Monday, 23 October 2017

Mkurugenzi TAA ataka Tughe kutetea wafanyakazi

Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Viwanja vya ndege Tanzania (TAA), Bw. Richard Mayongela (katikati mstari wa mbele), akinyanyua mikono juu kuashiria mshikamano daima na baadhi ya viongozi wa matawi wa chama cha wafanyakazi mahala pa kazi (TUGHE) matawi ya Makao Makuu na Kiwanja cha Ndege cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNIA), alipokutana nao.

Na Mwandishi Wetu

KAIMU Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Tanzania (TAA), Bw. Richard Mayongela amewataka viongozi wa Chama cha Wafanyakazi kusikiliza malalamiko

ya wafanyakazi bila kubagua.

 

Bw.Mayongela alisema viongozi wa Wafanyakazi kupitia matawi mawili ya Chama cha Wafanyakazi, TAA Makao Makuu na Kiwanja cha Ndege cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNIA), kutenda haki kwa kusikiliza malalamiko ya wafanyakazi wote na kuyawasilisha kwa wasilisha kwa mwajiri ili yafanyiwe kazi.

Alitoa kauli hiyo juzi wakati viongozi wa matawi hayo walipokwenda kujitambulisha ofisi kwake TAA Makao Makuu, ambapo alisisitiza kuwa wafanyakazi wa chini ndio wenye matatizo makubwa, lakini hawasikilizwi na kutatuliwa matatizo yao kwa wakati.

Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Viwanja vya ndege Tanzania (TAA), Bw. Richard Mayongela (katikati mstari wa mbele), akinyanyua mikono juu kuashiria mshikamano daima na baadhi ya viongozi wa matawi wa chama cha wafanyakazi mahala pa kazi (TUGHE) matawi ya Makao Makuu na Kiwanja cha Ndege cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNIA), alipokutana nao jana.

“Ninashukuru uongozi mmekuja kuonana nami, ninahitaji ushirikiano wenu kama Chama cha Wafanyakazi, muwatumikie wafanyakazi kwa kutenda haki mkisikiliza matatizo ya kila mmoja na kufikisha sehemu husika na ninawaahidi kuwa nanyi bega kwa bega kutatua matatizo ya wafanyakazi kwani wao ndio wanafanya TAA iwepo, “alisema Mayongela.

Alisema wafanyakazi endapo wakifanya kazi bila manung’uniko wala makundi, mamlaka itasonga mbele kwa kuwa na uongozi sio kupigana vita bali unatakiwa kujijenga na kuwa kitu kimoja.

Hatahivyo alisema kwa sasa yupo mbioni kuangalia namna ya kuboresha maslahi ya wafanyakazi  kwa kupitia makusanyo yatakayotokana na vyanzo mbalimbali vya mapato ili kuongeza tija na ufanisi wa kazi ili kuongeza ari kwa wafanyakazi.

Viongozi wa Chama cha Wafanyakazi mahala pa Kazi (TUGHE) matawi ya Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Tanzania, Makao Makuu (TAA HQ) na Kiwanja cha Ndege cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNIA), wakimsikiliza kwa makini Kaimu Mkurugenzi Mkuu, Bw. Richard Mayongela (kushoto) alipokutana nao.

Aliendelea kusema kuwa inaonekana wafanyakazi wengi wa TAA wamekata tamaa kutokana na kufanya kazi nyingi na wakati mwingine kupitiliza muda wa kazi wa kawaida bila kupata stahiki yeyote.

“Kwa msaada wa Mungu nina imani atanionyesha wapi fedha zilipo na jinsi ya kuzitumia ipasavyo kwa masuala ya msingi, na ninakusudia hadi kufika Desemba mwaka huu niweze kuboresha maslahi ya wafanyakazi.

Watu wanafanya kazi sana lakini maslahi ni madogo, unaona kabisa jinsi mtu anavyoitumikia taasisi kwa moyo, lakini sura inaonesha jinsi alivyokata tamaa, ninaamini kwa kufanya hivi itaongeza tija na bidii ya kazi.” Alisema Bw. Mayongela.

Halikadhalika, Bw. Mayongela amesema atahakikisha wafanyakazi wanapata vitendea kazi vya uhakika kulingana na kazi zao, zikiwemo bajaji, pikipiki na magari kwa ajili ya doria na shughuli za uendeshaji ndani ya Viwanja vya Ndege.

Pia amewataka viongozi hao kuwa karibu na wafanyakazi ili kuhakikisha wanawahamasisha wanafanya kazi kwa bidii, uaminifu na uadilifu ili kuondoa mianya na tabia za upokeaji wa rushwa, kwa kuwa TUGHE ni daraja kati ya mwajiri na wafanyakazi.

Naye Mwenyekiti wa TUGHE tawi la TAA Makao Makuu, Bw. Nasib Elias mbali na kumshukuru Kaimu Mkurugenzi Mkuu kwa kuwapa fursa ya kukutana naye, lakini alimuomba kuendelea kudumisha mahusiano baina ya mwajiri na Tughe.

