Sunday, 16 February 2020

TAKUKURU Kubaini Mamluki Michezo Mei Mosi 2020


Wajumbe wa Kamati ya Michezo ya mashindano ya Mei Mosi wakiwa kwenye kikao cha Kwanza cha maandalizi ya michezo hiyo kilichofanyika mwishoni mwa wiki kwenye ukumbi wa mikutano wa Chuo cha Kikuu cha Sokoine cha Kilimo (SUA) mkoani Morogoro

 Na Bahati Mollel, Morogoro
TAASISI ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa Tanzania (Takukuru) mkoa wa Mwanza itashirikishwa kwenye Michezo ya Mei Mosi inayotarajiwa kuanza Aprili 16-29, 2020 kwenye Uwanja wa CCM Kirumba jijini humo, endapo kutakuwa na timu za Wizara, Taasisi za Umma  na Binafsi zitawatumia wachezaji wasiokuwa watumishi wao halali.

Katibu wa Kamati ya michezo hiyo, Moshi Makuka, alisema hayo mwishoni mwa wiki kwenye kikao cha kwanza cha maandalizi ya michezo hiyo kilichofanyika katika ukumbi wa mikutano wa Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo (SUA) Morogoro, ambapo suala hilo limewekwa kwenye kanuni namba 13 kati ya 15 zilizopitishwa na wajumbe wote walioshiriki kwenye kikao hicho.

Makuka alisema mbali na Takukuru kushirikishwa kubaini uhalali wa mchezaji aliyesajiliwa na timu iliyomchezesha, pia viongozi wote walioshiriki kumsajili mchezaji huyo wataripotiwa kwenye taasisi hiyo, ili sheria za nchi zichukue mkondo wake.

       Katibu Mkuu wa Kamati ya Michezo ya mashindano ya Mei Mosi, Moshi Makuka  (aliyenyoosha mikono) akisisitiza jambo kwenye kikao cha Kwanza cha maandalizi ya michezo hiyo kilichofanyika mwishoni mwa wiki kwenye ukumbi wa mikutano wa Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo (SUA) Mkoani Morogoro


“Haya mashindano yanajumuisha watumishi halali wa taasisi na wizara hivyo hairuhusiwi kuwachezesha wachezaji ambao sio watumishi halali, kwa lengo la kujipatia ushindi, hili ni katazo na kanuni yetu ipo wazi kabisa, hivyo timu zisithubutu kuja na wachezaji hao kabisa,” alisisitiza Makuka.

Alizitaja adhabu ambazo timu itakayobainika kumtumia mamluki ni pamoja na viongozi wake watafungiwa kushiriki michezo hiyo kwa muda wa miaka miwili na nakala ya barua itawasilishwa kwa Mwajiri wake; timu itatozwa faini  ya Tshs. 500,000; timu husika itapokonywa ushindi endapo itakuwa imeshinda; timu itaondolewa kwenye mashindano.

Kamati imesema mamluki wanadhibitiwa kwa wanamichezo kuwa na vitambulisho halisi vya kazi, Kadi ya Bima ya Afya, Kadi ya Mfuko wa Jamii na hati ya Malipo ya mshahara za miezi miwili ‘salary slip’.

Hatahivyo, Makuka alisema timu zote shiriki zinatakiwa kuwahi mkoani Mwanza tarehe 14 Aprili, 2020 ambapo ndipo sherehe za Sikukuu za wafanyakazi zitafanyika Kitaifa kama ilivyotangazwa awali, ambapo timu itakayochelewa hadi tarehe 20 Aprili, 2020 itakuwa imejiondoa kwenye michezo hiyo.

“Timu ikichelewa inawapa shida na kuwaumiza wachezaji kwa kuwa watacheza mfululizo ili kwenda na ratiba, hadi kufikia michezo yao iliyosalia, hivyo hii hatutaki kwani michezo itakuwa haina ushindani kwa kuwa wachezaji wa timu moja watakuwa wamechoka kwa kucheza mfululizo wa mechi mbili au tatu kwa siku, hivi huu ni mwezi wa pili muanze kufuatilia ruhusa za wachezaji wenu,” alisema Makuka.

Kamati inategemea ushiriki wa timu zaidi ya 25, kwa kuwa zinaongezeka kila mwaka ambapo mwaka jana zilishiriki timu 23. Michezo itakayoshindaniwa ni pamoja na soka, netiboli, kuvuta kamba, baiskeli, riadha, karata, bao na draft.

Pia Makuka amesisitiza timu shiriki kulipa ada ya ushiriki kwa wakati, ili fedha hizo zitumike katika ulipaji wa gharama mbalimbali za uendeshaji wa mashindano hayo.

Ada ya ushiriki ni Tshs. 1,000,000 ambapo kila timu inatakiwa kulipa mapema kabla ya tarehe 6 Aprili, 2020, ili timu ziweze kupewa kadi za ushiriki zitakazofanikisha usajili wao.

Halikadhalika Makuka amesema timu zote zilizotwaa vikombe kwa kuwa washindi wa Kwanza hadi wa tatu wanatakiwa kurejesha vikombe walivyoshinda kabla yatarehe 29 Machi, 2020 na timu itakayochelewa utatozwa faini ya Tshs. 200,000.

Wakati huo huo, Makuka amesema timu zinaruhusiwa kushiriki kwenye michezo ya mashirikisho mbalimbali yakiwemo ya Shimiwi, Shimmuta na Mei Mosi, na sio kusubiri michezo ya shirikisho moja, ambayo kwa wakati huo inakuwa haijafanyika kwa sababu mbalimbali.

