Thursday, 22 March 2018

Usain Bolt kufanya mazoezi na Dortmund


DORTMUND, Ujerumani
GWIJI wa riadha Usain Bolt, ambaye anania ya kuanza kucheza soka akiwa na umri wa miaka 31, leo Ijumaa ataanza mazoezi na klabu ya Borussia Dortmund , klabu hiyo inayoshiriki Ligi Kuu ya Ujerumani ya Bundesliga imetangaza.

"Bolt anakuja!" klabu hiyo ya Ujerumani ilitwitt wakati mkiambiaji huyo wa mbio fupi wa Jamaica alipoandika "BVB, kaeni tayari kwa ajili ya ujio wangu Ijumaa " aliandika katika akaunti yake rasmi.

Tukio hilo limetangazwa hadharani kufuatia wote Bolt na Dortmund kudhaminiwa na Puma.

Mazoezi hayo yamepangwa kufanyika kuanzia saa 10:30 asubuhi kwa saa za haoa na yatakuwa wazi kwa watu wote huku vyombo vya habari kibao vikitarajia kuripoti tukio hilo.

Bolt, ambaye anashikilia rekodi ya dunia yam bio za meta 100 na 200, alitangaza januari atafanya mazoezi ya soka na klabu ya Dortmund wakati wa mapumziko ya ya kipindi hiki.

Tangu alipopstaafu kukimbia mwaka jana, Bolt hakuficha ndoto yake ya kutaka kucheza soka.

Mashabiki wa Manchester United watajipanga kumshuhudia mwanamuziki nyota wa Pop wa Uingereza Robbie Williams katika mchezo wa kuchangia utakaofanyika kwenye Uwanja wa Old Trafford Juni 10.

Bolt, bingwa mara nane wa medali ya dhahabu wa Olimpiki, ataongoza wachezaji 11 wa timu ya Msaada ya Dunia kwa ajili ya kukusanya fedha kwa Shirika la Kimataifa la Watoto (Unicef).

Heart Marathon 2018 Sasa Kupigwa Aprili 29


Na Mwandishi Wetu
MSHINDI wa kwanza wa mbio za Heart Marathon ambazo sasa zitafanyika Aprili 29 badala ya Aprili 26, atazawadiwa kiasi cha Sh milioni 2.

Akizungumza na waandishi wa habari Mikocheni, Dar es Salaam jana, Katibu Mkuu wa mbio hizo, Rebecca John alisema kuwa, wamebadilisha tarehe ya kufanyika mbio hizo baada ya kuombwa na wadau.
Katibu Mkuu wa Kamati ya Maandalizi ya Mbio za Heart Marathon 2018, Rebecca John (katikati) akizungumza na waandishi wa habari leo Mikocheni Jijini Dar es Salaam kuhusu mbio hizo, Kulia ni Mwakilishi wa Riadha Tanzania (RT), Tullo Chambo na Katibu Mkuu wa Chama cha Riadha Mkoa wa Dar es Salaam (DAA), Lucas Nkungu.
John alisema kuwa lengo kuu la mbio hizo ni kuhamasisha mfumo bora wa maisha unaosaidia kupunguza kuenea kwa magonjwa yasiyoambukiza kama magonjwa ya moyo, kisukari, presha na saratani.

Mbali na mbio za kilometa 21, Heart Marathon pia inashirikisha mbio za baiskeli za umbali huo, zile za meta 700 kwa watoto wenye umri chini ya miaka 12, kimoeta 10 na zile za kilometa tano,
Mwakilishi wa Riadha Tanzania (RT), Tullo Chambo akizungumza wakati wa mkutano na waandishi wa habari kuhusu Heart Marathon leo. Kulia ni katibu Mkuu wa Kamati ya mbio hizo, Rebecca John, na Katibu Mkuu wa DAA, Lucas Nkungu.
Akitangaza zawadi kwa washindi kuwa mshindi wa kilometa 21 kwa upande wa wanawake na wanaume, kila mmoja ataondoka na Sh 2 wakati mshindi wa pili Sh milioni 1.5 na yule watatu atapewa Sh milioni 1.

Alisema kuwa zawadi zimeongezwa sana, ambapo katika mbio za mwaka huu mshindi wan ne hadi wa 10, kila mmoja atapewa kifuta jasho cha Sh 100,000 tofauti na miaka ya nyuma, ambapo washindi watatu tu ndio waliokuwa wakipewa zawadi hizo za fedha.