Pia alimuomba aitake menejimenti yake kuwa na utaratibu wa kuweka milango wazi kwa wafanyakazi kama yeye ili waweze kusikiliza na kutoa majibu sahihi kwa baadhi ya masuala ya kiofisi yanayowasilishwa na wafanyakazi kwao na sio kila jambo liwasilishwe kwake.

“Tunakuombea kwa Mungu akutie nguvu kwa haya unayotaka kufanya likiwemo la kuboresha maslahi ya wafanyakazi kwa kuwa litasaidia kuamsha morali ya kazi kwa wafanyakazi, lakini hii sera yako ya kuwacha milango wazi, tunaomba nayo itekelezwe katika ngazi ya menejimenti yako kwani kuna mambo ambayo yanaweza kumalizwa na Wakurugenzi na Mameneja wenyewe na sio lazima yafike kwako, “ alisema Bw. Elias.


Katika kuboresha maslahi ya wafanyakazi ambacho kimeonekana ni kipaumbele cha Kaimu Mkurugenzi mkuu kwa wafanyakazi, Bw. Elias amemuomba kuangalia namna bora ya kusimamia maslahi hayo ikiwemo kuuasili mkataba wa hali bora (SBA) kama inavyotekelezwa na taasisi nyingine za serikali.

Thursday, 19 October 2017

Naibu Waziri amtaka mkandarasi haraka

Na Mwandishi Wetu

NAIBU Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano (sekta ya Ujenzi),  Mhe. Elius Kwandikwa, amemtaka Mkandarasi wa kampuni ya ujenzi ya China ya CHICO aliyepewa zabuni ya ujenzi wa Kiwanja cha ndege cha Shinyanga kuanza ujenzi huo haraka.

Akizungumza mara baada ya kukagua maendeleo ya ujenzi wa kiwanja hicho katika eneo la Ibadakuli leo, mkoani Shinyanga, Mhe. Kwandikwa, amesema kuwa haoni sababu ya mkandarasi huyo kuchelewa kuleta vifaa vyake katika eneo la mradi hadi sasa wakati tayari mkataba wa kuanza kazi hiyo umeshasainiwa.

Naibu Waziri wa Ujenzi. Uchukuzi na Mawasiliano, (Sekta ya Ujenzi), Mhe. Elius Kwandikwa (katikati) akizungumza na Meneja wa Tanroads Shinyanga, Bw. Bartholomew Ndirimbi (kushoto) na Meneja wa Kiwanja cha Ndege cha Shinyanga, Bw. Julius Msollow (kulia)

"Mkandarasi hana sababu ya kuchelewa kuanza kazi wakati fedha zipo na zimeshatengwa kwa ajili ya mradi huu na mkataba umeshasainiwa,  sasa namwagiza kuleta vifaa vyake na kuanza kazi mara moja", amesema Mhe. Kwandikwa.

Aidha, Mhe. Kwandikwa amemtaka Meneja wa kiwanja hicho, Bw. Julius Msollow kuhakikisha anakuwa bega kwa bega na kutoa ushirikiano kwa kumsimamia mkandarasi huyo, ili kuhakikisha kiwanja hicho kinakamilika mapema na kwa viwango vinavyotakiwa.

"Naamini tukimsimamia vizuri mkandarasi huyu tutapata kiwanja kizuri na imara hapa Shinyanga na tutafungua fursa mbalimbali za kiuchumi katika mkoa huu", amesisitiza Mhe. Kwandikwa.

Naibu Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano (Sekta ya Ujenzi), Mhe. Elius Kwandikwa, akizungumza na wananchi wa Mwigumbi mkoani Shinyanga, alipofanya ziara ya kukagua barabara ya Mwigumbi – Maswa (KM 50.3), inayounganisha mkoa wa Shinyanga na Simiyu.

Kwa upande wake, Meneja wa kiwanja cha ndege cha Shinyanga, Bw. Msollow, amemhakikishia na kuahidi kuwa atatoa ushirikiano kwa mkandarasi huyo atakapowasili eneo la mradi.

Bw. Msollow amesema kuwa mradi huo utahusisha ujenzi wa barabara ya kuruka na kutua ndege, jengo la abiria, maeneo ya maegesho ya ndege na mnara wa kuongozea ndege.

Naibu Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano (Sekta ya Ujenzi), Mhe. Elius Kwandikwa, akifafanua jambo kwa Mkuu wa Wilaya ya Shinyanga, Bi. Josephine Matiro (Watatu kushoto), alipofika mkoani humo kukagua  maendeleo ya kiwanja cha ndege cha Shinyanga kilichopo eneo la Ibadakuli.

Amesema barabara ya kutua na kupaa kwa ndege inarefushwa kwa urefu wa Kilometa mbili na itakuwa kwa kiwango cha lami, ikigharimu zaidi ya shilingi Bilioni 49.

Wakati huohuo, Naibu Waziri Kwandikwa, amekagua maendeleo ya ujenzi wa barabara ya Mwigumbi - Maswa (KM 50.3), mkoani Simiyu na kumsisitiza mkandarasi anayejenga barabara hiyo kuikamilisha kwa wakati na kwa viwango.