TAA WATAKIWA KUTUMIA VIZURI MFUMO WA TANEPs


Kaimu Mkurugenzi wa Utawala na Rasilimali Watu wa Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Tanzania (TAA), akimkabidhi cheti cha kufuzu mafunzo ya mfumo wa Manunuzi kwa njia ya Mtandao (TANEPs),  Mkuu wa Kitengo cha Ukaguzi wa Ndani wa Bi. Irene Sikumbili (wa pili kushoto). Mafunzo hayo yaliendeshwa na Mwezeshaji Kenneth Nnembuka kutoka Mamlaka ya Udhibiti wa Manunuzi ya Umma (PPRA) (kulia)

Na Bahati Mollel
KAIMU Mkurugenzi wa Utawala na Rasilimali Watu wa Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Tanzania (TAA), Bw. Abdi Mkwizu amewataka wahitimu wa mafunzo ya mfumo wa Manunuzi kwa njia ya mtandao (TANEPs), kuutumia vyema mfumo huo ili kuongeza ufanisi katika taratibu za ununuzi wa Umma kwa maslahi ya taasisi na Taifa kwa ujumla.

Akifunga mafunzo hayo ya siku tano jana yaliyokuwa yakifanyika kwenye ukumbi wa mikutano wa Watu Mashuhuri wa Kiwanja cha Ndege cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNIA), Bw. Mkwizu alisema tayari Mamlaka imeanza kutumia mfumo huo ulioagizwa na serikali kupitia Mamlaka ya udhibiti wa Ununuzi wa Umma (PPRA).

Ofisa Manunuzi na Ugavi wa Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Tanzania (TAA), Bw. Honest Mushi (mwenye fulana) akipokea cheti cha kufuzu mafunzo ya mfumo wa Manunuzi kwa njia ya Mtandao (TANEPs), kutoka kwa Kaimu Mkurugenzi wa Utawala na Rasilimali Watu, Bw. Abdul Mkwizu. Kulia ni Mwezeshaji wa Mafunzo hayo Bw. Kenneth Nnembuka kutoka Mamlaka ya Udhibiti wa Manunuzi ya Umma (PPRA)

Mkufunzi wa mafunzo hayo Bw. Kenneth Nnembuka kutoka PPRA, aliwataka wahitimu kuanza haraka kutumia maarifa waliyoyapata ili wasije wakasahau. Pia aliwasihi kutosita kuomba msaada mara wapatapo mkwamo kuhusu mfumo huo mpya.

Naye Kaimu Mkuu wa Kitengo cha Manunuzi na Ugavi cha TAA, Bw. Josephat Msafiri alishukuru uongozi wa juu wa TAA kukubali kufanyika kwa mafunzo hayo muhimu yenye lengo la kuongeza ufanisi wa utendaji wa ndani wa taasisi.

Aliahidi kuendelea kutumika bila kuharibu kada hiyo.


Kaimu Mkuu wa Kitengo cha Manunuzi cha Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Tanzania (TAA), Josephat Msafiri (wa pili kulia) akiandika mambo mbalimbali yanayofundishwa na Mwezeshaji Kenneth Nnembuka kutoka Mamlaka ya Udhibiti wa Manunuzi ya Umma (PPRA), katika mafunzo ya mfumo wa manunuzi kwa njia ya mtandao (TANePs), yanayoendelea kwenye ukumbi wa Mikutano wa Watu Mashuhuri wa Kiwanja cha Ndege cha Kimataifa cha Julius Nyerere (VIP -JNIA-TB2).
Kwa upande wake Mkuu wa Kitengo cha Ukaguzi wa ndani ya Taasisi, Bi Irene Sikumbili aliweka msisitizo kwenye matumizi sahihi ya mfumo kwa mujibu wa miongozo, taratibu, kanuni na sheria za serikali.

Mkurugenzi wa JNIA, Bw. Paul Rwegasha, alisisitiza mapendekezo ya TAA na wadau mbalimbali kuhusu changamoto za kimfumo yafanyiwe kazi ili kuepusha uwezekano wa ukwamishaji wa huduma viwanjani.
Naye mratibu wa mafunzo hayo, Bw. Soud Saad amesema mafunzo hayo yalishirikisha watendaji wakuu wa TAA; Wakaguzi wa ndani; wataalam wa TEHAMA na Wataalam wa Ununuzi na Ugavi kutoka Makao Makuu na JNIA.

Wednesday, 5 February 2020

Kamwelwe Ataka MAB Kuweka Uzalendo Mbele

Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Tanzania (TAA), Mhandisi Mshauri, Julius Ndyamukama (aliyesimama kulia) akitoa taarifa fupi kwa Waziri wa Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, Mhandisi Isaack Kamwelwe (mbele), wakati wa uzinduzi wa Bodi ya Ushauri ya TAA, (MAB) uliofanyika mwishoni mwa wiki kwenye Jengo la TPA (One Stop Centre) jijini Dar es Salaam. 

Na Bahati Mollel,TAA
WAZIRI wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, Mhandisi Isaack Kamwelwe ameiasa Bodi ya Ushauri ya Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Tanzania (MAB), kutanguliza Utaifa na Uzalendo mbele katika majukumu yao.

Kauli hiyo ameitoa mwishoni mwa wiki katika halfa ya uzinduzi wa Bodi hiyo, ambao umefanyika kwenye Jengo la Bandari nchini (TPA One Stop Centre) lililopo jijini Dar es Salaam.

