Monday, 8 May 2017

Taifa laomboleza msiba mkubwa wa wanafunzi 33

Na Waandishi Wetu
MAKAMU wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan Leo ataongoza maelfu ya wananchi kuaga miili ya wanafunzi 33 na wafanyakazi watatu wa shule ya Lucky Vicent ya Arusha waliokufa katika ajali ya gari katika korongo la Mto Marera, Kata ya Rhotia wilayani Karatu mkoani Arusha.

Wanafunzi hao walikuwa wakienda Karatu kwa ajili ya mitihani ya kujipima ya ujirani mwema kati ya shule yao na ile ya Tumaini ya Karatu.

Tangu baada ya taarifa za ajali za msiba huo kusambaa katika mitandao ya kijamii, siku nzima ya juzi ikawa ya majonzi makubwa, ambayo yameendelea kwa siku nyingine ya jana na zaidi leo wakati wa ibada maalumu kwenye Uwanja wa Michezo wa Sheikh Amri Abeid Kaluta uliopo katikati ya Jiji la Arusha.

Makamu wa Rais, Samia Suluhu Hassan, alitarajia kutua mjini Arusha jana jioni na leo ataongoza wakazi hao wa Arusha pamoja na vitongoji vyake kuaga miili hiyo.

Mbali ya Makamu wa Rais, viongozi wengine wa serikali watakaoshiriki ibada hiyo ni Kaimu Jaji Mkuu wa Tanzania, Profesa Ibrahim Juma, Waziri wa Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (Tamisemi), George Simbachawene, Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto,

 Ummy Mwalimu, Waziri wa Elimu, Sayansi, Teknolojia na Mafunzo ya Ufundi, Profesa Joyce Ndalichako na Katibu Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Abdulrahman Kinana.

Tayari Rais Mstaafu wa Awamu ya Nne, Jakaya Kikwete, Waziri Mkuu Mstaafu, Fredirick Sumaye, Waziri Mkuu Mstaafu, Edward Lowassa wameshafika kwenye Uwanja huo wa michezo kwa ajili ya hafla hiyo ya maombolezo.

Gambo atoa ratiba
Mkuu wa Mkoa wa Arusha, Mrisho Gambo aliwaambia wanahabari kuwa viongozi hao wamethibitisha kushiriki ibada hiyo itakayoanza saa mbili asubuhi.

Gambo alisema miili yote ya wanafunzi waliokufa katika ajali hiyo itakuwepo kwenye uwanja huo na kufanyiwa ibada kabla ya kuchukuliwa na ndugu, jamaa kwa ajili ya kwenda katika maziko mahali watakapokuwa wamekuchagua.

Aliwataka Watanzania waliopo jijini Arusha na nje ya Arusha kuja kwa wingi katika ibada hiyo yenye simanzi kubwa kwa Watanzania wote kote nchini.

Wanafunzi hao walipata ajali katika eneo la Rhotia na gari aina ya Mitsubishi Rosa lenye namba za usajili T871 BYS lililokuwa likitoka jijini Arusha kwenda katika Mji wa Karatu kupata ajali ya kutumbukia mtoni na kusababisha vifo hivyo.

Wanafunzi hao waliondoka jijini Arusha saa mbili asubuhi kuwahi mtihani huo wa majaribio wa kirafiki na wenzao wa Shule ya Msingi ya Tumaini Junior ya Karatu.

Majina ya waliokufa
Majina ya wanafunzi walikufa wametajwa kuwa ni Aisha Said, Anold  Alex, Gladness Goodluck, Junior Mwashuy, Praise Ronald, Witness Moses na Heavenlight Mcharo.

Wengine ni Eliapenda Eliudi, Rukia Halfan, Justine Alex, Rehema Msuya, Irene Kishari, Prisca Charles, Ian Tarimo, Shedrak Bikhet, Sabrina Saidi, Rachel Gidion, Irene Moses, Hagai Lucas.

Pia wamo Rehema Eliwadi, Rebeca Daudi, Dismas Kessy, Innocent Papian (mwalimu), Oumuh Rashid, Gema Gerald, Grayson Masawe, Julius Bonge Mollel (mwalimu), Joel Lucas, Naomi Hosea, Ruth Ndemno, Saada Ally, Neema Martin, Witness Philemon na Musa Khamis.