Amesisitiza kuwa kukamilika kwa barabara hiyo ambayo ni kiungo kwa wananchi wa Maswa, Bariadi, Lamadi na Mwanza, kutarahisisha huduma za usafirishaji wa abiria na mizigo katika maeneo hayo.

Naye, Meneja wa Wakala wa Barabara (TANROADS), mkoani Simiyu, Mhandisi Albert Kent, amesema kuwa mradi upo katika hatua nzuri na unatarajiwa kukamilika ndani ya miaka miwili kutoka sasa.


Naibu Waziri Kwandikwa amefanya ziara ya kikazi katika mkoa wa Shinyanga na Simiyu ambapo amekagua miradi mbalimbali inayotekelezwa na Wizara yake.

Multichoice Yatimiza miaka 20 kwa Mbwembwe.. Ofa kabambe kwa watakaohudhuria maonesho Mlimani City!

Na Mwandishi Wetu

KAMPUNI ya Multichoice Tanzania inatimiza miaka 20 toka kuanza kutoa huduma katika soko la Tanzania. 

Multichoice inajivunia mafanikio yake katika soko la Tanzania toka kuanzishwa kwake mwaka 1997, katika kipindi cha miaka 20, tumelihudumia soko la Tanzania Kwa kutoa burudani za kiwango cha juu na ambazo hazipatikani sehemu yeyote ile.

Katika kipindi cha miaka 20 tumewaletea watanzania michuano ya mpira (World Cup, Euro Champions League, Europa League, EPL, La Liga, AFCON na makombe mengine mengi), pia tumeweza kuwaletea maudhui mengi kupitia chaneli yetu ya MNET, Africa Magic na nyingine nyingi.

Multichoice tumekua mstari wa mbele katika kukuza tasnia ya Burudani nchini kwa kipindi chote cha miaka 20 wote mnakumbuka mchango wetu katika mziki kupitia chanel “O” Trace, MTV Base na sasa Trace Mziki. Tasnia ya Filamu tumechangia ukuaji wake kupitia Africa Magic na baadae Maisha Magic East na sasa Maisha Magic Bongo (MMB) ambayo ni maalum kwa kazi za Kitanzania. Tumekuza michezo kupitia uwekezaji wetu kwenye riadha na michezo mingineyo.

Katika Kusheherekea maadhimisho ya miaka 20, Multichoice imeandaa maonesho ya siku 2 yatakayofanyika katika ukumbi wa Mlimani City kuanzia leo Alhamis Oktoba 19 hadi kesho Ijumaa  kuanzia saa nne asubuhi hadi saa 11:00 jioni.

 Katika maonesho haya utapata kushuhudia maendeleo ya Teknolojia yetu ya tangu 1997 mpaka sasa na huduma mbali mbali  zitolewazo na Multichoice. Kutakuwa na mabanda kadhaa likiwemo la Supersport, MNET, Maisha Magic Bongo, Fashion, Banda la watoto na mengine mengi.

Kutakua na Ofa kabambe ndani ya siku 2 za Maonesho, ambapo Mteja atajipatia full set ya DStv kwa sh. 59,000 tu  hii ikijumlisha kifurushi cha mwezi mmoja BURE kwa king’amuzi cha HD cha Zappa.

Kwa King’amuzi cha Explora Mteja atapata Kwa sh. 240,000 pamoja na kifurushi cha Compact cha mwezi mmoja BURE…

Ofa hii ni kwa siku za maonesho tu, ambazo ni Alhamisi na Ijumaa hii tu, Hii si ya kukosa!!!


#20YearsOfAwesomeness!!!!!

Ukarabati KIA kukamilika Desemba 2017

Mafundi wakiendelea na ukarabati katika jengo la abiria la Kiwanja cha Ndege wa Kimataifa cha Kilimanjaro (KIA). Ukarabati huo unatarajiwa kukamilika Desemba 2017.

Na Mwandishi Wetu

KIWANJA cha ndege cha Kimataifa cha Kilimanjaro (KIA) kinafanyiwa ukarabati mkubwa unaohusisha miundombinu mbalimbali, ambapo unaotarajiwa kukamilika Desemba 2017.

Maeneo yanayofanyiwa ukarabati ni pamoja na jengo la kupumzikia abiria, upanuzi wa maegesho ya ndege  na mifumo ya maji  taka.

Akizungumza baada ya kukagua maendeleo ya ukarabati huo, Naibu Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, Mhe. Elius Kwandikwa amesema ameridhika na hatua iliyofikia, ikiwa ni zaidi ya asilimia 90.

"Nimeridhishwa na ukarabati unaoendelea katika kiwanja hiki na nafikiri mmejionea wenyewe kazi inaendelea vizuri, hivyo naamini kutokana na hali hii kazi itakamilika hivi karibuni, amesema Naibu Waziri Kwandikwa.