Mbali na kutoa zawadi kwa watakaokuwepo katika 10 bora, pia waandaaji wameongeza zawadi kwa washindi kutoka Sh 500,000 ya mwaka jana hadi milioni 2 za mwaka huu.
Katibu Mkuu wa Chama cha Riadha Mkoa wa Dar es Salaam, Lukas Nkungu akizungumza na waandishi kuhusu mbio za Heart Marathon leo Mikocheni, Dar es Salaam.
Mwakilishi wa Riadha Tanzania, Tullo Chambo alisema kuwa wako tayari kuwasaidia waandaaji wa mbio hizo ili kuhakikisha wanafikia malengo yao ya kuuendeleza mchezo huo nchini.

Katibu Mkuu wa Chama cha Riadha Mkoa wa Dar es Salaam (DAA), Lukas Nkungu alisema kuwa wako pamoja na waandaaji hao, ambapo aliwaomba watu kujitokeza kwa wingi ili kupima afya zao baada ya kushiriki mbio hizo siku hiyo


Tuesday, 20 March 2018

Real, Barca, PSG Wamfukuzia Salah kwa Fedha Nene


LONDON, England
LIVERPOOL inapambana ili kumbakisha mchezaji wake Mo Salah anayetakiwa na klabu kibao kwa ada ambayo ni rekodi ya dunia ya pauni milioni 200.

Real Madrid, Barcelona na Paris Saint-Germain (PSG) zote zinamtaka nyota huyo wa Misri kwa fedha kibao.

Mchezaji huyo amekuwa mpachikaji mzuri wa mabao msimu huu kwa Anfield, ambapo tayari ameshafunga mabao 37 katika mechi 43 alizoichezea klabu hiyo.

Na hiyo ina maana kuwa kocha Jurgen Klopp atakataa ada hiyo ya rekodi ili kuendelea kumbakisha mchezaji huyo katika klabu hiyo.

Salah, ambaye aliigharimu Liverpool kiasi cha pauni milioni 34.3 kutoka Roma katika kipindi cha majira ya joto, akifananishwa na Lionel Messi na bao zake 28 katika  Ligi Kuu ikiwa na maana amefunga mabao matatu zaidi ya ligi zaidi ya mchawi huyo wa Argentina.

Real itatupilia mbali nia yake ya kumsajili Eden Hazard wa Chelsea endapo itamnasa Salah wakati Barca tayari imeshapiga kelele kuhusu Mmisri huyo.

Swali ni je, Liverpool itaendelea kumbakisha Salah au itaweka mbele fedha kama ilivyofanya kwa Coutinho.

Mtoto wa George Weah Aitwa Kikosi cha Marekani


PARIS, Ufaransa
CHIPUKIZI mshambuliaji wa Paris Saint-Germain (PSG) Tim Weah, mtoto wa Rais wa Libelia na mchezaji bora wa dunia wa mwaka 1995 George Weah, ndiye mchezaji ndogo zai kuitwa katika kikosi hicho kwa ajili ya mchezo dhidi ya Paraguay.

Kocha wa muda wa timu ya taifa ya Marekani Dave Sarachan alitangaza orodha ya wachezaji kwa ajili ya mechi ya kimataifa ya kirafiki Machi 27 itakayofanyika Cary,

Kaskazini ya Carolina, ambayo itashirikisha wachezaji 17 kati ya 22 wenye umri wa miaka 24 au chini ya hapo.

Weah, 18, anajiunga kwa mara ya kwanza katika klabu hiyo ya timu ya taifa ya Marekani baada ya kukichezea mara mbili kikosi cha kwanza cha PSG wakati ikishinda 2-0 huko Troyes na ule wa 5-0 dhidi ya Metz.

Wamarekani wameamua kumuinua mchezaji huyo mwenye  umri wa miaka 23 na siku 84 kwa ajili ya kukutana na nchi hizo, ambazo zimeshindwa kufuzu kwa Kombela Dunia Juni nchini Urusi.

"Mchezo huu kwa mara nyingine tena inawakilishwa na baadhi ya sura mpya, alisema Sarachan. "Sehemu kubwa ya kundi hili ni wachezaji vijana ambao tunafikiri watakuwa na muda mrefu na timu hiyo ya taifa pamoja na wachezaji wengine wazoefu.