“Napenda kutumia nafasi hii kuwaasa kwamba, nafasi hizi mlizopewa ni kwa ajili ya kulitumikia Taifa letu kwa weledi, uaminifu na uadilifu mkubwa huku mkitanguliza maslahi mapana ya taifa na uzalendo mbele”. Amesema Waziri Kamwelwe
Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, Mhandisi Isaack Kamwelwe (mbele) mwishoni mwa wiki akiongea na Walioteuliwa kuunda Bodi ya Ushauri ya Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Tanzania (MAB), pamoja na Menejimenti ya TAA wakati wa uzinduzi wa bodi hiyo katika Jengo la TPA (One Stop Centre) jijini Dar es Salaam.
Pia Waziri Kamwelwe ameitaka Bodi hiyo kuhakikisha inashirikiana bega kwa bega na menejimenti ya Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Tanzania (TAA), na taasisi za serikali hususan Wakala wa Barabara nchini (TANROADS) katika ujenzi wa viwanja vingi zaidi ya wanavyovisimamia 58 kwa lengo ya kuviongeza, ili ndege za Shirika la ndege Tanzania (ATCL) na mashirika mengine yaweze kupanua wigo wa safari.

Halikadhalika amesema ulinzi na usalama katika viwanja vya ndege ukaimarishwe, ingawa bado kunachangamoto ya kukosekana kwa uzio wa ndani na nje ya viwanja vya ndege, ambapo pia suala la ugonjwa wa homa ya virusi vya Corona ulioanzia nchini China lipewe kipaumbele kwa kuzingatiwa maslahi mapana ya Taifa yazingatiwe.

“Hili la ugonjwa wa Corona liangaliwe kwa ukaribu zaidi ili viwanja vya ndege visiwe ndio njia ya kuingiza ugonjwa huu, pia usalama wa watendajikazi uangaliwe pia,” amesema na kuongeza.
Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, Mhandisi Isaack Kamwelwe (wa nne kulia), akiwa katika picha ya pamoja na Mwenyekiti Dkt Masatu Chiguma (wa nne kushoto) na Wajumbe ya Bodi ya Ushauri ya Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Tanzania (MAB), baada ya kuizindua Bodi hiyo mwishoni mwa wiki kwenye Jengo la TPA.
“... Vilevile mkahakikishe kuwepo na usimamizi mzuri wa wa ardhi na miundombinu ya viwanja vyetu ikiwemo Jengo la Tatu la abiria –JNIA na utoaji wa huduma bora zaidi kwa wateja, ukiangalia kwa sasa ni viwanja vichache tu ndio vina hati na hili sio jambo jema, hakikisheni viwanja vyote vinapimwa na hati kupatikana, kwani itasaidia kuongeza uhalali na kuongeza mapato ya TAA kwa kutumia ardhi hiyo,” amesema Waziri Kamwelwe.

Pia ameitaka Bodi hiyo kuhakikisha TAA inapata “control number” ili malipo mbalimbali yatafanyika kupitia huko, ambapo pia ameitaka kubuni njia mbalimbali za kuendesha viwanja vya ndege kibiashara, wakati sasa suala la TAA kuwa Mamlaka zaidi badala ya sasa kuwa Wakala pamoja na kwamba lipo chini ya Wizara linahitaji msukumo wa Bodi hiyo.
   Menejimenti ya Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Tanzania (TAA), leo wakiwa kwenye picha ya pamoja na Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, Mhandisi Isaack Kamwelwe (wanne kutoka kushoto), na Mwenyekiti, Dkt Masatu Chiguma na Wajumbe wa Bodi ya Ushauri ya Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Tanzania (MAB), iliyozinduliwa mwishoni mwa wiki kwenye Jengo la TPA.
Hatahivyo, Waziri Kamwelwe amesema pamoja na TAA kuwa na mafanikio bado inakabiliwa na changamoto za kushindwa kuboresha miundombinu mbalimbali iliyopo viwanjani.

Bodi hiyo inaundwa na Mwenyekiti Dkt. Masatu Chiguma na wajumbe ni Mhandisi Ven Kayamba, Dkt. Paschal Mugabe, Mhandisi Daniel Kiunsi, Mhandisi Christopher Mukoma na Alex Haraba.

Awali Mkurugenzi Mkuu wa TAA,  Mhandisi Mshauri, Julius Ndyamukama amesema Mamlaka hiyo imekuwa ikikua tangu kuanzishwa kwake hadi sasa, na kutolea mfano wa mapato kuongezeka kutoka Shilingi Bilioni 6.3 hadi kufikia Bilioni 105.2 kwa mwaka, ambalo ni sawa na ongezeko la asilimia 1,570.

Pia amesema Mamlaka ilianza na ikiwa na miruko na mituo ya ndege 62,221 kwa mwaka na sasa imefikia 146,593 kwa mwaka ni sawa na ongezeko la asilimia 135.6.

Kwa upande wa abiria, amesema ilianza ikiwa na idadi ya abiria 846,906 kwa mwaka na sasa imefikia 3,473,658 kwa mwaka ikiwa ni sawa na ongezeko la asilimia 310.

Naye Mwenyekiti wa MAB, Dkt. Masatu Chiguma, alimuahidi Waziri kuwa atafanya kazi bega kwa bega na TAA, ili kufanikisha malengo yalilowekwa.

Wednesday, 11 December 2019

TAA Yasaidia Kutokomeza Mimba za Utotoni Tabora


Mbunge wa Viti Maalum wa Jimbo la Tabora, Mhe. Munde Tambwe (wenye gauni la kijani na njano) hivi karibuni akiwa na Kaimu Meneja Masoko wa Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Tanzania (TAA), Rose Comino (wa tatu kushoto) akimwakilisha, Mhandisi Julius Ndyamukama kukabidhi saruji tani 12.5 kwa ajili ya ujenzi wa mabweni ya wanafunzi wa kike wa Kata mbalimbali za Tabora.
Na Mwandishi Wetu
 MAMLAKA ya Viwanja vya Ndege Tanzania (TAA), imeungana na Mbunge wa Viti Maalum na Wakazi wa Mkoa wa Tabora kusaidia jitihada zao za kutokomeza mimba za utotoni kwa kutoa msaada wa tani 12.5 za saruji kwa ajili ya ujenzi wa mabweni ya wanafunzi wa kike wa shule za sekondari.