Naibu Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano (Sekta ya Ujenzi), Mhe. Elius Kwandikwa (wa tatu kulia), akitoa maelekezo kwa wasimamizi wa mradi wa ukarabati wa Kiwanja cha Ndege cha Kimataifa cha Kilimanjaro (KIA), wakati alipofanya ukaguzi wa ukarabati huo.

Aidha, Mhe Naibu Waziri amefafanua kuwa ukarabati huo ambao pia umehusisha maboresho ya mfumo wa maji taka unalenga kuleta tija kwa mkoa huo na Taifa kwa ujumla kutokana na kuwepo ongezeko la abiria, huduma za kijamii na kibiashara.

Amesisitiza kuwa Serikali itaendelea kukarabati na kujenga viwanja vya ndege nchini ili kurahisisha huduma za usafiri wa anga kwa wananchi wake lengo likiwa ni kuchochea fursa za kiuchumi ambazo zitasaidia kulipeleka Taifa katika uchumi wa kati.

Naye Meneja Miradi wa KIA, Mhandisi Mathew Ndossi,  amesema kuwa maegesho yatakapokamilika yatakuwa na uwezo wa kuegesha jumla ya ndege kubwa 11 kwa wakati mmoja badala ya 6 zinazoegeshwa sasa.

Ameongeza kuwa abiria wanatarajiwa kuongezeka kutoka 800,000 kwa mwaka hadi kufikia 1.2 milioni mara baada ya kukamilika kwa ukarabati huo.

Hivi karibuni KIA imeandaa mbio za marathoni zitakazofanyika Novemba 19 kwa kushirikisha raia mbalimbali wa nadani na nje ya nchi, ili kuvutia zaidi watalii na watumiaji wa usafiri wa anga kwa ujumla.

  1. Meneja mradi wa ukarabati Kiwanja cha Ndege cha Kimataifa cha Kilimanjaro (KIA), Mhandisi Mathew Ndossi, akimuonesha Naibu Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano (Sekta ya Ujenzi), Mhe. Elius Kwandikwa (Mb), (Kushoto), upanuzi wa maegesho ya ndege yanayofanyika kiwanjani hapo. 

Kia pamoja na Kiwanja cha ndege cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNIA) ni milango ya kuingia nchini kwa usafiri wa anga kwa watalii wanaotoka nchi mbalimbali duniani, kuja kutembelea mbuga za wanyama na  vivutio vinavyopatikana kwenye mikoa mbalimbali ya Tanzania Bara na Zanzibar.

Wakati huo huo, Naibu Waziri Kwandikwa amekagua barabara ya Sakina - Tengeru (km 14.1) na barabara ya mchepuko ya Arusha (Arusha Bypass km 42.4) ambapo amesema kuwa kukamilika kwa barabara ya Sakina - Tengeru  ni mkombozi mkubwa kwa wananchi wa mkoa wa Arusha na wageni wanaoingia katika mkoa huo kwani kumepelekea  kupungua kwa  ajali na msongamano wa magari  katika eneo hilo.

Ametoa wito kwa wananchi kuzitunza barabara  na kutunza mazingira yanayozunguka barabara hizo ili ziweze kudumu kwa muda mrefu kwa vizazi vya sasa na vijavyo.

Naye, Meneja wa Wakala wa Barabara (TANROADS), mkoa wa Arusha Mhandisi, Johny Kalupale,  amemhakikishia Naibu Waziri huyo kufanya kazi kwa ubora na kwa weledi ili kutimiza malengo ya Serikali ya kuwajengea wananchi miundombinu bora na ya kisasa.

Awamu ya pili ya mradi huo sehemu ya barabara ya mchepuo ya Arusha (Arusha Bypass), inayofadhiliwa na Benki ya Maendeleo ya Afrika (AfDB), inatarajiwa kukamilika mwakani na kugharimu kiasi cha shilingi bilioni 67.

Naibu Waziri Kwandikwa amemaliza ziara ya kikazi katika mkoa wa Kilimanjaro na Arusha ambapo amekagua miradi mbalimbali inayotekelezwa na Wizara yake.

Tuesday, 17 October 2017

Kocha Napoli aipa City ubingwa wa Ulaya

MANCHESTER, England

KOCHA wa timu ya Napoli Maurizio Sarri anasema kuwa Manchester City sasa iko viwango sawa kama Barcelona na Real Madrid na inaweza kuendelea kufanya vizuri hadikutwaa ubingwa wa Ligi ya Mabingwa wa Ulaya.

Man City iliyocheza kandanda safi na kushambulia kwa dakika 20 na kufanikiwa jkupata mabao mawili ya kuongoza dhidi ya Napoli katika mchezo uliopigwa kwenye Uwanja wa Etihad juzi lakini Waitalia hao ambao bado hawajapoteza pointi katika Ligi Kuu ya Italia ya Serie A, iling’ang’ania na kuibuka na ushindi wa mabao 2-1.

Alipoulizwa baada ya mchezo huo kama Man City sasa iko katika kiwango sawa na vigogo vya Hispania na kama inaweza kutwaa taji hilo la Ligi ya Mabingwa wa Ulaya, Sarri alisema: "Ndio, Nafikiri hivyo.

