Tuesday 28 July 2015

Mapadri, mtawa wafa ajalini Kagera




Na Mwandishi Wetu
MAPADRI watatu na mtawa mmoja wa kanisa katoliki Jimbo la Rulenge Wilayani Ngara mkoani Kagera wamefariki dunia papo hapo huku watu 13 wakijeruhiwa, katika ajali ya barabarani wakiwahi Karagwe kwenye misa ya shukrani ya mwenzao aliyepata daraja hilo hivi karibuni.  

Katika ajali nyingine ya barabarani, watu saba wamekufa na wengine 44 kujeruhiwa katika ajali iliyohusisha basi na treni ya mizigo mkoani Tabora juzi.

Katika ajali hiyo, watu wanne walikufa katika eneo la tukio na wengine watatu kufia hospitalini baada ya kukimbizwa katika hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Tabora ya Kitete.

Kwa mujibu wa moja wa mapadriwaliokuwa katika msafara huo, Erasto Nakule, ajali hiyo imetokea leo saa 2:00 asubuhi katika  barabara iendayo nchi jirani ya Uganda katika eneo la Bugorora  wilayani Missenyi mkoani Kagera.   

Alisema gari aina ya Land Cruser lenye namba ya usajili T.650 BYI la Jimbo Katoliki la Rulenge lililokuwa likiendeshwa na Padri Florian Tuombe ambaye amefia katika hospitali ya mkoa Kagera, liligongana uso kwa uso na basi la Kampuni ya Sabuni lenye namba za usajili T.166 AGU.  

Alisema basi la Sabuni lilikuwa likitokea wilayani Karagwe kwenda mkoani Mwanza, ambapo Land Cruser hilo lilikuwa likitokea Biharamulo kwenda Karagwe.

Padri Nakule aliwataja waliofariki dunia katika ajali hiyo kuwa ni pamoja na padri, Michael Mwelinde (70), Padri, Onesmo Buberwa (40), padre Florian Tuombe aliyekuwa dereva wa gari la mapadri na Sister  Magreth Kadebe (60).

Habari zaidi zilieleza kuwa mapadri hao walikuwa ni walimu wa seminari ya Rutabo wilayani Muleba na kwamba walikuwa wakienda kwenye misa ya shukrani ya padre Evisius Shumbusho  iliyouwa ikifanyika Karagwe.

Naye Kamanda wa Polisi mkoa wa Kagera, Augustine Ollomi alisema chanzo cha ajali hiyo ni kutokana na dereva wa Land Cruser kuendesha bila kuchukua tahadhari, ambapo alitaka kupita basi la Sabuni na hivyo kugongana uso kwa uso. 

Kamanda Ollomi alisema katika ajali hiyo watu wanne wamefariki dunia na kwamba majina yao bado hayajajulikana akiwemo na mwanafunzi anayesomea upadri katika seminari ya Rutabo.

Monday 27 July 2015

Dk. Salim awataka Watanzania kulinda amani na utulivu



Na Mwandishi Wetu
WATANZANIA wameaswa kulinda amani na utulivu kuelekea Uchaguzi Mkuu wa Madiwani, Wabunge na Rais mwezi Oktoba.

Hayo yalisemwa na Waziri Mkuu Mstaafu Dk. Salim Ahmed Salim kwenye ufunguzi wa Semina ya  siku tatu ya Urithi wa Utamaduni wetu iliyoandaliwa na Chuo Kikuu cha kiislam (Muslim University of Tanzania)  kupitia taasisi yake ya Urithi wa Utamaduni (Institute of Cultural Heritage).

“Cha msingi kuelekea uchaguzi mkuu, niwaombe watanzania kulinda amani na utulivu kwenye nchi yetu ili kuendeleza sifa hii nzuri inayotambulika kimataifa.

“Sasa tusiridhike na kujisahau tukaacha amani tuliyonayo ikapotea, ni muhimu kulinda amani ya nchi yetu, tusichukulie yanayotokea katika nchi nyingine ni ya uko uko tu, wote tuna wajibu wa kulinda amani ya nchi,”alisema Dk Salim ambae pia ni Mwenyekiti wa Taasisi ya Mwalimu Nyerere.