Weah ni mmoja kati ya wachezaji watano walioitwa kwa mara ya kwanza katika kikosi cha Marekani, pia kinamjumuisha mabeki Antonee Robinson wa Bolton Wanderers, Erik Palmer-Brown wa Ubelgiji.

Wengine ni Bortrijk wa Ubelgiji na Shaq Moore anayeichezea klabu ya Hispania ya Levante pamoja na mshambuliaji Andrija Novakovich wa timu ya Uholanzi ya Telstar.

"Huu ndio muda sasa kuwapatia hawa vijana uzoefu wa mechi za kimataifa, alisema Sarachan. Watapimwa dhidi ya timu yenye uzoefu ya Paraguay."

Palmer-Brown hivi karibuni lisajiliwa na vinara wa Ligi Kuu ya England ya Manchester City na yuko kwa mkopo katika klabu ya Ubelgiji, ambako alianza kuichezea wiki mbili zilizopita.

Mzaliwa wa Uingereza Robinson ameichezea mara 29 timu ya Daraja la Kwanza ya Bolton.

Brazil Kutumia Vifaa vya Spurs London

LONDON, England
TIMU ya taifa ya Brazil imesaini makubaliano na Tottenham Hotspur kutumia vifaa vya klabu hiyo ya Ligi Kuu kwa ajili ya maandalizi ya Kombe la Dunia, limesema Shirikisho la Soka la Brazil (CBF) juzi.

Mabingwa hao mara tano wa Kombe la Dunia watakuwa wakifanya mazoezi mjini hapa kwa ajili ya mechi za kirafiki dhidi ya Croatia Juni 3, kwenye uwanja wa klabu hiyo ya Uingereza,na Australia Juni 10 huko Vienna.

"Mbali na mechi hizo za kirafiki, tayari Brazil imeingia mkataba rasmi na Tottenham kwa ajili ya kushirikiana, ambapo watatoa vifaa vyao kuanzia Mei 28, ilisema taarifa ya CBF.

"Selecao (timu ya taifa ya Brazil) itatumia gym, bwawa la kuogelea na viwanja vizwili vya soka kwa ajili yao pamoja na jengo la hotel lililopo ndani ya eneo la mazoezi.

Brazil itaanza kampeni zake za kusaka taji la Kombe la Dunia kwa kucheza dhidi ya Uswisi Juni 17 kabla ya kukabiliana na Costa Rica na Serbia katika Kundi E.

Watacheza mechi za kimataifa za kirafiki dhidi ya wenyeji wa Kombela Dunia Urusi huko Moscow Ijumaa na mabingwa watetezi Ujerumani huko Berlin siku nne baadae.

Monday, 19 March 2018

Chuoni Yaitambia Miembeni City kwa Bao 1-0


Kocha Mkuu wa timu ya soka ya Chuoni, Suleiman Jabir `Mdau' (kulia) akiwa na Katibu Mkuu wa Kamati ya Olimpiki Tanzania (TOC), Filbert Bayi (katikati). Kushoto ni mpenzi wa michezo, Ally Nyonyi.

Na Mwandishi Wetu, Zanzibar

TIMU ya soka ya Chuoni juzi iliitambia Miembeni City kwa kuondoka na ushindi wa bao 1-0 katika mchezo wa Ligi Kuu ya Zanzibar Kanda ya Unguja uliochezwa kwenye Uwanja wa Amaan mjini hapa.

Mchezo huo uliochezwa majira ya saa 10:00 za jioni ulikuwa na ushindani kiasi huku kila upande yukionekana kutoa malalamiko ya kutotendewa haki na mwamuzi aliechezesha mchezo huo.

Bao hilo la pekee liliwekwa kimiani na mchezaji wake Rashid Roshwa mnamo dakika ya 73 za mchezo huo, ambao kabla ya huo Polisi ilishuka kuumana na Kipanga na kushinda mabao 3-1.

Chuoni licha ya ushindi huo bado ipo katika nafasi ya nne kutoka mkiani ikiwa na pointi 22 katika msimamo wa ligi hiyo inayoongozwa na KVZ wenye pointi 35.

Katika mchezo huo, Miembeni City ilikosa penalti katika dakika ya 85 kupitia kwa mchezaji wake, Yahya Haji Karoa, penalti ambayo ilitokana na Seif Salum kufanyiwa madhambi na mlinda mlango wa timu ya Chuoni.