 

"Mana City wana kikosi kisicho cha kawaida. Wako vizuri katika kila idara na wanaweza kufanya vizuri kutokana na ubora wao, “aliongeza kocha huyo.

Kwa ushindi huo Man City inaoongoza katika Kundi F ikiwa na pointi tisa baada ya kucheza mechi tatu na pia inaongoza katika Ligi Kuu ya England baada ya kushinda mara saba kutoka katika mechi nane.

Kikosi cha Guardiola sasa hakijafungwa katika mechi 18 katika mashindano yote, ambapo imeshinda mechi 14 kati ya hizo, tangu walipofungwa 2-1 na Arsenal katika nusu fainali ya Kombe la FA.

Mabao kutoka kwa Raheem Sterling na Gabriel Jesus katika dakika 13 za kwanza yalionekana kufungua mlango kwa Man City kuibuka na ushindi lakini Napoli walijipanga upya na Sarri alisema kuwa amefurahishwa na jinsi walivyojibu.


"Unatakiwa kuugawa mchezo katika dakika 25 za kwanza na baadae zilizobaki. Wanastahili sifa kubwa kwa jinsi walivyoanza mchezo, mbinu za kiufundi, kasi na jinsi movement yao, lakini na sisi hatukuwapa shinikizo kubwa, “alisema.

Wachezaji Munich wakabidhia magari ya anasa

Gari aina ya Uudi, ambayo wachezaji wa Bayern Munich wamekabidhiwa.

MUNICH, Ujerumani

NYOTA wa timu ya soka ya Bayern Munich wamekabidhiwa magari yao mapya ya anasa aina ya Audi AB.

Wachezaji hao kama akina Robert Lewandowksi, Mats Hummels na Javi Martinez wote walipokea `michuma’ yao mipya wakati wacheaji wa kikosi hicho wakisaini autographs wakati wa hafla ya kila mwaka ya kuabidhi magari huko Ingolstadt.

Hatahivyo, wachezaji wengi wa timu hiyo hawakuwepo kwani walikuwa na timu zao za taifa katika mechi mbalimbali za kimataifa.

Audi ni wadhamini wa kuu wa klabu ya Bayern Munich, ambapo imekuwa ikitoa gari kwa kila mchezaji wa timu hiyo tangu mwaka 2002, mwaka ambao walianza kuwa mhisa na vigogo hao wa soka wa Ujerumani.

Sehemu ya mkataba wao ni kuwa kampuni hiyo ya magari kila mwaka itakuwa ikitoa gari kwa kila mchezaji, ambapo wachezaji hao Jumatatu ya wiki iliyopita walikabidhiwa `michuma’ yao.

Karibu wachezaji wa kikosi hicho kila mwaka wamekuwa wakipata mamilioni, walikabidhiwa seti mpya ya matairi, ambapo sio kitu kigeni kwa wachezaji wa mabingwa hao wa Ujerumani.

Lakini gari hizo aina ya Audi zililetwa zikiwa tayari zina majina ya wachezaji hao katika vibao vya namba zikijulikana kama gari rasmi za Bayern.  Polisi wa Kikosi cha Usalama Barabarani wanajua kuwa gari hizo zenye namba zinaoanzia na M-DM zitakuwa zikiendeshwa na wachezaji au viongozi wa kikosi hicho chenye maskani yake Allianz Arena.

Herufi  'M' inasimama badala ya 'Munich', wakati ‘'DM' inasimama badala ya 'Deutscher Meister', au Mabingwa wa Ujerumani, kufuatia ubingwa wa Bayern Munich walioupata msimu uliopita.

Wakati Bayern sio mabingwa wa Ujerumani, kitu ambacho hakijatokea kwa miaka ya hivi karibuni- 'DM' inakuwa 'RM', ambayo inasimama kama 'Rekordmeister', au  mabingwa wa kihistoria.

Wachezaji wa Bayern walichukua magari yao huku wakiwa na mashabiki kibao wa timu hiyo waliohudhuria hafla hiyo, ambapo iliwachukua muda kupiga picha na mashabiki hao.

Kikosi hicho kiliungana na kocha mpya Jupp Heynckes, ambaye wiki iliyopita alitangazwa kama mbadala wa Carlo Ancelott.


Kocha huyo atatimiza miaka 72 wakati akiifundisha klabu hiyo kwa mara ya nne, ambapo walishinda taji la Bundesliga mwaka 1989, 1990 na 2013 na lile la Ligi ya Mabingwa mwaka 2013. 

Monday, 16 October 2017

Waegesha ndege 10 wa JNIA wapigwa msasa


Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Tanzania (TAA), Bw. Richard Mayongela (wa tatu kulia) akiwa kwenye picha ya pamoja na washiriki, wakufunzi na waandaaji wa mafunzo ya waegesha ndege yaliyoanza leo kwenye Chuo cha Usafiri wa Anga jijini Dar es Salaam. Wapili kushoto ni Kaimu Mkurugenzi wa Kiwanja cha Ndege cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNIA), Bw. Johannes Munanka na wa pili kulia ni Mkurugenzi wa Mfuko wa Avi Assist wa Uholanzi Bw. Tom Kok.