Dk  Salim alisema kwamba demokrasia imekuwa kwa kiwango kikubwa na hiyo inafanya watu kuwa na fikra tofauti na kusisitiza kwamba hakuna budi kukubaliana na fikra tofauti kwani ni matokeo ya kukuwa na kupanuka kwa demokrasia nchini.

“Kuna vyama vingi vya siasa nchini, vikubwa na vidogo, yote ni kutokana na kukua kwa demokrasia, uwingi wa vyama hivi unakuja na mawazo na fikra tofauti tofauti na hivyo hatuna budi kukubaliana navyo kwani wote ni watanzania,”alisema Dk Salim.

Alisema kwamba taifa linakabiliwa na changamoto kubwa ya ukosefu wa maadili unayofanya watu kuwania nafasi mbalimbali za uongozi kwa lengo la kwenda kula na sio kuwatumikia watanzania na kusema hali hiyo sio vyema ikiachwa iendelee kwa mustakabali mzuri wa taifa.

Rest In Peace Bobbi Kristina Brown


Bobbi Kristina Brown wakati wa uhai wake


Sunday 26 July 2015

Mtoto wa Whitney Houston afariki dunia

*Kifo chake kimetokea baada ya kuchomolewa mashine


NEW YORK, Marekani
MTOTO wa mwanamuziki Whitney Houston (sasa marehemu), Bobbi Kristina Brown amefariki dunia akiwa na umri wa miaka 22, alisema mwakilishi wa familia.

Msemaji wa familia hiyo Kristen Foster alisema Kristina alifariki dunia akiwa amezungukwa na familia yake na "hatimaye ana amani katika mikono ya Mungu ".

Brown alikutwa akiwa ajitambui katika bafu Januari 31 na tangu wakati huo alikuwa katika koma. Kamwe hakuwahi kuzinduka tangu wakati huo.
 
Baadae alihamishiwa katika hospitali ya wagonjwa mahututi katika jiji la Duluth, Georgia, mwezi mmoja uliopita baada ya hali yake kuzidi kuwa mbaya.

Brown ni mtoto pekee wa kike wa Houston aliyezaa na muimbaji nyota wa R&B Bobby Brown.

Whitney Houston alikutwa amekufa katika bafu la hoteli huko Los Angeles mwaka 2012.

"Bobbi Kristina Brown alifariki Julai 26 2015, akiwa amezungukwa na familia yake, " alisema Foster.

"Hatimae amepumzika kwa amani katika mikono y Mungu. Tunapenda kumshukuru kila mmoja kwa upendo wake na kutuunga mkono katika kpindi hiki cha miezi kadhaa ya matatizo."

Taarifa zingine kutoka Los Angeles zinasema Brown alikuwa na ndoto za kufuata nyayo za mama yake katika uimbaji na uigizaji, na tayari alikuwa na majukumu kidogo katika TV, lakini bado alikuwa hajaanza kuchanganya.

Lakini Januari Polisi walisema kuwa Brown alikuwa uso wake ukiwa chini bafuni nyumbani kwake Atlanta ambako alikuwa akishirikiana na Nick Gordon, mtu ambaye alikuwa akimuita mume wake.

Gordon alisema wakati huo kuwa alionekana kutopumua kabla ya kuwasili kwa huduma ya dhahrura.

Brown aliwekwa eneo la wagonjwa mahututi akipatiwa matubabu ambako alikuwa akipumua kwa kutumia mashine.

Inaelezwa kuwa kifo chake kimetokea karibu miezi sita baada ya polisi na watu wa uokoaji kupigiwa simu Januari 31, 2015 kwenda kumchukua baada ya kukutwa amepoteza fahamu ndani ya bafu.
 
Tangu wakati huo mtoto huyo wa muimbaji nyota alikuwa akiishi kwa msaada wa mashine na inaelezwa kuwa alikuwa mtumiaji mkubwa wa dawa za kulevya.
 

Wednesday 22 July 2015

Messi sasa mshambuliaji aliyekamili zaidi kuliko alivyokuwa mwaka 2009



BARCELONA, Hispania
LIONEL Messi yuko vizuri zaidi mwaka huu kuliko alivyokuwa mwaka 2009, kwa mujibu wa winga wazamani wa Barcelona, Lobo Carrasco.