Mchezo mwingine ambao uliwakutanisha Polisi na Kipanga ambapo Polisi ilitoka na ushindi wa bao 3-1, huku mabao yake yalifungwa na Suleiman Ali Nuhu dakika ya 11 na mawili yalifungw ana Suleiman Mwalimu dakika ya 55 na 78.

Polisi kwa matokeo hayo imefikisha pointi 26 na kuwa nafasi ya nane katika msimamo wa ligi hiyo, wakati Kipanga inabaki katika nafasi ya pili kutoka Mkiani ikiwa na pointi 11.

Ligi hiyo inatarajiwa kuendelea tena kesho kwa  mchezo mmoja ambao utawakutanisha Taifa ya Jang’ombe na Miembeni City.


Saturday, 17 March 2018

Mfanyakazi wa Emirates Aliyeanguka Afariki Dunia


KAMPALA, Uganda
MUHUDUMU wa katika ndege aliyeanguka kutoka katika mlango wa dharura wa ndege ya Emirates iliyokuwa imeegeshwa kwenye Kiwanja cha Ndege cha Entebbe, Uganda, amefariki dunia, imeelezwa.

Mwanamke, ambaye utaifa wake haujajulikana, alikimbizwa katika hospitali ya Kisubi kilometa 16 (sawa na maili 10) kutoka eneo la tukio, alikufa mara baada ya kufikishwa hospitalini hapo, ameeleza msemaji.

Ripoti hiyo imesema kuwa mfanyakazi huyo wa ndege ya Emirates alikuwa akiiandaa ndege hiyo kwa ajili ya kuchukua abiria wakati tukio hilo lilipotokea.

Mamlaka ya Anga ya Uganda inasema kuwa imeanzisha uchunguzi.

Katika taarifa yao imesema kuwa muhudumu huyo wa ndege “alikuwa akitaka kufungua mlango huo wa dharura” na kwa bahati mbaya alianguka nje ya ndege, ambsyo ilitua na kupaki salama”.

Msemaji wa hospitali ya Kisubi Edward Zabonna alisema kuwa muhudu huyo wa ndege akiumia katika “uso wake wote na magoti”.

Alisema kuwa alikuwa “amepoteza fahamu lakini hai” wakati alipowasili hospitalini hapa juzi jioni lakini alifariki muda mfupi baadae.

Taarifa kutoka Shirika la Habari la AFP zilikariria taarifa kutoka katika ndege ya Emirates inayosema: "Mfanyakazi wa ndege yetu bahati mbaya alianguka kutoka katika mlango wa dharura uliokuwa wazi wakati akiandaa ndege kupandisha abiria”.

Ndege hiyo yenye maskani yake Dubai ilimeahidi “kutoa ushirikiano mkubwa” kwa wachunguzi.

Wenger Aikwepa Atletico Robo Fainali UEFA Ndogo


ZURICH, Uswisi
KOCHA Arsene Wenger amefanikiwa kuikwepa Atletico Madrid baada ya timu yake kupangwa na CSKA Moscow katika robo fainali ya Kombe la Ligi.

Wenger tangu awali alikaririwa akisema kuwa hataki kabisa kusikia timu yake imepangwa na Atletico Madrid katika hatua hiyo ya robo fainali.

Alisema kwa kikosi hicho cha Diego Simeone kinapewa nafasi kubwa ya kutwaa taji hilo mwaka huu.

The Gunners itakuwa mwenyeji wa mchezo wa kwanza utakaofanyika kwenye Uwanja wa Emirates Aprili 5 huku mchezo wa marudiano utapigwa wiki moja baadae mjini Moscow.

Timu ya Hispania ya Atletico Madrid, ambayo inashika nafasi ya pili katika Ligi Kuu ya Hispania, La Liga, itakabiliana na Sporting Lisbon ya Ureno.
Katika mchezo mwingine, timu ya Ujerumani ya RB Leipzig itacheza dhidi ya Marseille ya Ufaransa, wakati klabu ya Italia ya Lazio itacheza dhidi ya Salzburg ya Austria.

Liverpool, City Robo Fainali Ligi ya Mabingwa Ulaya


ZURICH, Uswisi
LIVERPOOL itamenyana na wapinzani wake wakubwa wa Ligi Kuu ya England, Manchester City katika hatua ya robo fainali ya Ligi ya Mabingwa wa Ulaya.

