Tuesday 14 November 2017

Italia Yashindwa Kufuzu Kombe la Dunia 2018

Wachezaji wa Italia wakifarijiana baada ya kushindwa kufuzu kwa fainali za Kombe la Dunia 2018. Timu hiyo ilitoka suluhu na Sweden katika mchezo uliofanyika San Siro, Italia baada ya kufungwa 1-0 katika mchezo wa kwanza nchini Sweden, hivyo imetolewa kwa kufungwa 1-0.

ROME, Italia

MABINGWA mara nne wa dunia Italia wameshindwa kufuzu kwa fainali za Kombe la Dunia kwa mara ya kwanza tangu mwaka 1958 baada ya kushindwa katika mchezo wa mchujo dhidi ya Sweden.

Suluhu dhidi ya Sweden, haikuisaidia Italia kusonga mbele na badala yake wapinzani wao hao ndio wamefuzu kucheza fainali hizo kwa mara ya kwanza tangu mwaka 2006 walipofuzu kwa fainali hizo.

Hiyo ina maana kuwa timu ya taifa ya Italia inayojulikana kama Azzurri itakosa mashindano hayo kwa mara ya pili tangu yalipoanzishwa baada ya kushindwa kushiriki wakati wa ufunguzi wa mashindano hayo mwaka 1930.

Katika mchezo wa kwanza uliofanyika Sweden wiki iliyopita, Italia walipokea kichapo cha bao 1-0 kabla ya kutoka suluhu katika mchezo huo wa juzi uliofanyika kwenye Uwanja wa San Siro jijini Milan.

Pamoja na suluhu hiyo, lakini wenyeji ndio walitawala zaidi mchezo huo kwa asilimia 76, licha ya kushindwa kuzifumania nyavu.

PIGO KWA KIPA

Mbali na kutolewa, Italia pia ilipata pigo jingine baada ya kipa wao na baadhi ya wachezaji wengine kuamua kustaafu baada ya timu yao kushindwa kufuzu kwa fainali za mwakani zitakazofanyika Urusi.

Nafasi safi ya Italia kupata bao ilitibuliwa na kipa wa Sweden Robin Olsen alipookoa mpira uliopigwa na mchezaji aliyetokea benchi Stephan El Shaarawy.

Mshambuliaji Ciro Immobile alikosa nafasi kibao na juhudi zake katika kipindi cha kwanza ziliokolewa katika mstari na beki wakati Andreas Granqvist.

Kipa Gianluigi Buffon alisema alikuwa na majonzi makubwa yeye pamoja na wadau wote wa soka wa Italia kwa nchi yao kushindwa kufuzu baada ya kufungwa na Sweden.

Mtu akisoma gazeti la michezo la Italia la "Gazetta dello Sport" huku ukurasa wa mbele ukisomeka "Mwisho" siku moja baada ya Italia kutolewa katika hatua ya kufuzu kwa Kombe la Dunia walipocheza dhidi ya Sweden juzi katika soko la vyakula jijini Rome, Italia.

Buffon, 39, alisema: "Ni aibu kwa mchezo wangu rasmi wa mwisho kwa kuumaliza kwa kushindwa kufuzu kwa Kombe la Dunia.

"Lawama zinagawanywa kwa kila mmoja. Hakuna mtu wa kutupiwa lawama hapa.”

Mchezaji mwenzake na Buffon wanayecheza pamoja na Juventus Andrea Barzagli na kiungo wa Roma Daniele de Rossi pia alimaliza kipindi chake cha kuichezea Italia, wakati Giorgio Chiellini anatarajia kujiunga nao. Wanne hao wamecheza mechi 461 miongoni mwao.


Kipa Buffon ameichezea timu hiyo mechi 175 katika kipindi cha miaka 20, ambapo alitwaa taji la Dunia 2006 – na anaamini kuwa bado timu hiyo inaweza kufanya vizuri mbeleni.

No comments:

Post a Comment