Akikabidhi saruji hiyo hivi karibuni katika Kata ya Itonjanda, Manispaa ya Tabora, kwa niaba ya Mkurugenzi Mkuu wa TAA, Mhandisi  Julius Ndyamukama, ambayo ni sawa na mifuko 250 ya saruji, Kaimu Meneja wa Biashara wa Kiwanja cha Ndege cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNIA), Rose Comino, amesema TAA, ipo bega kwa bega katika suala zima la kusaidia jamii katika masuala mbalimbali likiwemo la Elimu, ambapo watoto wote ni sawa na wanastahili kupata elimu na sio kukatizwa masomo kutokana na vikwazo mbalimbali zikiwemo mimba za utotoni.
Kaimu Meneja Masoko wa Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Tanzania (TAA), Rose Comino (wa pili kushoto) hivi karibuni  akimwakilisha, Mhandisi Julius Ndyamukama akiwa kwenye picha ya pamoja na Mbunge Viti Maalum (CCM), Mhe. Munde Tambwe (wa tatu kushoto) mara baada ya kukabidhi msaada wa saruji tani 12.5, kwa ajili ya ujenzi wa mabweni ya watoto wa kike wa shule za sekondari. Wengine pichani ni Kaimu Mkurugenzi wa Manispaa ya Tabora, Joseph Kashushura (kushoto) na Kaimu Meneja wa Kiwanja cha Ndege cha Tabora (wapili kulia).
 Rose amesema Wananchi wa Tabora waungane kwa pamoja kuunga mkono jitihada za  Mbunge wa Viti Maalum Munde Tambwe la ujenzi wa mabweni kwa ajili ya watoto wa kike wa shule za sekondari, ambao wanatembea umbali mrefu kwenda shule, ambapo sasa wanatokomeza mimba za utotoni na kushirikiana kuwabaini wale wote wenye kutenda matendo hayo maovu.

“Kwa pamoja tuoneshe jitihada za dhati kwa kuhakikisha watoto wetu wanakuwa sehemu salama mabwenini, nina uhakika wa asilimia 100 kwa 100 tutapata watoto wengi wa kike watakaomaliza shule na kufanya vizuri katika masomo yao,” amesema Rose.

Amesema TAA ni miongoni mwa taasisi ya serikali iliyoanzishwa kwa mujibu wa Sheria ya Wakala wa Serikali Na.30 ya mwaka 1997 na kupewa dhamana na Serikali ya kuvisimamia na kuviendesha jumla ya viwanja 58,  imekuwa ikitekeleza sera yake ya kurudisha kwa Jamii katika masuala mbalimbali yakiwemo ya elimu.

Moja wa Shule ya sekondari ya Kata ya Itonjanda ya Manispaa ya Tabora, ambayo itajengwa bweni la watoto wa kike ili kuondoa mimba za utotoni. Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Tanzania (TAA) hivi karibuni  imetoa msaada wa saruji tani 12.5 kwa ajili ya ujenzi wa mabweni hayo.
Rose amesema viwanja vya ndege vinatoa fursa mbalimbali za kibiashara zikiwemo za kuendesha migahawa, hoteli, maduka ya bidhaa mbalimbali, usafirishaji wa mizigo ikiwemo mazao ya kilimo, mifugo na uvuvi.

Pia viwanja vya ndege vimekuwa miongoni mwa eneo linalozalisha ajira rasmi na zisizo rasmi, ambazo zinahusisha mashirika mbalimbali ya ndani na nje ya nchi yenye kutoa huduma katika maeneo ya viwanja vya ndege.

Naye Tambwe ameushukuru uongozi mzima wa TAA kwa kusaidia jitihada hizo, ambazo anauhakika kwa lengo alilojiwekea ataweza kusaidia ujenzi wa mabweni mengi katika kila kata ya Mkoa wa Tabora.

“Naomba ndugu zangu tuunge mkono jitihada hizi nilizoanzisha, na pia kuungana na  Rais John Pombe Magufuli za kutoa elimu bure, mimi nimezaliwa hapa Tabora na nimeona jinsi gani mabinti zetu wanavyotembea umbali mrefu kwenda na kurudi shule jambo ambalo linachangia kupata vishawishi njiani na kujikuta wanapata mimba za utotoni.” Amesema Tambwe.

Hatahivyo, amesema mifuko 100 kati ya hiyo 250 itapelekwa kwenye Kata ya Itonjanda, ili ujenzi uanze mara moja, na 150 iliyosalia itapelekwa kwenye shule nyingine.

Naye Mwenyekiti wa Chama cha Mapinduzi (CCM) Kata ya Itonjanda ameshukuru msaada huu uliotolewa na TAA kwani watoto wamekuwa wakitembea umbali wa Kilometa 10 kwenda shule, na wamekuwa wakiathirika kutokana na kupata mimba.

“Tumuunge mkono Rais wetu kwani Tanzania bila elimu haitaenda tuunge jitihada hizi kwani watoto wanakuwa wananawiri sana wanapoingia shule za sekondari, kwani wamekuwa wakipewa fedha ndogo ndogo ambazo zimekuwa zikiwaponza na kujikuta wanapata ujauzito, ” amesema.