Timu hizo tayari zimekutana mara mbili katika Ligi Kuu ya England msimu huu,kila moja ikishinda mchezo wake wa nyumbani.

Uwanja wa Anfield utaandaa mchezo wa kwanza wa robo fainali utakaofanyika Aprili 3 na 4 huku ule wa marudiano utakuwa Aprili 10 na 11.
Man City ilitinga robo fainali baada ya kuifunga Basel kwa jumla ya mabao 5-2, wakati Liverpool iliibwaga Porto kwa mabao 5-0 katika mchezo wa kwanza huko Ureno.

Mabingwa watetezi Real Madrid itakutana na Juventus wakirudia fainali ya mwaka jana, Sevilla imetinga hatua hiyo badaa ya kuitoa Manchester United itakutana na mabingwa mara tano Bayern Munich, wakati Barcelona watakutana na Roma.
Ratiba Kamili ya robo fainali Ligi ya Mabingwa Ulaya:

Barcelona v Roma

Sevilla v Bayern Munich

Juventus v Real Madrid

Liverpool v Manchester City

Mechi za kwanza za robo faiali zitapigwa Aprili 3 na 4 na mechi za marudiano zitapigwa Aprili 10/11.

Azam Yatangaza Filamu Zinazowania Tuzo ya SZIFF


Mtendaji Mkuu wa Azam Media, Tido Mhando akizungumza na waandishi wa habari kuhusu Tuzo za SZIFF. Kushoto ni Mkurugenzi Mratibu wa Vipindi wa Uhai Production, Yahaya Mohamed Kimaro.
Na Mwandishi Wetu
WAANDAAJI wa Tuzo za Sinema Zetu International Festival (SZIFF), Azam TV wametangaza sinema ambazo zitashindania aina 19 ya tuzo, ambazo zitatolewa Aprili mosi katika ukumbi wa Mlimani City Jijini Dar es Salaam.

Akizungumza kabla ya kutangaza rasmi sinema zikakazowania tuzo hiyo, Mtendaji Mkuu wa Azam Media, Tido Mhando alisema wameamua kuandaa tuzo hizo za kila mwaka ili kuwatia moyo wasanii wa Bongo Movie.
Jaji Mkuu wa SZIFF, Martin Mhando akizungumza na waandishi wa habari. Kulia ni Msimamizi wa Sinema Zetu, Zamaradi Nzowa na kushoto ni Mkurugenzi Msaidizi waAzam Media Ltd, Jacob Joseph
Alisema tuzo hizo zinafanyika kwa mara ya kwanza zitasaidia pia kuwawezesha wasanii wa filamu Tanzania kuboresha kazi zao, kutafuta soko ndani nje ya nchi.

Mhando alisema kuwa tuzo za SZIFF ambazo pia zinahusisha wasanii kutoka Rwanda, Burundi, Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo na wenyeji Tanzania zitasaidia kurejesha heshima iliyopotea ya Bongo Movie.

WASANII MAARUFU
Mhando alisema kuwa hafla hiyo, mbali na kuwaleta pamoja wasanii maarufu duniani,pia kutakuwa na mgeni maalum kutoka Bollywood ya India Pritika Rao au maarufu kama Aliyah.
Mkurugenzi Msaidizi wa Azam Media Ltd, Jacob Joseph akizungumza. Kulia ni Jaji Mkuu wa SZIFF, Martin Mhando.
Alisema kuwa msanii huyo nyota wa Bollywood alikuwa kivutio cha watazamaji wengi wa filamu nchini kupitia Azam TV kupitia tamthilia ya Beitehaa.

Washindi wa tuzo kwa mujibu wa waandaaji kupitia chaneli ya Sinema zetu, watapata fedha taslimu, vyeti na zawadi zingine kama vikombe maalum.
Msimamizi wa Sinema Zetu, Zamaradi Nzowa akizungumza wakati wa hafla hiyo.
Mhando alisema tuzo za SZIFF ambazo zinaandaliwa kwa kushirikiana na Baraza la Sanaa la Taifa (Basata), Bodi ya Filamu na Cosota zilianza Januari na kumalizika Machi 12.

