuu wa Mikoa.

Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa jana na Katibu Mkuu wa Shimiwi Moshi Makuka, mbali na mazoezi ya viungo na mbio za pole (jogging), tamasha hilo litahusisha michezo ya mpira wa miguu, netiboli na ule wa kuvuta kamba.

Makuka alisema katika taarifa hiyo ni matumaini yake kuwa waajiri watatoa ruhusa kwa wahusika ili kuhakikisha bonanza hilo la michezo linafana kwa kushirikisha watu wengi bila kukosa.
Mkutano huo utafanyika Februari Mosi kuanzia saa 2:00 asubuhi na kufuatiwa na bonanza hilo litakalofanyika kwa siku mbili kuanzia Februari 2 kwenye Uwanja wa Jamhuri mjini Dodoma kuanzia saa 12:30 asubuhi.

Alisema kuwa waajiri mbali na kutoa ruhusa, pia wanatakiwa kuwapatia wafanyakazi wao nauli na posho ya kujikimu ili waweze kushiriki vizuri katika mkutano na bonanza hilo la michezo katika siku zilizotajwa.

Monday, 31 December 2018

Michuano ya Emirates FA Cup Sasa Ndani ya DStv


Na Mwandishi Wetu
Wateja wa DStv wanauanza mwaka kwa kicheko baada ya kutangazwa rasmi kuwa DStv itaonyesha michuano maarufu ya ya Emirates FA Cup kupitia chaneli za SuperSport kuanzia tarehe 4 Januari 2019. Hii inamaana kuwa mechi za mzunguko wa tatu sasa zitaonekana katika kisimbuzi cha DStv.

Akizungumzia kurejea kwa michuano hiyo katika chaneli za SuperSport, Mkurugenzi wa MutiChoice Tanzania, Jacqueline Woiso amesema “Lengo letu ni kuwa mstari wa mbele katika kutoa burudani ya soka bora duniani kwa wateja wetu wa DStv hivyo, kuanzia tarehe 4 Januari 2019, wateja wetu wataweza kufurahia michuano ya Kombe la Emirates maarufu kama FA Cup kupitia chaneli za SuperSport zizopatikana ndani ya vifurushi vya DStv".

 Amesema kuwa muda wote MultiChoice imahakikisha kuwa wateja wake wanapata burudani ya hali ya juu na ndiyo sababu wamekuwa wakiongeza maudhui mapya kila uchao katika vifurushi vya DStv.

Sambamba na mechi za michuano ya kombe la FA za mzunguko wa tatu zitakazoanza Januari 4 2019, wateja wa DStv pia wataendelea kuburudika na ligi kubwa za soka zinazotamba duniani ikiwemo ligi kuu ya Uingereza maarafu kama PL, ligi kuu ya Italia Seria A, michuano ya ligi kuu ya Hispania {La Liga} na ligi ya mabingwa Ulaya maarufu kama EUFA Champions League bila kusahau maudhui  mengineyo mengi zikiwamo filamu na tamthilia mpya kutoka nje na ndani ya Tanzania na vipindi vya watoto.

Mechi hizi za michuano  ya Kombe la FA zitakuwa zikipatikana mubashara kupitia chaneli za Supersport ndani ya DStv. Idadi ya mechi zitakazoonekana mubashara zinatofautiana kulingana na aina ya kifurushi huku baadhi ya mechi hizo zikionekana katika kifurushi cha chini cha DStv Bomba kwa Sh 19,000.

Kwa wateja wanaotaka kujiunga na DStv, bado wanaweza kunufaika na ofa inayoendelea ya msimu wa sikukuu ambapo kwa gharama ya Sh.79,000 tu!  Mteja anapata seti kamili ya DStv. Pia kupitia mtandao wa bongoshop.dstv.com mteja anaweza kupata maelekezo ya ziada ya namna ya kujiunga na DStv, ikiwemo kuunganishwa na mawakala na mafundi wa DStv popote alipo.