Tuesday, 3 December 2019

Uchukuzi Sports Club Yakabidhi Mataji ya Mei Mosi 2019


Kaimu Katibu Mkuu wa wizara hiyo Sekta ya Uchukuzi, Gabriel Migile (wa pili kushoto) akipokea moja ya vikombe vya Michuano ya Mei Mosi 2019 kutoka kwa Makamu Mwenyekiti wa Uchukuzi Sports Club (USC), Hassan Hemed. Wa pili kushoto ni Katibu wa USC, Mbura Tena na Mkurugenzi Msaidizi Utawala Hamidu Mbegu.

Na Mwandishi Wetu
TAASISI zilizopo katika Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano zimetakiwa kupanga bajeti ya michezo  katika bajeti zao za mwaka ili kuhakikisha wanashiriki vizuri katika michezo,  imeelezwa.
Hayo yalisemwa jana na Kaimu Katibu Mkuu wa wizara hiyo Sekta ya Uchukuzi, Gabriel Migile baada ya kukabidhiwa vikombe vya ushindi wa Mashindano ya Mei Mosi 2019 kutoka kwa Makamu Mwenyekiti wa Uchukuzi Sports Klabu (UCS), Hassan Hemed.

Akijibu changamoto zilizotolewa na Katibu Mkuu wa Uchukuzi Sports Club, Mbura Tenga, ambaye katika risala yake ya utangulizi alieleza moja ya changamoto zinazowakabili ni kwa baadhi ya taasisi kushindwa kutenga fedha kwa ajili ya michezo.

Tenga alisema kuwa hilo la kushindwa kutenga fedha linatokana na taasisi hizo kutokuwa na bajeti kabisa ya michezo na wengi wa maofisa rasilimali watu wake kutojua kabisa umuhimu wa michezo kazini na kuona kama ni kupoteza muda na fedha tu.

Migire alisema kuwa taasisi nazo zinatakiwa kuiweka michezo katika bajeti za idara zao za kila mwaka ili kuhakikisha wachezaji wao wanashiriki kutoa wachezaji katika Uchukuzi Sports Club.

Migile pia aliipongeza Uchukuzi Sport Klabu kwa kutwaa ubingwa wa jumla kwa mara ya pili mfululizo katika Mashindano ya Mei Mosi, baada ya mwaka huu kutwaa jumla ya vikombe tisa, vinne vikiwa katika nafasi ya kwanza, ambavyo ni Kuvuta Kamba kwa Wanaume na Wanawake na Baiskeli kwa Wanauame na Wanawake.

Uchukuzi Sports Klabu katika Mashindano ya Mei Mosi mwaka huu yaliyofanyika Mbeya, walitwaa vikombe tisa kati ya 14, ambavyo hushindaniwa kila mwaka.

Uchukuzi pia ndio klabu pekee katika mashindano hayo kupeleka timu za michezo yote 14 ya mashindano hayo, tofauti na wizara zingine, ambazo wakati mwingine hupeleka timu au mchezaji mmoja.

Akijibu kuhusu timu ya Uchukuzi mara mbili kualikwa Zanzibar (Unguja na Pemba) na Mamlaka ya Viwanja vya Ndege ya Zanzibar (ZAA) na kufanya utalii wa ndani,  alisema hilo ni suala ni muhimu sana, hasa ukizingatia linahusu Muungano, ambapo liwataka kupanga utaratibu kuona USC wanafanyaje ili kuwaalika Bara Wazanzibari.

Pia alisema changamoto ya kutokuwa na ofisi inayoikabili USC llinaweza kushughulikiwa, hasa ukizingatia kuwa Katiba ya UCS inaeleza kuwa Mwenyekiti wa klabu hiyo, lazim atoke wizarani, hivyo itakuwa rahisi kuwepo kwa ofisi wizarani kwa ajili ya klabu yao.

Akielezea kuhusu ushindi huo wa jumla, alisema kuwa ni mkubwa sana, hivyo hauwezi kupita kimya kimya, kwani lazima na wakubwa nao wajue nini kimeletwa na USC, hivyo hafla hiyo itaandaliwa tena kwa ukubwa wake.

Aidha, Tenga alisema wanatarajia Februari 7, 2020 kufanya Mkutano mkuu kwa ajili ya mabadiliko ya Katiba pamoja na kuchagua viongozi wapya, ambapo kila taasisi ina kuwa na mwakilishi katika klabu hiyo, tofauti na sasa ambapo taasisi moja inaweza kuwa na zaidi ya mjumbe mmoja na nyingine isiwe nayo kabisa.

MultiChoice waandaaseminamaalummsimu wa saba {7}tuzo za ‘Africa Magic Viewers’ Choice Awards !


Na Mwandishi Wetu
BAADA ya kusibiri kwa muda mrefu, hatimaye Africa Magic kwa kushirikiana na Kampuni ya Multi-Choice Africa, imetangaza rasmi kupokea maombi ya kushiriki kwenye msimu wa saba wa tuzo za kimataifa za Africa Magic Viewers’ Choice Awards 2019 maarufu kama AMVCA Awards.

Akizungumza katika semina maalum kwa ajili ya tuzo hizo za awamu ya saba na wadau wa tasnia ya filamu hapa nchini, Ofisa Uhusiano wa Kampuni ya MultiChoice Tanzania Bi. Grace Mgaya amesema kuwa baada ya muda mrefu hatimaye tuzo hizo zimerejea tena.

Tuzo hizo ni mahususi kwa ajili ya filamu za Afrika na hufanyika kila mwaka ili kutambua jitihada kubwa za watengenezaji filamu, waigizaji pamoja na mafanikio makubwa yaliyofikiwa katika sekta hii ndani ya mwaka husika.