“Tulipokea zaidi ya filamu 500 na vilichujwa hadi kufikia 143 ambazo sasa zinawania tuzo hizo 19, alisema Mhando katika mkutano huo na waandishi wa habari.

Mwenyekiti wa jop[o la majaji Martin Mhando, alitangaza sinema ambazo zinawania tuzo hizo 19, zikiwemo Chaguo la Watazamaji, ambazo kwa upande wa Filamu Bora ni Bantu, Genge, Safari ya Gwalu, Watatu, The Dream, Heaven Sent, Bandidu, Harusi ya
Teja na Haki ya Nani.
Filamu ambazo ziwania tuzo ya muongozaji bora ni Bantu, Chaguo Langu, Safari ya Gwalu, Watatu, The Dream, Nyoyo Zangu, Haki ya Nani, Bandidu na Genge.

Filamu ambazo waigizaji wake wanawania tuzo ya waigizaji bora ni Bantu, Father Ezra, Safari ya Gwalu, Watatu, Bandidu, Heaven Sent, Genge, The Dream, Nyoyo Zangu, Mama wa Marehemu, Kivuli cha Ahadi na Malaika.
Tuzo zingine ni zile za mchekeshaji bora, Muziki bora na zingine.

Jaji Mkuu huyo alisema watazamaji wa Sinema Zetu wataendelea kupiga kura kupitia ujumbe mfupi wa simu za mkononi na kutuma kwa namba 0757-339567.

Nyota Bollywood Kushuhudia Tuzo za Sinema Zetu

Na Mwandishi Wetu
MSANII maarufu wa tamthilia ya Kihindi ya Beintehaa, Preetika Rao au maarufu kwa jina la Aliyah atakuwa mgeni maalum katika hafla ya utoaji tuzo za Sinema Zetu utakaofanyika Aprili Mosi.

Aliyah ambaye anajulikana sana na watumiaji wa kingamuzi cha Azam, ambacho kilikuwa kikirusha tathilia ya Beintehaa kila kuanzia Jumatatu hadi Ijumaa kuanzia saa 3:30 usiku.
Mkurugenzi Mkuu wa Azam Media, Tido Mhando alisema jana kuwa, Alia atakuwa mgeni maalum wakati wa hafla ya utoaji tuzo hizo utakaofanyika katika ukumbi wa Mlima City jijini Dar es Salaam.

Azam TV kupitia chaneli yake ya sinema zetu imetangaza vipengele 18 vya filamu zitakazowania tuzo za Sinema Zetu International Film Festival ikiwemi kipengele cha chaguo la watazamaji.

Mhando alisema kuwa Usiku wa Tuzo za SIFF utaruka moja kwa moja kutoka Mlimani City kupitia chaneli ya Sinema Zetu, ambapo wageni waalikwa watapita katika zuria jekundu.

Baadhi ya vipengele ambavyo vinagombewa ni pamoja na Filamu Bora, Muongozaji Bora, Muigizaji Bora, Mchekeshaji bora.

Huku katika kipengele cha filamu fupi kuna tuzo ya filamu bora, muongozaji bora, muziki bora na mambo mengine.

Tido alisema kuwa mbali na Aliyah kutakuwa na watu wengine maarufu pamoja na mgeni rasmi, ambaye atatajwa baadae.

Jumla ya filamu 143 zilipata nafasi ya kupambanishwa na kuruka kila siku kupitia chanel ya Sinema Zetu, ambapo watazamaji walipata nafasi ya kupiga kura kwa njia ya ujumbe mfupi wa maneno.

Tuesday, 13 March 2018

Southampton wamtupia Virago Kocha Pellegrino


LONDON, England
KLABU Southampton imemtupia virago kocha wake Mauricio Pellegrino (pichani) huku timu hiyo ikiwa pointi moja na nafasi moja juu ya ukanda wa kushushwa daraja wakati zimebaki mechi nane kabla ya kumalizika kwa msimu.

Watakatifu hao wameshinda mechi moja tu kati ya 17 za ligi zilizopita na ilifungwa mabao 3-0 huko Newcastle United Jumamosi.

Pellegrino, mwenye umri wa miaka 46, aliteuliwa kuifundisha timu hiyo Juni akichukua nafasi ya Claude Puel.

Timu hiyo ina matumaini ya kuwa na kocha mpya kabla haijakabiliana na Wigan Jumapili kwa ajili ya kusaka nafasi ya nusu fainali ya Kombe la FA.