Mchezaji huyo aliiwezesha timu hiyo msimu uliopita kutwaa mataji matatu kama alivyofanya miaka sita iliyopita wakati wa msimu wa kwanza wa kocha Pep Guardiola, lakini Carrasco anaamini kuwa mshambuliaji huyo sasa amekamilika zaidi.

"Leo Messi wa sasa amekamilika zaidi, " alisema.

"Anaweza kukumaliza hata akiwa umbali wa mita 40 kutoka katika goli, na sio kwa sababu amechukua mpira na kuanza kuukokota kuwapita wapinzani, lakini kwa sababu anaweza kutengeneza nafasi ya kufunga goli.

Messi awali alikuwa akipambana kusaka kiwango katika nusu ya kwanza ya msimu uliopita lakini alibadilika nusu ya pili ya msimu na kufanya vizuri.

"Barcelona walitarajia mambo mazuri msimu uliopita lakini sio kutwaa mataji matatu. Ilikuwa inanekana kama haiwezekani kufikia mafanikio ya msimu wa ajabu wa mwaka 2009, lakini Messi ndio aliuwa mhimili wa mafanikio."

Carrasco alitwaa mataji 10 wakati alipoichezea Barcelona mechi zaidi ya 300, ikiwemo taji la La Liga mwaka 1985.

Pia alifikia fainali za Ulaya mwaka 1984, ambako Hispania ilifungwa na wenyeji Ufaransa kwa bao la Michel Platini.

Sunday 19 July 2015

Diamond Plutinumz ang'ara tuzo za MTV Mama Afrika Kusini




Na Mwandishi Wetu
MWANAMUZIKI wa muziki wa kizazi kipya, Nassib Abdul, Diamond Plutinumz ameng'ara kwenye shindano la MTV Mama Awards lililofanyika usiku wa kuamkia leo, Afrika Kusini na anatarajiwa kuwasili nchini Jumanne.

Katika tuzo hizo zilizofanyika jijini Kwazulu Natal katika Ukumbi wa Kimataifa wa Durban Diamond alishinda kwenye kipengele cha mburudishaji bora wa mwaka.

Katika kinyang'anyiro hicho wasanii kutoka Nigeria waling'ara zaidi katika vipengele mbalimbali huku Tanzania ikiwakilishwa na Diamond.

Akizungumza na gazeti hili kuhusianana ushindi huo Meneja wa msanii huyo, Babu Tale alisema kuwa ushindi huo ni mafanikio kwa Tanzania na sekta nzima ya muziki kwa kuwa umeliletea heshima taifa.

Alisema kuwa kwa ushindi huo umesaidia kumtangaza kimataifa zaidi na umeanza kufungua milango nje ya nchi kwa kuwa kwa sasa inakuwa kwake ni rahisi zaidi kumnadi msanii wake huyo.

Alisema " Hii ni zawadi kwa watanzania wote kwa ujumla na msanii wetu amewainua kimasomaso na huu ni mwanzo tu kwa kuwa kazi ndio kwanza inaanza na tuna uhakika wa kufika mbali zaidi na kuwakilisha vema sanaa ya Tanzania"
  
Katika shindano hilo wasanii mapacha wanaounda kundi la P square, Peter and Paul walichaguliwa kama wasanii bora wa mhongo huu

Kwa upande wa mwanamuziki bora wa kike nafasi ilichukuliwa na mwanamuziki Yemi Alade wa Nigeria huku mshindi wa kipengele cha mburudishaji bora wa kiume ikienda kwa Davido.

Kundi la P Square pia lilichaguliwa kama kundi bora la mwaka, Cassper Nyovest wa Nigeria aliibuka kama mwanamuziki bora wa Hip Hop na mwanamuziki AKA wa Afrika Kusini akiwa na mwenzake Burna Boy walishinda kwenye kipengele cha wimbo bora wa kushirikishwa.

Wimbo bora wa mwaka ulikuwa ni ule wa All Eyes On Me ulioimbwa na Da Les kwa ushirikiano na & JR huku ule wimbo wa  Dorobucci nao kutoka Nigeria ukishika nafasi ya kuwa wimbo bora wa jukwaani.