Naye Ofisa Maendeleo ya filamu , Bodi ya Filamu Tanzania, Clarence Chelesi aliongeza: “Kampuni ya MultiChoice imekuwa mstari wa mbele kuunga mkono juhudi za wazalishaji wa filamu hapa nchini kwetu, hivyo nitoe rai yangu kwa magwiji wote wa filamu hapa Tanzania kuweza kutumia fursa hii adimu kwa kushiriki katika mchakato huu ambao utawawezesha kujitangaza na kuzitangaza kazi zinazotengenezwa hapa nyumbani katika Nyanja za kimataifa kupitia tuzo hizi”, alieleza Chelesi.

Maandalizi kwa ajili ya msimu huu wa saba yanaendelea na tuzo hizi zitafanyika Machi mwakani ili kuwapata vinara mbalimbali wa filamu kutoka barani Afrika.

Maombi yanayokaribishwa kwa ajili ya kushiriki ni ya kazi za filamu na televisheni ambazo zilitayarishwa na kuoneshwa kuanzia April 1, 2018 hadi Novemba 30, 2019.
Ufuatao ni mwongozo wa jinsi ya kutuma kazi kwa ajili ya kushiriki:

Hatua ya 1: Andaa clip ya dakika 5 (reel) kwa ajili ya online submission.
Hatua ya 2: Ingia kwenye tovuti ya Africa Magic kupitia www.africamagic.tv/AMVCA. na click kwenye banner ya AMVCA Seventh edition itakayokupelekea kwenye ukurasa wa kutuma maombi

STEP 3: Jaza fomu za kuomba kushiriki halafu upload clip yako. Kila online submission iliyokamilika itapewa namba ya kumbukumbu kuthibitisha

STEP 4: Hakikisha video ya kazi yako ina uzito usiozidi mb 300

STEP 5: Weka namba yako ya kumbukumbu , kisha tuma hard drive ya kazi uliyoiwasilisha mtandaoni kwenda: Margaret Mathore
2 nd floor, MNET offices
Local Production Studio
Jamhuri Grounds off Ngong road
Nairobi Kenya

Friday, 22 November 2019

TAA Kujenga Madarasa Sekondari Wilaya Kibaha

Mwenyekiti wa Halmashauri ya Mji Kibaha, Leonard Mlowe (kushoto) leo akisalimiana na Kaimu Mkurugenzi wa Fedha na Biashara wa Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Tanzania (TAA), Josephine Kolola, ambaye alimwakilisha Mkurugenzi Mkuu, Mhandisi Julius Ndyamukama kutoa msaada wa mifuko 300 ya saruji kwa ajili ya ujenzi wa madarasa ya shule za sekondari. Kulia ni Mkurugenzi wa Mji Kibaha, Jenifer Omolo na kushoto ni Afisa Habari wa Mji Kibaha, Innocent Byarugaba.

Na Mwandishi Wetu, Kibaha
MAMLAKA ya Viwanja vya Ndege Tanzania (TAA), leo imetoa mifuko 300 ya saruji kwa ajili ya ujenzi wa madarasa ya shule za sekondari za Wilaya ya Kibaha, inayokabiliwa na upungufu wa madarasa 65.

Kaimu Mkurugenzi wa Fedha na Biashara wa TAA, Josephine Kolola aliyemwakilisha Mkurugenzi Mkuu, Mhandisi Julius Ndyamukama amesema Mamlaka hiyo inaunga mkono jitihada za serikali ya Awamu ya Tano, inayoongozwa na Mhe. Rais Dkt. John Pombe Magufuli za kutoa elimu bure kuanzia shule za msingi hadi sekondari, ambapo sasa kuongezeka kwa madarasa hayo kutachangia watoto wengi kupata elimu.

   Mkuu wa Wilaya ya Kibaha, Assumpter Mshama leo akizungumzia masuala mbalimbali ya wilaya hiyo, wakati wa hafla ya kuchangia mifuko 300 ya saruji, iliyotolewa na Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Tanzania (TAA), ambapo kulia ni Kaimu Mkurugenzi wa  Fedha na Biashara wa TAA,  Josephine Kolola, aliyemwakilisha Mkurugenzi Mkuu, Mhandisi Julius Ndyamukama.

“Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Tanzania, ipo bega kwa bega na jamii katika kuziunga mkono jitihada mbalimbali za maendeleo zinazofanywa na Serikali ya Awamu ya Tano, iliyopo chini ya Mhe. Dkt John Pombe Magufuli, ambapo inahakikisha vijana wengi wanapata elimu ya msingi na sekondari bure katika mazingira bora. Elimu wanayopata vijana wetu itawasaidia kukabiliana na changamoto za maisha kwa ajili ya ustawi wao na Taifa kwa ujumla,” amesema Kolola

Amesema katika kufanikisha jitihada hizo kwa vitendo na pia ni sera ya Mamlaka kurudisha kwa jamii kiasi cha mapato wanayozalisha ili waweze kutatua changamoto zinazowakabili, hivyo wametoa mifuko hiyo wakiwa na imani itasaidia kujenga madarasa hayo.

Amesema TAA ni taasisi ya serikali iliyoanzishwa kwa mujibu wa Sheria ya Wakala wa Serikali Na.30 ya mwaka 1997 na kupewa dhamana na Serikali ya kusimamia na kuendesha jumla ya viwanja 58 vilivyopo Tanzania Bara, ambapo Serikali inafanya jitihada kubwa katika kuboresha miundombinu mbalimbali Viwanjani ili viweze kuendana na mahitaji ya soko na ushindani wa kibiashara.

 Kaimu Mkurugenzi wa  Fedha na Biashara wa Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Tanzania (TAA),  Josephine Kolola, leo akizungumza na waandishi wa habari na watendaji wa Halmashauri ya Mji Kibaha (hawapo pichani), wakati alipomuwakilisha Mkurugenzi Mkuu wa TAA, Mhandisi Julius Ndyamukama na kukabidhi mifuko 300 ya saruji kwa ajili ya kujenga madarasa ya shule za sekondari za wilaya hiyo.