Na Mwandishi Wetu

WAEGESHA ndege 10 wa Kiwanja cha Ndege cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNIA), leo walianza mafunzo ya siku saba ya uegeshaji ndege kutoka kwa wakufunzi wa Kiwanja cha Ndege cha Hague cha Uholanzi yanayofanyika katika Chuo cha Usafiri wa Anga (CATS) jijini Dar es Salaam.

Akifungua mafunzo hayo Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa TAA, Bw. Richard Mayongela amesema kuwa mafunzo hayo ni muhimu kwani yatazidi kuwajengea uwezo na uzoefu washiriki hao.

Bw. Mayongela amewasisitiza washiriki hao kuzingatia kila wanachofundishwa ili waweze kuwa mahiri na weledi katika uongozaji wa ndege za ndani na nje ya nchi zinazotumia kiwanja cha ndege cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNIA).

“Waongoza ndege ni moja ya kazi inayohusisha mawasiliano ya moja kwa moja kati ya watoa huduma ndani ya kiwanja cha ndege, hivyo ni lazima tufikie viwango vinavyotakiwa kwa mujibu wa sheria kimataifa,” amesema Bw. Mayongela.

Wakufunzi Ralf Overduya (kushoto) na Martiyn Ouwendyki kutoka Kiwanja cha Ndege cha Hague cha Uholanzi leo wakianza kufundisha baadhi ya waegesha ndege wa Kiwanja cha ndege cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNIA) katika mafunzo yanayofanyika kwenye Chuo cha Usafiri wa Anga kinachomilikiwa na Mamlaka ya Usafiri wa Anga Tanzania.

Hata hivyo, amesema TAA inajukumu kubwa la kuwaongezea uwezo watumishi wake kwa kuwapeleka kwenye mafunzo mbalimbali ili kujijengea uwezo na maarifa.

Bw. Mayongela amewashukuru waendeshaji wa mafunzo hayo yanayotolewa na mfuko wa Avi Assist wa Uholanzi, ambapo amewahahakikishia kuendeleza ushirikiano waliouanzisha kwa kushirikiana katika utoaji wa mafunzo ya kada mbalimbali.

Naye Mkuu wa Kitengo cha Waongoza ndege cha JNIA, Bw. Lugano Mwinuka amesema mafunzo haya yamekuja wakati muafaka, kwa kuwa walikuwa yakiyahitaji kwa muda mrefu, na sasa anauhakika wa washiriki wataongeza ujuzi katika utendaji wao wa kazi.

Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Tanzania (TAA), Bw. Richard Mayongela (wa tatu kulia) akiwa kwenye picha ya pamoja na washiriki, wakufunzi na waandaaji wa mafunzo ya waegesha ndege yaliyoanza leo kwenye Chuo cha Usafiri wa Anga jijini Dar es Salaam. Wapili kushoto ni Kaimu Mkurugenzi wa Kiwanja cha Ndege cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNIA), Bw. Johannes Munanka na wa pili kulia ni Mkurugenzi wa Mfuko wa Avi Assist wa Uholanzi Bw. Tom Kok.

Bw. Mwinuka amesema mafunzo hayo yanatolewa kwa nadharia na vitendo, ambapo washiriki hao wamegawanywa katika makundi mawili ya watu watano, ambao ni Earisner Waihula, Emmanuel Nyaulingo, Anunciatus Alex, Fadhili Meena na Oscar Kibiki.


Watakaoingia kundi la pili ni pamoja na Denis Kinyaga, Zennobius Mwimba, Raynard Komba, Said Mussa na Meshack Elisante.

Tuesday, 10 October 2017

Messi apiga hat-tric Argentina ikifuzu Kombe la Dunia

QUITO, Ecuador

QUITO, Ecuador

LIONEL Messi amefunga hat-trick wakati Argentina ikitoka nyuma na kushinda ugenini 3-1 dhidi ya Ecuador na kufuzu kucheza fainali za Kombe la Dunia zitakazofanyika Russia mwakani.

Brazil wenyewe tayari walishafuzu huku Luis Suarez akizifumania nyavu mara mbili wakati Uruguay ikiichapa Bolivia 4-2 na kufuzu, pamoja na Colombia nayo pia ikifuzu licha ya kutoka sare ya kufungana bao 1-1 na Peru.

Peru ilimaliza mchakato huo ikiwa katika nafasi ya tano ya Kanda ya Amerika Kusini ya kufuzu kwa Kombe la Dunia na sasa itakutana na New Zealand katika mechi mbili za mchujo zitakazochzwa nyumbani na ugenini.

Lakini Alexis Sanchez na Chile wametupwa nje baad aya kupokea kichapo cha mabao 3-0 ugenini dhidi ya Brazil.

Argentina ilianza siku ikiwa katika nafasi ya sita na kuwa katika hatari ya kuweza kushindwa kufuzu kwa Kombela Dunia kwa mara ya kwanza tangu mwaka 1970.