Wako katika msimu wa sita mfululizo katika Ligi Kuu ya England na hawajawahi kumaliza chini ya nafasi ya 14 katika misimu mitno iliyopita.

Pellegrino alisema ameona baadhi ya wachezaji waliokatatamaa wakati wa mchezo wa Jumamosi.

Pellegrino, mcheszaji wazamani wa kimataifa wa Argentina, alipata pointi 0.93 kwa mchezo, ikiwa ni asilimia mbaya zaidi kwa kocha yeyote wa Southampton katika Ligi Kuu.

Klabu hiyo ilisema katika taarifa yake kuwa wanataka kuteua timu mpya ya uongozi haraka iwezekanavyo, tayari hilo liko katika mchakato.

Ni timu ya tisa ya Ligi Kuu kubadili kocha msimu huu.

Kocha msaidizi Carlos Compagnucci na kocha msaidizi wa kikosi cha kwanza Xavier Tamarit nao pia wameondoka katika klabu hiyo.

Chelsea Mikononi Mwa Barcelona Kesho Ulaya


BARCELONA, Hispania
KOCHA wa Chelsea, Antonio Conte amesema kuwa timu yake inatakiwa kuteseka hapa kesho ikiwa inataka kufuzu kucheza hatua ya robo fainali ya Ligi ya Mabingwa wa Ulaya.

Barcelona inaikaribisha Chelsea leo katika mchezo wa marudiano wa hatua ya 16 baada ya kutoka sare ya 1-1 katika mchezo wa kwanza uliofanyika Stamford Bridge mjini London.

Chelsea ina kibarua kigumu kwani inahitaji ushindi wa aina yoyote au sare ya kuanzia mabao 2-2 ili kusonga mbele katika mashindano hayo makubwa ya klabu barani Ulaya.

Barcelona ilifunga bao la kusawazisha katika dakika ya 75 kupitia kwa Lionel Messi kufuta bao la kuongoza lililofungwa katika kipindi cha pili na kiungo Willian katika mchezo wa kwanza mwezi uliopita.

Conte alisema timu yake itakabiliana na kibarua kigumu dhidi ya mabingwa hao mara tano wa Ulaya katika mchezo huo utakaofanyika Nou Camp.

"Tunatakiwa kuwa vizuri sana lakini unapocheza dhidi ya timu kama hii, ambayo nafikiri ni moja ya timu bora duniani, lazima ujiandae kutaabika, kama vile tulivyofanya katika mchezo wa kwanza, ambako tulijiandfaa vizuri, alise,a Conte katika mtandao wa klabu hiyo.

"Hii sio ile timu (Chelsea) yenye wachezaji wazoefu ambao wanacheza msimu wa kwanza au wa pili katika Ligi ya Mabingwa.

"Lakini tunatakiwa kucheza kama timu na na kujaribu kuwa tayari kutaabika, na katika kila muda tunatakiwa kujua kuwa tunaweza kuwa na nafasi ya kufunga.

Barcelona ilitawala katika mchezo wa awali, lakini kikosi cha Conte kwa bahati mbaya hakikupata ushindi baada ya Willian mara mbili kushindwa kufunga kabla ya mapumziko.
Barcelona imezidi kuimarika kwa ajili ya mchezo huo baada ya nahodha wake, Andres Iniesta, ambaye alikuwa nje ya uwanja kwa sababu ya maimivu, juzi alianza mazoezi kwa ajili ya mchezo huo.

Iniesta alifanya sehemu ya mazoezi pamoja na baadhi ya wachezaji wa kikosi cha kwanza cha Barca, akiongeza matumaini ya kurejea katika mchezo huo wa marudiano wa hatu ya 16 bora.

Iniesta aliumia Barcelona ilipocheza dhidi ya Atletico Madrid siku nane zilizopita na Jumamosi alikosa mchezo walioshinda 2-0 dhidi ya Malaga.

Pia timu hiyo Jumamosi ilimkosa nyota wake Lionel Messi, ambaye alikwenda kushuhudia kuzaliwa kwa mtoto wake, Ciro, lakini mshambuliaji huyo atakuwemo katika mchzo huo.

MultChoice Yazindua Tuzo za AMVCA 2018

Mkurugenzi Mkuu wa MultiChoice, Maharage Chande.