Tuesday, 18 December 2018

Ndege Mpya Mbili za ATCL Kuwasili Jumapili


Mkurugenzi Mkuu wa TAA, Richard Mayongela akimkaribisha Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, Isack Kamwele.

Na Mwandishi Wetu
SERIKALI imesema ndege mpya mbili za ATCL zinatarajiwa kutua Jumapili zikitokea nchini Canada tayari kwa kuanza kufanya kazi ya kusafirisha abiria.

Aidha, aliwaondoa watu hofu kuwa kusimamishwa kwa huduma za ndege ya Fastjet hakutawaathiri kwa vile wamejipanga kusafirisha abiria usiku na mchana ili kuhakikisha hawapati shida ya usafiri.

Akizungumza na waandishi wa habari,  Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Mhandisi Isack Kamwele alisema ndege hizo zitatua kama ratiba haitabadilika, kwani wameshapeleka rubani na wahudumu wa ndege kwenda nchini humo kwa ajili ya kurudi nazo.

“Mtengenezaji alituahidi mpaka Desemba 23, mwaka huu zitakuwa ziko tayari kurudi kuja kuanza kazi,  tayari tumepeleka wahudumu wa kuja nazo,”alisema.

Waziri huyo aliwatoa hofu Watanzania kuwa  hakuna atakayepata shida ya usfiri wa ndege kwani wamejipanga kwa viwanja vyenye taa kusafiri mpaka usiku na vile visivyokuwa na taa kama Songwe wataongeza ndege kutokana na uhitahiji ili watu wasikose usafiri kwenda na kutoka maeneo yote.

Aliwataka wahudumu wote wa ndege  na wale wa Mamlaka ya Usafiri wa  nchi Kavu na Majini (Sumatra) waliokwenda likizo kurudi haraka kusimamia huduma hizo hasa kipindi hiki cha sikukuu na kuhakikisha nauli haziongezwi upande wa mabasi yaendayo mikoani.

Alizungumzia kuhusu Fastjet kupewa notsi ya siku 28 kwa ndege hiyo kusitisha huduma baada ya kushindwa kulipa madeni yake na kutokidhi huduma za abiria na kwamba hawataruhusiwa kuruka popote hadi kuyalipa ikiwemo huduma, mishahara wanazodaiwa.

Pia Waziri Kamwele aliwataka viongozi na wafanyakazi wa Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Tanzania (TAA) kuhakikisha wanafanyia kazi malalamiko ya abiria wanayoyatoa juu ya mapungufu katika viwanja vya ndege vikiwemo vipoza hewa katika eneo la pili la kuwasili na kuondokea abiria katika Kiwanja cha Ndege cha Kimataifa cha Juliuys Nyerere Jijini Dar es Salaam.

Alisema abiria wamekuwa wakilalamika kuhusu joto lililopo Terminal Two, lakini wahusika hawajachukua hatua yoyote ya kurekebisha na wameendelea kufanya kazi kimazoa tu wakati hiki ni kipindi cha ushindani.

Pia alisema mtandao nao haufanyika  kazi vizuri, hivyo aliwataka TAA kuchukua hatua haraka kurekebisha matatizo hayo, sivyo kuanzia mwakani atachukua hatua kali.

Mkurugenzi Mkuu wa TAA, Richard Mayongela aliomba muda ili kufanyia kazi mapungufu hayo na kusema atachukua hatua za kiutawala kuhakikisha mambo yanakuwa sawa haraka iwezekanavyo.

Mayongela pia aliwataka waandishi wa habari kuwa makini kwa kuandika au kutangaza habari kutoka katika vyanzo vya uhakika au rasmi na sio kupokea taarifa upande mmoja tu, tena kutoka katika mitandao.

Waziri alitoa muda hadi Januari mwakani kufanyia kazi changamoto hizo na ikiwa watashindwa basi wajiondoe wenyewe huku akisisitiza kuwa, sehemu ya tatu ya abiria ya Kiwanja cha Ndeger cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNIA), kinatarajia kuanza kutumika Mei mwakani.