 

Timu hiyo ilianza vibaya katika mchezo huo uliofanyika katika ukanda wa juu uliopo hapa na wenyeji walikuwa mbele katika sekunde ya 38 kupitia kwa Romario Ibarra likiwa n bao la mapema zaidi kufungwa Argentina katika Kombe la Dunia.

Hatahivyo, Argentina, ambao ni washindi wa pili wa Kombe la Dunia mashindano yalipofanyikia nchini Brazil 2014, walipambana huku Messi akiwa katika kiwango cha hali ya juu.

Messi, ambaye ni bingwa mara tano wa tuzo ya mchezaji bora wa mwaka wa dunia, alisawazisha baada ya dakika 12 baada ya kushirikiana vizuri na kiungo wazamani wa Manchester United Angel di Maria.

Bao lake la pili lilikuja dakika nane baadae kwa shuti kali ndani ya eneo la hatari kabla hajafunga la tatu na kuiwezesha timu yake kufuzu kwa fainali za mwakani za Kombe la Dunia.

MAJAGA KWA CHILE

Chile,ambayo ilitwaa taji la Copa America katika mashindano mawili yaliyopita, ilikuwa nalengo la kufuzu kwa mara ya tatu mfululizo katika Kombe la Dunia baada ya mara ya mwisho kucheza hatua ya 16 bora mwaka 2010 na 2014.

Walianza raundi hiyo ya mwishi wakiwa katika nafasi ya tatu, lakini walishindwa baada yakufungwa mabao mawili na Brazil ndani ya sekunde tatu yaliyofungwa na Paulinho na Gabriel Jesus.

Wakati Peru ikifunga bao la kusawazisha katika dakika za mwisho za mchezo huo dhidi ya Colombia, Chili ilikuwa ikihitaji kufunga tu ili kucheza hatua ya mtoano.

Sunday, 1 October 2017

Chaneta waibuka na mikakati ya kuinua netiboli

Na Mwandishi Wetu

UONGOZI mpya wa Chama cha Netiboli Tanzania (Chaneta) umesema kuwa umejipanga kuhakikisha unaleta maendeleo ya mchezo huo hapa nchini.

Akizungumza jana Katibu Mkuu mpya wa Chaneta, Judith Ilunda (pichani) alisema kuwa, wanajua changamoto zilizopo katika chama hicho, lakini wamejipanga kukabiliana nazo ili kuleta maendeleo katika mchezo huo.

Ilunda ambaye ni mchezaji wazamani wa timu ya Bandari Dar na timu ya taifa ya netiboli kwa muda mrefu, alisema kuwa watahakikisha mchezo huo unachezwa katika shule za msingi, sekondari na mitaani.

Alisema pia watahakikisha wanaendesha mashindano ya mara kwa mara na timu zenye ubora zinashiriki, ili kuhakikisha mchezo huo unarudi katika chati kama zamani kitaifa na kimataifa.

Alisema kamati yao mpya itakutana hivi karibuni mara baada ya kukabidhiwa ofisi na uongozi uliopita na kutangaza zaidi mipango yao ya muda mrefu na mfupi.

Uchaguzi Mkuu wa Chaneta ulifanyika mjini Dodoma juzi, ambapo Dk Devetha Marwa  aliutwaa uenyekiti baada ya kupata kura 53 dhidi ya Damian Chonya aliyepata kura nne.

Makamu ni Anna Gidaria aliyepata kuta 44 dhidi ya Winfrida Emmanue kura 10 na Pili Mogella alipata kura tatu.

Nafasi ya Katibu Mkuu ilikwenda kwa Ilunda aliyepata kura 50 dhidi ya makamu mwenyekiti aliyepita Zainabu Mbiri aliyeambulia kura sita, huku katibu msaidizi ni Hilda Mwakatobe aliyepata kura 30 dhidi ya 26 za Mwajuma Kisengo.

Nafasi ya mhazini haijajazwa baada ya mgombea pekee, Grace Khatibu kupata kura nne za ndio na hapana 49 na hivyo kutoweza kuchaguliwa kwa kuwa alikuwana kura nyingi za hapana.


Wapiga kura walikuwa 57 kutoka mikoa 21 ya Tanzania Bara.

Pakacha Group laendesha kongamano la kujadili utatuzi wa changamoto za maji Kwembe, Kibamba, Msigani

Viongozi wa asasi ya Pakacha Group wakiwa na viongozi wa Kata ya Kwembe wilaya ya Ubungo mkoani Dar es Salaam kabla ya kongamano la kujadili changamoto zinazokabili maji katika kata hiyo jana.

Na Mwandishi Wetu

DIWANI wa Kata ya Kwembe wilayani Ubungo, Dweza Kolimba amesema asasi za kiraia zina nafasi kubwa ya kuleta maendeleo katika jamii kwa kushirikiana na wananchi na watendaji wa serikali.