Aidha, kwa mujibu wa mtu wa mtumishi wa chumba cha maiti Hospitali ya Mkoa ya Mount Meru, ambaye hakupenda kutaja jina lake, baadhi ya miili ya watoto hao imehamishiwa Hospitali ya Selian kwa sababu mochwari ya Mount Meru ilikuwa imejaa, hivyo maiti zilizohamishiwa huko ni saba ambazo ni Neema Martin, Oumuh Rashid, Gema Mchome, Irene Moses, Rebeka Daudi, Hagai Lucas na Rachel Gidion.

Wazazi na walezi walikusanyika tangu asubuhi ya jana kwenye Hospitali ya Mount Meru kwa ajili ya kuwaona watoto hao huku wakisoma majina yaliyobandikwa ili kujua kama wapo hospitali hiyo au Hospitali ya Selian.

Wazazi wasimulia walivyopokea msiba

Katika hatua nyingine, badhi ya wazazi wameelezea jinsi walivyopokea msiba kwa huzuni na wengine wakisema ni jambo la kushukuru kwa yote kwani mapenzi ya Mungu yametimizwa.

Wakizungumza katika maeneo tofauti ya Kwamrombo katika eneo la Baa Mpya na Mtaa wa Mlimani Kata ya Terrat, baadhi ya wazazi hao walioondokewa na watoto wao, walisema inaumiza kwani baadhi ya watoto walikuwa wakikaa shuleni wakiwa darasa la saba huku wengine wakitokea nyumbani kwenda ziara ya kimasomo Karatu.

Mzazi wa marehemu, Irene Moses (13) ambaye ni Mosses Kivuyo anayefanya kazi Shirika la Umeme Tanzania (Tanesco) wilayani Kahama Mkoa wa Shinyanga ambaye sasa yupo masomoni Chuo cha Ufundi Arusha, alisema mtoto wake Irene alikwenda Karatu na wenzake, lakini ghafla alisikia taarifa kuwa watoto hao wamepata ajali.

Alisema hakujua kama mwanawe ni miongoni mwa waliokufa, lakini alijipa moyo na kisha kuanza safari ya kutoka Arusha kwenda Rothia kwa ajili ya kuona watoto hao akiwemo mwanawe Irene na alipokuwa njiani, alipigiwa simu na wauguzi wakisema mtoto wake anataka kufanyiwa upasuaji, lakini wameamua kwanza wampigie simu.

Ashuhudia mwanawe akikata roho

Alisema aliwajibu wauguzi hao kwamba yuko njiani anakwenda na alipokaribia eneo la tukio hakumwona binti yake hivyo akaenda hospitali sababu alipigiwa simu kwani mtoto wake ndiye alisema apigiwe simu akiwa majeruhi “ndipo niliondoka kwenda kumuona Hospitali ya Karatu kumuona ndipo nilipofika tu mtoto wangu namuona akifa.”


“Ukweli nimeumia kama mzazi. Huyu ni mtoto wangu wa kwanza kati ya watoto watatu sasa huu msiba ni mzito sana kwetu wazazi tulioondokewa na watoto... inauma jamani, lakini haya ni mapenzi ya Mungu nashukuru kwa hili. Lakini nimeumia nafika tu hospitali mtoto anakufa jamani Irene wangu,” alieleza Moses.

Monday, 1 May 2017

Ndondi za taifa zamalizika Dar es Salaam








Tottenham yazidisha presha kwa vinara Chelsea

Kocha wa Arsenal, Arsene Wenger (kushoto) na mwenzake wa Tottenham Hotspur, Mauricio Pochettino kabla ya kuanza kwa mchezo wa timu zao, ambapo Arsenal ilichapwa 2-0 juzi. 
LONDON, England
USHINDI wa Tottenham dhidi ya Arsenal una maana kuwa umeongeza shinikizo la kisaikolojia kwa Chelsea katika kilele cha msimamo wa Ligi Kuu ya England, anasema kocha Mauricio Pochettino.

Kocha huyo Muargentina alisema juzi kuwa, ushindi wa mabao 2-1 ni muhimu kwa mashabiki wetu, wakati Spurs ikithibitisha kuhitimisha miaka 22 ya kusubiri kumaliza juu ya wapinzani wao hao wakubwa.

Lakini kocha huyo aliongeza "kitu muhimu" ni kuendelea kubanana na vinara Chelsea, ambayo iliifunga Everton kwa mabao 3-0.

"Tuko katika mbio na tofauti imerejea kuwa pointi nne kama mwanzo,alisema Pochettino.