Na Mwandishi Wetu
WASANII wa Tanzania wametakiwa kuwasilisha kazi zao kuanzia sasa hadi Aprili 30 kwa ajili ya kushindania tuzo maarufu ya AMVCA 2018.

Mkurugenzi Mkuu wa MultiChoice, Maharage Chande alisema jana, tuzo hizo za Africa Magic Viewers (AMVCAs)wasanii wa filamu wanatakiwa kuwasilisha kazi zao kwa ajili ya kushindanishwa.

Chande alisema kuwa tuzo hizo, ambazo hufanyika kila mwaka zimekuwa zikihusisha maelfu ya wasanii wa filamu kushindana.

Alisema kuwa tuzo zilibuniwa ili kuthamini na kutambua mchango wa watengeneza filamu wa Afrika, waigizaji, waigizaji na wataalam wa sekta ya filamu na telvisheni barani Afrika.

Alisema kuwa tuzo za mwaka huu zinatarajia kuwa kubwa zaidi na ushindani unatarajia kuwa wa aina yake kutoka kwa wasanii mbalimbali.

Alisema kuwa baada ya kimya cha muda mrefu,
Africa Magic ikishirikiana na MultiChoice, hatimaye wametangaza rasmi kuanza kwa kinyanganyiro cha moja ya tuzo maarufu duniani katika tasnia ya sanaa ya filamu.

Tuzo hizo ambazo hufanyika kila mwaka zimekuwa zikihusisha mamia ya washiriki kutoka kila kona ya bara la Afrika na zimekuwa moja ya tuzo zilizojizolea umaarufu mkubwa barani Afrika na duniani kwa ujumla na limekuwa ni jukwaa muhimu la kutambua na kuenzi vipaji vya tasnia ya filamu katika bara la Afrika.

Baada ya mapumziko mafupi, tunayo furaha kutangaza kwamba  mwaka 2018 utakuwa na toleo la mwaka wa sita mfululizo wa MultiChoice na Africa Magic kuandaa AMVCAs kwa mafanikio na tunaendelea kujivunia mabadiliko yanayoonekana kwenye nyanja ya filamu tangu Tuzo zilipoanzishwa.

Katika msimu uliopita, Filamu za Kitanzania ziliwika katika Kundi la Filamu Bora Afrika Mashariki, ambapo Aisha ya  Amil Shivji, Naomba Niseme ya Staford  Kihore, na Homecoming ya Seko Shamte zilichaguliwa huku  Siri ya Mtungi ikijitokeza kwenye Kundi la Filamu Bora za lugha ya Kiswahili.

Msimu uliopita, filamu ya Kitendawili ya Richard Mtambalike ilinyakua tuzo ya filamu bora ya lugha ya Kiswahili wakati Elizabeth Michael Lulu alivuma katika tuzo hizo katika filamu yake ya Mapenzi iliyoteuliwa kuwa filamu bora kabisa Afrika Mashariki.
Kwa maelezo zaidi juu ya mahitaji ya kujiunga na taratibu za uwasilishaji, tafadhali ingia www.dstv.com.


Kuingia AMVCAs ni bure na tarehe ya kufungwa kwa maingizo ni 30 Aprili 2018. Filamu au sinema zilizotayarishwa kwa ajili ya televisheni au tamthiliya za kwenye televisheni ambazo ziliingizwa mwanzoni au kuteuliwa kwa ajili ya tuzo, au kutuzwa zawadi katika shindano lingine la filamu na televisheni zinaruhusiwa kuingizwa kwenye AMVCAs kama zinarushwa au kuoneshwa katika kipindi cha kuanzia Oktoba, 2016 hadi Machi, 2018.

Maelekezo ya kushiriki:

HATUA YA 1

Prepare a 2 to 3 minute long showreel for your online submission. /Andaa ufupisho wa filamu yako wenye muda wakati ya dakika 2 hadi 3 kwa ajili ya kuuwasilisha kwa njia ya mtandao.

HATUA YA 2

Ingia www.africamagic.tv na uende kwenye ukurasa wa kuwasilisha.

HATUA YA 3
Jaza fomu za uwasilishaji na upandishe video yako. Namba ya kipekee ya utambulisho itatolewa kwa kila ingizo la mtandaoni lililokamilika. Kisha kutegemea na eneo ulipo, tuma ingizo lake akionesha namba zake za utambulisho.