Akizungumza katika kongamano lililoandaliwa na asasi ya Pakacha Group kwa wananchi wa kata hiyo kwa ajili ya kujadili utatuzi wa changamoto ya maji, kuanzia ufuatiliaji wa rasilimali fedha na utekelezaji wake, Kolimba alisema asasi hiyo itasaidia kufanya watendaji na wananchi kufanya kazi kwa pamoja.

Alisema ushirikiano huo utasaidia kuibua changamoto zinazokwamishwa na rasilimali fedha au kutowajibika kwa baadhi ya watendaji.

Alisema asasi zinaweza kuleta mabadiliko kwa kufuatilia miradi ya maji, ambayo inakwamishwa kwa sababu mbalimbali na kuwaelimisha wananchi jinsi ya kulinda miundo mbinu ya maji na ufuatiliaji wake.

"Pia zinasaidia kutoa msukumo kwa utelekezaji wa miradi kwa kuibua hoja kwa wananchi, kwa lengo moja tu, kuleta maendeleo na sio malumbano yasiyo na msingi”, alisema mheshimiwa Kolimba.

Ofisa Mtendaji wa Kata ya Kwembe, Hamisi Moto alisema kuwa jitihada zinafanyika ile kuondoa adha ya upatikanaji wa maji kwa wananchi.

Kongamano hilo limefanyika kwa ufadhili wa The Foundation For Civil Society kwa ajili ya kutoa elimu kwa wananchi kufuatilia fedha zinazotengwa kwa ajili ya utoaji wa huduma ya Maji katika kata tatu za Kwembe, Kibamba na Msigani.

Diwani huyo alisema wananchi wanaweza kufanya ufuatiliaji kupitia mfumo wa Pets ukiwa na malengo ya kuboresha huduma za kijamii, kuhakiki utendaji wa serikali za mitaa na kuwezesha uandaaji wa mipango shirikishi.

Pets ni mfumo unaowezesha ufuatiliaji matumizi ya rasilimali za umma zinazotoka Serikali Kuu au halmashauri kwa maendeleo ya wananchi kuanzia ngazi za mitaa hadi kata na kuendelea.

Verisiyus Magoti, mwakilishi wa mhandisi wa maji kutoka Manispaa ya Ubungo alisema wananchi washirikiane na watendaji ili kutatua kero za maji na jitihada zinaendelea kuhakikisha huduma hiyo muhimu inapatikana wakati wote.

Haroun Jongo, katibu wa Pakacha Group alisema kongamano hilo ni moja kati ya matatu yatakayofanyika katika Kata za Kibamba, Kwembe na Msigano kwa siku tofauti tofauti.


Alisema makongamano hayo hayana lengo la kuwagombanisha wananchi na viongozi, bali yanaweka msukumo katika kuhakikisha miradi inasimamiwa vizuri na inatekelezwa.








Tigo Fiesta yatikisa Ali Hassan Mwinyi Tabora

Mkuu wa Mkoa wa Tabora, Aggrey Mwanri akifungua Tamasha la Tigo Fiesta kwenye Uwanja wa Ali Hassan Mwinyi mjini Tabora juzi.

Tamasha la Tigo fiesta limeendelea tena usiku wa kuamkia jumamosi mkoani Tabora.

Akifungua tamasha hilo mkoani humo, mkuu wa mkoa Aggrey Mwanri alisema hii nafasi nyingine kwa mkoa wetu kuletewa fursa kwa wakazi wetu, nawapongeza sana Tigo na Clouds Media. Pia nawasihi vijana kuondokana na mimba za utotoni na utumiaji wa madawa ya kulevya.

 Nandy

Naye meneja wa Tigo Kanda ya Ziwa, Gwamaka Mwakilembe amesema, mwaka huu tumeamua kudhamini tamasha hili kubwa kwa lengo la kuwapa burudani wateja wetu na kuendeleza muziki wetu wa ndani, hii itasaidia kuwapatia kipato wasanii wetu na kuendeleza vipaji vyao. Kwa wateja wetu ndani ya msimu huu wataweza kujipatia ofa mbalimbali wanunuapo tiketi kwa tigopesa.


Kwa upande wa burudani yenyewe, jumla ya wasanii 13 walipanda jukwaani kwa nyakati tofauti lakini msanii Ben pol aliingia kivingine alipowashilikisha kikundi cha ngoma za utamaduni wa kinyamwezi cha mapambano na kuimba nao nyimbo tofauti tofauti za kinyamwezi na za Ben ikiwemo wimbo 'Tatu'na kutengeneza 'remix' ya aina yake

Nao kundi la Rostam kama ilivyoada walifunga tamasha kwa kuamsha mashabiki kwa shangwe walipoimba wimbo wao wa 'huku ama kule'.



Wasanii waliopanda jukwaani ni

1.Rostam

2.Ney wa Mitego

3.Darassa

4.Chege

5.Mr Blue

6.Nandy

7.Maua

8.Young Dee

9.Aslay

10.Jux

11.Msami

12.Ben Pol

13.Ommy Dimpoz

Tamasha hilo linaendelea jumapili hii mkoani Kigoma kwenye uwanja wa Tanganyika.