"Sasa tunatakiwa kuelekeza nguvu zetu katika kila mchezo. Tuna mchezo mwingine mkubwa dhidi ya West Ham Ijumaa, ikiwa ni mpambano mwingine mgumu.

"Hiyo itakuwa nafasi ya kuongeza shinikizo la kisaikolojia kwa Chelsea. Tutacheza kabla yao, na kama tukishinda itakuwa shinikizo tosha la kisaikolojia na tutaangalia nini kitatokea wakati Chelsea watakapocheza dhidi ya Middlesbrough Jumatatu kwenye Uwanja wa Stamford Bridge."

Ushindi wa Chelsea dhidi ya Everton katika mchezo uliopigwa mapema juzi Jumapili umekipandisha kikosi hicho cha kocha Antonio Conte pointi saba dhidi ya mpinzani wake mkubwa, lakini sasa tofauti imerejea katika pointi nne baada ya Spurs nayo kushinda.

Lakini bao la 21 la Dele Alli katika klabu hiyo msimu huu na lile la penalti la Harry Kane yaliiwezesha Spurs kupata ushindi wa tisa mfululizo katika ligi, ikiongeza kipindi chao bora tangu Oktoba 1960, wakati waliposhinda mechi 13 mfululizo.

Chelsea imekuwa ikishikilia uongozi wa ligi tangu Novemba 5, na walikuwa wakiongoza kwa pointi tisa Machi 19.
Tangu wakati huo, Chelsea ilifungwa mara mbili, wakipokea kichapo kutoka kwa Crystal Palace na baadae Manchester United.

"Naweza kuwaelewa mashabiki wetu kuwa watafurahia sana kama tutamaliza tukiwa juu ya Arsenal, lakini sijisikii sawa nao kwa sababu kwangu mimi ni suala la kujaribu kutwaa taji na sio kuwa juu ya Arsenal tu, aliongeza Pochettino.

"Ni muhimu sana sasa kujaribu na kushinda mataji kila msimu, hilo ndilo lengo letu kubwa.

"Ni ukweli kuwa itakuwa ngumu kutwaataji lakini tutaangalia nini kitatokea.

Mchezo wa Jumapili ndio lilikuwa pambano la mwisho kucheza kwenye Uwanja wa White Hart Lane katika hali ya sasa.

Tottenham itakuwa ikicheza mechi zake za nyumbani kwenye Uwanja wa Wembley katika msimu wa mwaka 2017-18 wakati ujenzi ukiendelea kwenye uwanja wao mpya.

Uwanja huo mpya wa klabu hiyo utakuwa na uwezo wa kuchukua watazamaji 61,000 waliokaa ambao unajengwa jirani na makazi yao ya sasa.


Mechi zilizobaki za Tottenham 2016-17:

Ijumaa, Mei 5     West Ham (Ugenini)

Jumapili, Mei 14  Man Utd (Nyumbani)

Alhamisi, Mei 8   Leicester (Ugenini)

Jumapili, Mei 21 Hull (Ugenini)


Mechi zilizobaki za Chelsea 2016-17


Jumatatu, Mei 8 Middlesbrough (Nyumbanbi)

Ijumaa, Mei 12:   West Brom (Ugenini)

Jumatatu, Mei 15  Watford (Nyumbani)

Jumapili, Mei 21  Sunderland (Nyumbani)

Jumamosi, Mei 27  Arsenal (Fainali FA Cup)

Kwa mara ya mwisho Tottenham ilimaliza juu ya Arsenal ilikuwa mwaka 1995, wakati walipomaliza wa saba na the Gunners walimaliza katika nafasi ya 12.


SHEREHE ZA MEI MOSI ZILIVYOFANA DAR ES SALAAM


Siku ya Wafanyakazi Duniani imeadhimishwa leo duniami kote huku mkoa wa Dar es Salaam sherehe hiyo ilifanyika kwenye Uwanja wa Uhuru, ambako mgeni rasmi alikuwa Mbunge wa Urambo Mashariki, Margaret Sitta.

Wafanyakazi wa Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Tanzania (TAA), ambao wako chini ya Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano wakiwa katika maandamano ya Siku ya Wafanyakazi leo kwenye Uwanja wa Uhuru jijini Dar es Salaam.


Wafanyakazi wa Kiwanja cha Kimataifa cha Ndege cha Julius Nyerere (JNIA).