“Hivyo kupitia juhudi hizi za serikali zimezalisha fursa mbalimbali viwanjani zikiwemo fursa za kibiashara, ajira rasmi na zisizo rasmi”, amesema.

Naye Mkuu wa Wilaya ya Kibaha, Assumpter Mshama pamoja na kuishukuru TAA kwa msaada huo mkubwa, amesema katika Kampeni yao ya “Elimisha Kibaha”, wamekusudia kujenga madarasa 65, na kununua viti 3250 na meza 3250 ili kuweka mazingira bora ya kusoma kwa wanafunzi.

“Tunaupungufu mkubwa wa madarasa ambapo wanafunzi 700 wa kidato cha Kwanza mwaka huu (2019) wamekumbwa na kadhia hii, nasi tukaamua waingie darasani kwa awamu mbili asubuhi na mchana, lakini bado ikawa shida kutokana na kuwa na watoto wengi, ndio maana tukaanzisha kampeni hii kwa lengo la kupunguza na ikiwezekana kuondoa kabisa tatizo na watoto wasome katika mazingira bora,” amesema Mkuu huyo.

Mkuu wa Wilaya ya Kibaha, Assumpter Mshama (kushoto) akipokea mifuko 300 ya saruji kutoka kwa Kaimu Mkurugenzi wa Fedha na Biashara wa Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Tanzania (TAA), Josephine Kolola (kulia), katika hafla iliyofanyika leo nje ya jengo la Halmashauri ya Mji Kibaha. Kushoto ni Mkurugenzi wa Halmashauri hiyo, Jenifer Omolo.
Amesema hadi sasa tayari wamekusanya vifaa vya kutosheleza ujenzi wa madarasa 26, lakini bado hawajaanza ujenzi kutokana na fedha zilizowasilishwa Hazina kushindwa kutolewa hadi sasa kutokana na kuwa na utaratibu mrefu, ambapo amekuwa na hofu huenda hadi kufika Januari mwaka 2020 wakakumbwa na kadhia ya wanafunzi kushindwa kuendelea na kidato cha Kwanza kutokana na kukosekana na madarasa ya kutosha.

“Tunaomba huko tulipopeleka hizi fedha cash basi wazitoe ili ujenzi uanze mlolongo ni mrefu sana hatujui tatizo lipo wapi, na watui ndio kama hivi wanachangia vifaa tunashindwa kuanza ujenzi,” amesisitiza Mhe. Mkuu wa Wilaya.  

 Kamati ya Ulinzi na Usalama ya Wilaya ya Kibaha (kulia), ikiwa katika picha ya pamoja na Mkuu wa Wilaya hiyo, Assumpter Mshama (wapili kushoto), Mkurugenzi wa Halmashauri ya Mji Kibaha, Jenifer Omolo (kushoto), Katibu Tawala wa Mji Kibaha, Sosi Ngate (mwenye kilemba) wakiwa pamoja na Kaimu Mkurugenzi wa Fedha na Biashara wa Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Tanzania (TAA), Josephine Kolola aliyemwakilisha Mkurugenzi Mkuu, Mhandisi Julius Ndyamukama.


Hatahivyo, amemshukuru. Rais Dk John Pombe Magufuli kwa jitihada zake za kutoa elimu bure ambayo imesababisha mwamko mkubwa kwa wazazi wengi kuwapeleka watoto wao shule. Hali kadhalika kawashukuru wananchi, walimu na wadau wote waliojitokeza kuchangia kwa kutoa fedha taslimu, vifaa na ahadi, ambapo tayari wameshakusanya Shilingi milioni 950
.

Wednesday, 20 November 2019

Wataalam Usafiri wa Anga Jumuiya ya Afrika Mashariki Wakutana Dar es Salaam


 Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Usafiri wa Anga Tanzania (TCAA), Hamza Johari (mbele), leo  kwenye ukumbi wa Watu Mashuhuri wa Kiwanja cha Ndege cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNIA-TBII), akifungua mkutano wa siku tatu wa Wataalam wa Usafiri wa Anga WA Jumuiya ya Afrika Mashariki, ambao wanajadili namna ya kuboresha huduma na miundombinu ya usafiri huo kwa nchi wanachama. Mkutano huo unashirikisha wajumbe zaidi ya 90.

Mkurugenzi wa Kiwanja cha Ndege cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNIA), Paul Rwegasha (aliyesimama kushoto)  akiwasilisha maelezo yanayohusu majengo matatu ya abiria ya Kiwanja hicho kwa Wataalam wa Usafiri wa Anga wa Jumuiya ya Afrika Mashariki, leo wameanza mkutano wa siku tatu wa kujadili namna ya kuboresha huduma na miundombinu ya usafiri huo kwa nchi wanachama.
Meneja wa Jengo la Tatu la Abiria la Kiwanja cha Ndege cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNIA-TBIII), Mhandisi Burton Komba (mwenye koti la bluu kushoto), leo akiwaelezea mifumo mbalimbali ya jengo hilo Wataalam wa Usafiri wa Anga wa Jumuiya ya Afrika Mashariki, ambao wanashiriki mkutano wa siku tatu wa kujadili namna bora ya kuboresha huduma na miundombinu ya usafiri huo kwa nchi wanachama.


Wataalam wa Usafiri wa Anga wa Jumuiya ya Afrika Mashariki, ambao wapo nchini kushiriki mkutano wa siku tatu wa kujadili namna bora ya kuboresha huduma na miundombinu ya usafiri huo, ambapo leo wametembelea majengo ya mizigo yaliyopo kwenye Kiwanja cha Ndege cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNIA).

Friday, 15 November 2019

Mchezo Mpya wa Teq Ball Wazinduliwa Rasmi Nchini

Makamu wa Rais na Katibu Mkuu wa Kamati ya Olimpiki Tanzania (TOC), Henry Tandau (kushoto) na Filbert Bayi (kulia) wakiwa na Mkuu wa Uhusiano wa Kimataifa FITEQ, Marius Vizer Jr kabla ya uzinduzi wa mchezo huo Kibaha jana.

Na Mwandishi Wetu, Kibaha
MCHEZO mpya ujulikanao kama Teq Ball umetambulishwa rasmi Tanzania, ikiwa ni nchi ya kwanza katika Kanda ya Tano ya Afrika, imeelezwa.

Mchezo huo ulitambulishwa rasmi juzi katika Kituo cha Michezo cha Filbert kilichopo Mkuza Kibaha mkoani Pwani na wawakilishi wa Shirikisho la Kimataifa la Teq Ball (FITEQ), viongozi wa Kamati ya Olimpiki Tanzania (TOC), na viongozi wa kituo hicho pamoja na wanafunzi.

FITEQ imetoa meza tatu na mipira 12, ambapo mbili zitakuwa katika Kituo cha Olimpafrica, ambacho kinatumia vifaa vilivyopo katika Kituo cha Michezo cha Filbert Bayi mjini hapa.
Kwa Tanzania, meza mbili, moja ya TOC zitakuwa katika Kituo cha muda cha Olimpafrica kilichoko FBS Mkuza, nyingine Dole Zanzibar. Meza ya Zanzibar ilitarajia kukabidhiwa jana kisiwani humo.

Akizungumza katika uzinduzi huo, Mkuu wa Uhusiano wa Kimataifa FITEQ, Marius Vizer Jr, alisema shirikisho hilo makao yake makuu yako Hungary na sasa wako kwenye mikakati ya kuusambaza zaidi Duniani, baada ya kupata usajili wa kimataifa mwaka 2017.
Mwenyekiti wa Bodi ya Shule za Filbert Bayi, Fibert Bayi akizungumza wakati wa uzinduzi wa mchezo wa Teq Ball uliofanyika Mkuza, Kibaha jana.
Vizer Jr, alisema katika mikakati hiyo, mwaka huu wameingia mkataba na Kamati za Kitaifa za Olimpiki Afrika (ANOCAs), kuusambaza mchezo huo katika mashirikisho 40.
Hadi sasa nchi 14 tayari zimefikiwa na mchezo huo.

Alisema FITEQ itatoa Euro 6,000 (sawa na Sh 15,276,600) kwa mwaka kwa shirikisho la nchi husika kwa ajili ya uendeshaji, sambamba na kuendesha mafunzo kwa makocha na waamuzi.
Makamu Mwenyekiti wa Kamati ya Olimpiki Tanzania, TOC, Henry Tandau akipeana mkono na Mkuu wa Uhusiano wa Kimataifa FITEQ, Marius Vizer Jr wakati wa makabidhiano ya meza za mchezo huo Kibaha, Pwani jana. Kushoto ni Katibu Mkuu wa TOC, Filbert Bayi.
Naye Makamu wa Rais Kamati ya Olimpiki Tanzania (TOC), Henry Tandau, aliishukuru FITEQ na kusema kuwa historia imeandikwa kwa kuutambulisha mchezo huo.

Tandau, alisema wataitumia fursa hiyo kuhamasisha mchezo huo kwa kuundwa chama cha kitaifa, kuusambaza mikoani, kisha mashindano ya ngazi mbalimbali ili baadae uweze kuwa mchezo mkubwa nchini.
Alisema watajitahidi Tanzania ipate kuwa mwenyeji wa kwanza wa Fainali za Afrika za mchezo huo.

Naye Mwenyekiti wa Bodi ya Shule za Filbert Bayi (FBS), Filbert Bayi, mbali na kushukuru alisema watautendea haki msaada huo kwa kuhakikisha unachezwa na kuundwa timu mbalimbali.

Mchezo huo ni mchanganyiko wa Mpira wa Meza na Mpira wa Miguu, ambapo huhesabiwa kwa pointi zifikapo 20 kwa utofauti wa pointi mbili.
Huchezwa kwa mchezaji moja moja au wawili wawili, ukitumia meza iliyopinda, mpira kama wa miguu na viungo vya mwili miguu, kifua, mabega na kichwa, isipoluwa mikono hairuhisiwi.

Mchezaji hatakiwi kutumia kiungo kimoja mara mbili, pia kuugusa mpira zaidi ya mara tatu.
Mkurugenzi wa Shule za Filbert Bayi, Anna Bayi (kulia) akipiga mpira kwa kichwa wakati akicheza mchezo wa Teq Ball Kibaha mkoani Pwani jana. Kulia ni Makamu wa Rais na Katibu Mkuu wa Kamati ya Olimpiki Tanzania (TOC), Henry Tandau (kulia mbele) na Filbert Bayi. 
Na kabla ya uzinduzi wakufunzi wa mchezo huo kutoka hungary, Gondos Zoltan na Vasas Lea walionesha umahiri mkubwa wa kuucheza mchezo huo kwa kumiliki mpira na kuupiga kwa kutumia kichwa, mabega, miguu, magoti na viungo vingine isipokuwa mikono.
Mchezo huu uliasisiwa mwaka 2013 na umewahi kuchezwa na wanasoka maarufu Duniani kama akina Luis Figo na Ronaldihno Gaucho ambaye pia ndiye Balozi wa mchezo huo.